STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Thursday, July 14, 2011

Banka yu tayari wa lolote Simba



KIUNGO nyota wa timu ya Simba na timu ya taifa, Taifa Stars, Mohammed Banka, amesema ingawa hajapata taarifa rasmi ya kutemwa ndani ya kikosi hicho, lakini yupo tayari kwa lolote mradi alipwe chake kwa kuvunjwa mkataba alionao na klabu hiyo.
Aidha amedai kusikitishwa na lawama anazotupiwa kwa kushindwa kung'ara kwenye pambano la fainali za Kombe la Kagame dhidi yao na Yanga, wakati ilifahamika kuwa ametoka majeruhi kitu ambacho hata kocha Moses Basena alikuwa akifahamu.
Akizungumza na MICHARAZO mapema leo, Banka alisema hana taarifa za kuachwa na Simba kama baadhi ya vyombo vya habari vilivyoripoti jana, lakini kama jambo hilo ni kweli hana jinsi zaidi ya kukubaliana na mapendekezo ya viongozi wake.
Banka alisema kitu cha msingi ni klabu ya Simba imlipe chake kwa kuvunja mkataba wao, ili akatafute maisha pengine, ingawa alisema amesikitishwa na kushutumiwa kwa kuwa miongoni mwa walioikosesha Simba taji la saba la michuano ya Kagame.
"Kwa kweli sijapewa taarifa yoyote rasmi zaidi ya kusoma kwenye vyomvo vya habari, lakini kama uongozi umeazimia hivyo, sitakuwa na jinsi zaidi ya kusubiri kulipwa changu kwa kuvunjwa mkataba nitafute mahali pa kwenda," alisema.
Aliongeza, kucheza kwake chini ya kiwango katika mechi ya Simba na Yanga katika fainali za Kagame ilitokana na kutoka kuwa majeruhi, kitu ambacho hata mwenyewe alishtuka alipoagizwa na kocha Basena kuingia dimbani.
"Kocha aliniambia kabla ya mechi atanichezesha kipindi cha pili ili kuangalia maendeleo yangu ya kupona majeraha, hivyo alivyoniambia niingie nilishangaa, lakini kama mchezaji ninayezingatia nidhamu sikuweza kumbishia, ila Simba wasinielewe vibaya," alisema Banka.
Kiungo huyo alisema anaamini mchango wake ndani ya Simba ni mkubwa kuliko lawama anazopewa sasa, lakini kwa kuwa soka ndivyo lilivyo anajiandaa kutafuta maisha mahali pengine kwa kuamini 'riziki' yake imeisha ndani ya klabu hiyo.
Banka, pamoja na Mussa Hassani Mgosi na Athumani Idd 'Chuji' walitajwa kuwa miongoni mwa waliopendekezwa kutemwa ndani ya Simba kwa ajili ya msimu ujao wa Ligi Kuu Tanzania Bara na michuano ya kimataifa kutokana na kuonyesha kiwango duni kwenye Kombe la Kagame, ambapo Simba ilifungwa na Yanga bao 1-0.

Mwisho

No comments:

Post a Comment