STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, March 28, 2014

Ashanti, Oljoro nani kulia Chamazi, vita ipo J'pili

Oljoro JKT
Ashanti United
VIBONDE vya Ligi Kuu Tanzania Bara, Ashanti United na Oljoro JKT kesho zinatarajiwa kupepetana katika pambano pekee kwa siku ya Jumamosi, huku kila moja ikiwa inahitaji ushindi ili kufufua matumaini ya kuendelea kusalia kwenye ligi ya msimu ujao.
Timu hizo zinazofuata toka mkiani zikiwa juu ya Rhino Rangers inayoburuza mkia na pointi zake 13 zitaumana kwenye uwanja wa Chamazi, Dar es Salaam.
Ni ushindi pekee kwa kila timu utafufua matumaini ya kuendelea kucheza ligi ya msimu ujao, vinginevyo huenda wakajiweka pabaya zaidi kushuka daraja kama walivyo wenzao wa Rhino ambao watashuka dimbani  Jumapili dhidi ya JKT Ruvu.
Ashanti inayonolewa na kocha Abdallah Kibadeni ina pointi 18 ikiwa nafasi ya 12, huku wapinzani wao wakiwa chini yao na pointi 16 kila moja ikiwa imecheza mechi 22.
Kila timu inahitaji ushindi ikizingatiwa zimetoka kuchezea vichapo katika mechi zao zilizopita, Ashanti ikizamishwa mabao 2-0 na Ruvu Shooting na Oljoro ikizabuliwa na Azam.
Timu hizo zilizobadilisha makocha baada ya kuyumba kwenye duru la kwanza, zimekuwa kama homa ya vipindi kwa viwango vyao kupanda na kushuka kulingana na aina ya mechi.
Kivumbi zaidi cha ligi hiyo kitakuwa Jumapili ambapo viwanja sita vitawaka moto kwa kuzikutanisha timu 12 zikiwamo tatu zinazowania taji la ubingwa wa ligi hiyo linaloshikiliwa kwa sasa na Yanga.
Azam watakuwa kwenye uwanja wa Taifa kuivaa Simba, ikihitaji ushindi ili kuujongelea ubingwa huo na pia kuiombea mabaya Yanga watakaokuwa ugenini mjini Tanga kupepetana na Mgambo JKT iteleze katika mechi yake hiyo itakayopigwa uwanja wa Mkwakwani.
Azam ina pointi 50, nne na ilizonazo Yanga licha ya kuwa mbele kwa mchezo mmoja na timu yoyote ikiteleza itatoa nafasi kwa mwenzake kuubeba ubingwa huo kwa msimu wa 2013-2014.
Mbeya City waliopo nafasi ya tatu na pointi 42 wakiwa nao wanauota ubingwa watakuwa uwanjwa wa Sokoine kuumana na ndugu zao Prisons wanmaougulia kipigo cha mabao 5-0 walichopewa na Yanga juzi.
Ushindi wowote kwa Mbeya utamaanisha unaiweka pabaya Simba katika mbio zake kutaka kuambulia angalau nafasi ya tatu kama ilivyokuwa msimu uliopita.
Simba wana pointi 36 na wamesaliwa na mechi nne, ambazo kama watashinda zote itafikisha pointi 48 zilizopitwa na Azam tayari.
Simba itavaana na Azam ikiwa inauguza kipigo cha bao 1-0 ilichopewa na Coastal Union mwishoni mwa wiki iliyopita kqwenye uwanja wa Taifa.
Mabingwa hao wa soka wa 1988 wenyewe watawafuata Mtibwa Sugar kuumana nao katika mchezo utakaochezwa uwanja wa Manungu, huku timu zote zikiwa hazina nafasi ya ubingwa wala hofu ya kushuka daraja.
Michezo nyingine ya Jumapili ni pamoja na Kagera Sugar watakuwa wenyeji wa Ruvu Shooting katika pambano linalosubiriwa kwa hamu kubwa mjini Bukoba, ambapo Msemaji wa Ruvu Masau Bwire ametamba kwamba wanaenda Kaitaba kuvuna pointi tatu.
Hata hivyo Bwire anatamba akitambua wazi kuwa Kagera Sugar huwa wagumu kwene uwanja wao wa nyumbani.
Timu hizo mbili zinafukuzana kwenye nafasi ya tano na sita zikitofautishwa na pointi moja, Kagera wakiwa na pointi 32 na Ruvu wenyewe wana pinti 31.

TMK, Tip Top kuzindua Yamoto

WASANII nyota toka makundi ya Tip Top Connection na TMK Wanaume Family wanatarajiwa kupamba uzinduzi wa video za Yamoto na Inno za kundi jipya linalooundwa na chipukizi toka Kituo cha Mkubwa na Wanawe.
Kundi hilo linaloundwa na wasanii Dogo Aslay, Beka, Maromboso na Bella, litazinduliwa Jumapili Masaki na nyota wa Tip Top wakiongozwa na Madee huku TMK litakuwa chini ya Chegge.
Kwa mujibu wa mmoja wa mabosi wa wasanii hao, Said Fella 'Mkubwa' aliliambia MICHARAZO uzinduzi wa kundi hilo utaenda sambamba na utambulisho wa kazi mpya za wasanii hao.
"Tunatarajiwa kuwatambulisha rasmi na kuzindua kundi la Moto linaloundwa na wasanii wanne walioibuliwa na Mkubwa na Wanae watakaosindikizwa na makundi ya Tip Top na TMK," alisema Fella.
Fella alisema makundi hayo yote yatakuwa na wasanii wao wote nyota na kuwataka mashabiki wa muziki kujitokeza kwa wingi Jumapili ili kupata burudani murua.

Mashali, Kaseba kupima uzito leo

Kaseba na Mashali wakishoo
MABONDIA Japhet Kaseba na Thomas Mashali na wengine watakaowasindikiza katika pambano lao la kuwania ubingwa wa UBO Afrika wanatarajiwa kupima uzito wao siku ya Ijumaa jijini Dar.
Kwa mujibu wa taarifa ya mmoja wa waratibu wa pambano hilo, Ibrahim Kamwe mabondia hao watapima uzito kuanzia saa 3 asubuhi kwenye ukumbi wa hoteli ya National iliyopo eneo la Keko.
Mbali na Mashali na Kaseba watakaopambana katika pambano la raundi 10 uzito wa LightHeavy (kilo 79), pia mabondia wengine watakaopima uzito na afya zao ni Allan Kamote ambaye atapigana na Karage Suba katika pambano la kuwania taji la kimataifa ya UBO.
"Mabondia wote wameshataarifiwa na wanatakiwa kuwahi mapema siku ya Ijumaa, National Hotel ili kupima afya na uzito wao kabla ya Jumamosi kuonyeshana kazi kwenye ukumbi wa PTA," alisema.
Kamwe aliwataja wengine watakaochuana katika michezo hiyo iliyoandaliwa na promota Ally Mwazoa, ni pamoja na Fredy Sayuni dhidi ya Rajab Mahoja watakaowania ubingwa wa taifa wa PST.
Baina Mazola atacheza na Bakari Dunda,Issa Omar ataonyeshana kazi na Zuberi Kitandula, Juma Fundidhidi ya Haji Juma, Shabaan Mtengela vs Jumanne Mohamed, Jocky Hamis dhidi ya Said Chaku

Subira ya Shaa mwezi ujao

Shaa katika pozi
'AUDIO' na VIDEO ya wimbo mpya wa msanii, Sarah Kais 'Shaa' unaofahamika kama 'Subira' unatarajiwa kuachiwa rasmi mapema mwezi ujao.
Wimbo huo uliobadilishwa jina kutoka 'Sifa Ujinga' hadi kuwa 'Subira' ni kazi ya pili ya mshindi huyo wa zamani wa Coca Cola Pop Star chini ya familia ya Mkubwa na wanae inayongozwa na Said Fella.
Akizungumza na MICHARAZO, Fella alisema wamepanga kutoa 'audio' na video ya wimbo huo mwezi ujao baada ya kurekodiwa mapema tangu Februari mwaka huu.
Fella alisema waliamua kuuzuia wimbo huo kutoka mapema ili kutoa nafasi ya kazi ya msanii huu iitwayo 'Sugua Gaga' kuendelea kutamba kwenye soko la muziki kutokana na ukali wake.
"Kazi mpya ya Shaa tutaiachia rasmi mapema mwezi ujao ikiwa ni 'audio' na video yake, hivyo mashabiki wajiandae kupata uhondo," alisema Fella waliyeingia mkataba na Shaa kwa muda wa miezi sita.
Kabla ya kutua Mkubwa na Wanae, Shaa alikuwa akifanya kazi chini ya umeneja wa Master J.

Ac Milan yazinduka, Juve moto chini

http://news.bbcimg.co.uk/media/images/73837000/jpg/_73837135_carlos-tevez-getty.jpg
Tevez akishangilia moja ya mabao yake

KLABU ya AC Milan imezinduka nchini Italia baada ya juzi kuikwanyua Fiorentina kwa mabao 2-0 nyumbani kwao, huku usiku wa jana wapinzani wao wa jiji la Milan, InterMilan walilazimishwa sare ya 0-0 na Udinese.
Milan ambaye imekuwa na matokea mabaya kwenye Ligi Kuu ya Seria A, walipata ushindi huo kupitia magoli yaliyofyungwa na Mexes dakika ya 23 kabla ya Mario Balotelli kufunga kipindi cha pili katika dakika ya 64 na kuipaa pointi tatu mabingwa hao wa zamani wa Ulaya.
Katika mechi nyingine za ligi hiyom, Juventus wakiwa nyumbani walipata ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Parma na kuzidi kujiweka karibu na kutetea taji la ubingwa wa ligi hiyo.
Magoli  yote mawili yalitupiwa kambani na Carlos Tevez katika dakika ya 25 na 32 na kuwapa pointi zinazowafanya wafikishe 81 na kusaliwa na mechi nane mkononi ambapo kama akishinda mechi tatu ikiwamo ya Jumapili dhidi ya Napoli atatawaza kuwa bingwa. Wageni walimpoteza Amauri aliyeonyesha kadi nyekundu.
Matokeo ya mechi nyingine za ligi hiyo;

Chievo     3 - 0     Bologna
Cagliari     1 - 0     Hellas Verona
Genoa     2 - 0     Lazio
Atalanta     2 - 0     Livorno   
Fiorentina     0 - 2     Milan
Catania     2 - 4     Napoli  
Juventus     2 - 1     Parma
Sassuolo     1 - 2     Sampdoria
Inter Milan 0-0 Udinese

Askofu Mhogolo afariki dunia

ASKOFU wa Dayosisi ya Central Tanganyika, Godfrey Mhogolo amefariki dunia nchini Afrika Kusini, alikokuwa amekwenda kwa matitabu. 
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kanisa la Angilikana Dodoma jana, ilisema kuwa Askofu Mhogolo kabla ya kufikwa na mauti alikuwa akitibiwa katika hospitali ya Milpark huko Johanesburg, Afrika Kusini. Askofu Mhogolo alikuwa askofu wa tano wa dayosisi ya Central Tanganyika na atazikwa katika viwanja vya kanisa Kuu la Roho Mtakatifu Mjini Dodoma.  
Hata hivyo Mchungaji Michael Nchimbi alisema mipango ya mazishi inaendelea na taarifa zitatolewa baadaye. 
matukio na vijana

Golden Bush kupeleka makali yao Kilombero

Kikosi cha Golden Bush
Makocha wa Golden Bush, Madaraka Seleman na Herry Morris waliosimama wakiteta na wachezaji wao katika moja ya mechi zao
 MABINGWA wa kandanda wa soka la maveterani, Golden Bush Veterani inatarajiwa kupeleka makali yake wilaya ya Kilombero Morogoro kumenyana na Kilombero Veterani katika mechi inayochezwa kesho.
Kwa mujibu wa Msemaji wa klabu hiyo, Onesmo Waziri 'Ticotico' kikosi cha Golden Bush kitaondoka kesho asubuhi kikiwa na wachezaji 25 wakiongozwa na mkuu wa msafara,  Waziri Mahadh 'Mandieta'.
Ticotico alisema kikosi chao kitashuka dimbani jioni ya kesho kwenye uwanja wa Ruaha kuumana na wenyeji wao watakaokuwa wakiongozwa na nahodha wa zamani wa Simba, Mustafa Hozza.
Ticotico alitamba kuwa wanaenda Kilombero kuendeleza ubabe wao ambao umewafanya kukimbiwa na wapinzani na kwamba wenyeji wao wajiandae kwa kipigo.
Alisema kikosi chao chini ya kocha Madaraka Seleman 'Mzee wa Kiminyio' kitaongozwa na nahodha wao Wisdom Ndhlovu a.k.a Mwakalinga.

TFF kuuendeleza uwanja wao wa Tanga

SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF) limeanza mchakato wa kuendeleza uwanja wake uliopo eneo la Mnyanjani jijini Tanga.
Rais wa TFF, Jamal Emil Malinzi alisema shughuli inayoendelea kwa sasa ni kupima udongo (soil test) na kuandaa michoro kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha michezo (Sports Complex) ukiwemo uwanja wa mpira wa miguu na majukwaa yake.
Amesema TFF imetuma maombi rasmi kwa Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro kuomba eneo la kujenga kituo cha michezo ikiwemo uwanja wa mipira wa miguu na majukwaa yake.
“Pia Mkuu wa mkoa ameombwa kuingilia kati kuwaondoa wafanyabiashara waliovamia uwanja wa mpira wa miguu wa Jamhuri (King George Memorial ground) mjini Moshi,”amesema Malinzi.
Amesema TFF inawakumbusha viongozi wa vyama vya mikoa ambao hawajaomba maeneo ya kujenga vituo vya michezo vikiwemo viwanja vya mpira wa miguu, waongeze jitihada za kufanya hivyo na shirikisho hilo litawaunga mkono.
“TFF inachukua fursa hii kuvipongeza vyama vya mpira wa miguu ambavyo ama tayari vimeshachukua hatua au viko mbioni kuchukua hatua kutafuta na kuendeleza maeneo kwa ajili ya matumizi ya mpira wa miguu. TFF inaahidi kuunga mkono juhudi hizi na pale itakapohitajika kuongeza nguvu haitasita kufanya hivyo,”amesema.