STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Monday, May 28, 2012

Uigizaji haulipi kama muziki-Kitale

MSANII KITALE AKTIKA KATIKA POZI TOFAUTI
MSANII nyota wa filamu cha vichekesho nchini, Mussa Yusuf 'Kitale' amedai licha ya fani ya uchekeshaji kutolipa kama muziki, lakini katu hawezi kuachana na fani hiyo. Akizungumza na MICHARAZO, Kitale alisema ndio maana kwa sasa akishirikiana na Husseni Mkiety 'Sharo Milionea' wameandaa filamu zao binafsi zaidi ya tano. Alisema katika muziki msanii ananufaika kwa vile huwa ni kazi yake binafsi tofauti na filamu ambapo mabosi ndio wanaoneemeka na msanii hutumika tu kama kibarua. "Kwenye filamu na uchekeshaji tunaambulia sifa tu, lakini kimasilahi ni kidogo tofauti na muzikio, hata hivyo siwezi kuachana na fani hii kwani nimeshaizoea na kwa sasa kuna kazi mpya ninazoandaa na Sharo Milionea," alisema. Alizitaja kazi hizo kuwa, "Sharo Madimpoz', 'Sharo Crazy', 'Sharo Taxi Driver' na 'Drug Dealer' ambazo anaziandaa kwa kushirikiana na Sharo Milionea ambaye wamekuwa wakiendana katika uigizaji wao. "Hizi ni baadhi ya filamu tutakazotoa ndani ya mwaka huu, sambamba na kazi zetu za muziki ambazo kila mmoja anaifanya na kumpa mafanikio makubwa," alisema. Kitale anayeigiza kama 'teja', alisema amepanga kabla ya kumalizika kwa mwaka huu albamu yake binafsi iwe imeshaingia sokoni.

Manyika avunja ukimya na Wololowololo

NYOTA wa zamani wa Yanga aliyetumbukia kwenye muziki, Manyika Peter, ameachia wimbo mpya uitwao 'Wolowolo', akijiandaa kutolea video yake. Akizungumza na MICHARAZO, kipa huyo aliywahi kung'ara na timu za Mtibwa Sugar, Sigara, Yanga na klabu kadhaa za kimataifa alisema kazi hiyo ni ya pili tangu alipotoa albamu yake mwaka 2004. Manyika, alisema 'Wololowololo' umetoka ikiwa ni miaka minne tangu atoe wimbo wake wake wa mwisho mwaka 2007 uitwao 'Manabii'. "Baada ya kimya kirefu nimetoka na wimbo wa 'Wololowololo' ninaouandalia video yake, hiki ni kibao cha pili baada ya albamu yangu ya 'Unanipeleka Puta' ilitoka mwaka 2004," alisema. Manyika, alisema tofauti na alipotumbukia kwenye fani hiyo mwaka 2001 wakati akiwa anaichezea Yanga, kwa kutoa albamu, safari hii hana mpango huo kwa madai utoaji wa albamu haulipi kama kutoa 'singo'. "Sina mpango wa kutoa albamu, nitaendelea kutoa wimbo mmoja mmoja kwa lengo la kupata shoo ambazo ndizo zinazolipa vema," alisema. Alisema wakati akihangaikia kuitolea video wimbo huo wa 'Wololowololo', tayari kuna nyimbo nyingine mbili ameshaziandika ambazo atazirekodi baadae ili kudhihirisha nia yake ya kujikita jumla kwenye muziki.
MANYIKA PETER KATIKA POZI TOFAUTI KAMA MSANII WA MUZIKI WA KIZAZI KIPYA

Mpeni muda Kim atufikishe mbali kimataifa-Manyika

NYOTA wa zamani wa kimataifa aliyewahi kuzichezea timu za Mtibwa, Sigara na Yanga, Manyika Peter, amewataka wadau wa soka nchini kumpa muda kocha Kim Poulsen, ili afanye kazi zake kwa manufaa ya soka la Tanzania. Pia, aliwataka wadau hao kutoweka matumaini makubwa ya timu yao ya taifa, Taifa Stars kufuzu fainali za Afrika 2013 au Kombe la Dunia 2014, ila nguvu ziwekezwe kwa fainali za mbele zaidi akiamini timu itakuwa imewiva. Manyika, alisema Tanzania imekuwa ikikwama kufika mbali kwa vile makocha wanaozifundisha timu za taifa na hata klabu hawapewi muda mrefu wa kukaa na timu husika, kitu alichotaka kisitokee tena kwa kocha wa sasa wa Stars. "Tumpeni nafasi Kim aweze kufanya kazi zake na naamini kwa uwezo alionao tunaweza kufika mbali zaidi na hapa tulipo, ila kama tutaendelea na tabia ya kulaumu kisha aondolewe tutadumaa hapa hapa kisoka," alisema. Alisema Kim, ni mmoja wa makocha wazuri kutokana na kufanya nae kazi akiwa kama Mkufunzi wa FIFA wa makipa wa timu za taifa za vijana, hivyo aliwataka wadau wa soka wasimbughudhi ili afanye kazi zake kwa ufanisi. Aliongeza, licha ya kuwataka wadau wawe na subira pia wasiweke tumaini kubwa la Tanzania kufuzu fainali zijazo za Afrika zitakazofanyika Afrika Kusini au Kumbe la Dunia la Brazil, ingawa alikiri lolote linaweza kutokea. "Tukifuzu itakuwa ni bahati, lakini nadhani tunapaswa kuweka nguvu kwa ajili ya fainali za mbele, tumechelewa mno kujipanga hivyo lolote litakalotokea tulichukulie poa na kujipanga zaidi ili tufuzu michuano ijayo," alisema. Tanzania ipo kwenye mbio za kuwania kufuzu fainali za Afrika ikitarajiwa kuvaana na Msumbiji katika mechi ya marudiano Juni 15 baada ya awali kutoka sare. Pia ipo kundi C na timu za Ivory Coast, Morocco na Gambia katika mbio za kuwania kucheza fainali za Kombe la Dunia za 2014 zitakazofanyika nchini Brazil, ikianza kibarua Juni 2 kwa kuumana na Ivory Coast.

Sijasaini kokote-Nsa Job

MSHAMBULIAJI nyota wa timu ya Villa Squad, Nsa Job, amesema licha ya kuzungumza na watu wa Coastal Union ya Tanga, bado hajasaini fomu yoyote ya kujiunga kuichezea timu hiyo kwa msimu ujao wa Ligi Kuu Tanzania Bara. Kutokana na kutosaini, Nsa alisema milango i wazi kwa klabu yoyote ambayo imevutiwa naye, mradi aridhishwe na dau watakalokubaliana. Akizungumza na MICHARAZO, Nsa alisema ni kweli amefanya mazungumzo na Coastal Union, ila hawaafikiana na ndio maana hajasaini fomu na hivyo kutoa ruksa kwa timu nyingine kuweza kuzungumza nae. "Sijasaini kokote ndugu yangu, ingawa ni kweli nilishafuatwa na kuzungumza na watu wa Coastal Union," alisema. Nsa, alisema yeye kama mchezaji anaangalia masilahi hivyo timu yenye dau kubwa la kuvutia ndio atakayoichezea kwa msimu huo ujao. Nyota huyo aliyewahi kuzichezea timu za Moro United, Simba, Yanga na Azam, alisema hawezi kukurupuka kusaini timu bila kuangalia masilahi yake ikizingatiwa soka kwake ndio ajira inayomuingizia kipato. "Soka la sasa sio la kuchezea sifa, naangalia masilahi kwanza timu baadae," alisema.

Boxer Johnny Tapia has died at the age of 45

Tapia, whose career was marked by cocaine addiction, alcohol, depression and run-ins with the law, was found dead on Sunday in his hometown of Albuquerque, New Mexico. He won the WBO super-flyweight title in 1994, two belts at bantamweight and the IBF featherweight belt in 2002. Police spokesman Robert Gibbs said the death "did not appear to be suspicious". His tragic start in life - both parents were murdered, several stints in jail and numerous rivalries, garnered him a cult following in the sport. Tapia was orphaned at eight when his mother was murdered in brutal circumstances and, despite his successes in the ring, trouble stalked him for the rest of his life. Having been banned from boxing for three and a half years in the early 1990s because of his cocaine addiction, he beat Henry Martinez to become a world champion for the first time. Tapia went 11 years unbeaten as a professional before Paulie Ayala defeated him in 1999 in The Ring magazine's Fight of the Year, taking his WBA bantamweight title. Tapia lost a rematch with Ayala in 2000. In 2002 he beat Manuel Medina to secure the IBF featherweight crown and was good enough to take Mexican great Marco Antonio Barrera the distance later that same year. In 2007, he was hospitalised after an apparent cocaine overdose. Several days later, his brother-in-law and his nephew were killed in car accident on their way to Albuquerque to see the ailing boxer. In his 2006 autobiography, Tapia described how he had been declared clinically dead five times, each time due to a drug overdose. He also survived shootings, a bus crash and a near-drowning. Tapia last fought in June, outpointing Mauricio Pastrana. He finished with a 59-5-2 record.

Friday, May 25, 2012

Jackson Chove ajipigia debe

KIPA wa timu iliyoshuka daraja ya Moro United, Jackson Chove, amesema yupo tayari kujiunga na timu yoyote itakayomhitaji kwa sababukiwango chake kipo juu licha ya timu yake kuporomoka. Chove, ambaye aliwahi kuzidakia Yanga, Prisons-Mbeya, JKT Ruvu na Azam kabla ya kutua Moro United, alisema kama mchezaji anatambua soka ndio ajira yake, hivyo kila siku anaendelea kujivua kujiweka fiti ili aendelee kutesa. Alisema, timu yoyote ambayo itaridhiana nae atakuwa tayari kujiunga nayo kwa ajili ya msimu ujao, ingawa alisisitiza kuwa yupo katika maandalizi ya kwenda Msumbiji kucheza soka la kulipwa. "Kwa kweli nipo tayari kutua timu yoyote baada ya timu yangu ya Moro Utd kushuka daraja, soka ndio kazi yangu hivyo kokote mie nacheza," alisema. Chove, aliyewahi kucheza soka la kulipwa nchini DR Congo na Rwanda kwa nyakati tofauti baada ya kutemwa Yanga, alisema anaamini yeye ni miongoni mwa makipa mahiri nchini, ila hajapata sehemu ya kuonyesha makali yake. Kipa huyo anayefahamika kama Mandanda, alisema kwa kuwa msimu mpya ndio unaanza sasa kwa klabu kusajili wachezaji wapya na kuacha wa zamani, naye anasubiri mahali atakapoangukia kwa ajili ya msimu ujao. Chove, alikuwa miongoni mwa makipa tegemeo wa Moro Utd iliyoshindwa kuhimili vishindo vya Ligi Kuu Tanzania Bara msimu huu iliyoirejea toka daraja la kwanza na kuteremka pamoja na Polisi Dodoma na Villa Squad. Mwisho

TPBO yamlilia Mafisango, yaasa wachezaji Simba

OGANAIZESHENI ya Ngumi za Kulipwa nchini, TPBO, imetuma salamu za rambirambi kwa klabu ya soka ya Simba kutokana na msiba wa kiungo wao nyota, Patrick Mutesa Mafisango aliyefariki wiki iliyopita kwa ajali ya gari. Rais wa TPBO, Yasin 'Ustaadh' Abdallah, alisema wameshtushwa na kifo cha ghafla cha mchezaji huyo aliyekuwa kiigizo chema kwa wachezaji vijana nchini na kuungana na ndugu, jamaa na wadau wa klabu ya Simba kwa msiba huo. Ustaadh, alisema wadau wa ngumi hasa wanaopenda kuhudhuria michezo mbalimbali ya soka, wanajua namna gani Simba imepata pigo kwa kufiwa na kiungo huyo rais wa Rwanda ingawa mwenyeji wa DR Kongo. "TPBO tunaupa pole uongozi wa Simba na wadau wote wa klabu hiyo na soka kwa ujumla kwa kuondokewa na Patrick Mafisango, kama wadau tunaungana nao katika majonzi na kuwatakia moyo wa subira," Ustaadh alisema. Aliongeza kwa kuwataka wachezaji wenzake ambao anafahamu itawachukua muda mrefu kusahau kifo cha Mafisango kumuenzi mwenzao kwa kuiheshimu kazi yake aliyoifanya enzi za uhai wake kwa kuipa Simba mafanikio zaidi. "Najua ni vigumu wadau wa Simba kusahau msiba wa Mafisango, lakini TPBO tunaamini nnia pekee ni kumshukuru Mungu kwani kazi yake haina makosa na pia kumuenzi kwa kuipa Simba mafanikio zaidi," alisema. Patrick Mutesa Mafisango, aliyezikwa Jumapili iliyopita nyumbani kwao, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, alifariki usiku wa kuamkia Alhamisi iliyopita kwa kupata ajali ya gari akitokea Maisha Club 'kujirusha'. Kiungo huyo aliyewahi kung'ara na timu za TP Mazembe, APR, Azam kabla ya kutua Simba akiichezeapia timu ya taifa ya Rwanda 'Amavubi', amefariki akitokea kuisaidia Simba kutwaa taji la Ligi Kuu Tanzania Bara 2011-2012.

ZFA yaifungulia milango Yanga kutua Zenji

MSEMAJI WA ZFA, Munir Zakaria CHAMA cha Soka cha Zanzibar, ZFA, kimesema kipo tayari kuipokea klabu ya Yanga, iliyotishia kutaka kuhamia visiwani humo, mradi wafuate taratibu zinazokubalika. Wazee wa klabu ya Yanga walinukuliwa wiki iliyopita kwamba wanafanya mpango wa kuihamishia Yanga visiwani Zanzibar kutokana na kukerwa na maamuzi ya uongozi wa Shirikisho la Soka Tanzania, TFF 'kumbeba' Mwenyekiti wao, Llyod Nchunga. Wanachama hao wa Yanga wamekuwa na mgogoro na Nchunga kiasi cha kuitisha mkutano na kuung'oa uongozi huo, jambo lililopingwa na TFF kwa madai ya kutozingatia katiba inayoiongoza klabu hiyo. Jambo hilo lilionyesha kuwakewa wazee hao ambapo kupitia Katibu wake, Ibrahim Akilimali alinukuliwa akitishia kuihamisha Yanga Zanzibar kama njia ya kuikomoa TFF na Nchunga, kitu kilichoufanya uongozi wa ZFA kusema upo tayari kuwapokea. Msemaji wa ZFA, Munir Zakaria alinukuliwa na kituo kimoja cha redio alisema wao wanaisubiri Yanga kutua visiwani humo wakiamini itasaidia kuinua soka la Zanzibar. Zakaria, alisema pia kuhamia kwa Yanga visiwani humo kutaifanya Zanzibar itambe kimataifa na hivyo wanafungua milango kwa klabu hiyo, ila wakiitaka kuzingatia taratibu za kuweza kucheza ligi ya visiwani humo. "Tunawasubiri waje, hatuna vikwazo kwao kwa vile tunaamini watasaidia kuinua soka la visiwani humo, ila wafuate taratibu ikiwemo kama wanaweza wainunue klabu yoyote ya ligi kuu kisha waibadilishe jina kwa kuiita Yanga ili waweze kucheza ligi yetu," alisema. Msemaji huyo ambaye pioa ni Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya ZFA, alisema wao hawaoni tatizo kwa Yanga kujiunga katika ligi yao kwani ni moja ya timu yenye mashabiki wengi visiwani humo na ina jina kubwa katika anga la kimataifa. Hata hivyo, tishio hilo la wazee wa Yanga kutaka kuhamia Zanzibar linaonekana kama 'danganya toto' kwani baadhi ya wanachama wake wamewapuuza wazee hao wakiona kama wanaotapatapa katika kuubana uongozi wa Yanga. "Hatudhani kama hilo linaweza kufanyika, nadhani wazee wanatafuta njia ya kutaka kuungwa mkono katika kile walichokifanya ambacho kinaendana kinyume na katiba hata kama ni kweli viongozi wa Yanga wanakosa," alisema mmoja wa wanachama wa klabu hiyo aliyekataa kutajwa jina la kwa madai ya uhusiano wake wa karibu na wazee. Klabu ya Yanga imekuwa katika hali tete tangu walipopoteza taji lao la ubingwa wa Ligi Kuu kwa watani zao, na pia kupokea kichapo cha aibu cha mabao 5-0 mbele ya Simba katika mechi ya kufungia msimu wa ligi Tanzania Bara. Hata hivyo tayari Nchunga ameshatangaza kuachia ngazi mwenyewe kwa hiari yake, na hivyo suala au tisho la Yanga kuhamia Zenji huenda lisiwepo tena. TUSUBIRI TUONE!

Watanzania zidini kuniombea, tumaini la kupona lipo-Sajuki

NYOTA wa filamu ambaye yupo nchini India kwa matibabu, Juma Kilowoko 'Sajuki' amewataka Watanzania kuzidi kumuombea kwa Mungu ili aweze kupona matatizo yake, akisema wakati akituoa nchini humo kwa matibabu hali yake ilikuwa tete. Akizungumza toka India, Sajuki alisema hali yake ilikuwa mbaya alipofika nchini humo ambapo alipimwa na kukutwa hana damu na huku akiwa kadhoofika kiasi cha kushindwa kufanyiwa chochote. Alisema hata hivyo uangalizi aliopewa katika siku chache zilizopita hali yake imeimarika na sasa anasubiri kupimwa tena kuona kama anaweza kufanyiwa upasuaji kuondoa uvimbe ambao alidai umeongezeka sehemu nyingine ya tumbo lake. "kwa kweli mpaka nazungumza hivi ujue nimeimarika, nilikuwa na hali mbaya hasa baada ya kubainika kuwa kulikuwa na vivimbe vingine vilivyodhoofisha afya yangu na pia nilikuwa na upungufu wa damu, hivyo nikawa katika uangalizi maalum, ila nashukuru mno na ninawaomba Watanzania waniombee," alisema. Sajuki, alisema wakati wowote kuanzia sasa huenda akafanyiwa upasuaji ambao ndio unaoelezwa ni salama ya maisha yake. Wakati akiondoka nchini, Sajuki aliwaliza watu kutokana na kushindwa kutembea mwenyewe na pia alionekana kadhoofu maradufu tofauti na siku za nyuma kabla ya kusafiri kwenda kufanyiwa matibabu nchini humo. Msanii huyo anatibiwa katika hospitali ya Saifee iliyopo Mumbai na sio Apollo kama ilivyokuwa ikiripitiwa awali na vyombo vya habari.

Hili Dude la Kitale ni nouma!

MCHEKESHAJI maarufu nchini, Mussa Yusuf 'Kitale' ameachia wimbo mpya uitwao 'Hili Dude' ukiwa miongoni mwa nyimbo anazoziandaa kwa ajili ya albamu ya kwanza. Akizungumza na MICHARAZO, Kitale ambaye amepata umaarufu mkubwa kwa kuigiza kama 'teja', alisema tayari ameshausambaza wimbo huo mpya katika vituo vya radio huku video yake ikiwa katika hatua za mwisho kabla ya kuachiwa. Kitale alisema kibao hicho ni cha pili kwake baada ya awali kufyatua 'Chuma cha Reli' alichokiimba na Gondo Msambaa. "Nimekamilisha dude jipya, linaitwa 'Hili Dude' ambalo limeshaanza kurushwa hewani ikiwa ni utambulisho wa albamu yangu ambayo tayari nyimbo saba kati ya nane zimeshakamilika," alisema. Alisema katika wimbo huo mpya, ameimba kwa kushirikiana na Mide Zo na Corner ambaye pia ndiye prodyuza wa wimbo huo kutoka studio za Kwanza Records ya mjini Morogoro. Msanii huyo alizitaja nyimbo nyingine zitakazokuwa katika albamu hiyo kuwa ni 'Anajifanya Msela' alioimba na Juma Nature, 'Hili Toto' alioimba na Sharo Milionea na Mide Zo, ' Tulianzishe', 'Kinaunau' na 'Chuma cha Reli'. "Wimbo wa mwisho nimeshautunga, ila sijaurekodi kwa sababu bado naendelea kufanya mazungumzo na mmoja wa wasanii kwa ajili ya kuimba nae," alisema. Aliongeza, ameamua kutumbukia kwenye muziki baada ya kuona fani ya uchekeshaji ikiwa haimlipi kwa vile kazi nyingi hufanya chini ya watu ambao ndio hunufaika.

Dogo Aslay kupagawisha Dodoma

DKAMPUNI ya Ruhazi Promotion ya jijini Dar es Salaam, inatarajia kumtambulisha msanii chipukizi anayetamba hivi sasa katika muziki wa kizazi kipya nchini Aslahi Isihaka ‘Dogo Aslay’ kwa mashaki wa mjini Dodoma . Akizungumza na mwandishi wa habari hizi jijini Dar es Salaam jana mratibu wa onesho hilo Jackline Masano, alisema kuwa onesho hilo litafanyika Jumamosi Juni 9 kwenye uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma . Alisema kuwa wasanii wengine kutoka kituo cha Mkubwa na Wanawe watamsindikiza na kuwa mazungumzo na wasanii wengine watakaopamba onesho hilo yanaendelea na kwamba watawatangaza pindi watakapomalizana nao. “Tumeamua kuwaletea wapenzi wa burudani wa Dodoma burudani ya uhakika Jumamosi ya Juni 9, litaanza saa 6:00 mchana na litamalizika saa 12:00 jioni ambapo Dogo Aslay akisindikizwa na wasanii kutoka mkubwa na Wanawe na wasanii nyota nchini ambao tutawatangaza majina yao tukishamaliza makubaliano nao,” alisema Jackline. Alisema pamoja na kwamba onesho hilo litapambwa na wasanii wengi lakini wameamua kiingilio kiwe cha shilingi 5,000 tu kwa wakubwa na shilingi 1000 kwa watoto ili kuwawezesha wapenzi wengi zaidi waweze kukimudu na kushuhudia burudani hiyo.

Steve Nyerere kusomesha yatima kwa miaka 7

MSANII wa filamu nchini ambaye pia huiga sauti za viongozi mbalimbali, Steve Mengele 'Steve Nyerere' jana amezindua filamu yake mpya inayojulikana kama 'Mwalimu Nyerere', huku akiahidi kuwasomesha watoto wawili yatima wa kituo cha Maunga Centre ulipofanyikia uzinduzi wa filamu hiyo. Akizungumza mara baada ya kuzindua filamu hiyo akiwa pamoja na watoto yatima wa kituo hicho, Steve Nyerere alisema ameamua kufanya hivyo kutokana na ukweli kwamba Baba wa Taifa Mwali Nyerere hakubagua watu. Alisema ujio wa filamu hiyo ni kama azma yake aliyoipanga tangu awali kuhakikisha anamuenzi Baba wa Taifa kwa kutoa filamu itakayokuwa inaonesha mambo mbalimbali aliyowahi kuyafanya Baba wa Taifa. "Jina lililonibeba zaidi katika tasnia hii ya filamu ni jina la Steve Nyerere kiasi ambacho hata jina la Baba yangu halijanizoea, hivyo kutokana na ukubwa wa jina hili limenifanya mimi kutambulika na jamii nzima ya Tanzania hivyo ili kulienzi jina hili nimeamua kutoa filamu hii ya Mwalim Nyerere,"alisema Steve. Alisema msaada alioutoa kwa watoto yatima hautaishia kwao bali ataendelea kutoa kile atakachokipata kupitia filamu hiyo kuwasaidia na wale wasiojiweza. Alisema filam ya Mwalimu Nyerere ameifanyia Butiama alipozaliwa Baba wa Taifa ili kujenga uhalisia wa kile alichodhamiria na kwamba ameitengeneza filamu hiyo kwa kipindi cha miezi mitatu huku akishirikiana vema na mke wa Hayati Baba wa Taifa Mama Maria Nyerere. Alisema jumla ya sh. milioni 25 ametumia katika kuikamilisha filam hiyo ambayo itaanza kuingia sokoni leo ikiwa chini ya usambazaji wa Steps Entertaiment. Kabla ya kutoa filam hiyo Steve Nyerere alitamba na filam ya 'Mr President' aliyoitunga kwa kuvaa uhusika wa Rais wa Jamhuri ya Muungano Tanzania Dkt.Jakaya Kikwete ambayo aliitaja kama zawadi kwa Rais Kikwete katika kuadhimisha miaka 50 ya Uhuru wa Tanganyika

Twiga yapaa kuwafuata wahabeshi, wamwagiwa 'mihela'

TIMU ya taifa ya soka ya wanawake Tanzania, Twiga Stars imeondoka jana jioni kwa ndege ya Ethiopian Airlines kuelekea Ethiopia ikiwa imekabidhiwa Bendera ya Taifa na Naibu Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Amos Makalla. Twiga Stars yenye msafara wa watu 24 wakiwemo wachezaji, benchi la ufundi na viongozi itacheza na Ethiopia katika mechi ya kwanza ya raundi ya pili ya michuano ya mchujo kwa ajili ya Fainali za Nane za Kombe la Afrika kwa Wanawake (AWC) zitakazofanyika Novemba mwaka huu Equatorial Guinea. Mechi hiyo itafanyika Mei 27 mwaka huu kwenye Uwanja wa Addis Ababa wakati ile ya marudiano itachezwa Juni 16 mwaka huu kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Twiga Stars ikifanikiwa kuitoa Ethiopia itakuwa imepeta tiketi ya kwenda Equatorial Guinea. Wachezaji walioondoka na kikosi hicho ni Amina Ally, Asha Rashid (nahodha), Ester Chabruma, Ettoe Mlenzi, Evelyn Sekikubo, Fadhila Hamad, Fatuma Bashiri, Fatuma Khatib, Fatuma Mustafa, Fatuma Omari, Maimuna Said, Mwajuma Abdallah, Mwanahamisi Omari, Mwanaidi Tamba, Mwapewa Mtumwa, Rukia Hamis, Semeni Abeid na Zena Khamis. Kwa upande wa Benchi la Ufundi ni Charles Mkwasa (Kocha Mkuu), Nasra Mohamed (Kocha Msaidizi), Furaha Francis (Meneja wa Timu), Mwanahamisi Abdallah (Mtunza Vifaa) na Christina Luambano (Daktari wa Timu). Twiga Stars ambayo msafara wake unaongozwa na Mwenyekiti wa Chama cha Mpira wa Miguu kwa Wanawake Tanzania (TWFA) ambaye pia ni mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) itarejea nyumbani Mei 28 mwaka huu saa 6 mchana kwa ndege ya Ethiopian Airlines. Timu hiyo imeondoka ikiwa imemwagiwa posho toka serikalini na wadhamini wengine kama motisha ya kufanya vema katika mechio yao dhidi ya wahabeshi watakaoumana nao kesho Jumamosi. Katika hatua nyingine, Ligi ya Taifa inayoshirikisha mabingwa wa mikoa sasa itaanza Mei 27 mwaka huu badala ya Mei 26 mwaka huu kama ilivyokuwa imepangwa awali. Uamuzi wa kusogeza mbele kwa siku kuanza kwa ligi hiyo uliofanywa na Kamati ya Mashindano ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) iliyokutana jana (Mei 23 mwaka huu). Timu 23 zitachuana katika kinyang’anyiro hicho kitakachofanyika katika vituo vya Kigoma (Uwanja wa Lake Tanganyika), Musoma (Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume) na Mtwara (Uwanja wa Umoja) ambapo kinatarajia kumalizika Juni 13 mwaka huu. Kituo cha Kigoma kina timu za Aston Villa ya Singida, Bandari (Kagera), CDA (Dodoma), JKT Kanembwa (Kigoma), Majimaji (Tabora), Mwadui (Shinyanga) na Pamba (Mwanza). Ashanti United ya Ilala, Flamingo (Arusha), Forest (Kilimanjaro), Korogwe United (Tanga), Nangwa VTC (Manyara), Polisi (Mara), Red Coast (Kinondoni) na Tessema ya Temeke ziko kituo cha Musoma. Kituo cha Mtwara kina timu za Kurugenzi ya Iringa, Lindi SC (Lindi), Mighty Elephant (Ruvuma), Mkamba Rangers (Morogoro), Mpanda Stars (Rukwa), Ndanda (Mtwara), Super Star (Pwani) na Tenende (Mbeya)

Nchunga aachia ngazi baada ya 'kutishwa'

Mwenyekiti wa Yanga, Lloyd Nchunga akisoma taarifa yake mbele ya waandishi wa Habari (hawapo pichani)jana jijini Dar, kutangaza kujiuzulu uongozi ndani ya klabu ya Yanga. MWENYEKITI wa Yanga, Wakili Lloyd Baharagu Nchunga ametangaza kujiuzulu wadhifa wake jioni hii ofisini kwake, jengo la NSSF, barabara ya Bibi Biti, Dar es Salaam, siku moja baada ya kuvamiwa na kundi la watu nyumbani kwake, Mbezi, Jijini usiku wa wa manane. Hata hivyo, Nchunga amekataa kulihusisha tukio la kuvamiwa kwake usiku wa juzi na kujiuzulu kwake, akisema kwamba amefikia uamuzi huo kuinusuru Yanga, kwa sababu wapo watu wako tayari Yanga ife, lakini wamng'oe yeye madarakani, kitu ambacho yeye hapendi kitokee. Nchunga alisema kwamba majira ya saa nane usiku wa jana, alivamiwa na kundi la watu takribani 15, lakini hawakufanikiwa kufanya chochote kutokana na ulinzi mkali uliopo katika nnyumba hiyo. "Kwanza mbwa walianza kubweka, walinzi wakashituka wakaomba msaada kwa walinzi wenzao, nasi tukapuga simu polisi, wakaja haraka sana na kukuta watu hao wamekwishakimbia,"alisema ISOME TAARIFA RASMI YA KUJIUZULU KWA NCHUNGA: LLOYD NCHUNGA BIHARAGU C/O LLOYD ADVOCATES, Morogoro/Bibi TIti Mohamed Rd,7th Floor, J.K. Nyerere Pension towers P.BOX 75111, Dar-Es- Salaam,Tanzania. TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI KUHUSU KUJIUZULU NAFASI YA UENYEKITI WA KLAB YA YANGA. Ndugu wana Habari, najua kwamba taarifa hii itawafedhehesha wajumbe na wanayanga wanaotuunga mkono,hasa ukizingatia maamuzi ya pamoja ya vikao vyetu vya kamati ya utendaji vilivyopita kwamba hakuna wa kujiuzulu kati yetu mpaka tujue hatma ya mkutano mkuu ambao tulipanga ufanyike tarehe 15 Julai 2012, ukiachia mbali shinikizo la kujiuzulu linalotolewa na baadhi ya wazee na wanaojiita vijana wa klab, kwa wajumbe wa kamati ya utendaji, na hasa mimi kama mwenyekiti. Nawashukuru wajumbe kwamba tulifanya kazi kwa pamoja na kwa ushirikiano mzuri, na hata pale tulipotofautiana tulifanya hivyo kwa hoja na kufikia maazimio ambayo wote tulikuwa tunawajibika nayo. Tangu tumeingia madarakani tumeweza kushirikiana na kupata mataji matatu katika kipindi cha mwaka mmoja, yaani; Ngao ya Hisani 2010, Ubingwa wa ligi kuu ya Vodacom 2010/2011, na Ubingwa wa Afrika Mashariki na Kati (Kagame Cup), 2011. Zaidi ni kwamba tuliuwa uteja kwa watani wetu wa jadi kila tulipokutana katika ligi ukiachia mbali mechi ya tarehe 6 Mei 2012, ambayo tulifungwa goli 5 bila, na kuleta mtafaruku mkubwa katika klab yetu. Hali kadhalika tumeshirikiana mpaka tumeweza kuboresha mkataba kati yetu na TBL kupitia Kilimanjaro Premium Lager, tumeingia mkataba na kampuni ya NEDCO kuendeleza mali zetu katika mtaa wa mafia na uwanja wetu wa KAUNDA baada ya kufikia hatua nzuri katika kupata hati miliki za maeneo yote mawili. Nafahamu kwamba kampuni hiyo iko katika hatua za mwisho za kumalizia michoro. Hali kadhalika tuliingia mkataba wa kuzalisha na kuuza bidhaa zenye nembo yetu na hasa baada ya kufanya marekebisho yatokanayo na matakwa ya sheria kule BRELA na pia mkataba na kampuni ya NEXUS LTD, ambayo itakuwa inatutafutia wadhamini wa nje na ndani, kufanya promosheni zetu na kampeni kwa njia ya electronic kupitia mitandao mbalimbali na kukusanya data za wanachama na kusajili wapya tukiwa na malengo ya kukusanya shilingi 300,000,000/= hadi 800,000,000/= kwa mwaka katika kipindi cha miaka mitatu. Haya yote tuliyafanya tukilenga kujitegemea kujazia mapengo yaliyokuwa yakitokana na kutegemea ufadhili wa mtu mmoja mmoja. Kwa ridhaa yenu tumekua tukiendelea na mazungumzo na makampuni mbali mbali kwa ajili ya udhamini na kwa sababu maalum, nitazitaja katika hati ya makabidhiano kwa kiongozi ajaye. Aidha, tumeshirikiana katika kufanya mambo mbali mbali ya kijamii, ikiwa ni pamoja na sikukuu ya kuadhimisha miaka 77 ya Yanga, sikukuu za pasaka, kuchangia jamii na waliokumbwa na maafa, na kongamano la vijana lililolenga kuwaamsha vijana kuitambua nafasi yao katika Yanga ikiwa ni pamoja na kupata azimio la kuanzisha SACCOSS ya Yanga, ambapo maombi yapo kwa msajili Manispaa ya Ilala. Haya yote nayataja ikiwa ni kuwashukuru kwa ushirikiano na ikiwezekana muweze kuyakamilisha yaliyobaki ambayo mtaona yalikuwa mazuri. Lakini pia tulipopata matatizo tulikuwa pamoja. Nichelee kusema tu kwamba tulisimama pamoja baada ya kujiuzulu Makamu Mwenyekiti wetu Ndugu Davis Mosha na mjumbe wetu ndugu Seif A. Seif, Ali Mayayi, na wengineo, kwani tulifungwa na katiba.Tulisimama pamoja pia katika suala la kujiuzulu ndugu Yusuf M. Manji, aliyekuwa mdhamini mteule na mfadhili mkuu ambaye sasa ameonyesha nia ya kurudi nanyi mkaridhia mkutane naye. Awali, tulitumia kila jitihada za kumrejesha lakini ikashindikana. Hata hivyo doa limetupata baada ya kufungwa na watani wetu goli 5 bila, ambapo kuna wanachama wanaoelewa na wasioelewa kabisa. Ninachokiona mimi ni usaliti wa hali ya juu uliombatana na matukio mbalimbali yaliyopita na yanayoendelea hadi kujaribu kupindua uongozi wa halali wa kidemokrasia. SIWATUHUMU WACHEZAJI MOJA KWA MOJA, isipokuwa mfululizo wa matukio wiki tatu kabla ya mchezo ule na sasa, inaonyesha kwamba kulikuwa na usaliti mkubwa ambao sisi hatukuweza kuubaini mapema. Sioni mantiki katika hoja kwamba wachezaji walikuwa wakidai mishahara, posho n.k. Au ati mtendaji wetu alishikiliwa Arusha kwa deni la hoteli, ndiyo tuvune bao 5! Kwa wanaoijua Yanga, imewahi kuwa na madeni makubwa katika Hoteli mbali mbali, mawakala wa ndege n.k, na baadhi tumeyakuta na sisi tumekuja tukayalipa. Hii imewahi kutokea kabla na wakati akiwepo mfadhili, sembuse sisi tulioachwa baki, na bado wachezaji walicheza kwa morali. Hata hivyo, utamaduni wa kutimuana baada ya matokeo mabaya ni dhambi ambayo itatula kama hatutaiacha, kwani wenye hila na uchu wa madaraka wataendelea kutumia mbinu hiyo ili kuuondoa uongozi wa kidemokrasia. Baada ya mapinduzi kushindikana na TFF kuonya kuhusu mapinduzi hayo, wazee kupitia msemaji wao , Mzee Akilimali wamesikika katika kipindi cha Michezo cha Redio moja maarufu hapa nchini wakidai kwamba ni bora Yanga ishushwe daraja au kufungiwa kuliko mimi kuendelea kuongoza! Hii imenikumbusha HEKMA ZA MFALME SELEMANI akiamulia ugomvi wa wanawake wawili waliokuwa wakigombea mtoto naye akaamuru wamgawane nusu kwa nusu. Yule mwenye mtoto kweli alimuomba Mfalme amuachie mwenzie kuliko kumkata nusu. Kwa hekma hiyo nimeamua kujiuzulu nafasi yangu katika Uenyekiti wa Yanga kwani ni klab ninayoipenda hata kama sio kiongozi kwa mujibu wa ibara ya 28 ya katiba yetu. Vile vile siko tayari kuona klab yangu ikisalitiwa au kuhujumiwa eti kwa sababu tu mimi ni kiongozi. Natumaini kamati ya utendaji kwa pamoja na wale tuliowateua chini ya ibara ya 29(3) ya katiba ya Yanga pamoja na bodi ya wadhamini, itawaongoza wanachama mpaka kufikia mkutano mkuu kwa mafanikio zaidi. Nitaendelea kuwa mwanachama mwadilifu na nitatoa mchango wangu wa hali na mali pale nitakapo hitajika na nikiwa na uwezo wa kufanya hivyo. YANGA DAIMA MBELE, NYUMA MWIKO. Wasalaam, LLOYD NCHUNGA BIHARAGU. Nakala kwa:- Mama Fatma Karume,Mdhamini Francis Kifukwe, Mdhamini Bwana Yusuf Manji – Kwa taarifa

Wednesday, May 23, 2012

Msondo Ngoma kupeleka mpya Masasi, ikienda kuzindua ukumbi wa Emirates

BENDI kongwe ya muziki wa dansi ya Msondo Ngoma, inatarajiwa kuipeleka albamu yake mpya ya 'Suluhu' mjini Masasi, Mtwara watakapoenda kuzindua ukumbi mpya mjini humo. Msemaji wa Msondo, Rajabu Mhamila 'Super D' alisema bendi yao itaenda kuzindua ukumbi huo uitwao Emirates, siku ya Juni 2 ambapo watatumia nafasi hiyo kutambulisha albamu hiyo mpya na nyimbo zao za zamani. Super D, alisema Msondo imepewa fursa hiyo ya kwenda kuzindua na kutumbuiza ukumbini hapo baada ya maombi ya mashabiki wao wa Masasi kuililia bendi hiyo iende kuwapa burudani. Alisema, msafara wao utaongozwa na mkongwe Muhidini Gurumo 'Kamanda' aliyerejea upya kupanda jukwaani baada ya kitambo kirefu kusumbuliwa na maradhi. "Kamanda Gurumo ndiye atakayeongoza jahazi sambamba na Dokta Said Mabela ambapo tutatambulisha albamu yetu kwa mashabiki hao wa Masasi, sawi na kukumbushia vibao vyetu vya zamani," alisema. Albamu hiyo ya Msondo Ngoma ina nyimbo sita ambazo ni 'Suluhu', 'Lipi Jema', 'Dawa ya Deni', 'Baba Kibene' 'Nadhiri ya Mapenzi' na 'Kwa Mjomba Hakuna Urithi'. Mwisho

Twiga kupaa kesho Ethiopia

Timu ya soka ya Taifa ya wanawake 'Twiga Stars' inatarajia kuondoka nchini kesho Mei 24 kwa ndege ya Ethiopian Airlines kwenda Addis Ababa kwa ajili ya mechi ya mchujo ya Fainali za Afrika kwa Wanawake (AWC) dhidi ya Ethiopia. Pambano baina ya timu hizo mbili linatarajiwa kuchezwa Mei 27 mwaka huu mjini Addis Ababa. Kwa mujibu wa taarifa toka TFF, msafara wa Twiga Stars utakuwa na watu 25 wakiwemo wachezaji, benchi la ufundi na viongozi. Mwenyekiti wa Chama cha Mpira wa Miguu wa Wanawake Tanzania (TWFA) ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Lina Kessy ndiye atakayeongoza msafara huo. Twiga Stars itarejea nyumbani Mei 28 mwaka huu kusubiri mechi ya marudiano itakayochezwa Juni 16 mwaka huu Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Mshindi ndiye atakayepata tiketi ya kucheza Fainali za Nane za AWC zitakazochezwa Novemba mwaka huu nchini Equatorial Guinea.

Joto la usajili laanza kuwachoma nyota, Simba, Yanga Azam

JOTO la usajili wa klabu kwa ajili ya msimu ujao, limeanza kuwaunguza baadhi ya nyota wa Simba na Yanga kutokana na taarifa za kuonyeshwa milango ya kutokea, huku Coastal Union ikitangaza kuwatema washambuliaji wake, Ben Mwalala na Ally Ahmed 'Shiboli'. Japo viongozi wa Simba na Yanga wamekuwa wasiri wa panga wanalotarajia kutembeza kwa baadhji ya wachezaji wake, lakini taarifa tulizonazo ni kwamba kuna wachezaji sita wa Simba na 15 wa Yanga wataonyeshwa mlango wa kutimka katika klabu hizo. Wachezaji hao ni wale ambao walishindwa kuonyesha makali yao katika msimu huu kutokana na kuwa majeruhi au kukosa nafasi katika vikosi vya kwanza vya timu hizo mbili. Taaifa hizo zinasema kuwa wachezaji ambao bado wana mikataba na klabu hizo watapelekwa kwa mikopo mahali pengine na wale ambao mikataba yao inaisha wameshajitambua hawana chao na kuanza kutafuta mahali pa kukimbilia kabla ya kutupiwa virago vyao. Hata hivyo Coastal wenyewe wameshaweka bayana wachezaji iliyoachana nao wakiwemo Mwalala na Shiboli, kama mikakati yao ya kuimarisha kikosi chao. Azam wenyewe wamekuwa wakisisitiza kupitia viongozi wao kwamba wanamsubiri kocha wao mkuu, Stewart John Hall arejee toka mapumziko aje kukipangua kikosi chao. Hata hivyo mpaka sasa wameshawanyakua wachezaji wawili ambao ni kipa Deogratius Munishi 'Dida' na George Odhiambo 'Black Berry' kutoka Kenya.

Samata, Ulimwengu waiongezea nguvu Stars

Washambuliaji Mbwana Samata na Thomas Ulimwengu wanaocheza mpira wa kulipwa katika klabu ya TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC) wamejiunga na kambi ya timu ya Taifa (Taifa Stars) juzi. Wachezaji hao ambao ndiyo pekee kutoka nje walioitwa na Kocha Kim Poulsen kwa ajili ya mechi ya mchujo ya Kombe la Dunia Kanda ya Afrika dhidi ya Ivory Coast itakayochezwa Juni 2 mwaka huu jijini Abidjan waliwasili juzi saa 1.30 usiku kwa ndege ya Kenya Airways. Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager inaendelea na mazoezi jijini Dar es Salaam kwenye viwanja vya Karume na Taifa itacheza mechi ya kirafiki Mei 26 mwaka huu dhidi ya Malawi. Mechi hiyo itafanyika Uwanja wa Taifa, na Malawi itawasili nchini Mei 24 mwaka huu. Baadaye Malawi itakwenda Zanzibar kwa ajili ya mechi ya kirafiki dhidi ya Zanzibar Heroes itakayofanyika Mei 28 mwaka huu kabla ya kuondoka Mei 30 mwaka huu kwenda Uganda ambapo Juni 2 mwaka huu itcheza mechi ya mchujo ya Kombe la Dunia Kanda ya Afrika. Katika hatua nyingine, kiungo wa timu hiyo, Nurdin Bakar atalikosa pambano la kirafiki dhidi la Malawi kutokana na kuchanika nyama ya paja hali inayomfanya awe nje kwa wiki moja kabla ya kurejea tena dimbani. Bakari, alipata majeraha hayo katika mazoezi ya timu hiyo inayoendelea kujivua kwenye viwanja vya Karume, Ilala Dar es Salaam.

Azam yapewa 'shavu' Kagame Cup

WASHINDI wa pili wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, Azam FC watashiriki michuano ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, maarufu kama Kombe la Kagame Julai, mwaka huu, Dar es Salaam, imeelezwa. Kuingia kwa Azam kwenye michuano hiyo, iliyofanyika kwa mara ya kwanza mwaka 1974, kunamaanisha Tanzania Bara, wenyeji watawakilishwa na timu tatu, nyingine zikiwa ni mabingwa watetezi wa Kombe hilo, Yanga na mabingwa wa Ligi Kuu, Simba SC. Katibu Mkuu wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Angetile Osiah alisema jana mjini Dar es Salaam kwamba maandalizi ya michuano hiyo, yanaendelea vizuri na tayari wadhamini wamekwishapatikana na watatangazwa katika Mkutano maalum hivi karibuni. Azam inayoshikilia pia taji la Kombe la Mapinduzi, itakuwa ni mara yao ya kwanza kushiriki michuano hiyo mikubwa kwa ngazi ya klabu kwa ukanda wa Afrika Mashariki na Kati. Timu nyingine za Tanzania Bara zitakazoshiriki michuano hiyo ni mabingwa watetezi wa taji hilo, Yanga na mabingwa wapya wa Tanzania, Simba.

Tuesday, May 22, 2012

Ramadhani Singano: Messi wa Simba anayemzimia Boban

<
KIPAJI kikubwa cha soka alichonacho hasa kumiliki mpira, kupiga chenga, mbio na kufunga, kimemfanya kinda la timu ya Simba, Ramadhani Singano kufananishwa na nyota wa Barcelona, Lionel Messi. Wadau wa soka hasa wa klabu ya Simba humfahamu zaidi kwa jina la Messi kuliko majina yake halisi, wakimlinganisha kiuchezaji na nyota huyo wa Argentina anayetajwa kama mwenye kipaji cha pekee duniani. Licha ya kufurahia jina hilo, Singano anakiri hajafikia hata robo ya umahiri wa Messi anayemhusudu na kumuiga uchezaji wake. Singano, aliyewapoteza wazazi wake akiwa na miaka 11, alisema anamshukuru Mungu kwa kumjalia kipaji hicho, ila anaamini ana kazi kubwa ya kufika alipo 'wajina' wake. Hata hivyo, Messi aliyeanza kucheza kama beki enzi za soka la chandimu, alisema nidhamu, mazoezi, kujituma na kumtumainia Mungu kutamfikisha mbali kisoka. "Naamini nikijituma zaidi, nikazingatia nidhamu na kumtanguliza Allah, katika kila kitu, nitafika mbali kwani najiamini naweza," alisema. Messi, alizichezea timu za Ubatani na Bombom kabla ya kuonwa na Simba B, alisema japo hana muda mrefu katika soka, anashukuru mafanikio aliyopata. "Soka limenisaidia mengi kimaisha na kiuchumi, ila sipendi yaandikwe, lakini kufahamika, kuheshimiwa na kumudu kuwasaidia ndugu na jamaa zangu, ni vitu vya kujivunia," alisema. Pia, alisema kutwaa mataji, medali na tuzo mbalimbali akiwa na Bombom na Simba B, ikiwemo kuwa Mchezaji Bora mara tatu katika michuano ya Rolling Stone, Uhai Cup na Copa Coca Cola 2009 ni mengine yanayomfariji. "Mwaka jana pekee nimetwaa mataji mawili ya Uhai na Kinesi nikiwa Simba B na msimu huu nimesherehekea ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara nikiwa na Simba," alisema. Messi, anayemzimia na kuvutiwa na soka la Haruna Moshi 'Boban', alisema hakuna tukio la furaha kwake kama alipochaguliwa kwa mara ya kwanza kuwa mchezaji bora wa michuano ya Uhai-2009. "Furaha niliyokuwa nayo ilinifanya nigawe fedha za zawadi kwa wachezaji wenzangu wa Simba B, nakumbuka nilitoa Sh. 150,000 kati ya 400,000," alisema. Kwa matukio ya huzuni, Messi alisema ni kuwapoteza wazazi akiwa mdogo na kunusurika kufa kwa ajali ya gari alipotoka kumzika baba yake mjini Tanga mwaka 2003. Mchezaji huyo anayependa kula mihogo ya kuchemsha, ugali kwa bamia na kunywa juisi ya Parachichi, alisema hupenda kutumia muda wake mwingi kufanya ibada na kuangalia 'muvi' hasa za filamu za Jean Claud van Damme. Aliwashukuru makocha wake, Ahmed Mohammed Kibonge, Teddy na Bosco waliokivumbua na kukiendeleza kipaji chake kiasi cha leo kuonekana 'lulu'. "Nawashukuru mno hasa Kibonge aliyetambua kipaji changu wakati anasoma Shule ya Sekondari Al Farouk na kunipeleka katika timu yake ya Bombom." Alisema, Simba B ilivutiwa naye baada ya kung'ara katika mechi dhidi ya Bombom na kusajiliwa katika kikosi hicho mwaka 2009 na kuja kupandishwa timu ya wakubwa msimu huu akiwa na wenzake wanne. Messi, anayemudu karibu nafasi zote dimbani, japo hufarahia kucheza kama mshambuliaji, alisema hawezi kuzisahau mechi mbili akiwa na Simba dhidi ya Azam na Kiyovu Sport ya Rwanda katika Kombe la Shirikisho Afrika. "Nazikumbuka kwa vile zilizokuwa mechi kubwa za kwanza kwangu na namna nilivyoonyesha kiwango cha hali ya juu nikisaidia moja ya mabao mawili ya ushindi dhidi ya Azam katika Ligi Kuu," alisema. Mkali huyo anayeota kucheza soka la kulipwa nje ya nchi na kuanzisha asasi ya kusaidia yatima na wenye matatizo, alisema soka la Bongo lipo juu, ila baadhi ya wachezaji hawajitambui na kuchangia kulikwamisha. Alisema huenda kukosa misingi bora ya soka ni tatizo kwa wachezaji nchini, ila aliwataka wazinduke na kutambua soka ni ajira yao hivyo walitumikie kwa ufanisi ili wafike mbali kama nyota wa mataifa mengine ni tatizo. Pia, alidai tabia ya wadau kuwaingilia kazi makocha na kuwakatisha tamaa wachezaji ni tatizo jingine, sawa na kukosekana kwa wadhamini katika soka la vijana. Alisema angekutana na Rais, licha ya kumuomba aboreshe miundo mbinu na huduma za jamii, angemsihi pia atumie nafasi yake kushawishi wawekezaji na wafadhili kuangalia soka la vijana na timu nyingine ndogondogo. Ila yeye angelikuwa ni Rais, angeboresha huduma za jamii hasa elimu na kuwekeza katika michezo akidai ni njia nzuri ya kusaidia ajira kwa wengi. Kuhusu Stars, alisema timu hiyo inashindwa kufanya vema kutokana na tabia ya u-Simba na u-Yanga inayoendekezwa na wadau wakiwemo hata wachezaji, pia kuingiliwa kazi kwa makocha wa timu hiyo. "Tunaweza kufuzu fainali za Afrika na Dunia, kama wadau wataacha u-simba na u-yanga unaowaathiri hata wachezaji, pia makocha waachiwe wafanye kazi na timu ziandaliwe vema," alisema. Shabiki huyo wa Manchester United anayechizishwa na nguo za rangi yoyote, alisema anaamini kila mmoja akitimiza wajibu wake katika klabu au timu ya taifa, Tanzania zitaweza kutamba kimataifa. Ramadhani Yahya Singano, alizaliwa Desemba 31, 1992 akiwa ni mtoto wa mwisho wa familia ya watoto sita wa Yahya Singano mwenyeji wa Tanga akitanguliwa na kaka wanne na dada mmoja. Shule ya Msingi alisoma Mgulani kati ya mwaka 2000-2006 kabla ya kusoma kama yatima katika Shule ya Sekondari Al Farouk alipozidi kung'ara katika soka baada ya awali kuanza kucheza akiwa darasa la nne. Chandimu alilichezea timu ya G Spar Kavela, kabla ya kutua Ubatani akicheza nao michuano ya mchangani kisha kusajiliwa Bombom na baade Simba B. Kwa upande wa timu za taifa, alianza kuchezea timu za vijana U17 na U20 tangu 2010 kabla ya wiki iliyopita kuitwa Taifa Staras na kocha Kim Poulsen. --------------------

Doyi Moke: Kipa wa zamani aliyejitosa kwenye biashara ya madini

TANGU alipostaafu baada ya kucheza kwa mafanikio makubwa, kipa wa zamani wa timu za Majimaji ya Songea, Simba na Yanga, Doyi Moke, amewekeza nguvu zake katika biashara za kununua na kuuza madini katika nchi za Afrika. Nyota huyo aliyeibebesha taji la ubingwa wa Ligi ya Muungano, Majimaji mwaka 1997, alisema amejikita katika shughuli hiyo kwa fedha za soka. Alisema japo soka halikumpa fedha nyingi, lakini kidogo alichopata aliweka akiba inayomfanya leo aishi maisha mazuri akifanya biashara hiyo ya madini akishirikiana na nduguze. Moke, mzaliwa wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, aliyeanza kucheza soka tangu Shule ya Msingi na kucheza soka la kulipwa akiwa na miaka 17 tu katika timu ya Muungano ya Bukavu, anauza madini chini ya kampuni yake. Kampuni hiyo inaitwa GFK Limited, yeye akiwa ndiye Mkurugenzi akinunua madini kama almasi na dhahabu toka Kongo na kuuza Tanzania na nchi nyingine za Afrika na kumfanya awe mtu wa kusafiri. Moke alisema kabla ya kufanya biashara hiyo alijikita katika biashara nyingine mara alipotundika daluga mwaka 2003 hata hivyo hazikumlipa kama biashara yake ya sasa. Mkali huyo aliyewahi kuwika pia na timu za Aspwara, Rayon za Rwanda na Afya Sport ya Goma, alisema ni vema wachezaji wa sasa wakawa makini na kile wanazovuna katika soka kwa ajili ya manufaa ya ya baadae. "Tulipokuwa tukicheza fedha hazikuwepo kama leo, hata hivyo baadhi yetu tulikuwa na fikra za mbali ndio maana leo tunaishi vema, kwa wanaocheza sasa ni wajibu wao kukumbuka kesho yao kwa kujiwekea akiba," alisema. ALIPOTOKA Doyi Moke alizaliwa Oktoba 4, 1967 Bukavu nchini Zaire, sasa Kongo akiwa ni mtoto wa sita kati ya 10 wa familia yao. Shule ya Msingi aliisoma College Alfajiri kisha Atenend Banda Sec kabla ya kusomea Diploma ya Lugha ya Kifaransa. Kisoka alianza kucheza tangu kinda akidakia timu za shule na kutwaa nao mataji ya mashindano ya shule nchini mwao, akimtaja kocha Gabie Mugimbi kuwa ndiye aliyekivumbua kipaji chake. Moke alikiri alimvutiwa kisoka na nyota wa zamani wa Ufaransa Michel Platin na kuitaja klabu yake ya kwanza ya kulipwa kuwa ni Muungano aliotwaa nao taji la Ligi ya Mkoa wa Bukavu mwaka 1987. Baada ya kung'ara na timu hiyo kocha wa zamani wa Yanga, Raoul Shungu alimuona na kumpeleka Rwanda kuichezea ASPWARA 1989 kabla ya kutua Rayon Sport kwa muda na kurudi Kongo kuichezea Afya ya Goma. Alitua baadae Vital'O ya Burundi na kufanya mambo makubwa akiwapiku makipa wanne aliowakuta kikosi ikiwemo mmoja, Ramadhani Ally aliyemsusia jezi alipopewa nafasi mara ya kwanza kikosini. Alisema anakumbuka kocha alimpa nafasi katika mechi dhidi ya wapinzani wao Port Louis walioifunga mabao 2-0 na kujihakikishia namba akiipa ubingwa na kucheza Ligi ya Mabingwa Afrika 1992. Alisema aliachana na Vital'O mwaka 1995 aliposhuhudia mchezaji mwenzake, Kamala Jeff akipigwa risasi na waasi wa Burundi mpakani mwa nchi hiyo na Kongo na kuamua kuachana na soka ili aende Afrika Kusini kusaka maisha. "Hata hivyo nilipofika Tanzania nikielekea 'Bondeni', nilikutana Mackenzie Ramadhani aliyenishawishi kuendelea na soka na kunikutanisha na kocha Nzoysaba Tauzany, aliyenisajili kuichezea timu yake ya Majimaji," alisema. Alisema hakuamini alipopokelewa kama 'Mfalme' mjini Songea na viongozi wa mkoa akiwemo RC, ambaye kwa sasa ni Spika wa Bunge, Anne Makinda akitaja dau alilosajiliwa likiwa Sh 700,000. Baada ya kuipa ubingwa wa Muungano kutokana na kumaliza Ligi ya Tanzania Bara wakiwa watatu nyuma ya Yanga na Simba, mwaka 1999 alihama na kutua Simba alioichezea kwa mafanikio kabla ya kusajiliwa Yanga. Alisema aliamua kuachana na Simba baada ya 'kuzikwa' fedha zake za usajili na mmoja wa viongozi (jina kapuni) na kuhamia Yanga mwishoni mwa mwaka 2000 na kuichezea hadi mwaka 2003 alipoenda Rayon Sport na kustaafu huko. Alisema tangu alipostaafu amekuwa mshauri kwa klabu ya Yanga na wachezaji wanaocheza sasa, pia akimpiga tafu shemejie, Henry Kalekwa anayemiliki timu ya Sofapaka ya Kenya. Moke anayependa kula wali kwa kisamvu na kunywa bia ya Safari, alisema kati ya klabu zote alizochezea, Vital'O na Yanga ndizo bomba kwake. Alisema mbali na kuichezea, pia yeye ni mshabiki mkubwa wa Yanga, Arsenal na TP Mazembe, huku akidai anapenda kuogelea na kubadilishana mawazo. HUJUMA Moke aliyemtaja Mbwana Samatta anayecheza TP Mazembe kama 'nembo' ya Tanzania katika soka la kulipwa kwa kipaji kikubwa alichonacho, alisema ndani ya soka amekumbana na mambo mengi. Alitaja mojawapo ni tuhuma alizodai kubambikiwa klabu ya Simba akidaiwa kuihujumu timu hiyo dhidi ya Yanga katika mechi iliyochezwa mwaka 2000 ambapo Yanga walishinda 2-0 kwa mabao ya 'Bwana Harusi' Idd Moshi. "Jambo hilo linaniuma hadi sasa na ndilo lililonifanya niichukie Simba kwa vile uongozi uliamua kunipakazia baada ya kuumbua kwa wanahabari juu ya kunizika fedha zangu za usajili," alisema. Juu ya mechi ngumu, Moke, alisema ni ile ya Ligi ya Mabingwa Afrika mwaka 2001 akiichezea Yanga na Highlander ya Zimbabwe lililochezwa Harare ambapo Yanga ilishakata tamaa baada ya kutoka sare ya mabao 2-2 nyumbani. "Naikumbuka kwa namna nilivyowaapia wanayanga waliokata tamaa na kutishwa na kauli ya kocha wa Highlander aliyetutaka tusisumbuke kuwafuata kwao kwa maana tulikuwa tunajisumbua tu," alisema. Alisema hata hivyo aliwapa moyo wenzake na kwenda kufanya vitu adiumu uwanjani na kuisaidia Yanga kushinda mabao 2-0 na kusonga mbele. Moke aliyemhofia Mohammed Husseni 'Mmachinga', alisema soka la Bongo, litasonga mbele iwapo nyota wa zamani watapewa nafasi za kuongoza klabu na FA badala ya 'wavamizi' wanaotambia elimu zao kubwa. Alisema wengi wa viongozi waliojipenyeza kwenye soka wanafanya hivyo kwa kusaka masilahi ikiwemo umaarufu wa kugombea nafasi za kisiasa, huku wakiliacha soka likiporomoka. "Ni kweli elimu ni kitu cha muhimu, ila wachezaji wa zamani wana umuhimu katika kuinua soka la Tanzania, watumiwe kama wenzetu wanavyowatumia wachezaji wao," alisema. Moke anayesikitishwa na kifo cha baba yake kilichotokea akiwa na miaka 13 tu, ameoa na ana watoto wawili, pia aliwashukuru mama yake mzazi kwa jinsi alivyomlea na kumuongoza hadi kufika alipo, sambamba na Rashid Haradee na marehemu Tauzany. Aliwaasa wachezaji kujituma na kutambua soka ni ajira lao, sambamba na kuzipigania klabu na timu za taifa pale wanapozichezea ili kuzisaidia na kujitangaza vema kimataifa. --------------------

Stanley Msungu: 'Seneta' anayemzimia Ramsey Nouah

INGAWA filamu ya 'Second Wife', aliyoigiza na 'Ray' ndio inayoonekana kama iliyomtambulisha kwa mashabiki, ukweli ni kwamba msanii Stanley Msungu, alishaanza kuonyesha makeke yake kitambo kirefu katika fani hiyo ya uigizaji. Msanii huyo anayefahamika kisanii kama 'Seneta Msungu', tangu akiwa shuleni alikuwa mahiri katika fani hiyo sambamba na uchezaji wa ngoma na uimbaji na alishauza sura katika michezo kadhaa ya runinga kupitia kituo cvha ITV akiwa na kundi la Amka Sanaa. Miongoni mwa michezo hiyo iliyodhihirisha kipaji cha msanii huyo ambaye pia ni mahiri katika muziki akiwa ameshafyatua nyimbo tatu mpaka sasa ili kutoa albamu kamili ni pamoja na 'Lulu', 'Safina' na 'Dunia'. Mwenyewe alisema michezo hiyo ilimpa uzoefu wa kutosha katika uigizaji na haikuwa ajabu kwake kuamua kujiengua katika kundi hilo na kutumbukia kwenye uigizaji za filamu kazi yake ya awali kabisa ikiwa ni Last Minutes iliyotoka miaka minne iliyopita. "Baada ya kujiona nimeiva na hali ilivyokuwa katika kundi letu, niliamua kujiengua na kujitosa kwenye filamu na kazi ya kwanza kucheza ni Last Minutes kabla ya kufungukiwa neema kwa kucheza filamu zinazokaribia 30 kwa sasa," alisema. Msungu, aliyetumbukia kwenye uigizaji kutokana na kuvutiwa na Ramsey Noauh wa Nigeria, alisema baada ya Last Minutes, alicheza filamu za Peace of Mind, Devorce, Devil's Kingdom, Moses, Ndoa Yangu, I Hate My Birthday, The Shell, Shortcut na sasa akitamba na Rude, moja ya kazi binafsi za mwanadada Jenifer Kyaka 'Odama'. Mkali huyo, aliyewahi kung'ara katika soka akiichezea timu yake ya shule na zile mtaani, alisema kati ya kazi zote alizocheza, filamu za Moses, Devil's Kingdom aliyoigiza na marehemu Steven Kanumba na Ramsey Nouah, Rude na Second Wife ndizo kali kwake. Alisema wakati alipoitwa kwenda kucheza filamu ya Devil's Kingdom alikaribia kuzimia kutokana na kushindwa kuamini kama angeigiza na Ramsey Nouah anayemhusudu mno. "Sio siri Kanumba ni kama alinifanyia 'surprise' kwa kunipa taarifa ya ghafla kwenda kuigiza na hata nilipofika na kuonana uso kwa uso na Ramsey sikuamini. Kwa kweli namzimia mno huyu jamaa na anaweza kazi," alisema. KIFO Msungu, aliyezaliwa mwaka 1979 wilayani Lushoto, mkoani Tanga akiwa mtoto wa kwanza kati ya sita wa familia yao, alisema wakati tukio la kukutana na Ramsey likiwa ni furaha kwake, kwa upande wa huzuni yapo mambo makuu mawili. Moja alisema kifo cha wazazi wake, na kunusurika kwake kuuwawa kwa risasi katika tukio la uhalifu lililowahi kutokea eneo la Kigamboni. Alisimulia, Msungu alisema alishawishiwa na rafiki zake aliokuwa akiwaonea wivu kwa namna walivyokuwa 'mambo safi' na kumueleza kama anaweza aungane nao kusaka fedha bila kujua kama walikuwa wezi. "Siku moja wananiambia niambatane nao kwenda kuvuna fedha na kuibukia TIPPER ambako kabla sijajua kilichoendelea tulijikuta tukivamiwa na kuwekwa chini ya ulinzi na askari wenye silaha. Kwa kweli nilitahayari mno," alisema. Alisema askari aliyemwelekezea silaha, alimwambia akisogea hatua moja tu, angemlipua risasi, lakini kwa ujasiri na kukata kwake tamaa, alimwambia askari yule kama ni risasi basi ampige ya kichwa ili afe mara moja. "Nilimweleza mie sikuwa mhalifu ila niliwafuata wenzangu bila kujua kama ni wezi, hivyo ni bora aniue kwa kunitwanga risasi ya kichwa badala ya kwingine nikihofia kuwapa tabu wadogo zangu niliokuwa nawatunza," alisema. Alisema aliyatamka hayo huku akitembea kuelekea baharini akiamini askari yile angemuua, cha ajabu alikuja kuzinduka keshoye akiwa majini alfajiri bila jeraha lolote ilihali mwanzoni aliamini alikuwa amekufa. Alidai tangu tukio hilo, alishika adabu na kuwaepuka rafiki zake hao na kuamua kuhangaika kwa kutumia vipaji vyake vya uigizaji na muziki. Msungu anayependa kula ugali kwa bamia au wali kwa njegere na kunywa juisi, alisema japo hajanufaika sana na sanaa, lakini anashukuru fani hiyo imemsaidia kwa mengi kimaisha. "Sina cha kujivunia, ila nashukuru sanaa imenisaidia kwa mengi na jinsi fani inavyozidi kukua naamini nitafika mbali kimaisha, na kutimiza ndoto za kuwa mtayarishaji na kumiliki kampuni binafsi ya filamu," alisema. MUZIKI Msungu, anayezishabikia timu za Yanga, Barcelona na Liverpool, akiwazimikia nyota wa timu hizo, Haruna Niyonzima, Lionel Messi na Luis Suarez, alisema baada ya kutamba kwenye filamu sasa amehamishia makali kwenye muziki. Alisema mpaka sasa amepakua nyimbo tatu, ya kwanza ikiendelea kutesa kwenye runinga unaoitwa 'Unanitesa' alioimba na Milan wa Bana Marquiz, 'Nalia' na mapema wiki hii alirekodi kibao kiitwacho 'Mikosi'. "Lengo langu kabla ya mwisho wa mwaka huu niwe nimeshatoa albamu kamili itakayokuwa na nyimbo nane za miondoko mchanganyiko ya Zouk na Kwaito," alisema. Alidokeza atakuwa akisambaza video za nyimbo hizo tu kabla ya kutoa 'audio' baadae ili kuepuka 'kuchakachuliwa' na baadhi ya wajanja wanaiba kazi za wasanii. Msungu anayewakubali waigizaji kama Sajuki, marehemu Kanumba, Ray, Gabo, Odama, Riyama Ally na Jackline Wolper, alisema ili wasanii wa Tanzania wafike mbali ni lazima wapendane, kushirikiana na kuwa wa moja. "Sio siri wasanii wengi nchini hatupendani na tunaendekeza majungu na unafiki vitu ambavyo sio vizuri kwa maendeleo ya sanaa zetu," alisema. Alisema, pia ni vema wasanii hasa watayarishaji na waigizaji wa filamu kuwa wabunifu kwa kutunga visa vinavyorandana na mazingira ya Tanzania. "Tubuni kazi zinazoendana na uhalisi wa maisha wa watanzania, pia serikali itusaidie na kuturuhusu kutumia maeneo yatakayoitangaza nchi," alisema. Alisema wasanii wanapotaka kuigiza katika maeneo yatakayotoa uhalisia wa simulizi la kazi zao, hupata usumbufu na kuchangia kazi nyingi kulipuliwa na kutokuwa na uhalisia wa mambo. Msungu aliyepania kuja kuwasaidia vijana wenye vipaji, alisema kuna haja pia ya serikali kusaidia kukomesha wizi wanaofanyiwa wasanii katika kazi zao, sambamba na kutazama sanaa kama eneo la kupatia pato la taifa. Mkali huyo anayechizishwa na nguo za rangi ya kahawia (brown), hajaoa ila ana watoto wawili ambao mmoja anasoma mjini Morogoro na mwingine Kigamboni anapoishi yeye. Mwisho

Bango la TFF kuhusu mapinduzi ya wazee wa Yanga

TAARIFA YA TFF KUHUSU MAPINDUZI YALIYOFANYIKA KATIKA KLABU YA YANGA SIKU YA JUMAPILI

Malawi njiani kuja kuivaa Stars

TIMU ya soka ya taifa ya Malawi inatarajia kuwasili nchini keshokutwa Alhamisi kwa ajili ya mechi ya kirafiki ya kimataifa dhidi ya wenyeji wao Taifa Stars itakayofanyika Jumamosi kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam. Katibu Mkuu wa Shirikisho la Soka Nchini (TFF), Angetile Osiah, alisema jana jijini kuwa kikosi hicho cha Malawi kinatarajia kuja na msafara wa watu 27 na maandalizi ya mechi hiyo yako kwenye hatua za mwisho. Osiah alisema kuwa wanaamini mechi hiyo ya Jumamosi itakuwa ni kipimo sahihi kwa wachezaji wa Taifa Stars ambao wanakabiliwa na mechi ya mchujo ya Kombe la Dunia hatua ya makundi dhidi ya Ivory Coast huko jijini Abdijan. Aliongeza kuwa wachezaji wa Taifa Stars walioko kambini wanaendelea na mazoezi chini ya kocha wao mpya, Kim Poulsen, na wote wanajua umuhimu wa mchezo huo wa kirafiki. "Tunafahamu Stars inakabiliwa na mechi ya ushindani, Malawi pia ni kipimo kizuri kwao, wenzetu wako juu katika viwango vya FIFA, ni mechi itakayotusaidia," aliongeza Osiah. Hata hivyo, wachezaji watatu kati ya 25 walioutwa Stars kwa sasa wanakosa kushiriki katika programu ya mazoezi inayoendelea ya kocha Kim Piulsen kutokana na kutokuwepo nchini. Wachezaji ambao hawako kambini ni pamoja na Mbwana Samatta, Thomas Ulimwengu, ambao watatua nchini Jumatatu Mei 27 wakitokea Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo wanakoichezea TP Mazembe huku mwingine akiwa ni Haruna Moshi 'Boban' ambaye alikwenda Kinshasa kumzika kiungo wa Simba, marehemu, Patrick Mafisango, aliyezikwa juzi. Katika mechi ya kwanza ya kuwania tiketi ya kucheza fainali hizo za Dunia zitakazofanyika Brazil mwaka 2014, Taifa Stars iliyokuwa chini ya kocha aliyemaliza mkataba wake, Jan Poulsen, ilitoka sare ya 1-1 kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam. Mechi hiyo ya Jumamosi ndio utakuwa mchezo wa kwanza kwa Kim kuiongoza Taifa Stars huku akiwa na matokeo mazuri na timu ya vijana ya umri chini ya miaka 20, Ngorongoro Heroes. Chanzo:NIPASHE

Sita Simba hatarini kupigwa panga

HATMA ya wachezaji sita wa mabingwa wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara, Simba ya jijini Dar es Salaam, iko shakani baada ya mikataba ya kuichezea klabu hiyo kumalizika huku kikao cha Kamati ya Usajili kilichofanyika juzi usiku kikishindwa kufikia maamuzi ya kuwapa mikataba mipya. Nyota hao ambao kanuni zinawaruhusu kufanya mazungumzo na klabu yoyote sasa ni pamoja na Ally Mustapha 'Barthez', Uhuru Suleiman, Juma Jabu, Juma Nyosso, Derick Walulya na Gervais Kago, ambaye ni kutoka Jamhuri ya Afrika ya Kati. Uhuru alithibisha kuwa hana mkataba na Simba hivi sasa na yoyote anayemuhitaji milango iko wazi kumfuata. "Ila Simba ni zaidi, wamenisaidia sana (wakati alipovunjika mguu) siwezi kuwasahau," alisema kiungo huyo. Hata hivyo, wachezaji Mganda Walulya na Kago tayari wameshatupiwa virago na msimu ujao hawatavaa jezi tena za klabu hiyo, habari hizo zilisema. "Kago si mbaya ila ameshindwa kuendana na mfumo unaotumika sasa katika timu yetu ila bado timu yake ya taifa (Jamhuri ya Afrika ya Kati) inamuhitaji, Walulya amekuwa mzito na anashindwa kumudu kasi ya washambuliaji anaowakaba," alisema mmoja wa viongozi wa kamati ya usajili. Kiongozi huyo alisema kuwa kamati inaendelea kufanyia kazi ushauri kutoka katika benchi la ufundi la timu hiyo ili kuziba nafasi zenye mapungufu na hatimaye kufanya vizuri kwenye mashindano ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati (Kombe la Kagame) yanayotarajiwa kufanyika hapa nchini kuanzia mwezi ujao. Aliwataja wachezaji wapya waliosajiliwa kuwa ni mshambuliaji Abdallah Juma kutoka JKT Ruvu, kiungo mmoja wa DC Motema Pembe huku pia Simba ikipanga kwenda Uganda kumfuata Mussa Mude ambaye pia anawaniwa na Azam na Santos ya Afrika Kusini. Kamati ya Usajili ya Simba inaongozwa na mwenyekiti wake, Hanspope Zacharia, ambaye Ijumaa iliyopita alitarajia kumsainisha marehemu Patrick Mafisango, lakini mipango hiyo haikutimia kufuatia ajali iliyotokea asubuhi ya siku hiyo na kuchukua uhai wa kiungo huyo mkabaji aliyekuwa na uraia wa Rwanda. Wachezaji nyota wengine waliobaki akiwemo Juma Kaseja, Emmanuel Okwi, Mwinyi Kazimoto, Shomary Kapombe, Kevin Yondani, Haruna Moshi 'Boban', Salum Machaku, Felix Sunzu, Nassor Masoud 'Chollo', Amir Maftah na yosso kutoka Simba B waliopandishwa wote mikataba yao bado haijaisha. Chanzo;NIPASHE

TFF yawagomea wanachama wa Yanga, yadai haitambuii mapinduzi yao dhidi ya Nchunga

SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF) limesema kuwa msimamo wake ni kuwa halitatambua maamuzi yoyote yanayofanywa na wanachama wake ambayo yako nje ya taratibu na maelekezo yaliyoainishwa katika katiba ya klabu hiyo. Kauli hiyo ya TFF imekuja kufuatia mkutano wa wanachama wa Yanga uliofanyika juzi Jumapili kwenye makao makuu ya klabu hiyo ambapo walitangaza kuwa wamemuondoa madarakani Mwenyekiti wa Klabu hiyo, Lloyd Nchunga, kwa madai kwamba ameshindwa kuwaongoza na anavunja katiba yao. Akizungumza jana jijini Dar es Salaam, Katibu Mkuu wa TFF, Angetile Osiah, alisema kuwa wanachama wote wanatakiwa kuheshimu na kulinda katiba za klabu yao na hawana budi kufuata katiba hizo katika kufanya mabadiliko ya uongozi endapo wana sababu ya kutekeleza maamuzi hayo. Osiah alisema kuwa hakuna mwanachama (klabu au vyama vya michezo) ambaye atafanya mabadiliko bila kufuata katiba na mabadiliko hayo yakatambuliwa. "Wasivuke taratibu kuanzia chini halafu wakafikiri wakija huku kwetu tutawatambua, tunasisitiza kuwa msimamo wetu ni kutotambua uongozi ambao utateuliwa kwa muda, hiyo ni kwa mujibu wa ibara ya 12 (2) ya TFF inavyoeleza," alisema Katibu huyo. Aliwataka wanachama kuwa na subira na kuwaeleza kwamba hakuna katiba inayokataa mabadiliko ya uongozi na wafahamu kwamba hakuna matatizo au migogoro itakayotatuliwa nje ya katiba. Alieleza kuwa tayari shirikisho limeshakutana na viongozi wa Yanga na kuwaeleza kwamba wakutane na upande wa pili ili kumaliza matatizo yao kwa njia ya busara kwa lengo la kuhakikisha wanajipanga kusajili wachezaji wenye uwezo na kufanya maandalizi ya kutetea ubingwa wao wa mashindano ya Kombe la Kagame yanayotarajiwa kuanza Juni 23 hadi Julai 8 mwaka huu. Naye mwenyekiti wa Yanga, Llyod Nchunga, alikielezea kilichofanywa na wanachama wa Yanga waliokutana Jumapili si jambo sahihi na anaeleza kuwa mkutano huo ulikuwa ni kama 'sinema'. Mwenyekiti huyo aliendelea kusema kuwa wanachama wake wanatakiwa kuwa na subira endapo wanaitakia mafanikio klabu hiyo kongwe hapa Afrika Mashariki. Alisema kuwa Julai 15 sio mbali na Kamati yake ya Utendaji ilipanga siku hiyo kwa kuzingatia taratibu zilizoelezwa katika katiba yao kwa uongozi kuitisha Mkutano Mkuu. Aliongeza kuwa mkutano huo aliouitisha ni Mkutano Mkuu wa mwaka na agenda zake zimeelezwa katika Ibara ya 21 ya katiba ya Yanga. Aliwataka wanachama kuendelea na maandalizi ya kujitokeza katika mkutano huo aliouitisha huku akisema kwamba uongozi uko kwenye mchakato wa zoezi la usajili wa wachezaji na kusaka mrithi wa kocha Mserbia Kostadin Papic. Kwa mujibu wa katiba ya Yanga Ibara ya 17, Mkutano Mkuu ni ule tu ulioitishwa kwa kufuata utaratibu na ndio wenye mamlaka ya kufanya maamuzi. Na miongoni mamlaka ya mkutano huo kama yalivyoelezwa katika Ibara ya 19 kipengele cha (13) na (15), ni kubatilisha mamlaka ya mwanachama na pia kumsimamisha au kumfukuza mwanachama.

Mr Nice akamailisha albamu, atamba itamtoa

MSANII anayefurukuta kurejesha makali yake ya zamani, Lucas Mkenda 'Mr Nice' amekamilisha albamu yake mpya itakayofahamika kwa jina la 'Tabia Gani'. Albamu hiyo inatarajiwa kuingizwa sokoni muda wowote kuanzia sasa, itakuwa na nyimbo nane zilizoandaliwa chini ya mtayarishaji nyota, Lamar wa Fishcrab Records. Akizungumza na MICHARAZO, Mr Nice alisema albamu hiyo imekamilika na sasa wanafanya mipango ya kuiigiza sokoni baada ya kutambulishwa na vibao viwili vya 'Tabia Gani' na 'Nionje' alioimba na Muimbaji Bora wa Kiume nchini, Barnaba. Mr Nice alizitaja nyimbo zitakazokuwa katika albamu hiyo kuwa ni 'Tabia Gani' yenyewe, 'Nionje', 'Kupata', 'Maneno Maneno', 'Mfalme', 'Nionaje', 'Amini' na 'Ulisemaje'. "Kaka nimekamilisha ile albamu yangu mpya ya kunirejesha upya katika ulimwengu wa muziki baada ya kimya cha muda mrefu, itakuwa na nyimbo nane na kwa sasa najipanga na wasimamizi wangu ili kuiingiza sokoni," alisema. Mr Nice, alisema kwa namna albamu hiyo ilivyoandaliwa na Lamar, huenda akarejesha heshima na makali yake yaliyomfanya abatizwe jina la 'Mfalme wa TAKEU'. "Ni moja ya kazi yenye kiwango cha hali ya juu, si unajua makali ya Lamar na ukichanganya na vionjo vyangu vya 'TAKEU Reloaded', sina shaka itabamba sokoni," alisema. Mr Nice, aliyevuma miaka saba iliyopita na nyimbo matata kama 'Fagilia', 'Kikulacho', 'Friday Night', 'Bwana Shamba' na nyingine, ameibuka upya baada ya kushindwa kusimama hata alipojitosa kwenye muziki wa Injili alipotoa albamu ya 'Fungu la Kukosa'.

Viuno vya Shilole hadharani

NYOTA wa filamu aliyetumbukia kwenye fani ya muziki, Zuwena Mohammed 'Shilole' amefyatua wimbo mpya uitwao 'Viuno kwa Viuno' ameanza kuusambaza jana Jumatatu. Kisura huyo, alisema kibao hicho ambacho ni cha tatu kwake baada ya awali kuachia 'Lawama' na 'Dume Dada' vinavyokimbiza nchini kwasasa, ameshirikiana kuimba na wakali Kalidjo Kitokololo wa Fm Academia na Rich Mavoko. Shilole, alisema amepanga kuusambaza katika vituo mbalimbali vya redio leo ili uanze kuchezwa hewani, huku akijipanga kuachia nyimbo nyingine kwa ajili ya kuhitimisha albamu aliyopanga iwe na nyimbo sita au nane. "Nimekamilisha kibao kipya kiitwacho 'Viuno kwa Viuno ambao nadhani nitaanza kuusambaza redioni siku ya Jumatatu (jana ili uanze kurushwa hewani," alisema. Shilole, alisema anaamini kama ilivyokuwa kwa nyimbo zake mbili za awali, hata 'singo' hiyo itawabamba mashabiki kutokana na namna ulivyoandaliwa na kazi kubwa iliyofanywa nae na wasanii alioshirikiana nao. "Nataka kuwathibitishia mashabiki wangu, sijavamia fani, bali nauweza muziki kwa vile ni kipaji cha kuzaliwa licha ya kwamba naonekana ni mkali zaidi katika filamu," alisema. Mwanadada huyo, ambaye hujishughulisha na ujasiriamali, alisema mbali na kujipanga kutoa albamu pia anaendelea na maandalizi ya kupakua filamu zake binafsi.

Warembo Redd's Miss Bagamoyo waanza kambi Dar

WAREMBO 10 waliojitokeza kushiriki kinyang'anyiro cha kumsaka kisura wa Bagamoyo 'Redd's Miss Bagamoyo 2012', wameanza rasmi kambi ya mazoezi jijini Dar. Mkurugenzi wa Asilia Decoration inayoratibu shindano hilo, Awetu Salim, alisema warembo hao wameanza kambi katika ukumbi wa Meridian Hotel, iliyopo Kinondoni tayari kujiwinda na mchuano huo utakaofanyika Juni 15, mjini Bagamoyo, Pwani. Awetu, alisema kambi hilo ilianza Jumapili na itaendelea hadi siku ya shindano hilo litakalofanyika kwenye ukumbi wa Chuo cha Taifa cha Sanaa, TaSUBA- Bagamoyo. Mratibu huyo aliwataja baadhi ya warembo hao watakaokuwa chini ya mkufunzi wao Sadah Salim kuwa ni Julieth Jeremiah, Rose Lucas, Beatrice, Rachel, Celine Wangusu na Maria. Aliongeza, kwa kushukuru kujitokeza zaidi kwa wadhamini akiitaja kampuni ya Kishen Enterprises ilijitokeza hivi karibuni kuwapiga tafu katika shindano lao. Awetu, alisema wadhamini hao wapya wameungana na wale wa awali ambao baadhi ni Twanga Pepeta', Kiu Investment, Asilia Boutique & Hair Dressing, Dr Osborn na Dk Kalenga. Juu ya burudani itakaowasindikiza warembo hao, mratibu huyo aliitaja bendi ya African Stars 'Twanga Pepeta' ndio watakaotumbuiza ukumbini siku ya onyesho lao.

Kumekucha Miss Kurasini 2012

WAREMBO 16 wanatarajiwa kupanda katika jukwaa la ukumbi wa Equator Grill jijini Dar es Salaam Ijumaa ya May 25 katika shindano la kumsaka Miss Kurasini 2012. Mkurugenzi wa ZUM Fashion & entertainment,inayoandaa shindano hilo Zuwena Mustapha alisema jana kwamba maandalizi kwa ajili ya shindano hilo yanaendelea vema na kwamba mwaka huu wataendeleza historia ya kutoa mrembo bomba atakayetikisa hadi ngazi ya Taifa. Alisema mpaka sasa wameshapatikana wadhamini 14 kwa ajili ya kusaidia shindano hilo ambalo linatarajiwa kuwa bomba, huku likiambatana na burudani kabambe.Taji la kitongoji hicho linashikiliwa na Top Model wa Miss Tanzania 2011, Mwajabu Juma (pichani). “Leo napenda kuwaambia kuwa hadi sasa tunajumla ya wadhamini 14 ambao wamejitokeza kudhamini shindano hilo, lakini bado milango ipo wazi kwa yeyote anaependa kutuzamini na kusaidia warembo wetu wa kurasini kupata zawadi nono na shindano kuwea zuri,”alisema Mustapha. Mustapha alisema wadhamini wakuu wa shindano hilo ni Nameems Wear wakisaidiwa na kampuni ya bia Tanzania (TBL) kupitia bia ya Redds, Dodoma wine, Clouds FM, Lady Pepeta, Father Kidevu Blog, Jambo Leo, Aucland Tours & Safaris, Candy Bureau de Change, Flexip, PJ Amusement, Renzo Salon na Madishisha Video Production. Aliwataja warembo waliopo kambini na kunolewa na Mwajabu Juma akisaidiwa na Malkia wa vipaji wa Miss Tanzania 2011, Rose Hurbert ni Mariam Sadic (19), Johari Juma (20),Linda Deus (20),Irene Sostheness 20),Neemadoree Sylvery(29),Edna Magige (22), Lindanancy Joseph(20), Elizabeth Mkende (19), Betty Peter (22), Jennifer Njabili (18), Lilian Joseph (20), Farida Mrope (23),Christina Moses (20), Angle Gasper (19), Flaviana Maeda(22) na Sia Kimambo (19).

Monday, May 21, 2012

Matibabu ya Sajuki nchini India shakani, kisa...!

IMEELEZWA kwamba upungufu wa damu na kudhoofika mwili kupita kiasi kumemfanya mtayarishaji na mcheza filamu mashuhuri nchini, Salum Juma Kilowoko ‘Sajuki’, kushindwa kufanyiwa upasuaji mapema nchini India alikokwenda kwa matibabu. Sajuki ambaye aliondoka nchini Jumapili iliyopita na kufikia katika Hospitali ya Saifee iliyopo Mumbai, nchini India, anakopatiwa matibabu, ameanza kuongezewa damu na kupewa vyakula ambavyo vitaweza kuupa mwili wake nguvu ili kukabiliana na zoezi la upasuaji. Kwa mujibu wa rafiki wa karibu wa Sajuki, Denis Sweya ’Dino’ ambaye alizungumza na gazeti hili muda mfupi baada ya kuwasiliana na mke wa Sajuki, Wastara, alisema hali ya msanii huyo imezidi kutengemaa kila kukicha na kuwaomba Watanzania kumuombea zaidi kwa Mungu aweze kurudi haraka katika hali yake. Sajuki anasumbuliwa na tatizo la uvimbe pembeni ya ini, ambapo wataalamu wa afya wanadai kuwa ni dalili za ugonjwa wa Hepatoma (kansa ya ini). Taarifa za awali zinaeleza kwamba Sajuki alianza kwa kupata uvimbe sehemu tofauti katika mkono wake mmoja, lakini baadaye tatizo hilo lilihamia ndani na kuanza kupata maumivu makali pembeni ya ini. Katika mahojiano yake na gazeti moja la wiki, Sajuki alikaririwa akisema madaktari walibaini ana uvimbe pembeni ya ini tatizo ambalo limekuwa likinisumbua kwa muda mrefu. Kutokana na hali hiyo, wadau mbalimbali wa filamu wakiwemo wasanii waliweza kumchangia nyota huyo kiasi cha fedha ambacho alitakiwa kukipata ili kuweza kufanyiwa matibabu nje ya Tanzania. Tanzania Daima inamtakia kila la kheri Sajuki. CHANZO:TANZANIA DAIMA

Boban azuiwa Airport akimsafirisha Mafisango, kisa...!

Michael Momburi, Kinshasa SAFARI ya mwisho ya kiungo wa Simba, Patrick Mafisango kuonekana duniani, inakamilishwa leo wakati sanduku lenye mwili wake litakapoteremshwa kaburini baadaye jioni. Mafisango alifariki alfajii ya Alhamisi iliyopita baada ya gai lake kuacha njia na kuingia mtaroni. Alikuwa akitoka Maisha Club kurudi nyumbani. Kiungo huyo aliyeacha mke na watoto watatu, aliagwa juzi kwenye Viwanja vya Klabu ya Sigara, Chang'ombe Dar es Salaam. Msafara wa uliosindikiza mwili wa Mafisango ulitua jijini hapa jana saa 6.10 mchana na kulakiwana mashabiki wengi wa kike huku askari wa usalama ndani ya Uwanja wa Ndege wahapa wakishindwa kujizuia na kumwaga machozi. Mafisango atazikwa leo kwenye makaburi ya Kinkole yaliyoko karibu na Uwanja wa Ndege wa Kinshasa. Baada ya mwili wa mchezaji huyo kutua, askari wa uhamiaji pamoja na wahudumu wa afya wanaokagua kadi za chanjo kwa wasafiri ndani ya uwanja wa ndege walianza kuuliza kwamba ni nani huyo lakini walipoelezwa bado hawakuelewa kwa vile mchezaji huyo hakuwahi kutamba na timu yoyote ya Kinshasa. Kiungo wa DC Motema Pembe, Mussa Hassan Mgosi alikuwa miongoni mwa waombolezaji. Mkuu wa msafara wa Simba, Itang'are alipotoa nakala za magazeti ya Tanzania na kuwaonyesha waliacha kazi zao na kuuzingira mwili huo huku wanawake wakishindwa kujizuia nakuanza kumwaga machozi kwa jinsi walivyoona gari lake lilivyochakaa baada ya ajali hiyo. Askari hao walitumia takribani dakika 10 kuangalia jeneza la mchezaji huyo huku wengine wakikimbia ofisi zao na kwenda kuliangalia na walisaidia kulitoa nje kuwakabidhi ndugu ingawa walizuia kabisa kupiga picha eneo la uwanja. Licha ya barabara nyingi kuwa chakavu kwenda Lemba nje ya kidogo ya jiji alikokuwa akiishi marehemu, mwili wake ulibebwa kwa gari ndogo ukiongozwa na ving’ora ingawa msafara huo uliingiliwa na 'daladala'. Msafara mzima ulikuwa na magari manane. Nyumbani kwa marehemu, kulikuwa na wanawake wengi waliokuwa wakimlilia mchezaji huyo wa Rwanda na ilitumia karibu saa nzima kuwatuliza kabla ya Mzee Kinesi kumkabidhi baba mlezi wa Mafisango, Papaa Pierre mwili wa mchezaji huyo kisha kumwelezea tukio zima la ajali na hali ilivyokuwa Tanzania. Pierre alishindwa kujizuia na kuanza kulia kwa sauti ya juu. Mwili huo wa mchezaji huyo ambaye hapa anafahamika kwa jina la Patrick Tabu Ete ambayo ndiyo majina halisi ya wazazi wake, haukukaa sana nyumbani hapo kutokana na nafasi kuwa ndogo na waliuhamishia kwenye Uwanja wa mpira wa Terrain ambao Mafisango alianzia kucheza soka ili kutoa nafasi ya mashabiki kumuaga zoezi linaloendelea hadi leo mchana. Ingawa anaonekana si maarufu sana jijini hapa kama ilivyo Lubumbashi na Rwanda, mchezaji huyo picha zake zilikuwa zimebandikwa kwenye magari mbalimbali ya vijana na hadi jana jioni hakuna mke wake aliyekuwa amewasili wala mtoto. Pierre alisema; “Msibahuu unauma sana, hakuna jinsi ninavyoweza kuelezea lakini nashukuru Wanasimbana Tanzania kwa kumpa heshima stahili mwanangu, hii ni kazi ya Mungu, tumpumzishe aende kwa amani.” Ujumbe wa Shirikisho la Soka la Rwanda, Ferwafa pamoja na familia na wageni mbalimbali mashuhuri walitarajiwa kuwasili usiku wa kuamkia leo kwa shughuli hiyo. Katika hatua nyingine, nguo za Mafisango zimeyeyuka kiaina huku Haruna Moshi ‘Boban’ akionja joto ya jiwe kwenye Uwanja wa Ndege wa hapa. Ndugu wa Mafisango waliokuwa wakiishi naye jijini Dar es Salaam walidai kupakia nguo hizo kwenye ndege na walipofika Kinshasa hazikuonekana huku wahudumu wakidai zitakuwa zimesahaulika Nairobi. “Sisi tuliziweka sehemu ya mizigo lakini tunashangaa hapa hazionekani wanasema labda zimebaki Nairobi, kule ndani ya begi lake vilikuwa vitu vyake vyote mpaka zile nguo alizopatia ajali yaani sijui itakuwaje,” ndugu mmoja alimueleza Papaa Pierre ambaye ni baba mlezi wa Mafisango. Lakini wahudumu wa ndege iliyosafirisha mizigo hiyo wameahidi kwamba leo Jumapili huenda nguo hizo zikapatikana kama kweli zilikwama Nairobi. Wakati huo huo, Haruna Moshi aliyesindikiza mwili wa marehemu, alizuiwa kwa zaidi ya nusu saa na maofisa wa uhamiaji ndani ya Uwanja wa Ndege wa Kinshasa kwa madai kuwa pasi yake ya kusafiria si halali. Maafisa hao walikuwa wakidai pasi hiyo ya dharura anayotumia Boban hairuhusu kuingia nchini Congo bali kwenye nchi za Afrika Mashariki lakini baadaye wakalainika na kumruhusu. “Huyu anarudi Dar es Salaam hawezi kuingia Congo na hii karatasi nyie ondokeni, huyu gari lile pale anarudi nalo mpeni kila kilicho chake,”alisema Afisa mmoja akimwambia mkuu wa msafara wa Simba Mzee Kinesi. Lakini baadaye maafisa hao walipoona picha za Boban kwenye magazeti ya Tanzania yaliyoripoti ajali ya Mafisango walilainika na kuamua kumruhusu Boban aingie ingawa alishachanganyikiwa na kutaka kulia huku akigoma kwenda licha ya kwamba askari hao haswa wa kiume walimsukuma mara kadhaa. “Sasa mimi niende wapi wakati ubalozi wenu umenipa visa na kuniruhusu nije kuwawakilisha wachezaji wenzangu kwenye mazishi ya ndugu yetu,”alisikika Boban akimwambia askari mmoja. Hata hivyo baadhiya askari walisikika waziwazi wakiomba kitu kidogo ili wamuachie Boban apite kwani alisahau hata karatasi yake ya chanjo jijini Dar es Salaam. Habari hii kwa hisani ya Michael Momburi kupitia ShafiiDauda.Blogspot.com