STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Monday, May 21, 2012

Matibabu ya Sajuki nchini India shakani, kisa...!

IMEELEZWA kwamba upungufu wa damu na kudhoofika mwili kupita kiasi kumemfanya mtayarishaji na mcheza filamu mashuhuri nchini, Salum Juma Kilowoko ‘Sajuki’, kushindwa kufanyiwa upasuaji mapema nchini India alikokwenda kwa matibabu. Sajuki ambaye aliondoka nchini Jumapili iliyopita na kufikia katika Hospitali ya Saifee iliyopo Mumbai, nchini India, anakopatiwa matibabu, ameanza kuongezewa damu na kupewa vyakula ambavyo vitaweza kuupa mwili wake nguvu ili kukabiliana na zoezi la upasuaji. Kwa mujibu wa rafiki wa karibu wa Sajuki, Denis Sweya ’Dino’ ambaye alizungumza na gazeti hili muda mfupi baada ya kuwasiliana na mke wa Sajuki, Wastara, alisema hali ya msanii huyo imezidi kutengemaa kila kukicha na kuwaomba Watanzania kumuombea zaidi kwa Mungu aweze kurudi haraka katika hali yake. Sajuki anasumbuliwa na tatizo la uvimbe pembeni ya ini, ambapo wataalamu wa afya wanadai kuwa ni dalili za ugonjwa wa Hepatoma (kansa ya ini). Taarifa za awali zinaeleza kwamba Sajuki alianza kwa kupata uvimbe sehemu tofauti katika mkono wake mmoja, lakini baadaye tatizo hilo lilihamia ndani na kuanza kupata maumivu makali pembeni ya ini. Katika mahojiano yake na gazeti moja la wiki, Sajuki alikaririwa akisema madaktari walibaini ana uvimbe pembeni ya ini tatizo ambalo limekuwa likinisumbua kwa muda mrefu. Kutokana na hali hiyo, wadau mbalimbali wa filamu wakiwemo wasanii waliweza kumchangia nyota huyo kiasi cha fedha ambacho alitakiwa kukipata ili kuweza kufanyiwa matibabu nje ya Tanzania. Tanzania Daima inamtakia kila la kheri Sajuki. CHANZO:TANZANIA DAIMA

Boban azuiwa Airport akimsafirisha Mafisango, kisa...!

Michael Momburi, Kinshasa SAFARI ya mwisho ya kiungo wa Simba, Patrick Mafisango kuonekana duniani, inakamilishwa leo wakati sanduku lenye mwili wake litakapoteremshwa kaburini baadaye jioni. Mafisango alifariki alfajii ya Alhamisi iliyopita baada ya gai lake kuacha njia na kuingia mtaroni. Alikuwa akitoka Maisha Club kurudi nyumbani. Kiungo huyo aliyeacha mke na watoto watatu, aliagwa juzi kwenye Viwanja vya Klabu ya Sigara, Chang'ombe Dar es Salaam. Msafara wa uliosindikiza mwili wa Mafisango ulitua jijini hapa jana saa 6.10 mchana na kulakiwana mashabiki wengi wa kike huku askari wa usalama ndani ya Uwanja wa Ndege wahapa wakishindwa kujizuia na kumwaga machozi. Mafisango atazikwa leo kwenye makaburi ya Kinkole yaliyoko karibu na Uwanja wa Ndege wa Kinshasa. Baada ya mwili wa mchezaji huyo kutua, askari wa uhamiaji pamoja na wahudumu wa afya wanaokagua kadi za chanjo kwa wasafiri ndani ya uwanja wa ndege walianza kuuliza kwamba ni nani huyo lakini walipoelezwa bado hawakuelewa kwa vile mchezaji huyo hakuwahi kutamba na timu yoyote ya Kinshasa. Kiungo wa DC Motema Pembe, Mussa Hassan Mgosi alikuwa miongoni mwa waombolezaji. Mkuu wa msafara wa Simba, Itang'are alipotoa nakala za magazeti ya Tanzania na kuwaonyesha waliacha kazi zao na kuuzingira mwili huo huku wanawake wakishindwa kujizuia nakuanza kumwaga machozi kwa jinsi walivyoona gari lake lilivyochakaa baada ya ajali hiyo. Askari hao walitumia takribani dakika 10 kuangalia jeneza la mchezaji huyo huku wengine wakikimbia ofisi zao na kwenda kuliangalia na walisaidia kulitoa nje kuwakabidhi ndugu ingawa walizuia kabisa kupiga picha eneo la uwanja. Licha ya barabara nyingi kuwa chakavu kwenda Lemba nje ya kidogo ya jiji alikokuwa akiishi marehemu, mwili wake ulibebwa kwa gari ndogo ukiongozwa na ving’ora ingawa msafara huo uliingiliwa na 'daladala'. Msafara mzima ulikuwa na magari manane. Nyumbani kwa marehemu, kulikuwa na wanawake wengi waliokuwa wakimlilia mchezaji huyo wa Rwanda na ilitumia karibu saa nzima kuwatuliza kabla ya Mzee Kinesi kumkabidhi baba mlezi wa Mafisango, Papaa Pierre mwili wa mchezaji huyo kisha kumwelezea tukio zima la ajali na hali ilivyokuwa Tanzania. Pierre alishindwa kujizuia na kuanza kulia kwa sauti ya juu. Mwili huo wa mchezaji huyo ambaye hapa anafahamika kwa jina la Patrick Tabu Ete ambayo ndiyo majina halisi ya wazazi wake, haukukaa sana nyumbani hapo kutokana na nafasi kuwa ndogo na waliuhamishia kwenye Uwanja wa mpira wa Terrain ambao Mafisango alianzia kucheza soka ili kutoa nafasi ya mashabiki kumuaga zoezi linaloendelea hadi leo mchana. Ingawa anaonekana si maarufu sana jijini hapa kama ilivyo Lubumbashi na Rwanda, mchezaji huyo picha zake zilikuwa zimebandikwa kwenye magari mbalimbali ya vijana na hadi jana jioni hakuna mke wake aliyekuwa amewasili wala mtoto. Pierre alisema; “Msibahuu unauma sana, hakuna jinsi ninavyoweza kuelezea lakini nashukuru Wanasimbana Tanzania kwa kumpa heshima stahili mwanangu, hii ni kazi ya Mungu, tumpumzishe aende kwa amani.” Ujumbe wa Shirikisho la Soka la Rwanda, Ferwafa pamoja na familia na wageni mbalimbali mashuhuri walitarajiwa kuwasili usiku wa kuamkia leo kwa shughuli hiyo. Katika hatua nyingine, nguo za Mafisango zimeyeyuka kiaina huku Haruna Moshi ‘Boban’ akionja joto ya jiwe kwenye Uwanja wa Ndege wa hapa. Ndugu wa Mafisango waliokuwa wakiishi naye jijini Dar es Salaam walidai kupakia nguo hizo kwenye ndege na walipofika Kinshasa hazikuonekana huku wahudumu wakidai zitakuwa zimesahaulika Nairobi. “Sisi tuliziweka sehemu ya mizigo lakini tunashangaa hapa hazionekani wanasema labda zimebaki Nairobi, kule ndani ya begi lake vilikuwa vitu vyake vyote mpaka zile nguo alizopatia ajali yaani sijui itakuwaje,” ndugu mmoja alimueleza Papaa Pierre ambaye ni baba mlezi wa Mafisango. Lakini wahudumu wa ndege iliyosafirisha mizigo hiyo wameahidi kwamba leo Jumapili huenda nguo hizo zikapatikana kama kweli zilikwama Nairobi. Wakati huo huo, Haruna Moshi aliyesindikiza mwili wa marehemu, alizuiwa kwa zaidi ya nusu saa na maofisa wa uhamiaji ndani ya Uwanja wa Ndege wa Kinshasa kwa madai kuwa pasi yake ya kusafiria si halali. Maafisa hao walikuwa wakidai pasi hiyo ya dharura anayotumia Boban hairuhusu kuingia nchini Congo bali kwenye nchi za Afrika Mashariki lakini baadaye wakalainika na kumruhusu. “Huyu anarudi Dar es Salaam hawezi kuingia Congo na hii karatasi nyie ondokeni, huyu gari lile pale anarudi nalo mpeni kila kilicho chake,”alisema Afisa mmoja akimwambia mkuu wa msafara wa Simba Mzee Kinesi. Lakini baadaye maafisa hao walipoona picha za Boban kwenye magazeti ya Tanzania yaliyoripoti ajali ya Mafisango walilainika na kuamua kumruhusu Boban aingie ingawa alishachanganyikiwa na kutaka kulia huku akigoma kwenda licha ya kwamba askari hao haswa wa kiume walimsukuma mara kadhaa. “Sasa mimi niende wapi wakati ubalozi wenu umenipa visa na kuniruhusu nije kuwawakilisha wachezaji wenzangu kwenye mazishi ya ndugu yetu,”alisikika Boban akimwambia askari mmoja. Hata hivyo baadhiya askari walisikika waziwazi wakiomba kitu kidogo ili wamuachie Boban apite kwani alisahau hata karatasi yake ya chanjo jijini Dar es Salaam. Habari hii kwa hisani ya Michael Momburi kupitia ShafiiDauda.Blogspot.com

TPBO yamlilia Mafisango, waipa pole Simba

OGANAIZESHENI ya Ngumi za Kulipwa nchini, TPBO, imetuma salamu za rambirambi kwa klabu ya soka ya Simba kutokana na msiba wa kiungo wao nyota, Patrick Mutesa mafisango aliyefariki wiki iliyopita kwa ajali ya gari. Rais wa TPBO, Yasin 'Ustaadh' Abdallah, alisema wameshtushwa na kifo cha ghafla cha mchezaji huyo aliyekuwa kiigizo chema kwa wachezaji vijana nchini na kuungana na ndugu, jamaa na wadau wa klabu ya Simba kwa msiba huo. Ustaadh, alisema wadau wa ngumi hasa wanaopenda kuhudhuria michezo mbalimbali ya soka, wanajua namna gani Simba imepata pigo kwa kufiwa na kiungo huyo rais wa Rwanda ingawa mwenyeji wa DR Kongo. "TPBO tunaupa pole uongozi wa Simba na wadau wote wa klabu hiyo na soka kwa ujumla kwa kuondokewa na Patrick Mafisango, kama wadau tunaungana nao katika majonzi na kuwatakia moyo wa subira," Ustaadh alisema. Aliongeza kwa kuwataka wachezaji wenzake ambao anafahamu itawachukua muda mrefu kusahau kifo cha Mafisango kumuenzi mwenzao kwa kuiheshimu kazi yake aliyoifanya enzi za uhai wake kwa kuipa Simba mafanikio zaidi. "Najua ni vigumu wadau wa Simba kusahau msiba wa Mafisango, lakini TPBO tunaamini nnia pekee ni kumshukuru Mungu kwani kazi yake haina makosa na pia kumuenzi kwa kuipa Simba mafanikio zaidi," alisema. Patrick Mutesa Mafisango, aliyezikwa jana nyumbani kwao, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, alifariki usiku wa kuamkia Alhamisi baada ya kupata ajali ya gari akitokea Maisha Club 'kujirusha'. Kiungo huyo aliyewahi kung'ara na timu za TP Mazembe, APR, Azam kabla ya kutua Simba akiichezeapia timu ya taifa ya Rwanda 'Amavubi', amefariki akitokea kuisaidia Simba kutwaa taji la Ligi Kuu Tanzania Bara 2011-2012. Mwisho

Mil. 150 kudhamini tuzo za TASWA

KAMPUNI ya Bia ya Serengeti (SBL) jana imetangaza kudhamini tuzo za Mwanamichezo Bora wa Tanzania wa mwaka 2011 kwa Sh. milioni 150. Tuzo hizo zinaandaliwa na Chama cha Waandishi wa Habari za Michezo Tanzania (TASWA) na mwaka huu zitatolewa Juni 14 kwenye ukumbi wa Diamond Jubilee (VIP). Akizungumza jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi wa Mawasiliano na Uhusiano wa SBL, Teddy Mapunda, alisema kuwa lengo la kudhamini tuzo hizo ni kutaka kuona michezo na wanamichezo hapa nchini inakua na kujitangaza ndani na nje ya nchi. Alisema kampuni yake inaona fahari kuendelea kudhamini tuzo za TASWA ikiwa ni mwaka wa tatu mfululizo, hivyo mwaka huu wameongeza udhamini zaidi ili kuziboresha. Alisema tuzo hizo zitafanyika Juni 14 mwaka huu ukumbi wa Diamond Jubilee (VIP) Dar es Salaam na kwamba wana matumaini makubwa zitakuwa bora kuliko zilizopita. Mwenyekiti wa TASWA, Juma Pinto aliwashukuru Serengeti na kusema udhamini huo ni ishara ya namna kampuni hiyo inavyothamini wanamichezo nchini na kwamba umeongezeka kwa kiasi kikubwa kutoka Sh. milioni 80 ambazo walitoa mwaka jana. Pinto alisema kuwa milango bado iko wazi kwa kampuni nyingine kwa sababu bajeti nzima ya shughuli hiyo iliyopangwa ni Sh. milioni 370. Alisema kuwa mchakato wa kupata washindi wa tuzo hizo unasimamiwa na kamati maalumu iliyoteuliwa na TASWA na wanaamini inafanya kazi zake kwa uadilifu. Kwa miaka mitano iliyopita walioshinda Tuzo ya Mwanamichezo Bora wa TASWA walikuwa ni Samson Ramadhani (2006), Martin Sulle (2007), Mary Naali (2008), ambao wote ni wanariadha, wakati 2009 na 2010 alikuwa ni mcheza netiboli Mwanaidi Hassan. Mshindi wa mwaka jana, Mwanaid, ambaye alizawadiwa gari aina ya Toyota Cresta (GX 100), ndiye mfungaji aliyeisaidia timu ya taifa ya netiboli, Taifa Queens, kumaliza ikiwa ya pili kwenye mashindano ya mchezo huo ya Afrika yaliyofanyika nchini hivi karibuni.
Katibu Mkuu wa TASWA, Amir Mhando 'Mgosi'

Ngumi nazo zikumbukwe kama ilivyo kwa soka

INGAWA soka linatajwa kama mchezo unaopendwa na wengi duniani na hata nchini Tanzania, hata hivyo mchezo wa ngumi nao haupo nyuma kwa kuwa na mashabiki wengi. Kwa hapa nchini ukiondoa miaka ya hivi karibuni ambapo soka kurejesha heshima yake, mchezo wa ngumi ndio uliokuwa ukiongoza kwa kushabikiwa na watu wengi kiasi cha vijana wengi kuota kuwa mabondia. Hii ilitokana na mafanikio makubwa waliyopata mabondia wetu hasa wa ngumi za kulipwa kama akina Rashid Matumla, Rodger Mtagwa, Joseph Marwa, Mbwana Matumla na wengineo. Kabla ya mabondia hao kutamba katika ngumi za kulipwa kuna wakali wengine waliong'ara katika ngumi za ridhaa na kuiletea Tanzania medali katika mashindano mbalimbali ya kimataifa. Iwapo nitataka kuiandika orodha ya nyota walioiletea sifa katika ngumi enzi hizo, huenda nafasi isitoshe lakini baadhi yao ni akina Titus Simba, Habib Kinyogoli, Emmanuel Mlundwa, Bakar Seleman 'Match Maker' na wengine. Hata baada ya kuondoka kwa wakali hao na kuja kizazi cha akina Matumla, bado ngumi zimekuwa zikiendelea kutamba kwa kushuhudia mabondia kama Francis Cheka , Karama Nyilawila na wengine wakiitangaza vema Tanzania. Mataji ya kimataifa waliyotwaa katika mchezo huo likiwemo la hivi karibuni ya IBF-Afrika anaoushikilia Cheka, au ubingwa wa Dunia wa WBF ulioachwa kutetewa na Nyilawila ni mifano ya mafanikio machache ya mchezo wa ngumi. Hata hivyo pamoja na mafanikio hayo, bado mchezo huo haujapewa kipaumbele kama ilivyo kwa soka ambapo licha ya kusuasua na kutokuwa na tija ya kutosha linapewa hadhi ya kipekee nchini. Mchezo huo umekuwa na viwanja vya kutosha vya kuzalisha nyota wa baadae vikiwemo vya kimataifa ambavyo vimezidi kuwatia wazimu mashabiki wake, hali ikiwa ni tofauti kwa michezo mingine hususani ngumi. Mafanikio pekee ya kujivunia katika soka ni kufika fainali za Afrika za mwaka 1980 kwa timu ya taifa na klabu za Simba kutinga fainali za CAF-1993 na kufika nusu fainali za Klabu Bingwa Afrika mwaka 1974 na kucheza hatua ya makundi kwa Simba na Yanga mwaka 1998 na 2003. Pengine kwa mafanikio makubwa iliyopata mchezo wa ngumi kimataifa nilidhani kuna haja ya kuwepo uwanja au ukumbi maalum wa kufanyikia mashindano ya michezo huo kama soka ilivyo na viwanja vyake. Kitambo kidogo watu wa ngumi walikuwa na hakika wakienda ukumbi wa Arnatoglo au Relwe Gerezani, wangesuuza mioyo yao kwa kuwaangalia mabondia wakipasha misuli na wakati mwingine wakichuana mashindanoni. Mabondia wetu kwa sasa wamekuwa wakitangatanga na kutumia ama 'gym' zao zilizopo uchochoroni katika mazingira mabaya kukuzia vipaji vyao wakati wenzao wa soka wanatanua katika viwanja kadhaa vilivyopo nchini. Hata wanapokuwa na mipambano yao, utasikia kama sio Diamond Jubilee, ambao hata hivyo kwa sasa hautumiwi sana, basi ni PTA, Friends Corner au DDC Keko. Yaani hakuna ukumbi maalum wa kufanyikia mapambano ya ngumi kama ambavyo tumekuwa tukishuhudia katika mataifa mengine kama Marekani yenye kumbi za uhakika kama Madson Square Garden au MGM Grand. Ni vigumu kujilinganisha na Marekani, lakini nadhani kama kungekuwa na kumbi maalum au eneo maalum la kukutanishia mabondia ingesaidia kuwapoa uhakika mabondia na mapromota wao katika kukuza mchezo huo. Inawezekana Tanzania kuwa na kumbi za kisasa na zenye ubora zitakazotoa ushawishi kwa mapromota hata wa nje kuleta mapambano makubwa kucheza nchini kama uwanja wa Taifa ulivyozileta timu kubwa za soka nchini. Nani aliyekuwa akiota siku moja Brazil ingeweza kuja kucheza Tanzania? Lakini kwa kuwa na uwanja wa kisasa wenye uwezo wa kuchukua watazamaji 60,000 tuliwaona akina Robinho, Kaka na wengine kisha tukawaona akina Yaya Toure, Solomon Kalou, Didier Drogba na wengine wa Ivory Coast. Hivyo ni changamoto kwa serikali, vyama vinavyosimamia ngumi na wadau wote wa ngumi kupigania jambo hili la kuwepo kwa uwekezaji mzuri katika ngumi ili kuufanya mchezo huo uwe na hadhi kulingana na thamani yake. Nadhani kujengwa kwa kumbi au eneo litakalokuwa kama kitovu cha kuwakutanishia mabondia na la kufanyikia mapambano ya ngumi sio tu itawasaidia mabondia kufika mbali, lakini itawavuta watu wa nje kuja nchini. Kuja kwa kutasaidia kuitangaza Tanzania kimataifa katika sekta ya Utalii na hivyo kuliingizia taifa pato kubwa, kama ambavyo Brazil, New Zealand au Vancouver Whitecap ya Canada walivyokuja nchini kisoka. Mwisho

Twiga Stars yakiona cha moto kwa Banyana Banyana

WIKI moja tangu iangushiwe kipigo cha mabao 4-1 na madada wenzao wa Zimbabwe, kwa mara nyingine tena timu ya taifa ya soka ya wanawake ya Tanzania, Twiga Stars jana ilikumbana na kipigo kingine kizito toka kwa 'wababe' wa Afrika Kusini, Banyana Banyana. Katika mchezo huo wa kirafiki wa kimataifa, Twiga Stars ilicharazwa mabao 5-2 na wageni wao katika mechi zao za kujiandaa na michezo yao ya kufuzu fainali za Afrika. Twiga itacheza mechi yake ya kufuzu dhidi ya Ethiopia mjini Addis Ababa Mei 26, wakati Banyana itakuwa ugenini Zambia siku hiyo hiyo. Katika mechi ya jana iliyochezwa kwenye uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, Banyana walipata goli la kwanza katika dakika ya 23 kupitia kwa Patricia Modise aliyeuwahi mpira uliorudishwa nyuma na beki wa Twiga, Mwanaidi Tamba, na kufanya matokeo ya 1-0 hadi wakati wa mapumziko. Banyana Banyana iliongeza bao la pili kupitia tena kwa Modise tena aliyepachika wavuni kwa kichwa akiunganisha krosi ya Gabisile Hlumbane, Twiga ilizinduka na kujipatia bao la kwanza kupitia kwa Fatuma Bushiri aliifungia Twiga Stars kwa mkwaju wa penalti iliyotolewa na mwamuzi wa FIFA, Judith Gamba, baada ya Mwanahamis Omary 'Gaucho' kuangushwa na Janine van Wyk katika dakika ya 63. Wageni walipata goli la tatu katika dakika ya 73 kupitia kwa Sanah Mollo aliyeingia kuchukua nafasi ya Andiswe Mgloyi baada ya mabeki wa Twiga kujichanganya. Asha Rashid 'Mwalala' alifanya matokeo yawe 3-2 katika dakika ya 77 kufuatia pasi ya Fatuma Mustapha, lakini dakika mbili baadaye Banyana walipata goli la nne lililofungwa na Sanah tena. Na dakika nne kabla ya mechi kumalizika beki Janine van Wyk aliwafungia Banyana goli la tano kwa mpira wa 'fri-kiki' iliyokwenda moja kwa moja wavuni. Mara ya mwisho wakati timu hizo zilipokutana katika fainali za Mataifa ya Afrika nchini Afrika Kusuni, Twiga ililala 2-1. Kikosi cha Twiga Stars jana kilikuwa: Fatuma Omary, Fatuma Khatibu, Mwajuma Abdallah, Fatuma Bushiri, Mwanaidi Tamba, Everine Sekikobo, Esther Chabruma 'Lunyamila', Mwanahamisi Omary 'Gaucho', Asha Rashid 'Mwalala', Mwapewa Mtumwa na Fatuma Mustapha. Banyana: Roxanne Barker, Nodhano Vilakazi, Amanda Sister, Janine van Wyk, Zamandosi Cele, Amanda Dlamini, Mary Ntsweg, Patricia Modise, Gabisile Hlumbane, Rafilde Jane, Andiswe Mgloyi.

Licha ya bahati, lakini tulistahili taji-Cole

BEKI wa Chelsea, Ashley Cole amesisitiza kwamba uwezo wao, sio bahati, ndio kilichowapa ubingwa wa Ligi ya Klabu Bingwa Ulaya katika fainali usiku wa kuamkia jana. Cole, ambaye alifunga moja ya penalti za wakati wa kupigiana "matuta", alikiri kwamba Chelsea ilikuwa na bahati ilikuwa kwao katika fainali wakati Bayern Munich wakipotena zafasi nyingi nzuri za kushinda lakini mwisho wa mechi wao walikuwa washindi waliostahili. Aliiambia Sky Sports 1: "Maneno yamenikauka. Tulipaswa kuwa tumeshafungwa kutokana na nafasi nyingi walizitengeneza. "Tulikuwa na bahati, unahitaji bahati katika michuano hii kama unataka kuwa bingwa. Leo tulikuwa na bahati lakini pia tulistahili kushinda leo." Alipoulizwa hadhani kwamba bahati yao ilikuwa inaelekea kupotea baada ya Bayern kupata penalti dakika tano katika muda wa dakika 30 za nyongeza, mchezaji huyo wa kimataifa wa England aliongeza: "Hapana, kutokana na wachezaji tulionao tulifikiria, 'ok ni penalti lakini bado muda upo', na pale Petr alipookoa kiufundi yale ndiyo yunayoamini daima." Ubingwa ulimaanisha kwamba mara hii bahati ilikuwa upande wa Cole katika fainali ya Ligi ya Klabu Bingwa baada ya kupoteza mechi za fainali wakati akiichezea Arsenal mwaka 2006 na Chelsea 2008. Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 31, ambaye wakati akihamia katika klabu hiyo inayomilikiwa na tajiri alituhumiwa kuwa alifuata pesa na akapachikwa jina la "Cash-ley" Cole alisema: "Hii ndiyo sababu niko hapa." (Mail)

Nchunga 'angolewa' Yanga kwa mabavu

MWENYEKITI wa klabu ya Yanga, Llyod Nchunga 'ameondolewa' madarakani na kundi la wanachama zaidi ya 700 waliokutana jana kwenye mkutano wao wa dharura. Wanachama hao waliokutana kwenye makao makuu ya klabu hiyo mitaa ya Twiga na Jangwani, walikubaliana kumuondoa madarakani Nchunga, kwa madai ya kushindwa kuiongoza Yanga na pia kukiuka katiba kwa kutoitisha Mkutano Mkuu tangu alipochaguliwa mnamo mwaka juzi. Hata hivyo, maamuzi hayo ili yaweze kupata baraka kisheria yatapelewa katika ofisi za Msajili wa Klabu na Vyama vya Michezo wa Manispaa ya Ilala ambapo Yanga ndipo imesajiliwa. Akitangaza maamuzi ya wanachama hao baada ya kuwauliza na wao kuitikia kwa sauti ya juu kwamba ha
Picha za matukio za mkutano wa wanachama wa Yanga waliokutana jana klabuni kwao na kumuengua madarakani Nchunga. wamtaki Nchunga, Katibu wa Baraza la Wazee, Ibrahim Akilimali, alisema kuwa wamefikia maamuzi hayo kutokana na uongozi waliouchagua kushindwa kuiongoza Yanga na kuruhusu 'ufisadi' kufanyika ndani ya klabu yao. Akilimali alisema kuwa wamekosa imani na Kamati ya Utendaji ya klabu hiyo na baada ya kuona wameshindwa uongozi waliowapa na waliwataka waondoke ili kuepusha aibu ambayo hivi sasa inawakabili hasa kufuatia kupoteza ubingwa wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara na kufungwa magoli 5-0 na watani wao Simba. "Tulimshauri atupe timu ili tuweze kuiandaa vyema kumvaa mtani, alikubali, lakini baadaye akatuita sisi ni wahuni na majina mengi yasiyofaa, sasa kwa hili tunasema kuanzia sasa Nchunga na wenzake si viongozi tena wa Yanga," alisema Akilimali na kushangiliwa na wanachama ambao walikutana kwenye uwanja wao wa Kaunda huku kukiwa na amani. Alisema kuwa makundi yaliyoko ndani ya klabu hiyo ndiyo yamewafikisha walipo na wamekubaliana waungane na kumaliza tofauti zao ili Yanga iwe moja. Mkutano huo kwa kauli moja pia ulipitisha jina la Rais wao zamani, Abbas Tarimba, kuwa mshauri wa Kamati ya Usajili ambayo itaanza kazi leo na kuhakikisha wanasajili wachezaji wenye uwezo na hatimaye kutetea ubingwa wao wa Kombe la Kagame. Wanachama hao waliazimia kutowaruhusu viongozi waliobaki kwenye Kamati ya Utendaji kuingia kwenye jengo hilo kwa sababu hawana imani nao tena. Pia Akilimali alisema kuwa hivi sasa Yanga inapaswa kuitisha mkutano wa uchaguzi kufuatia wajumbe wa Kamati ya Utendaji kujiuzulu na kubakia watano. Yusuph Mzimba, alisimama kwenye mkutano huo na kuwataka wanachama wa Yanga wabadilike na kutorudia makosa waliyoyafanya kwenye uchaguzi uliopita kwa kumchagua kiongozi huyo. Mzimba alisema kwamba wasikubali tena kutumika na kuchaguliwa viongozi wasiojua maana ya utawala. "Yanga ibadilike, sio kama ilivyokuwa huko nyuma," alisema Mzimba na kupigiwa makofi. Alisema Nchunga ameshindwa kusoma alama za nyakati kwa kufahamu kwamba sasa wanachama hawamtaki na hivyo alitakiwa mapema kujiuzulu hatimaye kulinda heshima yake. Wanachama kuanzia 500 wanaweza kuomba mkutano mkuu na kutoa maamuzi lakini ikiwa chini ya mkutano ulioitishwa na uongozi. Hata hivyo, Nchunga alikaririwa jana akisema kwamba mkutano huo ni batili kwa sababu haukuwa mkutano wa wanachama kama wazee walivyoubadili 'kihuni', bali ulipaswa kuwa ni baina ya uongozi na wazee wa klabu. Hadi kufikia jana Kamati ya Utendaji ya Yanga imebakia na viongozi wanne huku nane wakiwa wameshajiuzulu hivyo waliobaki hawawezi kukutana na kutoa maamuzi yoyote. Wajumbe ambao kuanzia juzi waliwasilisha barua za kujiuzulu ni pamoja na Paschal Kihanga, Mzee Yusuph na Mohammed Bhinda, ambaye alipokelewa kwa shangwe kwenye mkutano huo wa wanachama na kuahidi leo ataweka wazi sababu zilizoepelekea yeye kufikia maamuzi hayo. Mzee Yusuph katika barua yake amesema kuwa amefikia maamuzi hayo baada ya kuona wameshindwa kusimamia na kuiendesha klabu hiyo katika misingi ya weledi, uwazi na uwajibikaji. Wajumbe wengine waliojiuzulu ni Ally Mayai, Sarah Ramadhani, Seif Ahmed 'Magari', Abdallah Binkleb na Davis Mosha, wakati Theonest Rutashoborwa alifariki na kuipunguzia nguvu kambi ya uongozi.

Sh50m awaits Epiq Bongo Star Search 2012

The winner of this year Epiq Bongo Star Search (EBSS) 2012 will pocket Shs 50 million, Zantel Vice President-Commercial, Ahmed Mokhles announced on Friday. Speaking during the launching ceremony held at the Serena Hotel, Mokhles said that they have decided to increase the winner prizes from Shs 40 million of last year aiming to make the search competitive and reward the winners. Mokhles said that they are proud to be associated with a successful Tanzanian talent competition focusing on discovering and promoting new musical talent among the youth. He said that through Epiq Nation related products aimed at the youth, they believe this year’s contest will be very energetic, full of color and pomp and many surprises. He explained that Zantel has incorporated a fashion aspect to this year’s competition whereas local and young designers will be given an opportunity to dress the contestants and will be assessed by professional fashion designers. “We all now BSS has changed lives of many young people and would like to see this continue under our firm stewardship and are creating additional segments to the show such as fashion to give opportunities to more youths and benefit from this one o a kind partnership,” added Mokhles. Benchmark Production Managing Director, Rita Paulsen elaborate her happiness during the launch “This is very unique day in Tanzania Music industry as we officially launch epiq bongo star search 2012 with avibrant new sponsor who has come up with a fresh look towards bongo star search.” Epiq Bongo Star search will continue with its usual format of having auditions from all major towns around the country an thisi year it will be extended to eight regional that are Zanzibar, Lindi, Mbeya, Mwanza, Arusha, Tanga, Dodoma and Dar es Salaam.