STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Wednesday, September 29, 2010

Mtakuwa wa kwanza kutupongeza kwa ubingwa-Adebayor

MSHAMBULIAJI nyota wa timu ya Azam, John Bocco 'Adebayor' amesema pamoja na kwamba hajaonyesha makeke yake kwenye msimu huu wa Ligi Kuu Tanzania Bara, bado anatumaini ya kunyakua tuzo ya Mfungaji Bora.
Aidha nyota huyo amekiri kufanya vibaya kwa timu yao katika baadhi ya mechi zake kumewaweka mahali pabaya, lakini anaamini mwisho wa siku wanaoiponda Azam watakuwa wa kwanza kuwapongeza kwa taji la ubingwa.
Akizungumza na Micharazo, Bocco, alisema ingawa amechwa na washambuliaji Jerry Tegete na Mussa Mgosi wenye mabao zaidi yake, bado anaamini ataibuka kinara wa mabao.
Bocco alisema mabao mawili aliyoyapata kupitia mechi mbili ni dalili za wazi kasi yake haijapungua, ila kilichotokea ni hali ya kawaida ya soka lenye ushindani kama ilivyo msimu huu nchini.
"Sina hofu ya kiatu cha dhahabu, kwani najiona nipo vema kutokana na ukweli nimecheza mechi mbili na nina mabao mawili, wakati wenzangu wamecheza mechi kibao wamenipita mabao mawili tu," alisema Bocco.
Kuhusu kuboronga kwa timu yake nyota huyo anayeichezea pia timu ya taifa, alisema ni wameyumba, lakini hiyo haina maana ndoto yao ya kutwaa ubingwa ndio imeyeyuka kwa sababu mechi za ligi hiyo bado zipo nyingi.
"Wanaotucheka sasa ndio watakaokuwa wa kwanza kutupongeza, naamini tutakaa vema na kufanya vizuri katika mechi zetu zijazo kwa vile tuna kikosi kizuri kinachocheza kitimu haswa," alisema Bocco.
Timu hiyo iliyoshika nafasi ya tatu msimu uliopita hivi karibuni iliyumba katika mechi zake tatu baada ya kufungwa na Simba, Kagera Sugara na Toto Afrika kabla ya kuzinduka mwishoni mwa wiki kwa kuilaza African Lyon.
Kikosi cha timu hiyo kimesheheni nyota kama Mrisho Ngassa, Bocco, Kally Ongala, Patrick Mafisango, Peter Ssenyonjo, Jabir Aziz na wengineo.

Mwisho

Mgossi hana hofu ya kiatu cha dhahabu

NYOYA wa Simba na mpachika mabao bora msimu uliopita, Mussa Mgosi amesema kasi ndogo ya ufungaji mabao aliyoanza nayo kwenye Ligi Kuu msimu huu, haina maana kwamba makali yake ya kuzifuma nyavu yamekwisha.
Msimu uliopita, Mgosi alitwaa kiatu cha dhahabu baada ya kuibuka mfungaji bora na kumshinda aliyekuwa akichuana naye kwa karibu Mrisho Ngassa aliyekuwa akiichezea Yanga kabla ya msimu huu kujiunga na Azam FC.
Mgosi aliyeifunga Yanga mara mbili msimu uliopita, amesema hana sababu ya kuwa na hofu katika kupachika mabao kwani ndio kwanza ligi iko hatua ya awali.
Mgosi ameongeza pamoja na Jerry Tegete kurejesha mbio zake za ufungaji kama ilivyokuwa msimu, hana huwezo wa kuifikia kasi yake itakayoibuka tena msimu huu.
"Ligi ndio kwanza imeanza, sioni sababu ya wapenzi na mashabiki wa Simba kuwa na hofu kiatu cha dhahabu nitakitwaa tena na taji la ubingwa litaenda Msimbazi mwishoni mwa msimu huu," alisema.
Kuhusu pambano lao lijalo dhidi ya Yanga, Mgosi alisema kama ilivyokuwa msimu uliopita pia safari hii kajiandaa kuwazamisha watani zao ili kulinda heshima yao ambayo ilitibuliwa kwenye mechi ya ngao ya hisani ambapo Simba walilazwa mikwaju ya penati 3-1.
"Sitaki kuanza kusema sana, tusubiri Oktoba 16 itafika na utaona kitu gani nitakachoifanyia timu yangu dhidi ya Yanga," alisema.
Wakati ligi ikiingia mapumzikoni kupisha pambano la kuwania kufuzu fainali za Afrika za mwaka 2012, kati ya Tanzania na Morocco, Jerry Tegete ndiye aliyekuwa kiongoza kwa ufungaji magoli akipachika mabao manne dhidi ya matatu ya Mgosi.
Hata hivyo Mgosi alikuwa na nafasi ya kumpita Tegete kwani timu yao ilikuwa ikiumana na Mtibwa Sugar dimba la Jamhuri Morogoro, wakati tukiingia mitamboni.

AIBU! Ulimboka anaswa akihonga Mtibwa



WINGA wa zamani wa Simba na timu ya taifa ya soka, Ulimboka Mwakingwe, alikamatwa na polisi na kulazwa korokoroni juzi kwa tuhuma za kumhonga fedha kipa wa Mtibwa, Shaaban Kado ili aachie magoli wakati Mtibwa itakapocheza dhidi ya Simba katika mechi yao ya Ligi Kuu ya Tanzania Bara kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro leo jioni.
Ulimboka alinaswa na kisha kutupwa mbaroni katika kituo cha polisi Mtibwa, ikiwa ni muda mfupi baada ya kunaswa kwenye eneo la kambi ya Mtibwa iliyopo Manungu, Turiani Morogoro, akidaiwa kumhonga Kado kiasi cha fedha kinachotajwa kuwa ni Sh. 400,000 ili aiachie Simba katika mechi yao.
Habari zilizoifikia Micharazo jana, zilisema kuwa Ulimboka, winga aliyeng’ara Simba kwa misimu kadhaa kabla ya kuomba apumzike msimu huu, alinaswa kirahisi kufuatia kile kinachodaiwa kuwa ni mtego uliowekwa mapema dhidi yake.
Chanzo kingine kilidai kwamba alikamatwa majira ya saa 2:30 usiku na kupata kashkash za kupewa kipigo baada ya kukutwa na Kado kwenye kota za Mtibwa, na kudaiwa vilevile kwamba alikutwa na fedha zote zinazodaiwa kuwa za hongo.
Alipoulizwa, Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Morogoro, Thobias Andengenye, alithibitisha juu ya kukamatwa kwa Ulimboka kambini kwa timu ya Mtibwa na kwamba kilichomkamatisha ni hizo tuhuma za kumhonga Kado.
Alisema kuwa polisi walimshikilia katika kituo chao cha Mtibwa hadi jana asubuhi kabla ya kumuachia kwa dhamana.
"Ni kweli… taarifa za kukamatwa kwa mchezaji huyo (Ulimboka) ninazo, ila sina uhakika kama alipigwa. Nilichoambiwa ni kwamba alinaswa na fedha na kufikishwa kituoni na watu wa Mtibwa Sugar ambapo alihojiwa, akafunguliwa kesi na kisha kuachiwa asubuhi hii (jana)," alisema Kamanda Andengenye.
Kamanda huyo alisema kuwa pamoja na kuachiwa kwake (Ulimboka), bado jeshi lao linaendelea na upelelezi zaidi kuhusiana na tukio hilo.
Awali, kocha msaidizi wa Mtibwa, kipa wa zamani wa Simba, Patrick Mwangata, alikiri pia kutokea kwa tukio hilo kambini kwao, lakini hakutaka kuzungumza zaidi kwavile yeye si msemaji rasmi na kwamba, suala hilo liko mikononi mwa polisi.
Micharazo haikumpata Ulimboka ili aelezee sakata hilo na sababu za kuhusishwa na Simba wakati akiwa ameshaachana nao na kubaki kuwa mchezaji mstaafu wa ‘Wekundu wa Msimbazi’.
Baadhi ya viongozi wa Simba hawakupatikana pia kupitia simu zao za mikononi, ingawa Afisa Habari wa klabu hiyo, Clifford Ndimbo, alipatikana awali na kuomba apigiwe baada ya dakika kumi, jambo ambalo halikufanikiwa kwani alipopigiwa tena baada ya muda huo kwa zaidi ya mara mbili, simu yake haikuwa ikipatikana.
Wakati Simba na Mtibwa zikishuka dimbani leo, Idda Mushi anaripoti kutoka Morogoro kuwa African Lyon walilazimisha sare ya 2-2 dhidi ya Kagera Sugar katika mechi yao ya ligi iliyofanyika kwenye Uwanja wa Jamhuri.
Kagera walipata goli la utangulizi katika dakika ya 43 kupitia kwa Gaudence Mwaikimba na Lyon wakasawazisha katika dakika ya 54 kwa penati iliyopigwa na Adam Kingwande kufuatia kipa Amani Simba kumdaka miguu Idrisa Rashid na kutolewa kwa kadi nyekundu.
Huku wakiwa 10 uwanjani, Kagera walipata goli la pili katika dakika ya 66 kupitia kwa Sunday Hinju kabla Kingwande tena kuisawazishia Lyon kwa goli la dakika ya 88.

Thursday, September 23, 2010

Vicky Kamata aimwagia sifa hospitali ya Geita


UONGOZI pamoja na watumishi wa hospitali ya mkoa wa Geita, wamemwagiwa pongezi kutokana na ubora wa huduma zao kwa wagonjwa hospitalini hapo.
Pongezi hizo zimetolewa na mshindi wa kura za maoni za Ubunge wa Viti Maalum Mkoa wa Geita, Vicky Kamata, alipozungumza na Micharazo kwa njia ya simu toka mjini humo.
Kamata ambaye alilazwa kwenye hospitali hiyo kumuugua mwanae mwenye umri wa miaka minne, alisema huduma wapewazo wagonjwa kwenye hospitali hiyo ni ya kupongezwa.
Alisema tofauti na siku za nyuma huduma zinazotolewa na madaktari na wauguzi wa hospitali hiyo ni za kuvutia na kuonyesha kuboreshwa kwa huduma na kuumwagia sifa uongozi na watendaji hao.
Kamata, ambaye pia ni mwanamuziki wa kizazi kipya, alisema hatoi pongezi hizo kwa kuwa alihudumiwa vema kwa wasifu wake, bali ukweli alioushuhudia kwa wagonjwa wengine ndani ya hospitali hiyo ambao baadhi walisifia pia.
"Kwenye ukweli lazima lisemwe, huduma katika hospitali ya Geita ni ya kuridhisha na inayoonyesha mabadiliko makubwa na ninaupongeza uongozi na watumishi kwa ujumla kwa husuma hizo," alisema.
Alisema mwanae aliyelazwa kwa siku nne kutokana na kusumbuliwa na malaria kali tayari ameshatoka na anaendelea vema.
Kuhusu matarajio ya uchaguzi mkuu, Kamata alisema anaamini CCM itashinda kwa kishindo katika uchaguzi ujao kutokana na kutekeleza ilani ya uchaguzi ya mwaka 2005 kwa ufanisi wakiwapelekea maendeleo wananchi.
"Japokuwa wapinzani safari hii wanaonyesha kucharuka, lakini bado ushindi wa CCM ni kwa kishindo na kuwaomba wananchi wajitokeze kwa wingi siku ya kupiga kura na kuelekeza kura zao kwa wagombea wa CCM kuanzia Urais, Ubunge na Udiwani kwa nchi nzima," alisema Kamata.

Mwisho

Friday, September 17, 2010

Super Nyamwela na safari yake kimuziki







KUJITUMA kwake na kiu kubwa ya mafanikio aliyokuwa nayo wakati akichipukia kwenye sanaa ndio silaha kubwa ya mafanikio ya dansa, Super Nyamwela, mmoja wa madansa wakongwe waliodumu katika fani hiyo kwa muda mrefu nchini.
Nyamwela ambaye majina yake kamili ni Hassani Mussa Mohammed, alisema juhudi za mazoezi na kujituma bila kuchoka ndivyo vilivyomfikisha alipo, akimiliki kundi lake binafsi la sanaa pamoja na kuendesha miradi kadhaa ya maduka mbali magari na nyumba ya kuishi.
Nyamwela aliyerejea nchini hivi karibuni akitokea nchi kadhaa za kiafrika kwa ajili ya 'shoo' za kundi lake binafsi, anasema katu hawezi kuidharau sanaa hiyo kwa kuwa imemfanya awe mtu katika watu tofauti na mtazamo wa watu wengi juu ya muziki na sanaa kwa ujumla.
"Leo hii kama sio sanaa hii ya kunengua, pengine nisingefika huko Namibia, Liberia, Afrika Kusini, Botswana na kwingineko kama ilivyokuwa miezi 11 ya ziara yangu katika nchi hizo acha zile ninazoambatana na bendi yangu ya African Stars 'Twanga Pepeta," alisema.
Dansa huyo aliyeanza fani hiyo tangu akiwa kinda, hajutii kwake kushindwa kuendelea na masomo ya sekondari kwa kuwa hakuna anachokikosa kwa sasa, ingawa mipango yake ni kujiendeleza pale alipoishia.
Akiwa amejinyakulia mataji mbalimbali ya mashindano ya disko nchini likiwemo lile la Mkoa wa Dar es Salaam, alisema safari yake ilianzia alipomaliza elimu ya msingi alipojitosa jumla kwenye fani hiyo aliyokuwa huku akiendelea na 'kitabu'.
Baadae aliungana na wasanii wenzake kadhaa kuunda kundi la Top Family lililotamba pale 'Kwa Macheni' kabla ya kwenda kuasisi kundi la Billbums ambalo lilisheheni wasanii wakali waliokuja kunyakuliwa na bendi ya African Stars.
Tangu awe Twanga Papeta, Nyamwela hajawahi kuhama hata mara moja licha ya kuwepo kwa majaribio kadhaa ya kutaka kumng'oa ASET bila ya mafanikio.
"Sidhani kama nitaondoka Twanga kirahisi, labda kama nitaenda kwenye bendi yangu binafsi ambayo naipigia mahesabu kuja kuunda siku za usoni wakati mambo yangu yamekaa vema, lakini si kwenda bendi zingine za hapa nchini," alisema.
Mkali huyo ambaye amejitumbukiza katika uimbaji na upigaji tumba na dramu, alisema kwa sasa akili zake zote ni kuhakikisha anaiboresha kampuni yake binafsi ya SN Stars Entertainment, ili iendeshwe kisasa na kujitanua nje ya Dar es Salaam.
Nyamwela aliyemaliza kuikarabati nyumba yake iliyopo Mbezi Beach ambayo iliunguzwa kwa moto na watu aliodai 'maadui' zake, alisema mbali na kuiboresha kampuni yake pia malengo yake ni kugeukia kazi ya kurapu na kufyatua filamu izungumziayo maisha yake.
Alisema filamu hiyo itafahamika kwa jina la My Talent ambayo itaanza kurekodiwa mara baada ya kumalizika kwa mfungo wa Ramadhani ikienda sambamba na maandalizi ya albamu yake mpya ya tatu ambayo imeshakilishika wimbo mmoja wa Tumechete.
Albamu yake ya kwanza iliyouza sana ilifahamika kwa jina la Master of the Tample na ile ya pili ni Afrika Kilomondo aliyoiingiza sokoni hivi karibuni ikiwa na nyimbo sita alzioshirikiana na waimbaji mbalimbali akiwemo Ally Choki, Richard Maalifa na Juma Nature.
Kuhusu matukio ambayo hataondoka akilini mwake hadi anaingia kaburini, Nyamwela alisema ni kuunguliwa kwa nyumba yake na kumpoteza mzazi mwenzie, marehemu Halima White.
"Aisee hili la kuunguliwa nyumba na lile la kumpoteza mzazi mwenzangu, marehemu Halima White, ni vigumu kuyasahau," alisema.
Aliongeza, amefarijika baada ya kumpata mwandani wake mpya Upendo Merere ambaye anatarajia kuuona nae hivi karibuni mipango yake ikienda vema, ili waweze kuwalea watoto watatu alionao.
Dansa huyo asiyependa majungu na uvivu kazini alisema atakuwa mchoyo wa fadhila kama hatamshukuru Mkurugenzi wa ASET Asha Baraka na uongozi na wasanii wote wa bendi ya Twanga Pepeta kwa kushirikiana naye kwa hali na mali.
"Siwezi kumsahau Da Asha Baraka kwa jinsi nilivyokaa naye tangu alipotuchukua toka Billbums hadi leo hii, pia uongozi mzima wa Twanga Pepeta, wasanii na vyombo vya habari vinavyonipa sapoti katika tangu nikiwa kinda katika sanaa hadi leo hii,"
Aliwaasa wenzake kujituma kama yeye na kutokubali kukata tamaa ili waweze kufanikiwa na kubwa ni kuipenda kazi zao na kujithamini wenyewe wakijilinda na ugonjwa wa Ukimwi.
Mkali huyo aliyezaliwa karibu miaka 30 iliyopita huko Zanzibar, alisema kutojidhamini kwa ujumla ndiko kunakopelekea wasanii wengine kutumbukia kwenye maambukizo ya ugonjwa huo.

Mwisho

Jane Misso kuzindua albamu yake Diamond Jumapili







MSANII nyota wa muziki wa Injili nchini, Jane Misso kesho anatarajia kuzindua albamu yake mpya na ya pili ya 'Uinuliwe' akisindikizwa na wasanii mbalimbali wa miondoko hiyo wa ndani na nje ya nchi.
Uzinduzi wa albamu hiyo utakaoenda sambamba na kuachiwa hadharani video yake, umepangwa kufanyika mchana wa kesho kwenye ukumbi wa Diamond Jubilee, jijini Dar es Salaam.
Akizungumza na Micharazo, Misso, ambaye ni mchungaji na mwalimu aliyewahi kufanya kazi nchini Uganda kabla ya kujikita kwenye miondoko hiyo na kuachia albamu yake ya kwanza ya 'Umoyo', alisema wasanii karibu wote watakaomsindikiza kesho wameshawasili jijini Dar es Salaam.
Misso aliwataja wasanii waliotua kwa ajili ya kumsindikiza katika uzinduzi wake ni pamoja na Mcongo, David Esengo, Peace Mhulu kutoka Kenya watakoshirikiana na nyota wa Kitanzania wa muziki huo na kwaya mbalimbali kumpambia onyesho lake.
Mwanamama huyo aliwataja wasanii wa Injili wa Tanzania watakaompiga tafu kesho ni Christina Shusho, Upendo Nkone, Martha Mwaipaja, Steve Wambura na Joseph Nyuki.
"Kwaya zitakazonisinidkiza ni pamoja na Joy Bring'res, The Whispers Band, AIC Chang'ombe na kwaya ya Watoto Yatima kutoka Dodoma inayoongozwa na mlemavu wa ngozi, Timotheo Maginga," alisema Misso.
Misso alisema albamu hiyo ina nyimbo sita na baadhi yake zinahamasisha wananchi juu ya ushiriki wao katika Uchaguzi Mkuu wa Taifa wa Urais, Ubunge na Udiwani unaotarajiwa kufanyika Oktoba 31.
Nyimbo zilizoibeba albamu hiyo ni 'Pokea Sifa', 'Motema', 'Nyosha Mkono Wako', 'Uinuliwe', 'Unaweza Yote' na 'Mimi Najua Neno Moja'.

Friday, September 10, 2010

Chagueni watu kwa sifa zao sio vyama-Sheikh Mapeyo

WAUMINI wa dini ya Kiislam na Watanzania kwa ujumla wameaswa kuchagua viongozi katika uchaguzi mkuu ujao bila kujali aina ya vyama vyao ilimradi ni watu wenye uchungu, uadilifu na dhamira ya kweli ya kuwakomboa.
Aidha waumini na watanzania wamehimiza kuhakikisha wanashiriki kwa wingi siku ya kupiga kura na kujichagulia viongozi wawatakao badala ya kusubiri kuchaguliwa kisha waje kulalama mambo yatakapokuwa yakienda kombo.
Wito huo umetolewa na Imamu wa Msikiti wa Mwenge Islamic Center, Sheikh Shaaban Mapeyo alipokuwa wakiwahutubia waumini baada ya swala ya Eid iliyoswaliwa msikini hapo, jijini Dar es Salaam.
Sheikh Mapeyo ambaye ni mgombea wa kiti cha Ubunge Jimbo la Kawe kupitia Chama cha Wananchi, CUF, alisema waumini wa Kiislam na wananchi kwa ujumla wasihadaiwe na propaganda za kuchagua viongozi kwa kuangalia chama bali wasifu wa mgombea kwa nia ya kujiletea maendeleo.
Alisema kuendelea kuchagua wagombea kwa kuzingatia chama ndio ambayo yamefanya Tanzania kuendelea kudumaa kwa muda mrefu kwa kuwa wapo baadhi ya wagombea hawana sifa za uongozi lakini wamechaguliwa kupitia vyama vyao.
"Waislam wakati tukizingatia 'darasa' tulilolipata kipindi cha Ramadhani ni vema tukajipanga kwa ajili ya uchaguzi mkuu ujao, tusiupuuze na muhimu ni kuhakikisha tunachagua watu wenye sifa na sio kuangalia chama," alisema.
Aliongeza kwa kuwataka waumini nao na watanzania kwa ujumla kushiriki kwa wingi kwenye uchaguzi huo kwa kujitokeza kupiga kura ili kuhakikisha wanajichagulia viongozi na makini watakaowaletea maendeleo ya maeneo yao.
"Bila kujali jinsia jitokezeni kwa wingi kushiriki kupiga kura Oktoba 31, puuzeni propaganda zinazosambazwa na baadhi ya watu kwamba kushiriki uchaguzi ni haramu, mtajiletea maendeleo vipi kama hampigi kura?" Alihoji.
Sheikh Mapeyo alisema mambo mengi hapa nchini yamekuwa yakienda kombo kwa sababu wananchi wengi wamekuwa sio makini katika kushiriki uchaguzi mkuu ambayo ndio silaha ya kujiletea maendeleo ya kweli.
Uchaguzi Mkuu wa kuchagua madiwani, wabunge na Urais utafanyika Oktoba 31 na kwa sasa wagombea wanaendelea na kampeni zao.

Mwisho

Monday, September 6, 2010

Mpeni kura Mkullo, namuamini mno-Dk KIkwete






RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye pia ni mgombea wa nafasi hiyo kwa tiketi ya CCM, Dk Jakaya Kikwete, amewaomba wakazi wa Jimbo la Kilosa, kumpa tena ubunge mgombea wa chama hicho na Waziri wa Fedha, Mustafa Mkullo kwa madai anamuamini.
Aidha mgombea huyo aliwaomba wapiga kura wa majimbo mengine yaliyopo wilayani Kilosa kuhakikisha wanaipa kura CCM kupitia viti vya ubunge na udiwani ili kumrahisishia kazi ya kuongoza nchi kwa mara ya pili mfululizo.
Akiwahutubia wakazi wa wilaya ya Kilosa kwenye mkutano wake wa kampeni uliofanyika kwenye uwanja uliopo njia panda Ilonga na Kimamba, Rais Kikwete alisema angependa kuona wakazi wa Kilosa wakimpa tena ubunge waziri Mkullo kwa vile ni mmoja wa mawaziri anayewaamini.
"Naombeni mnichagulie tena Mkullo kuwa Mbunge wa Kilosa kwa kuwa kumuamini kwangu ndiko kulikonifanya nimpe dhamana ya kuwa Waziri wa Fedha na Uchumi," alisema Dk Kikwete.
Dk Kikwete alisema, chini ya Mkullo Kilosa imeweza kupiga hatua kubwa ya maendeleo kwa serikali yake kushawishika kuidhinisha fedha za miradi ya maendeleo katika sekta za elimu, afya, maji, umeme na barabara.
Pia mgombea huyo wa Urais, aliwaomba wakazi wa wilaya hiyo kuwachagua pia wagombea wengine wa majimbo ya Gairo na Mikumi pamoja na wale wa udiwani wa kata zilizopo wilayani humo ili kumrahisishia kazi katika kuwaletea maendeleo katika maeneo yao.
Naye Mkullo, alipopewa nafasi ya kuwasalimia wapiga kura wake, aliwaomba wampigie kura na kumpa ubunge kwa mara ya pili ili aweze kukamilisha baadhi ya ahadi zake alizowatolea kwenye uchaguzi uliopita wa mwaka 2005.
"Sina cha ziada ila kuwaomba mnichague tena kwa awamu ya pili ya kiti cha jimbo la ubunge la Kilosa ili kutekeleza ahadi zangu na kuwaletea maendeleo kwa ujumla kwa sababu nia na sababu ninayo," alisema Mkullo.
Akisoma Ilani ya uchaguzi ya mwaka 2005, Katibu wa CCM wilayani Kilosa, Gervas Makoye, alisema asilimia kubwa zimetekelezwa au kuanza kutekelezwa na hivyo ni fursa ya wakazi wa mji humo kuhakikisha wanaichagua tena CCM Oktoba 31, ili kujiletea maendeleo ya kweli.

Mwisho

Sunday, September 5, 2010

Dk Kikwete akiri watumishi wake wengi ni wezi



MGOMBEA wa Urais wa Chama cha Mapinduzi, CCM, Dk Jakaya Kikwete, amekiri wazi kuwa, watumishi wengi wa Halmashauri ni wezi na ndio wanaokwamisha miradi mingi ya maendeleo.
Aidha mgombea huyo amesema kuwa watanzania wengi wanajitakia kupata maambukizo ya ugonjwa wa Ukimwi kwa kuendekeza starehe na 'kiherehere' cha kupapia mapenzi yasiyo salama licha ya hamasa mbalimbali zinazotokea juu ya kujikinga na maradhi hayo.
Dk Kikwete aliyasema hayo jana katika mkutano wake wa kuomba kura katika uchaguzi mkuu ujao na kuwanadi wagombea wa nafasi za udiwani na ubunge wa wilaya ya Kilosa, mkoani Morogoro.
Alisema kuwa, pamoja na juhudi za serikali chini ya CCM kutaka kuleta maendeleo kwa wananchi, wapoo baadhi yawatumishi wa Halmashauri ambao ni wezi na wanaoangalia masilahi yao kwa kuzifuja fedha za miradi katika maeneo yao.
"Watumishi wengi wa Halmashauri ni wezi na wanaokwamisha miradi ya maendeleo kwa kuzitumia vibaya fedha wanazopelekewa na serikali kwa ajili ya kuwainua wananchi katika sekta mbalimbali jambo ambalo ni baya," alisema Dk Kikwete.
Katika kukaribia na hilo, mgombea huyo alisema akipata nafasi ya kuchaguliwa tena atahakikisha anapambana nao kwa ari zaidi, nguvu zaidi na kasi zaidi kama ilivyo kauli mbiu yao kwa kuwa kufanya hivyo kutaondoa kikwazo cha kuwapelekea wananchi maendeleo.
Akizungumza suala la maambukizi ya Ukimwi, mgombea huyo wa CCM, alisema anaamini kuwa, ugonjwa huo unakingika na kuepukika iwapo wananchi wataamua kuzingatia mahubiri na makatazo ya viongozi wa kidini juu ya suala la zinaa.
Dk Kikwete alisema maambukizi mengi yaliyopo nchini ni kama wananchi wanajitakia wenyewe kwa kutawaliwa na kuendekeza starehe na kiherehere cha kukimbilia mapenzi yasiyo salama.
"Kama sio kiherehere ni vipi mwanafunzi badala ya kushughulika na masomo shuleni yeye anakimbilia mapenzi?" alihoji Dk Kikwete.
Alitoa ushauri kwa wananchi juu ya kuwa makini na ugonjwa huo kwa kuoa, kujizuia kuwa waaminifu au kutumia kinga.
Kwani kwa kutokufanya hivyo maambukizi yatazidi kuongezeka na taifa kupoteza nguvu kazi ilihali Tanzania Bila Ukimwi Inawezekana!
Alizungumzia dawa za kurefusha maisha ya waathirika, Dk Kikwete serikali yake inatoa dawa hizo bure na kudai kama kuna wanananchi wanaouziwa basi watakuwa wanaibiwa na wanapaswa kutoa taarifa ili wahusika washuighulikiwe.
Juu ya malaria, aliyodai seikali yake inaumia kuona wananchi wanakufa kwa ugonjwa huo kuliko hata Ukimwi na kudai wameweka mikakati ya kupambana nao kwa kuongeza ugawaji wa vyandarua, kupuliza dawa katika kila nyumba nchi nzima na kuhakikisha wanaua mbu wanaoambukiza ugonjwa huo.

Mwisho

Chagueni CCM Tanzania istawi-Dk Kikwete





MGOMBEA wa Urais wa kiteki ya CCM, Dk Jakaya Kikwete, amewataka wananchi kukichagua chama chake kwa mara nyingine ili kuistawisha nchi, kwa maelezo kwamba vyama vya upinzani vilivyopo ni vya msimu na havina uwezo wa kuongoza.
Dk Kikwete ambaye pia ni Rais wa Jamhuri ya Muungano aliyasema hayo leo alipokuwa akiwatuhubia wakazi wa wilaya ya Kilosa katika mkutano wa kampeni uliofanyika eneo la Wahanga wa Mafuriko lililopo njia panda ya Ilonga na Kimamba, mkoani Morogoro.
Rais Kikwete alisema kuwa, pamoja na kwamba wapinzani wamekuwa wakitoa kejeli dhidi ya utendaji wa CCM, ukweli ni kwamba vyama hivyo havina uwezo wa kuongoza na hivyo ni vema wananchi wakaichagua tena CCM kustawisha maendeleo yaliyopo.
Alisema pamoja na utitiri wa vyama vya upinzani, vingi vyake ni vya msimu tu, ambapo huibuka wakati wa uchaguzi na hasa wanapofanikiwa kuwapata wanaohama toka CCM.
"Wananchi wa Kilosa na Watanzania kwa ujumla nawaombeni muichague CCM kwa mara nyingine kwa kuwa ndio chama pekee bora kinachoweza kustawisha maendeleo ya nchi yaliyopo pamoja na kudumisha amani na utulivu, vyama vingi vya upinzani ni vya msimu tu na hasa vinapofanikiwa kuwanasa wanaohama toka CCM pale wanapogombea na kutochaguliwa," alisema Dk Kikwete.
Dk Kikwete alisema CCM imfanikiwa kutekeleza ilani ya uchaguzi ya mwaka 2005 kwa asilimia kubwa katika nyanja na sekta za Afya, Elimu, Maji, Miundo Mbinu, Kilimo na Ufugaji na ikipewa nafasi tena itamalizia sehemu zilizobakia.
Alitoa mfano suala la elimu kwa wilaya ya Kilosa, imefanikiwa kuongeza majengo ya shule kuanzia chekechea hadi sekondari, ambapo alisema kwa mfanoi mwaka 2005 idadi ya wanafunzi katika sekondari ilikuwa ni 6969 ambapo kwa sasa idadi hiyo imefikia 17666 ikiwa ni ongezeko la zaidi ya wanafunzi 10,000.
Pia alisema juhudi hizo za kuboresha sekta hiyo zinaendana na kuongeza idadi ya walimu ambapop alisema mwaka 2005 idadi ya wahitimu wa ualimu nchi nzima ilikuwa ni 600 tu, lakini awamu ya nne imejitahidi na kufanya idadi hiyo kufikia 16,000.
Alisema, anafahamu idadi hiyo bado haikidhi hivyo serikali yake kupitia CCM inafanya mipango ya kuongeza walimu zaidi kupitia vyuo vyake na vile vya watu binafsi ili kufikia lengo sambamba na kuwezesha kupatikana kwa vitabu, maabara na nyumba za walimu.
Kuhusiana na vitabu,Dk Kikwete alisema tayari jitihada zimeshafanywa kwa kuomba msaada toka kwa nchi marafiki ikiwemo Marekani ambayo imejitolea kutoa jumla ya vitabu 800,000 vya masomo mbalimbali ya sekondari na mapema mwakani itapokea vitabu vingine zaidi ya Mil 2.4.
Alisema hayo na mengine ambayo yamekuwa yakifanywa na CCM tangu iwe madarakani hayawezi kufanywa na vyama vya upinzani na kuwataka wapiga kura kutofanya makosa Oktoba 31 watakapochagua viongozi kwa ajili ya miaka mitano ijayo.
Katika hatua nyingine, mgombea huyo alizungumzia suala la wahanga wa mafuriko yaliyoikumba wilaya hiyo mnamo Desemba mwaka jana, kuwa serikali ipo katika mpango wa kuwajengea nyumba za kudumu wahanga hao wanaishi kambini kwa sasa.
Dk Kikwete alisema kazi ya ujenzi wa nyumba hizo utafanywa na Jeshi la Kujenga Taifa, JKT, kwa lengo la kuwarejesha maisha ya amani na utulivu wakazi hao ambao kwa sasa wanaishi katika nyumba za mabati.
Pia alisema, serikali imetenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa bwawa jipya la Kidete pamoja na kujenga tuta jipya la kudhibiti maji ya Mto Mkondoa ambao aliutaja kuwa ndio tatizo lililosababisha mafuriko hayo yaliyoleta maafa makubwa.
Katika ziara yake ya kampeni wilayani humo, mgombea huyo wa CCM alikuwa akisimamishwa yeye na msafara wake na wananchi mbalimbali wa vijiji kwa ajili ya kumueleza kero zao.
Alipofika kata ya Dumila wananchi wa eneo hilo kupitia Mwenyekiti wa serikali ya Mtaa wa Dumila, Douglas Mwaigumila, walimueleza mgombea huyo juu ya kero zinazowakabili ambapo walizitaja ni huduma ya maji, afya, umeme na uporwaji wa ardhi yao ipatayo ekta 400 shutuma alizozipeleka kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya yao.
Dk Kikwete aliwajibu wananchi hao kuwa serikali yao inayatambua kero hizo na tayari ilishaanza kuzitekeleza kwa awamu, huku akishangaa kusikia tukio la uporwaji huyo wa ardhi na kuahidi kulifuatilia.