STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Tuesday, May 22, 2012

Malawi njiani kuja kuivaa Stars

TIMU ya soka ya taifa ya Malawi inatarajia kuwasili nchini keshokutwa Alhamisi kwa ajili ya mechi ya kirafiki ya kimataifa dhidi ya wenyeji wao Taifa Stars itakayofanyika Jumamosi kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam. Katibu Mkuu wa Shirikisho la Soka Nchini (TFF), Angetile Osiah, alisema jana jijini kuwa kikosi hicho cha Malawi kinatarajia kuja na msafara wa watu 27 na maandalizi ya mechi hiyo yako kwenye hatua za mwisho. Osiah alisema kuwa wanaamini mechi hiyo ya Jumamosi itakuwa ni kipimo sahihi kwa wachezaji wa Taifa Stars ambao wanakabiliwa na mechi ya mchujo ya Kombe la Dunia hatua ya makundi dhidi ya Ivory Coast huko jijini Abdijan. Aliongeza kuwa wachezaji wa Taifa Stars walioko kambini wanaendelea na mazoezi chini ya kocha wao mpya, Kim Poulsen, na wote wanajua umuhimu wa mchezo huo wa kirafiki. "Tunafahamu Stars inakabiliwa na mechi ya ushindani, Malawi pia ni kipimo kizuri kwao, wenzetu wako juu katika viwango vya FIFA, ni mechi itakayotusaidia," aliongeza Osiah. Hata hivyo, wachezaji watatu kati ya 25 walioutwa Stars kwa sasa wanakosa kushiriki katika programu ya mazoezi inayoendelea ya kocha Kim Piulsen kutokana na kutokuwepo nchini. Wachezaji ambao hawako kambini ni pamoja na Mbwana Samatta, Thomas Ulimwengu, ambao watatua nchini Jumatatu Mei 27 wakitokea Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo wanakoichezea TP Mazembe huku mwingine akiwa ni Haruna Moshi 'Boban' ambaye alikwenda Kinshasa kumzika kiungo wa Simba, marehemu, Patrick Mafisango, aliyezikwa juzi. Katika mechi ya kwanza ya kuwania tiketi ya kucheza fainali hizo za Dunia zitakazofanyika Brazil mwaka 2014, Taifa Stars iliyokuwa chini ya kocha aliyemaliza mkataba wake, Jan Poulsen, ilitoka sare ya 1-1 kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam. Mechi hiyo ya Jumamosi ndio utakuwa mchezo wa kwanza kwa Kim kuiongoza Taifa Stars huku akiwa na matokeo mazuri na timu ya vijana ya umri chini ya miaka 20, Ngorongoro Heroes. Chanzo:NIPASHE

No comments:

Post a Comment