STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Thursday, October 20, 2011

Filamu ya CPU kuzinduliwa rasmi Novemba 24




FILAMU mpya ya kisasa ya CPU, iliyowashirikisha wasanii nyota nchini kama Sauda Kilumanga, Dotnata Posh, Masinde, Dude na wengineo inatarajiwa kuzinduliwa rasmi Novemba 24 kwenye ukumbi wa New World Cinema, Mwenge.
Mratibu wa filamu hiyo, Evance Bukuku, alisema CPU ambayo ni kifupi cha maneno Children Protection Unity (Kitendo cha Kuwalinda Watoto), imetengenezwa na kampuni ya Haak Neel Production ikishirikisha wasanii zaidi ya 150.
Bukuku, alisema filamu hiyo iliyorekodiwa kwa teknolojia ya kisasa kwa kutumia helkopta baada ya kuzinduliwa Novemba 24, itaanza kuonyesha eneo la Mlimani City kwa muda wa wiki moja kwa kiingilio kitakachotangazwa baadae.
"Filamu yetu ya CPU ambayo imewashirikisha wahusika wakuu wanne na wasaidizi 30, itazinduliwa Novemba 24 mwaka huu kabla ya kuanza kuonyesha kwenye juumba la sinema la Mlimani City kwa wiki moja kuanzia Novemba 25- Desemba 2," alisema.
Aliongeza baada ya maonyesho hayo, kampuni yao inafanya mipango ya kwenda kuionyesha bure filamu hiyo inayozungumzia masuala mbalimbali yanayopingana na unyanyasaji na ukatili wa watoto pamoja na matendo mengine ya kihalifu.
Bukuku aliitaja mikoa itakayoenda kuonyesha filamu hiyo bure ni Mwanza, Arusha, Dodoma, Dar, Mbeya na Zanzibar.
Baadhi ya washiriki wa filamu hiyo, Steven Singh Sandhu na Sauda Kilumanga waliiambia MICHARAZO kuwa, kile ambacho watanzania walikuwa wakikisubiri kwa muda mrefu katika tasnia ya filamu sasa wamekipata kupitia filamu hiyo ya CPU.
"Ni filamu bab kubwa, ikiwa imetengenezwa kwa kiwango cha hali ya juu na ni moja ya filamu yenye uhalisi na ujumbe maridhawa kwa jamii, kitu ambacho kabla ya hapo haikuwahi kutokea," alisema Sandhu maarufu kama Salvador au .The Pride'.
Naye Sauda alisema kama mhusika mkuu katika filamu hiyo ameonyesha namna gani jamii ikishirikiana inaweza kutatua matatizo yanayowakabili watoto vikiwemo vitendo vya kikatili na uhalifu mwingine.

Belle 9, Godzilla kupamba Miss Utalii Dodoma

WASANII nyota wa muziki wa kizazi kipya nchini, Belle 9 na Godzilla wanatarajiwa kupamba shindano la kumsaka mrembo wa utalii wa Dodoma, Miss Utalii Dodoma litakalofanyika wiki ijayo mjini Dodoma.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kamati ya Miss Utalii Tanzania kupitia Rais wake, Gideon Chipungahelo, shindano hilo litafanyika kwenye ukumbi wa Club La Aziz siku ya Oktoba 29.
Taarifa hiyo inasema, shindano hilo ambalo ni muendelezo wa kusaka wawakilishi wa mikoa kwa ajili ya fainali za taifa za kumsaka Miss Utalii Tanzania 2011-2012 litakalofanyika mapema mwakani.
Chipungahelo, alisema shindano hilo litapambwa na burudani mbalimbali ikiwemo
la wasanii wa kizazi kipya wanaotamba katika miondoko ya R&B na hip hop, Belle 9, Godzilla, na vikundi vya ngoma asilia kikiwemo Yangeyange Arts cha Dodoma.
"Shindano la Miss Utalii Dodoma, linatarajiwa kusindikizwa na burudani za wasanii Belle 9, Godzilla na vikundi vya ngoma asilia. Maandalizi kwa ujumla yapo vema kwa nia ya kulinogesha shindano hilo," Chipungahelo alisema katika taarifa hiyo.
Tayari wadhamini mbalimbali wamejitokeza kwa nia ya kulidhamini shindano hilo ambalo mbali na kusaka kisura wa mkoa, pia itatoa wawakilishi wa kushiriki shindano la taifa litakalofanyika mwakani ambalo litrahusisha washiriki toka mikoa na kanda tofauti.

Mwisho

Sare zatawala daraja la Kwanza, Polisi Dar, Mbeya City moto

MECHI za raundi ya pili ya Ligi Daraja la Kwanza Tanzania Bara, zimetawaliwa na 'mdudu' wa sare baada ya michezo minne kati ya sita iliyochezwa jana kutoa matokeo hayo katika mikoa tofauti.
Katika mechi hizo nne, Rhino Rangers ya Tabora ililazimishwa sare ya 1-1 na AFC Arusha, huku Manyoni Fc na Polisi Morogoro zilishindwa kutambiana kwa kutofunga katika mechi za kundi C.
Katika mechi za kundi A, TMK United na Transit Camp zilitoshana nguvu kwa kutofungana katika pambano lililochezwa Mkwakwani Tanga, , sawa na ilivyokuwa kwa mchezo wa kundi hilo kati ya Morani- Manyara dhidi ya wageni wao JKT Mgambo ya Tanga.
Mechi pekee ya kundi hilo la A lililotoa ushindi ni ile ya Polisi Dar es Salaam iliyoifunga Burkina Faso mabao 5-3 kwenye uwanja wa Mabatini-Mlandizi, na kuwafanya 'maafande' hao maarufu kama 'Vijana wa Kova' kujikita kileleni mwa kundi hilo.
Timu hiyo ya Polisi Dar inaongoza kundi hilo ikiwa na pointi sita, mabao sita ya kufunga na kufungwa mabao matatu, ikifuatiwa na Polisi Morogoro yenye pointi nne.
Katika pambano jingine lililotoa ushindi kwa mechi hizo za juzi ni kati ya timu ya Jiji la Mbeya, Mbeya City iliyoilaza JKT Mlale ya Ruvuma mabao 3-1 na kujikita kileleni mwa kundi hilo ikiwa na pointi sita na mabao manne ya kufunga.
Mechi nyingine za kundi hilo la B zinatarajiwa kuchezwa leo ambapo timu ya Small Kids itaikaribisha mjini Morogoro, Prisons ya Mbeya, huku Majimaji Songea itaumana na Polisi Iringa mjini Songea, na timu za 94 KJ na Polisi Tabora zitaumana katika kundi C kwenye pambano litakalochezwa uwanja wa Mabatini-Mlandizi.
Ligi hiyo inashirikisha jumla ya timu 18 ambazo zinawania nafasi tisa za kucheza hatua ya pili ya fainali za ligi hiyo ili kusaka timu nne za kupanda Ligi Kuu msimu ujao.

Pambano la Maugo, Odhiambo laiva Mwanza



BONDIA mchachari wa ngumi za kulipwa nchini, Mada Maugo, amesema maandalizi ya pambano lake dhidi ya Mkenya, Joseph Odhiambo litakalofanyika keshokutwa, yamekamilika ikiwemo kutarajia kumpokea mpinzani wake kesho jijini Mwanza.
Maugo na Odhiambo wanatyarajia kuonyesha katima katika pambano lisilo la ubingwa la raundi 10 uzani wa middle, litakalosindikizwa na mabondia wakongwe nchini Joseph Marwa na Rashidi Matumla, ambalo litafanyika Jumapili uwanja wa CCM -Kirumba.
Akizungumza na MICHARAZO kwa njia ya simu toka kwenye kambi yake mjini humo, Maugo, alisema mpinzani wake anatarajia kutua jijini Mwanza kesho tayari kwa ajili ya kupima uzito siku ya Jumamosi kabla ya kupanda ulingoni Oktoba 23.
Maugo, alisema pia ameshamalizana na wasanii watakaosindikiza pambano hilo ambalo lengo lake ni kuhamasisha na kuendeleza mchezo wa ngumi katika mikoa ya Kanda ya Ziwa.
"Maandalizi ya pambano langu dhidi ya Mkenya Joseph Odhiambo yanaendelea vizuri na nawaomba mashabiki wajitokeze kwa wingi siku ya Jumapili kuweza kushuhudia mpambano huo na yale yatakayotusindikiza," alisema Maugo.
Maugo alisema miongoni mwa mapambano yatakayowasindikiza ni lile la Rashid Matumla dhidi ya Emma Kichere wa jijini Mara na Joseph Marwa atakayepigana na Chuku Dusso., huku Marwa atapigana na Chuku Duso.
"Emma Kichere ni bondia chipukizi wa mkoa wa Mara atazipiga na Matumla na Marwa atapigana na Chuku Duso anayetoka mkoa wa Mwanza, ndipo mimi na Odhiambo tutapanda ulingoni kuhitimisha michezo ya siku hiyo,' alisema Maugo.
Maugo alisema wasanii watakaosindikiza pambano lao ni H-Baba, Dudu Baya na wengine chipukizi ambao wanatokea mikoa hiyo ya Kanda ya Ziwa.
Pambano hilo la Jumapili kwa Maugo ni maalum kwa ajili ya kujiandaa na mchezo wa kimataifa dhidi ya Mjerumani, atayechuana nae kuwania mkanda wa IBF.

Mwisho

Kamanda Kova kushuhudia Mbwana, Miyeyusho wakipigana Diamond Jubilee

WAKATI Mbwana Matumla 'Golden Boy' na Francis Miyeyusho 'Chichi Mawe' wakianza kutupiana 'madongo' juu ya pambano lao la kuwania mkanda wa Mabara wa UBO, Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika pambano hilo.
Mratibu wa pambano hilo la kuwania ubingwa wa Mabara wa UBO, litakalochezwa Oktoba 30, Mohammed Bawazir wa Dar World Link, alisema Kova ndiye atakayemvisha taji mshindi wa mchezo huo.
Bawazir, alisema kamanda Kova ambaye ni Mlezi wa mchezo wa ngumi nchini, amekubali mualiko wa pambano hilo litakalofanyika kwenye ukumbi wa Diamond Jubilee, Dar es Salaam.
"Maandalizi ya pambano la Mbwana Matumla atakayetetea taji lake la UBO -Inter Continental dhidi ya Francis Miyeyusho yanaendelea vema ikiwemo Kamanda Kova kukubali kuwa mgeni rasmi wa mchezo huo," alisema.
Mratibu huyo alisema kala ya wababe hao kupanda ulingoni yatafanyika mapambano mengine matano ya utangulizi likiwemo litakalowakuanisha mabondia wakike, Asha Ngedere na Salma Kiobwa.
Pambano jingine ni la kuwania ubingwa wa taifa wa PST kati ya Juma Fundi na Fadhil Majiha.
Wakati maandalizi yakiwa hivyo Mbwana na Miyeyusho kila mmoja kwa wakati wake jana amejitapa kuibuka na ushindi katika pambano hilo litakalokuwa la raundi 12 la uzani wa Bantam.
Miyeyusho alisema amejiandaa kumvua taji Matumla, licha ya kutambua ni bondia mzuri asiyetabirika.
"Niko fiti kwa ajili ya kushinda pambano hilo, sina wasiwasi, ila naomba mashabiki wake kushuhudia ninavyompiga Mbwana kwa KO," alisema.
Mbwana mwenyewe, alisema hana maneno mengi kwani anaamini yeye ndiye bingwa na haitakuwa rahisi kwake kukubali kupokwa taji lake na Miyeyusho.
"Mie sina maneno, nimezoea kutekeleza mabmbo kwa vitendo hivyo mashabiki wangu waje ukumbini kuona nitafanya nini, ila siwezi kukubali taji langu ya UBO liniondoke," alisema.
Mabondia hao watakutana katika pambano la tatu baina yao, ambapo mara mbili za mwanzo walipokutana Februari 21, 2004 na Januari 17, 2009, Mbwana aliibuka na ushindi kitu ambacho Miyeyusho amedai hakubali kupigwa tena katika mchezo huo wa Oktoba 30.

Mwisho

Ferguson awatoa hofu mashabiki Extra Bongo


RAPA nyota wa bendi ya Extra Bongo, Saulo John 'Ferguson' amewatoa hofu mashabiki wa bendi hiyo, juu ya taarifa kwamba yupo mbioni kuiacha na kurejea alipotoka.
Ferguson, ambaye ni mtunzi na muimbaji aliyetua Extra Bongo mapema mwaka huu akitokea African Stars 'Twanga Pepeta', alisema taarifa zilizosambazwa kwamba yupo mbioni kuondoka katika bendi hiyo ni uzushi wenye nia ya kumharibia.
Akizungumza na waandishi wa habari jana Dar es Salaam, rapa huyo aliyewahi kuzifanyia kazi Double Extra, Majahazi ya Zanzibar, Mchinga G8 'Timbatimba' na Extra Bongo 3x3, alisema wadau wa bendi yake wasiwe na hofu, kwani hana mpango wa kuondoka.
"Sina mpango wa kuondoka na wala sijawahi kuwaza kufanya hivyo kwa sababu ni vigumu niache embe bivu nililonalo na kulifuata bichi kwingine," alisema bila kufafanua.
Alisema, uzushi wa yeye kutaka kuondoka zilitolewa wakati akiwa ziarani mikoa ya Nyanda za Juu Kusini na bendi yake na kumfanya alazimike kuitisha mkutano huo ili kutoa ufafanuzi, kuwaondoa shaka wadau wa bendi hiyo wanaoweza kumfikiria vibaya.
"Nimepata usumbufu mkubwa kwa mashabiki na familia yangu wakiniona sina utulivu, ndio maana nimewaita ili kuweka bayana kwamba taarifa za mtaani uzushi unaoenezwa na watu wasionitakia mema," alisema.
Aliongeza kuwa, kuthibitiha kuwa 'yupo sana' Extra Bongo, amewaandalia mashabiki hao rapu mpya iitwayo Mdudu ambayo itawashindanisha mashabiki hao katika maonyesho yao ambapo mshindi atajinyakulia runinga ya inchi 24.
"Nimekuja na rapu mpya iitwayo mdudu, ili kuonyesha nipo sana Extra Bongo na kuzima uzushi huo kwamba natarajia kurejea nilipotoka," alisisitiza.
Wakati huo huo, Kiongozi wa Extra Bongo, Rogart Hegga 'Catapillar' ameeleza ziara yao mikoa ya Nyanda za Juu Kusini, ilikuwa ya mafanikio na kuonyesha namna gani bendi yao inavyokubalika, huku wakiwapongeza wakazi wa mikoa hiyo kwa mapokezi waliyowapoa.
Hegga, alisema bendi yao iliyorejea jijini Dar juzi, imewafanya waamini malengo waliyojiwekea ya kuteka soko la muziki wa Tanzania, linaelekea kufanikio na kuwaomba mashabiki wao kuzidi kuwaunga mkono.

Mwisho