STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Thursday, December 25, 2014

Ruvu Shooting yaanza tambo kisha Betram Mwombeki

KLABU ya Ruvu Shooting imetamba kuwa imelamba dume kwa kumsajili mshambuliaji wa zamani wa Simba, Betram Mwombeki na kudai timu pinzania zijiandae kukabiliana naye kutokana na uwezo mkubwa aliouonyesha kwenye mechi yao dhidi ya Mwadui ya Shinyanga.
Msemaji wa Ruvu, Masau Bwire amesema kuwa kwa mara ya kwanza amemuona Mwombeki akiichezea Ruvu Shooting na kubaini kuwa ni mchezaji ambaye atawasaidia mno, baada ya kutoa pasi ya bao la kwanza na kufunga bao la pili timu hiyo ilipotoka sare ya mabao 2-2 na Mwadui kwenye uwanja wa Mabatini Mlandizi mkoani Pwani siku ya Jumatatu.
"Nashangaa kuna timu zilimuona hafai, huyu Mwombeki amecheza kwa kiwango cha hali ya juu, ametoa pasi ya bao la kwanza lililofungwa na Abdurahman Mussa na kutufungia bao la pili, kwa kweli huyu ameziba kabisa pengo la Elius Maguri," alisema Masau.
Amezitahadharisha timu zote zinazoshiriki Ligi Kuu kuwa zitakutana na moto wa Mombeki, kwani amerejea kwenye kiwango chake cha kawaida, akicheza kwa kutumia nguvu kama kawaida yake na kuachia mashuti makali.
Mshambuliaji huyo wa zamani wa Simba, alisajiliwa na Ruvu kwenye kipindi hiki cha dirisha dogo kwa ajili ya kuziba pengo la Maguri ambaye kwa sasa yuko Simba.
Mwombeki alivuma akiwa na Simba msimu uliopita chini ya kocha Abdallah Kibadeni, lakini hali ilikuwa ngumu kwake alipokuja kocha matata Zdravko Logarusic ambaye hakupendezwa na aina yake ya uchezaji, kiasi cha kumtupia virago.
Ruvu ambayo itaanza kibarua cha ngwe nyingine ya Ligi Kuu kwa kuumana na ndugu zao Ruvu Shooting siku ya Jumamosi, imewasajili pia wachezaji wengine akiwamo Yahya Tumbo nyota wa zamani wa Africans Lyon na Yanga.

Ukishangaa fedha za Tegeta Escrow utayaona ya Yanga Jangwani!

https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEiMKxD1F7u6O8EspppaCk5UUX9XveRzSV5K6ThUlsHL7YtSo6HErtvL3Tfy7BuEdDRN50QMWIPv20EXlb3DyuFDLPYtZ2imcLeQ7bmJcmXfFHr1w9EGT-DdwwUiDDjfA2ZdMj0-pKCw5zI/s1600/07.JPGWAKATI watanzania wakiendelea kuweweseka na jinamizi la wizi wa fedha za akaunti ya Tegeta Escrow, imefahamika 'wizi' kama huo umetokea ndani ya klabu ya Yanga kwa kudaiwa kutafunwa kiasi cha zaidi ya SH. Bilioni 2.
Tayari inadaiwa aliyekuwa Katibu Mkuu wa klabu hiyo, Benno Njovu na mwanadada mmoja aliyekuwa akihusika na Idara ya Fedha klabu hapo wameshafunguliwa mashtaka kwa tuhuma hizo.
Hata hivyo Jeshi la Polisi limesita kutoa taarifa juu ya uwapo wa taarifa za ubadhirifu wa fedha hizo kiasi cha Sh. bilioni mbili katika Klabu ya Yanga ya jijini hapa.
Taarifa za ubadhirifu huo zimeitikisa Yanga huku baadhi ya waliokuwa watendaji wa klabu hiyo kufikishwa kwenye vyombo vya usalama kwa tuhuma za kutafuna kifisadi kiasi hicho cha fedha hizo.

Katibu Mkuu mpya wa Yanga, DK. Jonas Tiboroha amethibitisha kubainika kwa ubadhilifu wa fedha ingawa hakuwa tayari kutaja kiasi kamili kilichobainika kuchotwa kijanja na baadhi ya wafanyakazi wanaodaiwa kuwa ni wale waliomaliza muda wao katika klabu hiyo hivi karibuni.
Baadhi ya wafanyakazi wa zamani wakiongozwa na aliyekuwa katibu mkuu wa klabu hiyo, Beno Njovu na aliyekuwa mhasibu Rose Msamila, wamedaiwa kufikishwa kwenye Ofisi za Makao Makuu ya Polisi (Central) mjini hapa jana kuhojiwa kuhusu ubadhirifu huo.
“Ni kweli kuna suala hilo, lakini siwezi kuliongelea zaidi ni kina nani hasa wanahusika na kiasi cha fedha kinachotajwa kwa sababu tayari suala hilo liko chini ya Jeshi la Polisi. Watakapomaliza uchunguzi wao, watatujuza na sisi (Yanga SC) tutaliweka wazi,” amesema Tiboroha.
Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova hakuwa tayari kulizungumzia suala hilo baada ya kutafutwa na mtandao huu mjini hapa leo akisema: “Muulize RPC Ilala.”
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kipolisi wa Ilala, Mary Nzuki amedai hana taarifa za kuhojiwa na Polisi kwa waliokuwa watendaji wa Yanga SC.
“Mimi nimefuatilia kwenye vituo vyetu mbalimbali lakini sijapewa taarifa kuhusu kuhojiwa kwa watu wa Yanga. Pengine suala hilo limefanywa na kitengo cha upelelezi, ngoja niwasiliane nao kupata ufafanuzi,” amesema kamanda huyo.
RPC huyo pia amekiri kuona picha mitandaoni zikiwaonesha baadhi ya waliokuwa viongozi wa Yanga SC wakiwa na Polisi.
“Waandishi wa habari wananiuliza sana kuhusu suala hilo, nimeona pia baadhi ya picha mitandaoni zikiwaonesha watendaji wa Yanga wakiwa na polisi lakini zijapata taarifa rasmi juu ya suala hilo,” amesema zaidi.
Baadaye jioni hii RPC huyo amesemaL “Tumeangalia kwenye mafaili yetu hatuna suala hilo Mkoa wa Ilala, labda kwa Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam (Ofisi ya Kova).”
Inadaiwa kuwa fedha zilitafunwa kijanja kupitia malipo ya kambi mjini Antalya, Uturuki, nauli za usafiri wa ndege wa baadhi ya nyota wa kigeni.
Mwishoni mwa wiki, Yanga ilimtangaza Tiboroha kuwa katibu mkuu wa klabu hiyo akichukua nafasi ya Njovu. Mtangazaji wa zamani wa televisheni za ITV na TBC, Jerry Muro aliteuliwa kuwa Mkuu wa Habari na Mawasiliano, Omari Kaya aliteuliwa kuwa mkuu wa Idara ya Sheria ya klabu hiyo wakati Baraka Deusdetit aliteuliwa kuwa Mkuu wa Idara ya Fedha.
Muda mfupi baada ya uteuzi huo kumegundulika kulikuwa na kile kinacoelezwa kama ubadhirifu miongoni mwa watangulizi katika utendaji wa klabu hiyo ya Jangwani.

Alex Song atemwa Cameroon kuelekea Afcon 2015

http://c.smimg.net/14/25/alex-song-cameroon.jpgKOCHA wa timu ya taifa ya Cameroon, Volke Finke ametaja kikosi cha awali cha wachezaji 27 kwa ajili ya michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika itakayofanyika huko Guinea ya Ikweta. 
Kocha huyo raia wa Ujerumani ameteua wachezaji wengi waliokuwemo katika mechi za kufuzu, lakini amemuacha kiungo Alex Song. 
Song hajaichezea Cameroon toka alipotolewa nje kwa kadi nyekundu katika kipindi cha mabao 4-0 walichopata kutoka kwa Croatia katika michuano ya Kombe la Dunia nchini Brazil. 
Kiwango kizuri alichokionyesha msimu huu akiwa kwa mkopo katika klabu ya West Ham United akitokea Barcelona, kilizua tetesi kuwa angeweza kuitwa katika timu ya taifa. 
Cameroon wanatarajiwa kuanza maandalizi nyumbani na watacheza mechi ya kirafiki na Congo Brazzaville Januari 7 kabla ya kusafiri kwenda Gabon kwa ajili ya kambi yao nyingine na kucheza mechi nyingine ya kirafiki dhidi ya Afrika Kusini Januari 11.
Simba hao Wasiofugika wataanza kibarua chao katika michuano hiyo ya AFCON kama ratiba inavyoonesha hapo chini
20 Jan: v Mali in Malabo
24 Jan: v Guinea in Malabo
28 Jan: v Ivory Coast in Malabo
Kikosi kamili  kilichoteuliwa kabla ya kuchujwa baadaye ni hiki hapa;
Makipa: Joseph Ondoua (Barcelona, Spain), Guy Ndy Assembe (Nancy, France), Pierre Sylvain Abogo (Tonnerre Yaoundé)
Walinzi: Cédric Djeugoue (Coton Sport), Jérôme Guihi Ata (Valenciennes, France), Nicolas Nkoulou (Marseille, France), Ambroise Oyongo Bitolo (New York Red Bulls, USA), Brice Nlate Ekongolo (Marseille, France), Franck Bagnack (Barcelona, Spain), Henri Bedimo (Lyon, France),
Viungo: Stéphane Mbia (Seville, Spain), Enoh Eyong (Standard Liège, Belgium), Raoul Cedric Loe (CA Osasuna, Spain), Edgard Salli (Academica de Coimbra. Portugal), Georges Mandjeck (Kayseri Erciyesspor, Turkey), Franck Kom (Etoile du Sahel, Tunisia), Patrick Ekeng (FC Cordoba, Spain)
Washambuliaji: Eric-Maxim Choupo-Moting (Schalke 04, Germany), Benjamin Moukandjo (Reims, France), Jacques Zoua (Kayseri Erciyesspor, Turkey), Vincent Aboubakar (Porto, Portugal), Léonard Kwekeu (Caykur Rizespor, Turkey), Clinton N'Jie (Lyon, France), Franck Etoundi (Zurich, Switzerland)

Gianfranco Zola ateuliwa kuwa kocha mkuu Cagliari

http://metrouk2.files.wordpress.com/2013/09/177634350.jpg
Gianfranco Zola aliyetuliwa kuinoa timu ya Cagliari
NYOTA wa zamani wa kimataifa wa Italia aliyewahi kutamba na timu mbalimbali duniani ikiwamo Chelsea, Gianfranco Zola ameteuliwea kuwa kocha mkuu wa klabu ya Serie A ya Cagliari.
Zola, 48 anachukua nafasi katika timu hiyo baada ya Zdenek Zeman, kutimuliwa mapema wiki hii baada ya Cagliari kuvurunda katika ligi ya Italia na kukamata nafasi ya tatu toka mkiani.
Kocha huyo wa zamani wa West Ham alyeimalizia soka lake katika klabu hiyo ya Cagliari, hakuwa akiinoa timu yoyote tangu alipoachana na Watford mwishoni mwa mwaka jana.
Cagliari imesema mshambuliaji huyo wa zamani wa Azzurri ataanza rasmi kibarua chake siku ya Jumapili kujaindaa na pambano lake la ligi ya Serie A dhidi ya Palermo Januari 6.
Zola, alitumia kipaji chake kuitumikia Chelsea kwa misimu saba kabla ya kugeukia ukocha kwa kuinoa West Ham iliyomfukuza mwaka 2010 kisha kujiunga na klabu ya Watford  aliyokuja kuachana nayo baada ya kujiuzulu katikati ya msimu wake wa pili wa kuinoa klabu hiyo.
Zola anatua Cagliari ikiwa katika hali mbaya kutokana na kushinda mechi mbili tu msimu huu wa ligi kati ya mechi 16 ilizocheza mpaka sasa.

Nyota England anusurika kufa ajalini

MWENYEKITI wa zamani wa Chama cha Wachezaji wa Kulipwa nchini Uingereza, PFA, Clarke Carlisle, amenusurika kifo katika ajali mbaya ya barabarani iliyomfanya awahishwe hospitalini kwa kutumia ndege.
Jumatatu iliyopita Polisi walithibitisha kwa mtu anayekadiriwa kuwa na umri wa miaka 35 alikuwa amejeruhiwa vibaya baada ya kugongwa na lori katika eneo la A64, karibu na Bishopthorpe York kiasi cha kuhitajika ndege ya dharura kumkimbiza hospitalini.
Hata hivyo vyombo vya habari vilivujisha kuwa aliyegongwa alikuwa ni Carlisle aliyesherehekea miaka 35 Oktoba mwaka huu na kwamba nyota huyo wa zamani wa England amelazwa Leeds General Infirmary kwa ajili ya matibabu zaidi.
Carlisle aliyewahi kuichezea timu mbalimbali zikiwamo za Ligi Kuu kama Burnley aliyeipandisha Ligi Kuu mwaka 2009, QPR, Blackpool, Watfor, Leeds United na Preston North End, alikumbwa na masaibu hayo asubuhi ya Jumatatu na klabu yake pamoja na vyombo kadhaa vya habari nchini Uingereza vimekuwa vikimtumia na kuandika ujumbe wa kumtakia kila la heri ili apone haraka.
staafu kucheza soka mwishoni mwa msimu wa mwaka  akiwa anaichezea Northampton Town.
Mlinzi huyo wa zamani aliyewahi kuichezea timu ya taifa ya vijana ya Uingereza u21 alitangaza kutundika daluga zake mwishoni mwa msimu uliopita akiwa anaichezea timu ya Northampton Town.
Katika hatua nyingine mke wa mchezaji huyo mstaafu ameishukuru klabu ya Burnley kuonyesha kujali kwa kutangaza kusimama kwa dakika moja kumuombea mumewe apate nafuu.
"Clarke na mimi daima siku zote mioyo yetu ipo Bunrley," Gemma Carlisle aliandika kwenye Twitter.

Kivumbi Ligi Kuu ya VPL kuanza kutimka tena kesho

Simba
Kagera Sugar
Ndanda Fc

Mtibwa Sugar
BAADA ya mapumziko ya karibu miezi miwili, vumbi la Ligi Kuu Tanzania Bara inatarajiwa kuanza kutimka tena kuanzia kesho kwa pambano moja litakalochezwa kwenye uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam kwa kuzikutanisha Simba na Kagera Sugar.
Simba ambayo imelitumia vyema dirisha dogo la usajili kwa kufanya usajili wa baadhi ya nyota kuimarisha kikosi chao itaivaa Kagera ikitokea Zanzibar ilipokuwa imeweka kambi yao tangu Jumapili iliyopita.
Mabingwa hao wa zamani katika dirisha dogo imewaongeza kikosini, nyota kutoka Uganda, Dan Sserunkuma na mdogo wake, Simon Sserunkuma na beki Juuko Mursheed sambamba na beki wa pembeni kutoka Mtibwa Sugar, Hassan Kessy.
Timu hiyo ambayo katika mechi saba zilizopita iliambulia ushindi mmoja tu dhidi ya Ruvu Shooting ikiwa ni baada ya miezi nane ya kucheza bila kushinda tangu msimu uliopita itakuwa na kazi nguvu mbele ya Kagera ambayo katika dirisha dogo la usajili haikusajili mchezaji yeyote na rekodi yake mbele ya Simba kila wanapokutana jijini Dar es Salaam inawabeba.
Kwa misimu miwili mfululizo timu hiyo imekuwa ikiiwekea nguvu Simba kwenye uwanja wa Taifa, jambo linalotarajiwa kutokea hata katika mchezo huo kutokana na maandalizi iliyofanya timu hiyo chini ya kocha kutoka Uganda Jackson Mayanja.
Katika msimu wa 2012-2013 timu hizo zilitoshana nguvu ya kufungana mabao 2-2 na msimu wa mwaka jana matokeo yaliishia kwa sare ya 1-1 na kuibua vurugu kubwa kutoka kwa mashabiki wa Simba waliokuwa hawajafurahishwa na bao la kusawazisha la wapinzani wao.
Katika mechi hiyo ya kesho, Simba wanaivaa Kagera wakiwa wametoka kupata ushindi katika mechi ya Nani Mtani Jembe dhidi ya Yanga na huku ile dhana kwamba kundi la wanachama maarufu kama Ukawa walikuwa wakiisababisha timu kupata sare mfululizo haipo tena.
Katika msimamo wa sasa Simba wanakamata nafasi ya saba wakiwa na pointi 9 wakati wapinzani wao wapo nafasi ya tano wakijikusanyia pointi 10 baada ya kila mmoja kucheza mechi saba.
Ligi hiyo itaendelea pia mwishoni mwa wiki kwa michezo sita tofauti, Jumamosi timu za Mtibwa Sugar na Stand United ziaonyeshana kazi kwenye uwanja wa Manungu, mjini Morogoro, Prisons-Mbeya itaikaribisha Coastal Union mjini Mbeya na  'ndugu' JKT Ruvu na Ruvu Shooting zitakwaruzana uwanja wa Chamazi, huku Jumapili Mbeya City na Ndanda Fc zitakwaruzana uwanja wa Sokoine-Mbeya, Polisi Moro kuialika Mgambo JKT kwenye uwanja wa Jamhuri-Morogoro na wawakilishi wa Tanzania kwenye michuano ya kimataifa Yanga na  Azam zitaonyeshana ubabe kwenye uwanja wa Taifa.
Mabingwa watetezi wataivaa Yanga wanaouguza majeraha ya kipigo cha mabao 2-0 cha mechi ya 'bonanza' ya Nani Mtani jembe toka kwa watani zao Simba, wakiwa wanatokea Uganda walipoenda kuweka kambi ya siku 10.