STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Thursday, October 20, 2011

Ferguson awatoa hofu mashabiki Extra Bongo


RAPA nyota wa bendi ya Extra Bongo, Saulo John 'Ferguson' amewatoa hofu mashabiki wa bendi hiyo, juu ya taarifa kwamba yupo mbioni kuiacha na kurejea alipotoka.
Ferguson, ambaye ni mtunzi na muimbaji aliyetua Extra Bongo mapema mwaka huu akitokea African Stars 'Twanga Pepeta', alisema taarifa zilizosambazwa kwamba yupo mbioni kuondoka katika bendi hiyo ni uzushi wenye nia ya kumharibia.
Akizungumza na waandishi wa habari jana Dar es Salaam, rapa huyo aliyewahi kuzifanyia kazi Double Extra, Majahazi ya Zanzibar, Mchinga G8 'Timbatimba' na Extra Bongo 3x3, alisema wadau wa bendi yake wasiwe na hofu, kwani hana mpango wa kuondoka.
"Sina mpango wa kuondoka na wala sijawahi kuwaza kufanya hivyo kwa sababu ni vigumu niache embe bivu nililonalo na kulifuata bichi kwingine," alisema bila kufafanua.
Alisema, uzushi wa yeye kutaka kuondoka zilitolewa wakati akiwa ziarani mikoa ya Nyanda za Juu Kusini na bendi yake na kumfanya alazimike kuitisha mkutano huo ili kutoa ufafanuzi, kuwaondoa shaka wadau wa bendi hiyo wanaoweza kumfikiria vibaya.
"Nimepata usumbufu mkubwa kwa mashabiki na familia yangu wakiniona sina utulivu, ndio maana nimewaita ili kuweka bayana kwamba taarifa za mtaani uzushi unaoenezwa na watu wasionitakia mema," alisema.
Aliongeza kuwa, kuthibitiha kuwa 'yupo sana' Extra Bongo, amewaandalia mashabiki hao rapu mpya iitwayo Mdudu ambayo itawashindanisha mashabiki hao katika maonyesho yao ambapo mshindi atajinyakulia runinga ya inchi 24.
"Nimekuja na rapu mpya iitwayo mdudu, ili kuonyesha nipo sana Extra Bongo na kuzima uzushi huo kwamba natarajia kurejea nilipotoka," alisisitiza.
Wakati huo huo, Kiongozi wa Extra Bongo, Rogart Hegga 'Catapillar' ameeleza ziara yao mikoa ya Nyanda za Juu Kusini, ilikuwa ya mafanikio na kuonyesha namna gani bendi yao inavyokubalika, huku wakiwapongeza wakazi wa mikoa hiyo kwa mapokezi waliyowapoa.
Hegga, alisema bendi yao iliyorejea jijini Dar juzi, imewafanya waamini malengo waliyojiwekea ya kuteka soko la muziki wa Tanzania, linaelekea kufanikio na kuwaomba mashabiki wao kuzidi kuwaunga mkono.

Mwisho

No comments:

Post a Comment