STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Thursday, October 20, 2011

Sare zatawala daraja la Kwanza, Polisi Dar, Mbeya City moto

MECHI za raundi ya pili ya Ligi Daraja la Kwanza Tanzania Bara, zimetawaliwa na 'mdudu' wa sare baada ya michezo minne kati ya sita iliyochezwa jana kutoa matokeo hayo katika mikoa tofauti.
Katika mechi hizo nne, Rhino Rangers ya Tabora ililazimishwa sare ya 1-1 na AFC Arusha, huku Manyoni Fc na Polisi Morogoro zilishindwa kutambiana kwa kutofunga katika mechi za kundi C.
Katika mechi za kundi A, TMK United na Transit Camp zilitoshana nguvu kwa kutofungana katika pambano lililochezwa Mkwakwani Tanga, , sawa na ilivyokuwa kwa mchezo wa kundi hilo kati ya Morani- Manyara dhidi ya wageni wao JKT Mgambo ya Tanga.
Mechi pekee ya kundi hilo la A lililotoa ushindi ni ile ya Polisi Dar es Salaam iliyoifunga Burkina Faso mabao 5-3 kwenye uwanja wa Mabatini-Mlandizi, na kuwafanya 'maafande' hao maarufu kama 'Vijana wa Kova' kujikita kileleni mwa kundi hilo.
Timu hiyo ya Polisi Dar inaongoza kundi hilo ikiwa na pointi sita, mabao sita ya kufunga na kufungwa mabao matatu, ikifuatiwa na Polisi Morogoro yenye pointi nne.
Katika pambano jingine lililotoa ushindi kwa mechi hizo za juzi ni kati ya timu ya Jiji la Mbeya, Mbeya City iliyoilaza JKT Mlale ya Ruvuma mabao 3-1 na kujikita kileleni mwa kundi hilo ikiwa na pointi sita na mabao manne ya kufunga.
Mechi nyingine za kundi hilo la B zinatarajiwa kuchezwa leo ambapo timu ya Small Kids itaikaribisha mjini Morogoro, Prisons ya Mbeya, huku Majimaji Songea itaumana na Polisi Iringa mjini Songea, na timu za 94 KJ na Polisi Tabora zitaumana katika kundi C kwenye pambano litakalochezwa uwanja wa Mabatini-Mlandizi.
Ligi hiyo inashirikisha jumla ya timu 18 ambazo zinawania nafasi tisa za kucheza hatua ya pili ya fainali za ligi hiyo ili kusaka timu nne za kupanda Ligi Kuu msimu ujao.

No comments:

Post a Comment