STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, April 20, 2012

Shija Mkina achekelea kuitungua Yanga


MFUNGAJI wa bao pekee lililoizamisha na kuitemesha Yanga ubingwa wa Ligi Kuu
Tanzania Bara, Shija Mkina wa Kagera Sugar, amedai kufarijika mno kuitungua timu hiyo.
Mshambuliaji huyo za zamani wa Bandari Mtwara na Simba, alisema ingawa ni kawaida
yake kufumania nyavu, lakini kuifunga Yanga ni faraja kubwa kwake kwa vile imeisaidia timu yake kujihakikishia nafasi ya kusalia kwenye ligi kuu msimu ujao.
Mkina, aliyejiondoa Simba kwa lazima baada ya kushindwa kupewa nafasi na aliyekuwa
kocha wa timu hiyo, Mganda Moses Basena ambaye hayupo kwa sasa katika klabu hiyo,
alisema bao hilo dhidi ya Yanga lilikuwa muhimu kwa timu yake ya Kagera.
"Nashukuru kwa kuweza kufungia timu yao bao muhimu lililotuhakikishia pointi tatu
zinazotufanya tusiwe na hofu ya kushuka daraja," alisema.
Mchezaji huyo, aliyewahi kuwa mfungaji bora alipokuwa na Bandari Mtwara, alisema ligi ya msimu huu ilikuwa ngumu kuliko misimu ya nyuma na ndio maana hadi sasa ni vigumu kujua timu inayoshuka daraja au itakayonyakua ubingwa licha ya Simba kupewa nafasi.
"Naamini ligi zote zingekuwa hivi, basi soka letu lingekuwa lipo juu na klabu zetu kufanya vema kwenye michuano ya kimataifa," alisema Mkina.
Kwa ushindi iliyopata ya Yanga, imeifanya Kagera Sugar kufikisha jumla 26 na ikisaliwa na mechi tatu dhidi ya Toto Afrika inayotarajiwa kucheza kesho mjini Bukoba, Coastal Union watakaoumana nao Aprili 30 mjini Tanga kisha kufunga msimu kwa kuvaana na Azam.

Mwisho

Polisi Moro yaifuata Mgambo Ligi Kuu, vita yabakia kwa Prisons Mbeya, Polisi Dar

WAKATI timu za soka za Mgambo ya Tanga na Polisi Moro zikiwa zimeshajihakikishia
kucheza Ligi Kuu Tanzania Bara msimu ujao, vita vya kuwania nafasi hiyo imesalia kwa
timu za Polisi Dar na Prisons ya Mbeya ambazo zitafunga dimba Jumatatu.
Polisi Moro jana ilijihakikishia nafasi ya kupanda daraja baada ya kuilaza Mbeya City mabao 2-0 na kufikisha pointi 17 na kuongoza msimamo wa fainali za Ligi Daraja la Kwanza zinazochezwa kwenye uwanja wa Jamhuri, mjini Morogoro.
Mgambo ilikuwa timu ya pili kupata nafasi hiyo katikati ya wiki baada ya kuilaza Transit Camp mabao 3-0 na kufikisha pointi 15 zinazowaweka nafasi ya pili ya msimamo wa ligi hiyo.
Nafasi ya tatu ya kupanda daraja imesaliwa kwa timu za Polisi Dar ambayo jana ilipata ushindi wa mabao 3-0 mbele ya JKt Mlale ya Songea na kufikisha pointi 10 ikishika nafasi ya nne nyuma ya Prisons ambayo yenye ina pointi 11.
Hata hivyo Prisons Mbeya ambayo ilitarajiwa kushuka dimbani leo jioni ndiyo yenye
nafasi kubwa ya kuchukua nafasi hiyo kutokana na pointi ilizonazo pia kuwa na kiporo
cha mechi moja ya ziada itakayochezwa Jumatatu dhidi ya Polisi Dar.
Iwapo timu hiyo itateleza kwa Rhino au kutoka sare itamaanisha kwamba mechi yao ya Jumatatu dhidi ya 'Vijana wa Kova' itakuwa ni kama fainali katika kuwania
nafasi hiyo moja ya kucheza ligi kuu msimu ujao.
Uongozi wa Polisi Dar kupitia kocha wake, Ngello Nyanjaba, alisema hawajakata tamaa
kupanda ligi kuu, licha ya kuwa na nafasi finyu nyuma ya Prisons ya Mbeya.
"Tunasubiri kuona inakuwaje hadi dakika za mwisho," alisema Nyanjaba.

Msimamo wa Fainali za 9 Bora kabla ya mechi za leo:

TIMU P W D L F A Pts
1. Mgambo Shooting 7 4 3 - 12 3 15
2. Polisi-Moro 7 5 2 - 14 4 17
3. Prisons-Mbeya 6 3 2 1 8 5 11
4. Polisi Dar 7 2 4 1 9 4 10
5. Mbeya City 7 2 2 3 7 8 8
6. Rhino Rangers 7 2 2 3 4 6 8
7. Mlale JKT 7 1 2 4 5 13 5
8. Polisi-Tabora 6 1 2 3 5 11 5
9. Transit Camp 6 - 1 5 2 12 1

Mwisho

Kocha Julio kuweka historia ya aina yake nchini


KOCHA maarufu nchini, Jamhuri Kihwelu 'Julio' anatarajiwa kuweka rekodi ya aina yake
nchini leo atakapokalia benchi za timu mbili tofauti katika pambano moja kati ya Coastal Union ya Tanga anayoifundisha na CDA-Dodoma anayojiunga nayo.
Mchezo huo maalum wa kirafiki kwa timu hizo utachezwa kwenye uwanja wa Jamhuri
mjini Dodoma, ambapo Coastal watautumia kumuaga na CDA kumkarisha kocha huyo
kwa ajili ya kuinoa kwa michuano ya Ligi ya TFF-Taifa inayotarajiwa kuanza hivi karibuni.
Julio aliyeisaidia Coastal kusalia Ligi Kuu Tanzania Bara baada ya awali kuchechemea, ameodai ameombwa na uongozi wa CDA, timu aliyowahi kuichezea miaka ya nyuma, jambo alilodai ameliafiki kwa moyo mmoja.
Akizungumza kutoka mjini Dodoma, Julio alisema amekubali kuachana na Coastal Union
ili aifundishe CDA klabu iliyomuibua katika maisha yake ya soka na katika mechi ya leo atakaa kwenye benchi za timu zote kwa dakika 45 za kila kipindi.
Kocha huyo mwenye maneno mengi, alisema dakika 45 za awali atakalia benchi la timu
yake ya sasa ya Coastal Union na katika kipindi cha pili atahamia katika benchi la CDA.
"Najiandaa kuachana na Coastal Union na kutua CDA baada ya kufuatwa na viongozi na
Jumamosi timu hizo mbili zitacheza mechi maalum ya kirafiki Coastal ikiniaga na CDA
kunikaribisha na kitakaa kwenye mabechi ya timu zote mbili kwa kila kipindi," alisema.
Julio alisema japokuwa imekuwa ngumu kwa makocha wenye majina kama yeye kukubali
kuzinoa timu za madaraja ya chini, lakini yeye anataka kuisaidia timu hiyo hadi ipande Ligi Kuu Tanzania Bara kuwahamasisha wengine kujitolea kusaidia timu za chini.
Kitendo cha kocha huyo kukaa katika benchi za timu mbili tofauti katika mchezo huo
itamfanya Julio aweke historia ya aina yake nchini, ingawa marehemu Syllersaid Mziray aliwahi kuzifundisha Simba na Yanga kwa wakati tofauti katika michuano ya Kombe la AICC mwishoni mwa miaka ya 1980, iliyokuwa ikifanyika mjini Arusha.

Mwisho

Thursday, April 19, 2012

Rage awatuliza wana Simba kuhusu Ngassa

WAKATI klabu ya soka ya Azam ikikanusha taarifa kwamba winga wao nyota, Mrisho Ngassa kuwa na mipango ya kutua Simba, Mwenyekiti wa klabu ya Simba, Ismail Aden Rage, amewatoa hofu wanachama wa klabu hiyo kwa kuwaeleza 'SUBIRINI TUONE'. Rage, alisema kama Ngassa atatua Msimbazi au la, litafahamika baada ya kumalizika kwa Ligi Kuu Tanzania Bara, ila kwa sasa ni mapema mno kulizungumzia hilo. "Kama wao wamekanusha kwamba huyo mchezaji atakuja Simba, basi subirini, ila kwa sasa ni vigumu kuanza kulisemea hilo wakati hatujui mkataba wa Ngassa na klabu yake ukoje," alisema Rage. Mwenyekiti huyo mwenye 'kismati' na klabu hiyo ya Simba, alisema kuanza kumzungumzia Ngassa kabla hawajawasiliana na uongozi wa Azam ni kwenda kinyume na sheria za FIFA, ila amesisitiza watu wasubiri kujua ukweli wa mambo. Juzi chombo kimoja cha habari kiliripoti taarifa kwamba Simba inakaribia kumnyakua Ngassa kwa ajili ya kuichezea timu hiyo kwenye michuano ya kimataifa, hiyo itafanyika iwapo Simba itafuzu hatua ya makundi ya Kombe la Shirikisho-Afrika. Hata hivyo Azam kupitia msemaji wake, Jaffer Idd Maganga, alisema hakuna kitu kama hicho na wanashangaa uzushi huo. "Hakuna kitu kama hicho, Simba haijawahi kutufuata kutueleza jambo hilo, wala Ngassa, pia mchezaji huyu bado ana mkataba na klabu hiyo ni ajabu kusikia kwamba anataka kwenda Simba, kivipi?" alihoji msemaji huyo. Hata hivyo suala la Ngassa kutua Simba lilitajwa tangu mchezaji huyo alipoihama Yanga na kutua Azam, ambapo ilielezwa ilikuwa janja ya kumvuta mchezaji huyo kutua Msimbazi na hasa alipokuwa akitafutiwa nafasi ya kucheza soka la kulipwa.
Mrisho Ngassa (kushoto) akiwajibika uwanjani na timu yake ya Azam. Hapa alikuwa akichuana na aliyekuwa mshambuliaji wa Simba, Mussa Hassani Mgosi ambaye kwa sasa anacheza soka la kulipwa DR Congo.

Villa Squad mambo bado magumu

LICHA ya kufurahia ushindi wa mabao 4-2 iliyopata timu yao dhidi ya Coastal Union ya Tanga, iliyofufua matumaini ya kusalia Ligi Kuu Tanzania msimu ujao, uongozi wa klabu ya Villa Squad umedai mambo bado magumu kwao na kuomba msaada zaidi. Katibu Mkuu wa Villa, Frank Mchaki, alisema bado wanahitaji msaada wa hali na mali ili kuisaidia timu yao katika maandalizi ya mechi zake zilizosalia ili kuweza kujihakikishia nafasi ya kusalia ligi kuu msimu ujao. Mchaki, alisema japo ushindi wao wa mwishoni mwa wiki umewaongezea tumaini jipya la kujinusuru kushuka daraja, lakini ni vigumu kujihakikishia jambo hilo kulingana na ukaribu wa pointi uliopo baina ya timu zilizopo chini katika msimamo wa ligi hiyo. "Tunashukuru kupata ushindi ambao umefufua matumaini yetu ya kusalia ligi kuu, ila bado tuna kazi ngumu na tunahitaji wadau wa soka watusaidie kwani kiuchumi tuna hali mbaya huku tukikabiliwa na mechi ngumu za kumalizia msimu," alisema Mchaki. Mchaki alisema anaamini timu yao ikisaidiwa kwa hali na mali itajiandaa vema kwa mechi tatu zilizosalia ambazo kama wakizishinda zote zitawafanya wasalie kwenye ligi hiyo. Villa, iliyorejea ligi kuu msimu huu ikitokea Ligi Daraja la Kwanza kwa ushindi iliyopata dhidi ya Coastal imewafanya wafikishe pointi 22 ikiwa nafasi ya 12 huku ikisaliwa mechi dhidi ya timu za African Lyon itakayocheza nao keshokutwa jijini Dar, kishaa kuvaana na JKT Oljoro kisha Ruvu Shooting watakaofunga nao dimba la msimu huu.

Kinyogoli aandaa tamasha la ngumi

NYOTA wa kimataifa wa zamani wa ngumi nchini, Habib Kinyogoli kupitia taasisi yake ya Kinyogoli Foundation, inatarajiwa kuendesha michuano maalum ya ngumi iitwayo 'Top Ten Boxing Festival-2012' litakaloanza rasmi Mei 4, jijini Dar es Salaam. Michuano hiyo itakayoshirikisha mabondia wa ngumi za aina zote yaani za ridhaa na kulipwa itafanyika kwenye ukumbi wa Panandi Panandi kwa ajili ya kuibua na kuendeleza vipaji vya mchezo huo kwa kusaka wakali 10 wa kila uzito katika ngumi hizo. Akizungumza na MICHARAZO, Msaidizi wa Kinyogoli, Rajabu Mhamila 'Super D' alisema mabondia na klabu zinazotaka kushiriki michuano hiyo wanatakiwa kujiandikisha mapema kabla ya kuanza kwake akidai itakuwa ikichezwa hadi kupatikana wakali hao. Super D, alisema ameamua kubuni 'ligi' hiyo kwa lengo la kuleta mabadiliko katika mchezo wa ngumi kwa kuibua vijana watakaoisaidia taifa kwa michuano ya kimataifa. Naye Kinyogoli maarufu kama Master, alisema ameamua kuanzisha michuano hiyo katika kuendeleza juhudi zake za kukuza ngumi ambazo zilikwama miaka ya nyuma. "Japo michuano hii itaonekana kama mipya, lakini ni kama wazo nililolibuni miaka 30 iliyopita niliposaidia kuibua vipaji vilivyokuja kutanza nchini kama akina Matumla na wengine," alisema Kinyogoli. Alisema, anaamini michuano hiyo itakapokamilika itasaidia kuibua nyota wapya na kuvihimiza vyama na wadau wa ngumi kujitokeza kwa wingi kwa ajili ya kushuhudia mchuano sambamba na kuwapiga tafu wale watakaofanya vema kwa faida ya taifa.
Kocha wa ngumi, Rajabu Mhamila 'Super D' msaidizi wa nyota wa zamani wa ngumi nchini, Habib Kinyogoli 'Master' wanaoandaa ligi maalum ya mchezo huo itakayoanza Mei 4.

Mashale awataka Maugo, Cheka

BAADA ya kutwaa ubingwa wa taifa wa TPBO, bondia Thomas Mashale amesema sasa yupo tayari kupigana ama Mada Maugo au Francis Cheka kwa nia ya kuanza kusaka mataji yanayotambuliwa kimataifa. Akizungumza na MICHARAZO, Mashale alisema kwa kuwa mabondia hao wawili ndio walio kwenye viwango vya hali ya juu kwa sasa katika uzani wa kati ni vema akapata fursa ya kupigana ili kuanza mbio zake za kusaka ubingwa wa Dunia. "Kwa sasa natamani kupigana na bondia yeyote kati ya Cheka au Maugo ambao wanatarajiwa kupigana hivi karibuni, lengo ni kutaka kuanza mchakato wa kusaka mataji ya kimataifa," alisema. Alisema kati ya mabondia hao haoni wa kumtisha hasa baada ya kupata uzoefu wa kutosha katika michezo yake mbalimbali aliyocheza tangu aingie kwenye mchezo huo. Mashale, alisema cha muhimu anachoombea kwa sasa ni kupatikana promota wa kumuandalia pambano kati ya mmoja wa mabondia hao ambao wanacheza wote kwenye uzani mmoja wa Middle. Kuhusu ushindi wake alioupata wiki iliyopita dhidi ya Seleman Said 'Galile' Mashale, alisema ulitokana na kufanya vema katika raundi saba za awali na kukiri kwamba mpinzani wake ni mzuri na alimpa usumbufu mkubwa. Alipoulizwa kama yupo tayari kurudiana na Galile, Mashale alisem yu radhi iwapo mpinzani wake huyo atakuwa hajaridhika na matokeo ya ushindi wake uliokuwa wa pointi baada ya kuonyeshana umwamba katika pambano la raundi 10.
Bondia Thomas Mashale 'Simba wa Teranga', akiwa na taji lake la TPBO, mara baada ya kumpiga kwa pointi Seleman Said Galile. Kwa sasa bondia huyo anamtaka kati ya Mada Maugo au Francis Cheka ili apigane nao.

Barcelona yaleteza darajani, yadungwa 1-0

Didier Drogba akishangilia bao lake la pekee lililoisaidia Chelsea kuizima Barcelona kwenye Ligi ya Mabingwa Ulaya mechi iliyochezwa usiku wa kuamkia leo.
BAO lililoifungwa na mshambuliaji wa kimataifa wa Ivory Coast, Didier Drogba dakika za lala salama kabla ya mapumziko ilitosha kuisaidia Chelsea kuizima Barcelona ya Hispania katika pambano la kwanza la nusu fainali baina yao lililochezwa Uingereza.
Drogba alifunga bao hilo pekee dakika ya pili ya dakika za majeruhi baada ya kutimu dakika 45 za kipindi cha kwanza kwenye Uwanja wa Stamford Bridge, London, England Licha ya Barcelona ambao ndio mabingwa watetezi wa Ligi ya Mabingwa Ulaya kwa sasa kucharuka katika kipindi cha pili, ilijikuta ikishindwa kurejesha bao hilo hadi pambano lilipomalizika.
Kwa ushindi huo, Chelsea sasa inahitaji sare yoyote kwenye mechi ya marudiano ugenini, Uwanja wa Camop Nou ili kutinga fainali, ambako itacheza na mshindi kati ya Bayern Munich ya Ujerumani na Real Madrid ya Hispania.
Mechi ya kwanza ya kwanza baina ya timu hizo mbili wenyeji Bayern Munich waliitungua Real Madrid mabao 2-1, hivyo Real inahitaji ushindi wa bao 1-0 kama inataka kutinga fainali.

Mgambo Shooting yatinga Ligi Kuu Tanzania Bara, Prisons, Polisi Moro zanusa

TIMU ya soka ya maafande wa Mgambo Shooting ya Tanga imekuwa timu ya kwanza kutinga Ligi Kuu Tanzania Bara baada ya jana kuisasambua Transit Campo ya Dar kwa mabao 3-0.
Mgambo inayomilikiwa na Jeshi la Kujenga Taifa, ilipata ushindi huo uliowaingiza Ligi Kuu ikiifuata Coastal Union kwenye pambano lililochezwa kwenye uwanja wa Jamhuri, Mjini Morogoro kunakofanyika fainali za 9 Bora ya Ligi Daraja la Kwanza.
Katika mchezo huo Mgambo ilipata mabao yake kupitia kwa washambuliaji wake, Juma Mwinyimvua aliyefunga mabao mawili katika dakika za 16 na 37 na Nassoro Gumbo aliyefunga kwenye muda wa nyongeza za mchezo huo.
Kwa ushindi huo Mgambo imefikisha jumla ya pointi 15 ambazo haziwezi kufikiwa na timu nyingine ukiondoa Polisi Moro ambao nao wanainyemelea nafasi ya kucheza ligi hiyo msimu ujao.
Katika pambano jingine lililochezwa jioni kwenye uwanja huo, mabingwa wa zamani wa Tanzania, Prisons-Mbeya ilinusa kufuzu ligi kuu msimu ujao baada ya kuicharaza Polisi-Tabora mabao 3-0
Mabao ya Prisons waliofikisha pointi 11 kwa ushindi huo wa jana, yalifungwa na John Mtai aliyefunga mawili na jingine kutumbukizwa kimiani na Peter Michael katika dakika ya nne ya mchezo huo uliochezeshwa vizuri na Shabaan Shata wa Kigoma.
Ligi hiyo inatarajiwa kuendelea tena mchana wa leo kwa mechi kati ya Polisi Moro dhidi ya Mbeya City kabla ya JKT Mlale ya Songea kuumana na Polisi Dar.

Msimamo kamili wa Ligi hiyo ya 9 Bora hadi sasa ni kama ifuatavyo;


MSIMAMO WA 9 BORA LIGI DARAJA LA KWANZA

P W D L F A Pts
1. Mgambo Shooting 7 4 3 - 12 3 15
2. Polisi-Moro 6 4 2 - 12 4 14
3. Prisons-Mbeya 6 3 2 1 8 5 11
4. Mbeya City 6 2 2 2 7 6 8
5. Rhino Rangers 7 2 2 3 4 6 8
6. Polisi Dar 6 1 4 1 6 4 7
7. Mlale JKT 6 1 2 3 5 10 5
8. Polisi-Tabora 6 1 2 3 5 11 5
9. Transit Camp 6 - 1 5 2 12 1

Mwisho

Yanga yatemeshwa taji, Simba kidogo kulibeba jumla




KIPIGO cha bao 1-0 ilichopewa na Kagera Sugar jana kwenye uwanja wa Kaitaba, umeifanya Yanga kulitema taji la ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara.
Yanga iliyokuwa watetezi wa taji hilo ilikumbana na kipigo hicho ikiwa ni cha pili ndani ya siku tatu, baada ya awali kufungwa mabao 3-2 na Toto Afrika jijini Mwanza na kuwafanya wasalie na pointi 43 na michezo mitatu ambayo hata ikishinda yote haiwezi kuzifikia pointi za watani zao, Simba wanaojiandaa kulitwaa taji hilo.
Bao lililoizamisha Yanga lilitumbukizwa wavuni na Shija Mkina na kukatisha ndoto za Yanga ambao walikuwa wakisubiri pointi zao walizopokwa na Kamati ya Mashindano ya TFF kutokana na rufaa waliyokata ambayo imetupiliwa mbali na Kamti ya Nidhamu na Usuluhishi ya Alfred Tibaigana.
Wakati Yanga ikitota Kagera na kuweka rekodi na kupoteza pointi sita katika Kanda ya Ziwa kwa mara ya kwanza, watani zao Simba jana walitakata uwanja wa Taifa baada ya kuinyoa JKT Ruvu mabao 3-0.
Ushindi uliifanya Simba ifuzu kucheza michuano ya CAF msimu ujao baada ya kujihakikishia kumaliza katika moja ya nafasi mbili za juu kutokana na kufikisha pointi 56 ambazo haziwezi kufikiwa na Yanga.
Azam yenye pointi 50 huku ikiwa na mechi moja mkononi, itaikaribisha Mtibwa Sugar kwenye Uwanja wa Chamazi Jumamosi.
Simba ilianza kuhesabu goli la kwanza katika dakika ya kwanza ya mchezo kupitia kwa kiungo Uhuru Selemani aliyefunga kwa kichwa akiunganisha krosi ya Mganda Emmanuel Okwi na kiungo kipenzi cha mashabiki wa Simba, Haruna Moshi 'Boban' akafunga moja ya mabao bora ya msimu wakati alipokimbia na mpira kutokea katikati ya uwanja na kupiga shuti lililomshinda kipa Amani Simba wa JKT katika dakika ya 17.
Kiungo wa timu ya taifa, Taifa Stars, Mwinyi Kazimoto alifunga goli la 'kideoni' katika dakika ya 64 na kuisogeza Simba jirani zaidi na ubingwa.
Matokeo mengine ya ligi hiyo kwa jana, Ruvu Shootingi ilishinda 1-0 dhidi ya Moro United, bao lililotumbukizwa wavuni na Saleh Kitala dakika ya 90, huku Toto wakiendeleza wimbi la ushindi kwa kuicharaza African Lyon mabao 2-0.
Nao watoto wa Julio, Coastal Union, ilizinduka baada ya kichapo cha aibu cha mabao 4-2 toka kwa Villa Squad kwa kuitandika Polisi Dodoma mabao 3-l.
Kipigo hicho kimezidi kuiweka pabaya Polisi Dodoma kwani sasa ni kudra za Mungu tu ndizo zinazoweza kuinusuru isishuke daraja kurejea Ligi Daraja la Kwanza.

TIBAIGANA AICHINJA YANGA



Kamati ya Nidhamu ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) iliyokutana jana (Aprili 17 mwaka huu) imetupa rufani ya Yanga iliyowasilishwa mbele yake kupinga uamuzi wa kupokwa pointi tatu kwa kumchezesha mchezaji asiyestahili.
Aprili 2 mwaka huu Kamati ya Ligi ya TFF iliipa Coastal Union ushindi wa pointi tatu na mabao matatu baada ya Yanga kumchezesha beki Nadir Haroub ‘Cannavaro’ kwenye mechi ya Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) kati ya timu hizo iliyofanyika Machi 31 mwaka huu wakati akiwa na adhabu ya kukosa mechi tatu.
Yanga katika rufani hiyo iliwasilisha sababu nane za kupinga kupokwa pointi hizo, kubwa zikiwa Cannavaro hakustahili kutumikia adhabu ya kukosa mechi tatu, si aliyempiga refa Israel Nkongo, ripoti za refa na kamishna wa mechi yao dhidi ya Azam zilionesha dalili ya njama (conspiracy) kwani zilifanana.
Pia Cannavaro alikuwa miongoni mwa wachezaji ambao adhabu zao zilisimamishwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Nidhamu, Kamishna mstaafu wa Polisi, Alfred Tibaigana.
Katika uamuzi wake, Kamati imesema adhabu ya Cannavaro ya kukosa mechi tatu kwa mujibu wa Kanuni ya 25(c) ya Ligi Kuu ya Vodacom ilitolewa na refa na si Kamati ya Ligi kama ambavyo inalalamikiwa na Yanga, na kanuni hiyo haikatiwi rufani.
Pia barua ambayo TFF iliiandikia Yanga kuhusu adhabu ya mchezaji huyo ilikuwa wazi kwani ilikariri kanuni ya 25(c), hivyo kitendo cha klabu hiyo kumtumia mchezaji huyo ulikuwa ni uzembe wa kutoheshimu kanuni. Kama Yanga haikufahamu vizuri kanuni hiyo ilikuwa na fursa ya kuiandikia TFF kwa mujibu wa Kanuni ya 25(f) ili kupata ufafanuzi kabla ya kuamua kumtumia mchezaji huyo.
Vilevile adhabu zilizokuwa zimesimamishwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Nidhamu ni zile ambazo zilikuwa zimetolewa na Kamati ya Ligi, na si zile zilizotolewa uwanjani na refa.
Kuhusu madai ya conspiracy kwa ripoti za kamishna wa mchezo huo na refa, Kamati imebaini kuwa hazifanani, na suala lililokuwa likibishaniwa (contentious issue) lilikuwa ni kunyang’anywa pointi tatu.
Pia Kamati ilikariri Ibara ya 50 ya Kanuni za Nidhamu za Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) kuwa mchezaji anayembughudhi refa kwa njia yoyote ile anastahili kufungiwa kwa angalau mechi sita.

Boniface Wambura
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)

Saturday, April 7, 2012

MAMIA WAFURIKA MSIBA WA STEVEN KANUMBA





MEYA wa Manispaa ya Kinondoni na Ilala, Yusuf Mwenda na Jerry Slaa ni miongoni
mwa viongozi waliojitokeza kwenye msiba wa nyota wa filamu nchini, Steven Kanumba aliyefariki juzi usiku nyumbani kwake baada ya kuanguka katika mzozo na mpenzi wake.
Aidha umati mkubwa ulijitokeza kwenye msiba wa msanii huu uliopo nyumbani kwake
Sinza Vatican, jana ulisababisha msongamano mkubwa kiasi cha kuziba barabara ya
Makanya na kuwalazimisha askari polisi kufanya kazi ya ziada kuweka mambo sawa.
MiCHARAZO lililokuwepo msibani hapo, liliwashuhudia mameya hao na viongozi wengine kama Katibu wa Kamati ya Uchumi na Fedha CCM-Taifa, Mwigulu Nchemba na Diwani wa Kata ya Sinza, Renatus Pamba wakiwa na nyuso za huzuni wakitoa pole zao.
Viongozi hao kila mmoja alikuwa akiwapa pole wasanii waliofanya kazi na Kanumba
pamoja na watu wengine kabla ya baadhi yao kuondoka na kuwaacha mamia ya watu
wakiwemo wasanii nyota wa filamu wakiendelea na msiba huo.
Kutokana na wingi wa watu waliojitokeza kwenye msiba huo, iliwalazimisha waratibu wa msiba huo, kuwahamishi waombelezaji hao kwenye ukumbi wa Vatican Hoteli, huku wakiwazuia wengine kuingia ndani na kuleta tafrani za hapa na pale.
Mratibu wa Bongo Movie, Steven Mengele 'Steve Nyerere' alisema waliamua kuhamishia watu hotelini hapo kutokana eneo la nyumba ya marehemu Kanumba kutotosha kwa wingi wa waombolezaji waliojitokeza waliosababisha msongamano mkubwa.
Msongamano huo wa waombelezaji ulisababisha hata magari yanayotumia barabara ya
Makanya kushindwa kupita vema na kuwapa kazi ya ziada askari polisi wa kawaida na
wale wa barabarani kuyaongoza magari hayo.
Wasanii mbalimbali walikielezea kifo cha Kanumba kama pengo litakalochukua muda
mrefu kuziba katika tasnia ya sanaa hasa uigizaji wa filamu ambayo marehemu aliifanya kwa muda mrefu wa maisha yake tangu akiwa shuleni.
Mayasa Mrisho anayefanya kazi nyingi na Kanumba, alisema mpaka sasa haamini kama
Kanumba kafariki kwa namna kifo chake kilivyokuwa cha ghafla.
'Siamini, kama ni kweli Kanumba kafa," alisema huku akilia. Aliongeza Kanumba
amefariki wakati wakitoka kumalizia kazi yao mpya iitwayo 'Mr Price', huku pia
wakijiandaa kuingiza sokoni filamu yao mpya iitwayo 'Ndoa Yangu'.
Wasanii wengine kama Patcho Mwamba, Rajabu Jumanne 'Chilli', Issa Kipemba, Fatuma Makongoro 'Bi Mwenda' walisema itawachukua muda mrefu kumsahau mwenzao ambaye alikuwa mtu wa watu, asiye na makuu licha ya umaarufu mkubwa aliokuwa nao.
Nalo Baraza la Sanaa la Taifa, kupitia Katibu Mkuu wake, Ghonce Materego, walitoa
salamu za rambirambi kutokana na kifo hicho cha Kanumba wakidai kimeshtua na
kuwaachia pengo kubwa katika fani ya sanaa nchini.
"BASATA inaungana na familia za wafiwa na wasanii wote nchini kwa maombolezo ya msiba huu mkubwa na wa kihistoria. Kufiwa na msanii huyu mahiri kwenye tasnia ya filamu ni pengo kubwa kwa familia, Sekta ya sanaa na Taifa kwa ujumla kutokana na
ukweli kuwa, aliweza kuutangaza utamaduni na sanaa yetu nje ya mipaka," sehemu ya
rambirambi hiyo ya Basata inasomeka hivyo.
Steven Charles Kanumba, aliyezaliwa Januari 8, 1984 huko Shinyanga, alifariki usiku wa kuamkia jana kwa kile kinachoelezwa alisukumwa na kuanguka sakafuni na aliyekuwa
mpenzi wake, Elizabeth Michael 'Lulu' ambaye kwa sasa anashikiliwa na jeshi la Polisi.
Msanii huyo, aliyesoma Shule ya Msingi Bugoyi na Shule za Sekondari Mwadui, Dar
Christian Seminary na Jitegemee kabla ya kuanza kutamba kwenye sanaa kupitia kundi la Sanaa alilojiunga nalo mwaka 2002 hadi 2006 alipojiengua na kucheza filamu mbalimbali.
Baadhi ya kazi zake ni 'She is My Sister', 'Dar to Lagos', 'Cross My Sin', 'The Director', 'Hero of the Church', Sikitiko Langu, Dangerous Desire, Dar to Lagos, Cross My Sin, Village Pastor, Family Tears, Unfortunutes Love, My Valentine, The Shock, Deception na kazi ya mwisho kuitoa sokoni ni 'Kijiji Chatambua Haki'.

mwisho

SIMBA YATAKATA AFRIKA, LICHA YA KIPIGO YAFUZU 16 BORA KOMBE LA SHIRIKISHO




ANGURUMAPO SIMBA MCHEZA NANI? HAKUNAGA! Ndivyo tunavyoweza kusema baada ya klabu ya soka ya Simba kupenya kwenye hatua ya 16 Bora ya KOmbe la Shirikisho Afrika, licha ya kipigo cha mabao 3-1 ilichopewa usiku wa kuamkia leo na Entente Sportive de Setif ya Algeria.
Ikicheza wachezaji 10, Simba iliweza kupigana hadi dakika za nyongeza kupata bao pekee la kufutia machozi lililokuwa na faida kubwa kwao, kuwavusha hatua hiyo wakiwaduwaza waarabu wasiamini kilichowakuta baada ya kuamini wamemng'oa mnyama.
Shujaa wa Simba katika pambano hilo lililochezeshwa na waamuzi kutoka Tunisia alikuwa ni Mganda, Emmanuel Okwi aliyefunga katrika dakika ya 92 na kuifanya timu yake isonge mbele kwa faida ya bao la ugenini kutokana na matokeo ya jumla kuwa mabao 3-3.
Simba katika pambano lao la awali lililochezwa kwenye uwanja wa Taifa, Machi 25, ilishinda mabao 2-0 na hivyo kwa sare hiyo wamevuka kwa matokeo ya kuwa mabao 4-3.
Beki wa kutumainiwa wa Simba Juma Said Nyosso alitolewa uwanjani mapema baada ya kulimwa kadi nyekundu kwa kuonyesha ubabe uwanjani dhidi ya mshambuliaji wa Setif.
Wenyeji walitumia mwanya wa kutolewa kwa Nyosso kupachika bao la kuongoza lililofungwa dakika ya 34 na Mohammed Aoudia na kurejea kipindi cha pili kwa kasi kwa kufunga bao jingine kupitia mshambuliaji huyo mkali.
Bao la tatu la Setif, iliyokuwa ikiyotawala vipindi vyote viwili, ingawa juhudi zao za kuvuna mabao mengi zilizimwa na kipa Juma Kaseka, lilifungwa katika dakika ya 52 kupitia kwa Mokhtar Benmoussa.
Baada ya kupata mabao hayo Setif ilirejea nyuma na kulinda bao wakiamini wameshamaliza kazi kabla ya Okwi kuwaduwaza baada ya kuwachambua mabeki wa timu hiyo kisha kufumua shuti kali la mbali lililomshinda nguvu kipa wa Setif na kutinga wavuni.
Kwa ushindi huo, Simba sasa itakutana na mshindi kati ya Ferroviário Maputo ya Msumbiji au Al Ahly Shendi ya Sudan ambazo zinatarajiwa kuumana kesho Jumapili, huku timu ya Sudan ikiwa na faida ya bao moja iliyopata katika mechi yao wiki mbili zilizopita ilipowafunga wenyeji wao bao 1-0.
Katika mchezo wa jana kikosi cha Simba kilichoaanza dhidi ya ES Setif kiliwakilishwa na Juma Kaseja, Shomari Kapombe, Amir Maftah/Said Nassoro 'Chollo' , Juma Nyoso, Kelvin Yondani, Patrick Mafisango, Salum Machaku, Mwinyi Kazimoto, Felix Sunzu, Haruna Moshi 'Boban' na Emmanuel Okwi.

PICHA ZA BAADHI YA KAZI YA NDOA YANGU, MOJA YA FILAMU ZA MWISHO ZA KANUMBA INAYOTARAJIWA KUINGIA SOKONI KARIBUNI





ZA LEO LEO

BREAKING NEWS: STEVEN KANUMBA 'THE GREAT' IS NO MORE




MUIGIZAJI nyota wa filamu nchini, Steven Kanumba, 28, amefariki dunia usiku wa kuamkia leo nyumbani kwake Sinza Vatican, jijini Dar es Salaam.
Kwa mujibu wa habari za kuaminika na kuthibitishwa na rafikie wa karibu, Patcho Mwamba, Kanumba alifariki nyumbani kwake baada ya kuanguka akitokea bafuni kutokana na kuteleza.
Chanzo hicho kinasema kwamba Kanumba alianguka baada ya kusukumwa na mpenzi wake (jina tunalo) aliyekuwa akizozana nae badaa ya kupishana kiswahili.
"Brother Kanumba kafariki usiku wa kuamkia leo na maiti yake kwa sasa ipo Mumhimbili, ikisubiri taratibu za mazishi, ni kama utani ila ndio hivyo. Alisukumwa na kuangukia kisogo na kufariki papo hapo," chanzo hicho kilisema.
Aliongeza kwa sasa walikuwa wakiwasiliana na mama yake ambaye inadaiwa yupo Bukoba pamoja na familia yake iliyopo Shinyanga kujua taratibu za mazishi yake.
Patcho Mwamba alipoulizwa juu ya kifo cha Kanumba, alithibitisha lakini hakuweza kuweka bayana chanzo zaidi ya kusisitiza kuwa alianguka sakafuni nyumbani kwake na kufariki akiwahishwa Muhimbili, ambako kwa sasa mwili wake umehifadhiwa.
Steven Charles Kanumba alizaliwa Januari 8, 1984 mkoani Shinyanga akiwa ni mmoja kati ya watoto wa nne wa mzee Charles Kanumba.
Alisoma Shule ya Msingi Bugoyi, huko huko Shinyanga kabla ya kuendelea na masomo ya Sekondari katika Shule ya Mwadui, kisha kuhamia Shule ya Dar Christian Seminary, alipohitimu kidato cha nne. Baadaer alijiunga na masomo ya juu ya Sekondari na kumaliza Kidato cha Sita katika Shule ya Jitegemee, ambapo tayari alishaanza kujishughulisha na sanaa kupitia kundi la Kaole Sanaa alilotamba nalo na michezo mbalimbali iliyokuwa ikionyesha kwenye kituo cha ITV.
Baadae aliamua kujiengua katika kundi hilo na kucheza filamu akishirikiana na wasanii wenzake, Blandina Chagula 'Johari' na Vincent Kigosi 'Ray'.
Hadi anafariki msanii huyo alikuwa ni Muigizaji, Mtunzi, Mtayarishaji na muongozaji, akimiliki kampuni ya Kanumba the Great Films ambayo ilikuwa ikizalisha filamu na kuibua wasanii wengi chipukizi.
Marehemu alikuwa hajaoa wala kuwa na mtoto. Mungu aiweke roho ya marehemu mahali pema.