STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, February 25, 2011

NYota wa Simba waikamia Mtibwa Sugar J'pili

BAADHI ya nyota wa timu ya Simba, wametamba kuwa wataisambaratisha Mtibwa Sugar watakaoumana nao siku ya Jumapili.
Mabingwa hao watetezi wataikaribisha Mtibwa kwenye uwanja wa Uhuru, jijini Dar es Salaam katika pambano la mfululizo wa michuano ya Ligi Kuu Tanzania Bara.
Katika mechi yao ya awali iliyochezwa mjini Morogoro na kughubikwa na kashfa ya rushwa, Simba iliisambaratisha Mtibwa kwa bao 1-0.
Pamoja na kutambua ugumu wa pambano hilo, ambalo Mtibwa wameshanadi kutaka kulipiza kisasi na kujiweka kwenye nafasi nzuri katika msimamo wa ligi hiyo, wachezaji wa Simba wamedai hawatishiki kwa kuamini watashinda.
Juma Jabu 'JJ' beki wa kushoto wa mabingwa hao watetezi, alisema anaamini mechi ya kesho itakuwa na matokeo mazuri kwao kutokana na kiu yao ya kutaka kutetea tena taji lao.
"Hatuna shaka Mtibwa tutawasambatarisha, ili tuweze kutimiza lengo letu la kutetea taji, hivyo wanasimba wasiwe na hofu," alisema Jabu.
Jabu, alisema wanataka kushinda mechi hiyo ili kujiweka vizuri kabla ya kuvaana na watani zao, Yanga Machi 5 kisha kwenda kuvaana na TP Mazembe kwenye mechi ya kwanza ya Ligi ya Mabingwa Afrika.
Naye kiungo mshambuliaji, Rashid Gumbo alijinasibu hana hofu na mechi hiyo ya kesho wala ile ya watani zao, Yanga.
Gumbo, alisema hawawezi kurudia makosa waliyofanya kwenye pambano lao na Toto Afrika ambapo walilazimishwa sare ya 2-2 na hivyo kuitahadharisha Mtibwa ikae chonjo kwa kipigo.
"Wasitarajie mteremko, hatufanyi makosa kama ya Mwanza, tulipolazimishwa sare na Toto," alisema Gumbo mmoja wa wafungaji vinara wa klabu hiyo.
Kama Simba itaifunga Mtibwa ni wazi itarejea kileleni tena ikiiengua Azam, lakini itaombea pia watani zao watakaoshuka dimbani Jumatatu wafanye vibaya ili wasiporomoshwe kwenye msimamo kabla ya kukutana Machi 5.

Mwisho

Mwaisabula aungana na OLaba kumsikitia Kado

KOCHA wa zamani wa klabu ya Yanga, Kennedy Mwaisabula, ameungana na kocha wa Mtibwa Sugar, Tom Olaba kuilalamikia kadi nyekundu aliyopewa kipa Shaaban Kado, siku chache kabla ya kuvaana na timu ya Simba.
Kado, anayeichezea pia timu ya taifa, Taifa Stars, alionyeshwa kadi hiyo katika mechi baina ya timu yake na Toto Afrika na kumfanya alikose pambano la kesho dhidi yao na Simba litakalochezwa kwenye uwanja wa Uhuru, jijini Dar.
Mwaisabula maarufu kama 'Mzazi' alisema kitendo cha Kado kulikosa pambano la kesho limepunguza ladha kutokana na ukweli kipa huyo ndiye mhimili wa Mtibwa Sugar na hivyo kuipungizia nguvu timu yake.
Kocha huyo aliyewahi kuzinoa timu kadhaa ikiwemo Bandari-Mtwara, Cargo, Twiga Sports, Villa Squad na TMK United, alisema kwa jinsi mazingira ya kadi hiyo ilivyotolewa huko Mwanza anahisi kama kuna 'mchezo mchafu'.
Alisema japo hana hakika, lakini huenda kadi hiyo imetolewa kwa nia ya kuidhofisha Mtibwa katika mechi yao ya kesho, kitu alichodai mambo kama hayo yanachangia kuporomosha kiwango cha soka la Tanzania.
"Nadhani ifikie wakati mambo kama haya ya ujanja ujanja kwa nia ya kuzibeba timu kubwa zikaachwa ili soka lisonge mbele, nimesikitishwa na kadi ya Kado kwa vile imepunguza msisimko kwa pambano lao na Simba," alisema.
Kauli ya Mwaisabula imekuja siku chache, tangu kocha wa Mtibwa, Mkenya Tom Olaba kulalamikia kadi hiyo iliyotolewa na mwamuzi Judith Gamba, akidai imeinyong'onyesha timu yake kwa ajili ya pambano hilo dhidi ya Simba.
Kado alipewa kadi na mwamuzi huyo baada ya kuilalamikia penati iliyopewa wenyeji wao, Toto Afrika ambapo pambano lilishia kwa Mtibwa kushinda 2-1.

Mabondia kuzipiga kuwachangia wahanga wa mabomu


MABONDIA mbalimbali kutoka mikoa tofauti wanatarajiwa kupigana katika michuano maalum kwa nia ya kusaka fedha za kuwasaidia wahanga wa milipuko ya mabomu ya Gongo la Mboto, jijini Dar es Salaam.
Michuano hiyo itakayochezwa sehemu nne tofauti ndani ya mikoa ya Dar, Pwani na Morogoro, imeratibiwa na kampuni ya Funiko Inc, chini ya uratibu wa mkurugenzi wake, Rowland Raphael Chulu 'Chen Lee Master'.
Chulu alisema michezo ya kwanza itafanyika kwenye ukumbi wa Hugho Tower Pub, Kigogo-Mburahati Machi 6, ambapo yeye atapigana na K kutoka Tanga pamoja na kusindikizwa na mapambano mengine ya utangulizi.
Aliwataja mabondia wengine watakaopigana siku hiyo ni Deus Tengwa atakayepigana na Kitonge wa Arusha, Abbas dhidi ya Abuu, Rahim Cobra na Abdul, Masoud Fighter dhidi ya Mrisho Mwana, Husseni Magali na Idd Rashid na Said Omary atapigana na Jembe wa Majembe.
"Pambano la pili litafanyika Machi 13 eneo la Bunju kwenye ukumbi wa Proud Tanzania, ambapo nitarudiana na K, na wiki inayofuata tutakuwa Bagamoyo kwenye ukumbi wa Police Mass ambapo nitachapana na Juma wa huko huko," alisema.
Alisema onyesho la tatu litachezwa kwenye ukumbi wa Makuti-Pub, Ifakara mkoani Morogoro kwa kuumana na Charles wa huko wakisindikizwa na michezo mingine ya utangulizi.
Chulu, aliyewahi kung'ara kwenye Kick Boxing kabla ya kutumbukia kwenye utayarishaji wa filamu nchini, alisema fedha zote zitakazopatikana kwenye maonyesho ya michezo hiyo zitapelekwa kwa wahanga.
Tangu tukio la milipuko ya mabomu litokee wiki mbili zilizopita watu mbalimbali wamekuwa wakitolea kuwasaidia wahanga, ambapo kesho kwenye uwanja wa Uhuru wasanii wa Bongofleva na wale wa filamu wataumana kusaka fedha za kuwasaoidia wahanga hao wa Gongo la Mboto.

Mwisho