STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Thursday, July 14, 2011

Banka yu tayari wa lolote Simba



KIUNGO nyota wa timu ya Simba na timu ya taifa, Taifa Stars, Mohammed Banka, amesema ingawa hajapata taarifa rasmi ya kutemwa ndani ya kikosi hicho, lakini yupo tayari kwa lolote mradi alipwe chake kwa kuvunjwa mkataba alionao na klabu hiyo.
Aidha amedai kusikitishwa na lawama anazotupiwa kwa kushindwa kung'ara kwenye pambano la fainali za Kombe la Kagame dhidi yao na Yanga, wakati ilifahamika kuwa ametoka majeruhi kitu ambacho hata kocha Moses Basena alikuwa akifahamu.
Akizungumza na MICHARAZO mapema leo, Banka alisema hana taarifa za kuachwa na Simba kama baadhi ya vyombo vya habari vilivyoripoti jana, lakini kama jambo hilo ni kweli hana jinsi zaidi ya kukubaliana na mapendekezo ya viongozi wake.
Banka alisema kitu cha msingi ni klabu ya Simba imlipe chake kwa kuvunja mkataba wao, ili akatafute maisha pengine, ingawa alisema amesikitishwa na kushutumiwa kwa kuwa miongoni mwa walioikosesha Simba taji la saba la michuano ya Kagame.
"Kwa kweli sijapewa taarifa yoyote rasmi zaidi ya kusoma kwenye vyomvo vya habari, lakini kama uongozi umeazimia hivyo, sitakuwa na jinsi zaidi ya kusubiri kulipwa changu kwa kuvunjwa mkataba nitafute mahali pa kwenda," alisema.
Aliongeza, kucheza kwake chini ya kiwango katika mechi ya Simba na Yanga katika fainali za Kagame ilitokana na kutoka kuwa majeruhi, kitu ambacho hata mwenyewe alishtuka alipoagizwa na kocha Basena kuingia dimbani.
"Kocha aliniambia kabla ya mechi atanichezesha kipindi cha pili ili kuangalia maendeleo yangu ya kupona majeraha, hivyo alivyoniambia niingie nilishangaa, lakini kama mchezaji ninayezingatia nidhamu sikuweza kumbishia, ila Simba wasinielewe vibaya," alisema Banka.
Kiungo huyo alisema anaamini mchango wake ndani ya Simba ni mkubwa kuliko lawama anazopewa sasa, lakini kwa kuwa soka ndivyo lilivyo anajiandaa kutafuta maisha mahali pengine kwa kuamini 'riziki' yake imeisha ndani ya klabu hiyo.
Banka, pamoja na Mussa Hassani Mgosi na Athumani Idd 'Chuji' walitajwa kuwa miongoni mwa waliopendekezwa kutemwa ndani ya Simba kwa ajili ya msimu ujao wa Ligi Kuu Tanzania Bara na michuano ya kimataifa kutokana na kuonyesha kiwango duni kwenye Kombe la Kagame, ambapo Simba ilifungwa na Yanga bao 1-0.

Mwisho

Bujibu kuchapana na Mtambo wa Gongo


WAKATI michuano ya Ligi ya Kick Boxing iliyotarajiwa kufanyika mwishoni mwa mwezi huu ikiahirishwa hadi Desemba, mabondia wakongwe wa ngumi za kulipwa nchini, Maneno Osward na Ernest Bujiku wanatarajiwa kupamba ulingoni kupigana.
Maneno Osward maarufu kama Mtambo wa Gongo atapigana na Bujiku katika moja ya mapambano ya ngumi yatakayoshindikiza pambano la Kick Boxing kati ya Amour Zungu wa Zanzibar dhidi ya Mchumia Tumbo litakalofanyika Julai 30 kwenye ukumbi wa DDC Keko, Dar es Salaam.
Kaseba alisema, mbalio na pambano la Osward na Bujiku siku hiyo pia mabondia wa kike, Jamhuri Said wa Tanzania atapimana ubavu na Rukia Kaselete wa Kenya katika pambano jingine la Kick Boxing.
Alisema michezo mingine itakayosindikiza mipambano hiyo ni kati ya Fadhila dhidi Demu wa Kisarawe, Dragon Kaizum atakayepigana na Faza Boy, Idd dhidi ya Dragon Boy, Lion Heart dhidi ya Begeje na michezo mingine ya ngumi za kulipwa.
Kaseba alisema michezo hiyo inafanyika ili kuwapa burudani wakazi wa Dar es Salaam ambao walikuwa wakijiandaa kushuhudia ligi ya Kick Boxing ambayo imeahirishwa hadi Desemba kwa ajili ya kufanya maandalizi ya kutosha.
"Tumeamua kuahirisha ligi ya Kick Boxing hadi Desemba kutoa muda kwa mabondia kujiandaa na kufanya katika kiwango cha kimataifa, hivyo ili kutowanyima raha wadau wa mchezo huo tumeandaa michezo kadhaa ya Kick Boxing na ngumi za kulipwa siku ya Julai 30 itakayofanyika kwenye ukumbi wa DDC Keko," alisema Kaseba.
Alisema Bujiku na Osward kila mmoja kwa sasa yupo katika maandalizi makali ya kuonyeshana umwamba wakikumbushia enzi zao wakitamba kwenye mchezo huo.

Mwisho

Waajiri wapigwa msasa kuishi na wafanyakazi wa majumbani



WAAJIRI wa wafanyakazi wa ndani watakiwa kutowabagua na kuwanyanyasa watumishi wao wa ndani na badala yake kuishi nao kwa wema kutokana na ukweli wao ni watu wa karibu na wasiri wakubwa wa familia zao.
Wito huo umetolewa kwenye semina ya siku moja iliyoandaliwa na Asasi ya kiraia ya KIWOHEDE kwa lengo la kujenga mauhusiano mema baina ya waajiri na watumishi wa kazi za ndani ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakichukuliwa kama vijakazi.
Mgeni rasmi wa semina hiyo, Sheikh Shughuli Sheikh, ambaye ni Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Malapa Kata ya Buguruni na Mwezeshaji wa semina hiyo Edda Kawala, walisema kuna umuhimu wa waajiri kuwaona wafanyakazi wa majumbani kama sehemu ya familia zao.
Sheikh, alisema kutokana na mchango na umuhimu wa wafanyakazi wa ndani ambao ni tegemeo la waajiri katika kusaidiwa kazi za nyumbani ni vema watumishi hao wakapewa heshima na kuthaminiwa kama wanafamilia.
"Wao ndio wanaowapikieni, kuwafulieni na kazi nyingine za ndani, hivyo ni wasiri na watu muhimu katika familia zenu hivyo ni vema kukaa nao kwa wema mkiwajali na kuwathamini tofauti na baadhi yenu mnavyowafanyia," alisema Sheikh.
Naye Mwezeshaji alisema lengo la semina hiyo ni kuona waajiri na wafanyakazi hao wa ndani wanakuwa na mauhisiano mema, pamoja na kila mmoja kuhakikisha wanakuwa na mikataba au makubaliano yanayolinda haki na hadhi ya kila mmoja.
Alisema KIWOHEDE, imebaini zipo baadhi ya nyumba au waajiri wamekuwa wakiwabagua watumishi wao na kuwanyima haki zao stahiki na kuchangia kuwepo kwa uhasama na kuifanya kazi hiyo kudharaulika mbele ya jamii.
Washiriki wa semina hiyo wengi wao wakiwa ni akinamama, walisema kuna mambo mengine hawakuwa wanayajua juu ya haki za msingi za watumishi hao na semina hiyo imewafungua macho na kuahidi kuwa 'mabalozi' mema warejeapo makwao.
Semina hiyo ilielekeza umri stahiki wa wafanyakazi wanaopaswa kuajiriwa kwa kazi za majumbani, haki za msingi stahiki za watumishi hao na namna ya uwajibikaji wa kila mmoja kati ya waajiri na wafanyakazi hao.

Mwisho

Tanzania yapongezwa kuridhia mkataba wa ILO


SERIKALI ya Tanzania imepongezwa kwa kuwa miongoni mwa nchi zilizopitisha Mkataba wa Kimataifa wa Kutambuliwa kwa Wafanyakazi wa Majumbani, iliuyopitishwa kwenye Mkutano wa 100 wa Shirika la Kazi Duniani (ILO).
Kadhalika Rais Jakaya Kikwete amepongezwa kwa hutuba aliyoisoma kwenye mkutano huo juu ya serikali ya Tanzania kuwatambua wafanyakazi hao kama watumishi halali wanaoostahiki hakio zote wa waajiriwa, akiombwa kuhakikisha utekezaji unafanyika.
Mratibu wa Shirika la Wafanyakazi wa Majumbani Kanda ya Afrika (IUF), Vick Kanyoka, akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam alieleza maazimio ya mkutano wa ILO uliofanyika mwezi uliopita mjini Geneva, Uswisi.
Kanyoka, alisema kitendo cha Tanzania kuwa miongoni mwa nchi zilizopigia kura ya kupitisha mkataba huo wa 189 wa kuwatambua wafanyakazi wa majumbani ni ushindi kwa wafanyakazi wote ambao kabla ya hapo walikuwa wakichukuliwa kama watumwa.
Aliongeza IUF, inaipongeza Tanzania na Rais Jakaya Kikwete aliyehutubia kwenye mkutano huo Juni 15 mwaka huu na kuiomba serikali hiyo itekeleze kwa vitendo mkataba huo ili wafanyakazi wa majumbani kupata haki na kuthaminiwa kama wafanyakazi wengine.
Alisema ingawa sheria ya kuwalinda na kuwatetea wafanyakazi majumbani ipo, lakin i utekelezaji wake umekuwa ni tatizo na ndio maana IUF inaiomba Tanzania kuhakikisha jambo hilo linapata ufanisi ili kuleta usawa miongoni mwa watumishi hao.
"IUF tunaipongeza Tanzania na Rais wake kwa kuridhika kupitishwa kwa mkataba wa 189 wa kutambulika kwa wafanyakazi wa majumbani, uliopitioshwa Juni 16 mwaka huu ambapo ulipitishwa kwa kura 396, huku 16 zikiukataa miongoni mwa mataifa yaliyoukataa likiwa ni Uingereza," alisema Kanyoka.
Mratibu huyo alisema ni kutekelezwa kwa vitendo kwa mkataba huo kutatoa fursa ya waajiri kuwathamini na kuwajali watumishi hao kwa kuingia nao mkataba na kuwalipa haki zao stahiki kma ilivyo kwa watumishi wengine.
Alisisitiza ni muhimu wafanyakazi hao kusaidia kufanikisha uitekelezaji huo kwa kuwa wa kwanza kuhakikisha wanaingia mikataba na makubalino na waajiri wao kabla ya kuanza kazi ili watakapofanyiwa kinyume iwe rahisi kutetewa na kupata haki zao.

Mwisho