STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Tuesday, July 1, 2014

Lionel Messi kuendeleza makali yake Brazil

Lionel Messi
BAADA ya Neymar na Thomas Muiller kushindwa kuongeza bao lolote katika hatua ya 16 Bora ya Fainali za Kombe la Dunia na kusaliwa na mabao yao manne manne, nyota wa Argentina Lionel Messi ana nafasi ya kuwakacha wenzao hao wa kuwania Kiatu cha Dhahabu' iwapo atafunga leo na kumfikia kinara wa mabao wa sasa katika fainali hizo James Rodriguez mwenye mabao matano.
Rodriguez wa Colombia alifikisha idadi hiyo ya mabao baada ya kufunga mabao mawili wakati akiivusha nchi yake hadi Robo Fainali mbele ya timu ya Uruguay iliyokosa huduma za Luis Suarez aliuyefungiwa na FIFA kwa kosa la kumng'ata Giorgio Chiellini wa Italia.
Messi ambaye amefunga katika mechi zote zilizopita nchi yake leo itakuwa ikikabiliana na Uswisi katika mechi ya kuamua hatma ya timu ipi ya kuungana na Brazil, Uholanzi, Colombia, Ufaransa na Ujerumani katika Robo Fainali zitakazoanza Ijumaa.
Nyota huyo anayekipiga Barcelona katika fainali za mwaka huu ameonekana moto wa kuotea mbali kiasi cha kubashiriwa kuwa Mchezaji Bora na hata kunyakua kiatu cha Dhahabu kama ataendelea kutupia mabao kambani akichuana na wakali wenzake.
Nahodha huyo wa Argentina anategemewa kuendelea kuwatesa mabeki wakati wakikabiliana na Uswisi ambao kupitia kocha wake, Ottmar Hitzfeld ameahidi kutumia 'kijiji' kumkaba ili asiwaletee madhara kama alivyowafanyia timu hiyo katika fainali hizo za Brazil.
Nyota wenzake wa Brazil , Neymar na Muiller wa Ujerumani walishindwa kufunga bao lolote katika mechi zao za 16 Bora na kuendelea kusaliwa na mabao yao manne kama aliyonayo Messi na kuachwa kwa idadi ya bao moja na Rodriguez ambaye ameonekana ni mbadala halisi ya Radamel Falcao aliyezikosa fainali hizo kwa kuwa majeruhi.
Mbali na mechi ya Argentina na Uswisi pia leo kutakuwa na pambano jingine la kumalizia ratiba ya 16 Bora kati ya Ubelgiji dhidi ya Marekani.
ORODHA YA WAFUNGAJI:
5-James Rodriguez (Colombia)
4- Lionel Messi (Argentina)
    Thomas Muiller (Ujerumani)
    Neymar (Brazil)
3- Karim Benzema (Ufaransa)
    Arjen Robben (Uholanzi)
    Robin van Persie (Uholanzi)
    Xherdar Shaqiri (Uswisi)
    Enner Valencia (Ecuador)
2- Andre Ayew (Ghana)
    Wilfried Bony (Ivory Coast)
   Tim Cahill (Australia)
   Clint Dempsey (Marekani)
   Memphis Depay (Uholanzi)
   Asamoah Gyan (Ghana)

Kisiga afunikwa na Kisiga Mchangani

Na Adam Fungamwango
KIUNGO mshambuliaji wa Mtibwa Sugar Shaaban Kisiga, juzi alikutana na mchezaji mwingine kwenye uwanja wa shule ya msingi Mwananyamala anayetumia jina lake ambaye alimfunika vilivyo.
Shaaban Kisiga huyo 'feki' alikuwa anaichezea timu Morning Star ya Msasani, huku Kisiga mwenyewe akiwa anaichezea Morning Star ya Kiwalani.
Hata kwenye fomu za majina kwa waamuzi, pamoja na timu zote mbili kuwa na majina yanayofanana, lakini pia ilikuwa na majina yanayofanana, kila timu ikiwa na Shaaban Kisiga.
Ina maana kukawa na Kisiga halisi yaani 'original' na mwingine 'feki'.
Katika mchezo huo uliochezeswa na waamuzi wa kike watupu, Mwanahamisi Matiku, Germina Simon na Neuru Mushi, Kisiga 'feki' alionekana kumfunika Kisiga halisi kiasi cha kuisaidia timu yake kuibuka na ushindi wa bao 1-0 kwenye mechi ya robo fainali ya kwanza ya Wadau Cup.
Bao la Morning Star ya Msasani dhidi ya Morning Star ya Kiwalani lilifungwa na Oscar Magari katika dakika ya 52, baada ya pande safi kutoka kwa Kisiga 'feki'.
Mabeki wa Morning Star ya Msasani walikuwa na kazi moja tu, kuhakikisha kuwa Kisiga 'original' ambaye alicheza nafasi ya ushambuliaji haleti madhara na kweli walifanikiwa.
Timu hizo mbili zitarudiana wiki ijayo kwenye mechi ya robo fainali ya pili itakayochezwa kwenye uwanja huo huo wa shule ya msingi Mwananyamala.

Mbowe apigwa stop kugombea tena CHADEMA

Mwqenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe
Msajili wa Vyama vya Siasa Jaji Mutungi.
 
OFISI ya Msajili wa Vyama vya Siasa imesema haitambui kuondolewa kwa kipengele cha ukomo wa uongozi uliofanywa na Chadema bila kufuata idhini ya mkutano mkuu wa chama hicho.
 
Mwaka 2006, Katiba ya Chadema ilifanya marekebisho yaliyoruhusu wanachama kugombea uongozi bila ukomo wakati awali, waliruhusiwa kugombea kwa vipindi viwili vya miaka mitano.
 
Barua ya Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Francis Mutungi kwenda kwa Katibu Mkuu wa Chadema, inasema kipengele hicho katika Ibara ya 6.3.2 (C) kiliondolewa kwenye katiba bila idhini na mkutano mkuu wa chama hicho. 
Mutungi alisema baada ya kupitia muhtasari wa kikao cha mkutano mkuu wa mwaka 2006 suala la kuondoa kipengele cha ukomo wa uongozi halikuonyesha kujadiliwa katika mkutano huo.
Hata hivyo, akizungumza kwa simu jana, Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa alisema kipengele hicho kiliondolewa kwa vikao vya chama ambavyo ni wilaya na mkoa.
 
“Mjadala kuhusu ukomo wa uongozi ulishamalizika na haujadiliwi tena, ulishapitishwa na vikao halali vya chama, mkutano mkuu ulipitisha yale yaliyoamuliwa na vikao vya chini,” alisema Dk Slaa.
 
Hata hivyo, Jaji Mutungi alisema: “Chadema wamefanya mabadiliko bila kufuata katiba”
 
Alishauri waitishe mkutano rasmi na halali kwa mujibu wa katiba ya chama hicho ili waweze kurekebisha kasoro zilizopo.
Alisema kama chama hicho hakitarekebisha kasoro hiyo, Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa haiwezi kuitambua ibara hiyo.
Alisema ingawa hoja hiyo iliwasilishwa na aliyekuwa Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Arusha, Samson Mwigamba ambaye sasa si mwanachama wake, bado hoja hiyo ni muhimu na inahitaji kufanyiwa kazi.
 
“Ni vizuri mkaifanyia kazi hoja hiyo bila kujali kwamba aliyeiwasilisha si mwanachama tena wa Chadema,” alisema katika barua hiyo.
Credit:Info is Hot 

Subira ya Shaa sasa hiyooo

VIDEO ya wimbo mpya wa msanii Sara Kais 'Shaa' uitwao Subira unatarajiwa kuachiwa Ijumaa wiki hii baada ya kukamilika kwa kila kitu.
Meneja wa msanii huyo, Said Fella 'Mkubwa' alisema kuwa video hiyo imekamilika na wameshakabidhiwa na sasa wataanza kuisambaza wiki hii kabla ya kurushwa hewani siku ya Ijumaa.
"Ile video mpya yaShaa iitwayo 'Subira' itaachiwa rasmi siku ya Ijumaa, hivyo mashabiki waliokuwa wakiisubiri wajiandae kuipokea ni bonge la wimbo kama ilivyokuwa kwa 'Sugua Gaga'," alisema Fella.
Shaa yupo chini ya lebo ya Mkubwa na Wanae na wimbo huo ni wa pili kwake baada ya 'Sugua Gaga' unaoendelea kutamba kwenye vituo vya redio, runinga na mitandao ya kijamii.

Masai anasikilizia Yero Masai

Yero Subhai! Gilliard Severine 'Masai Nyota Mbofu latika pozi
MCHEKESHAJI mahiri nchini, Gilliad Severine 'Masai Nyota Mbofu' amesema bado hajaamua kufanya nini kwa sasa baada ya kuachana na kampuni ya Al Riyamy akidai anasikilizia kazi yake mpya 'Yero Masai' aliyoachia hivi karibuni.
Akizungumza na MICHARAZO mwishoni wa wiki, Masai alisema bado hajajua aibukie wapi kwa sasa akiendelea na mchakato wake wa kutoa video ya wimbo wake uitwayo 'Masai ya Wapi' alioimba na Christian Bella wa Malaika Band.
"Kwa kweli mpaka sasa sijajua hatma yangu itakuwaje, ila nahangaika kutoa video ya 'Masai ya Wapi' huku nikisikilizia kazi yangu mpya iliyopo hewani kwa sasa iitwayo 'Yero Masai' niliyoimba na Rich Mavoko na Kitokololo", alisema.
Mchekeshaji huyo alitangaza kujiondoa kwenye kampuni ya Al Riyamy inayozalisha filamu  na vichekesho vya kipindi cha Vituko Show na alisema anajiopanga kuibuka kampuni yoyote itakayokuwa ikimhitaji au aendelee kufanya kazi mwenyewe kama msanii huru.

Young Hassanal kumbe ni Mr Pendwapendwa

Muimbaji Hassani Ally
MUIMBAJI nyota wa muziki wa taarab wa kundi la Kings Modern, Ally Hassan 'Young Hassanal' anajiandaa kuingiza sokoni albamu yake binafsi ya 'Nyongo Mkalia Ini', huku akiendelea kutamba na wimbo mpya wa 'Mr Pendwapendwa'.
Wimbo huo upo kwenye albamu ijayo ya kundi lake la King Modern inayoandaliwa kabla ya kuja kuachiwa baadaye.
Akizungumza na MICHARAZO, muimbaji huyo alisema kuwa albamu yake aliyoizindua Machi mwaka huu itaingia sokoni wakati wowote kuanzia sasa ili mashabiki wake waipate.
"Naada ya uzinduzi uliofana kwa sasa nipo hatua za mwisho kabla kuingiza sokoni albamu yangu ya 'Nyongo Mkalia Ini'," alisema.
Young Hassanal aliongeza, wakati akijiandaa kuingiza sokoni albamu hiyo, kundi lake la Kings lipo katika maandalizi ya mwisho kukamilisha albamu yao mpya itakayokuwa na nyimbo tano.
"Albamu hiyo tayari inatambaulishwa hewani na wimbo nilioimba wa 'Mr Pendwapendwa' ambao unafanya vyema kwenye vituo vya redio," alisema.



Diamond: Asiyekubali kushindwa si mshindani

NYOTA wa nyimbo za 'My Number One' na 'Mdogomdogo', Naseeb Abdul 'Diamond Platnumz, ameonyesha uungwana kwa kuamua kukubali matokeo ya kushindwa kutwaa tuzo za kimataifa za BET 2014 alizokuwa akiwania na wakali wengine wa Afrika na kushuhudia Mnigeria Davido akimuangusha kwa mara nyingine tena.
Diamond alikuwa akiwania tuzo hiyo kupitia kipengele cha msanii wa kimataifa toka Afrika (Best International Act-Africa) na kujikuta akiangushwa na Davido ikiwa ni mwezi mmoja tu tangu na Mnigeria huyo aliyemshirikisha katika wimbo wake wa 'My Number One remix' kumbwaga katika tuzo za MTV Africa 2014.
Dakika chache baada ya kutangazwa kwa mshindi wa tuzo hizo zilizofanyika nchini Marekani, Diamond alitupia ujumbe katika akaunti yake ya mtandao wa kijamii akieleza kukubali matokeo hayo na kuwashukuru wote waliomuunga mkono kwenye tuzo hizo.
"Tusipopenda kukubali matokeo na ushindi wa wenzetu basi daima hatutaweza kuwa washindani...Muhimu ni kujua wapi tulipotoka na wapi tulipo leo, katika nchi zaidi ya 20 zenye wasanii zaidi ya milioni 40 kuchaguliwa Tanzania ni fursa, heshima na hatua kubwa...Cha muhimu ni kuitumia vyema fursa hii na kuhakikisha mwakani tunapiga hatua. Asante sana kwa wote wanaozidi kunisapoti," aliandika.
Katika tuzo hizo Diamond alikuwa akichuana na Davido pamoja na Mafikizolo wa Afrika Kusini, Sarkodie wa Ghana, Tiwa Savage na Toofan wa Togo. Nyota ya Diamond inazidi kung'aa hata hivyo baada ya Mafikizolo kumuomba kufanya naye wimbo.

Coutinho asainishwa mkataba wa miaka miwili Yanga


 


MABINGWA wa zamani wa kandanda nchini Yanga imeendelea kujipanga na mikakati ya kurudisha ubingwa walionyang'anywa na Azam msimu uliopouta kwa kumsainisha kiungo mshambuliaji kutoka Brazil.
Kiungo huyo Andrey Marcel Ferreira Coutinho raia wa Brazil jana alisaini mkataba wa miwili kuitumikia timu ya Young Africans (Yanga)  kwa ajili ya michuano mbalimbali ikiwemo ya Ligi Kuu ya Vodacom pamoja na mashindano ya Kombe la Shirikisho barani Afrika.
Katibu mkuu wa Young Africans  Bw Beno Njovu amesema usajili wa mchezaji Coutinho ni sehem ya muendelezo wa maandalizi ya msimu mpya wa Ligi Kuu na kama ilivyokawaida wao mambo yao ni kimyakimya.
Coutinho ambaye alizaliwa tarehe 12 Januari 1990 amekulia kwenye mji wa Berem ambapo alianza kucheza soka la kulipwa katika klabu ya Paysandu Sports Club kabla ya kwenda nchini Asia katika nchi ya Myanmar katika klabu ya Rukhapura United.
Mpaka anajiunga na klabu ya Young Africans Andrey Coutinho alikuwa akichezea timu ya Castanhal EC iliyopo kwenye Ligi Daraja la pili ambao aliweza kuichezea kwa michezo yote  ya mzunguko wa pili mwaka 2014.
Katika hatua nyingine kikosi cha Young Africans kinatarajia kuendelea na mazoezi kesho chini ya kocha Marcio Maximo katika ufuke wa Coco Beach ikiwa ni siku yake ya kwanza kuanza kazi baada ya leo kuwa na mkutano wa ndani na wachezaji wake pamoja na benchi la ufundi.

Mwenyekiti CCK yawapuuza wanaokiwabeza chama chao

Constantine Akitanda (kulia) alipokuwa akipokea hati ya usajili wa chama chake toka kwa aliyekuwa msajili wa vyama nchini, John Tendwa
MWENYEKITI wa Chama cha Kijamii (CCK), Constantine Akitanda, amewapuuza wanaokibeza chama chake kwa maamuzi yao ya kufanya ziara mikoani kuwaelimisha wananchi kuhusu umuhimu na manufaa ya kupatikana Katiba Mpya.
Aidha, chama hicho, kimesisitiza kuwa Chama cha Mapinduzi (CCM) ndiyo adui yao namba moja, hivyo katu hakiwezi kukubali kuwa kibaraka katika kuwasafishia njia ya kuendelea kukaa madarakani zaidi kama baadhi ya watu wasiokitakia mema chama hicho wanavyodai.
Akizungumza kwa njia ya simu jana akiwa safarini, Akitanda, alisema CCK na chama mshirika cha NRA wameamua kufanya ziara hiyo mikoani kutoa elimu juu ya upotoshaji unaofanywa na baadhi ya wanasiasa kuhusiana na Katiba Mpya.
Alisema ziara hiyo wanaifanya kwa nguvu zao wenyewe kama njia ya kuonyesha ukomavu wao na kiu kubwa ya kuwazindua wananchi ambao wamekuwa 'kizani' kuhusu mchakato huo wa Katiba.
"Wale wanaotubeza wanafanya hivyo kwa sababu wana wivu na hawatujui vyema, CCK kama taasisi ina mipango na mikakati yake na inajiendesha kwa kujitegemea bila msaada wa yeyote kama baadhi ya vyama vinavyofanya," alisema.
Alisema dai kwamba wanafanya ziara hiyo mikoani kwa ufadhili wa CCM ili kuvuruga mambo ambayo Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) umekuwa ukihubiri kuhusu mchakato mzima wa katiba, ni upuuzi.
"Tulishatangaza tangu awali kuwa, adui yetu namba moja ni CCM, sasa iweje adui huyo aje awe mfadhili wetu inaingia akilini kweli, watu waache mtazamo hasi kwa vyama vinavyotofautina na vingine," alisema.
Alisema chama hicho kipo tayari kutofautiana na chama chochote katika suala zima la upotoshaji wa Katiba Mpya kwani Rasimu ya Katiba Mpya kwani ina mambo mengi ya msingi yanayowagusa wananchi moja kwa moja kuliko suala la mfumo na muundo wa serikali.

"Vyama vidogo vimekuwa vikionekana mamluki vinapotofautiana na vyama vikuu, ila ukweli vyama vyote vina nafasi sawa mbele ya Msajili wa Vyama na Watanzania na tunachokifanya ni sahihi," alisema.
Mwishoni mwa wiki iliyopita, Akitanda na Mwenyekiti wa NRA, Rashid Mtuta walitangaza nia yao ya kuzungumza baadhi ya mikoa ili kutoa elimu kuhusu masuala ya Katiba kilichopokelewa kwa hisia tofauti na baadhi ya vyama vya siasa.

Mwanafunzi wa RUCO aliyechomwa moto Iringa afariki

Mwanafunzi (LEMA) aliyejeruhiwa kwa moto
Mwanafunzi huyu Daniel Lema alikuwa akisoma mwaka wa nne, kozi ya sheria katika chuo kikuu kishiriki cha Mt. Augustino cha Ruaha Iringa (Ruaha University College maarufu kama RUCO).
Mwanafunzi huyo alichomwa moto wiki iliyopita akihusishwa na tuhuma za wizi.
Baada ya kulazwa katika hospitali ya mkoa wa Iringa kwa wiki moja sasa, mwanafunzi huyo ameaga dunia majira ya saa nane mchana.
Taratibu za kuaga mwili wake zinaendelea kufanywa na uongozi wa chuo hicho, ndugu na wanafunzi wenzake.

Taarifa za awali zinaonesha kwamba mwili wake utaagwa kesho kuanzia saa moja asubuhi kabla ya kusafirishwa kupelekwa kwao mkoani Kilimanjaro kwa mazishi. Mazishi ya kijana huyo yanatarajia kufanyika jumatano ya wiki hii.

Juni 24, mwaka huu Daniel Lema alikutwa na mkasa wa kukamatwa na kuchomwa moto wakati akitoka kuangalia fainali za kombe la dunia katika moja ya Bar za mjini Iringa.

Akiwa amelewa aliingia katika moja ya migahawa ya mjini hapa akitafuta chakula, ilikuwa majira ya saa tano mwanafunzi huyo aliingia kwenye mgahawa ambao biashara hiyo ilikua imefungwa.

Binti aliyekuwepo katika mgahawa huo alianza kupiga kelele akidhani kavamiwa na mwizi. Mlinzi wa eneo hilo (mmasai) alimvaa kijana huyo na kumshambulia.

Baada ya tukio hilo taarifa zinasema walitokea watu wawili waliojitambulisha kuwa ni askari; askari hao walizuia watu waliozidi kujitokeza katika eneo hilo kuendelea kumpiga kijana huyo.

Wakiwa njiani, wananchi hao waliokuwa wakifuatilia kama atafikishwa kituo cha Polisi waliona wanachalewa na kuamua kuchukua sheria mkononi kwa kuendelea kumpiga kabla ya kumchoma moto.
chanzo: http://frankleonard.blogspot.com

Hatimaye Suarez aiomba radhi kwa kosa la kung'ata mtu Brazil

Suarez alipomng'ata Chiellini
MSHAMBULIAJI 'mtukutu' wa Uruguay aliyefungiwa na FIFA kwa kosa la kumng'ata mchezaji mwenzake wa Italia, Luis Suarez amepoza shutuma dhidi yake baada ya  kuomba radhi.
Suarez alimng'ata bega beki wa Azzuri Giorgio Chiellini katika mechi yao ya makundi na kufungiwa na FIFA kwa muda wa miezi minne.
Katika hali isiyo kawaida nyota huyo ameomba radhi usiku wa jana na kuahidi hatorudia kufanya kosa kama hilo, japo inaelezwa Barcelona ilimpa shinikizo la kufanya hivyo ili kuweza kuiwania saini yake.
Siku nne baada ya kufungiwa miezi minne na ameambia FIFA kwamba tukio hilo lilitokea katika mechi ya Kombe la Dunia kati ya Uruguay na Italia mjini Natal lilitokana na kushindwa kujizuia.
Mshambuliaji huyo wa Liverpool ameibuka kikamilifu na kujutia kosa lake. Lakini kuomba kwake radihi kunakuja katika wiki ambayo habari zimevuma mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 27 anatakiwa kwa dau la Pauni Milioni 80 Nou Camp.
Gary Lineker, mshambuliaji wa zamani wa Barcelona, amesema klabu hiyo ya Katalunya imemuambia Suarez bombe msamaha kama wanataka waendelee na jitihada za kumnunua.

Katika taarifa yake aliyoitoa kwenye ukurasa wake wa Twitter, Suarez amesema: "Baada ya siku kadhaa za kuwa nyumbani na familia yangu, nimepata fursa ya kutuliza jazba na kufikiria haswa kilichotokea katika mechi ya Italia na Uruguay Juni 24, 2014.
"Kutokana na kilichotokea na yote yaliyofuatia baadaye, kiasi cha kuathiri hata kiwango cha timu yangu ya taifa, ukweli ni kwamba mchezaji mwenzangu Giorgio Chiellini ameumizwa na kilichotokea kwa kumng'ata,".
"Kwa hili: Najuta kwa kiasi kikubwa kufanya hivyo. Naomba radhi kwa Giorgio Chiellini na familia ya soka kwa ujumla. nauambia umma kwamba halitatokea tukio kama hili tena,".
Beki wa Juventus, Chiellini ameretweet msamaha wa Suarez katika mtandao wake, baada ya awali kusema adhabu ya kumfungia miezi minne Suarez ni kubwa. 
Chiellini amejibu kwenye akaunti yake ya Tweeter moja kwa moja akisema: "Yote yamesahaulika. Natumai FIFA itakupunguzia adhabu,".

Afrika majanga! Nigeria, Algeria zafurushwa Brazil



Andre Schuller akiifungia Ujerumani bao la kuongoza
WAAFRIKA hawana chao tena kwenye Fainali za Kombe la Dunia zinazoendelea nchini Brazil baada ya usiku wa jana timu pekee mbili zilizokuwa zimesalia kwenye michuano hiyo kung'olewa na timu za Ulaya.
Super Eagles ya Nigeria ilianza kuaga mapema na kuendeleza mzimu wa kushindwa kuvuka hatua ya 16 katika fainali zake zote ilizocheza kwa kukubali kipigio cha mabao 2-0 toka kwa Ufaransa, huku baadaye Mbweha wa Algeria walikufa kiume kwa kulazwa mabao 2-1 katika muda wa nyongeza baada ya kukomaa kwa dakika 90 bila kufungana na Ujerumani.
Katika mechi ya Nigeria na Ufaransa iliyoanza mapema, Nigeria ilishindwa kuonyesha soka kama ilivyoumana na Argentina na kuruhusu Ufaransa kuwatawala na kujipatia mabao yake kupitia ya Paul Pogba na jingine la kujifunga la beki Joseph Yobo na kuhitimisha mbio zao kwenye fainali hizo zinazoingia hatua ya Robo Fainali.
Pogba anbayekipiga Juventus alifunga bao lake katika mchezo huo uliochezwa uwanja wa Garrincha, Brasilia, katika dakika ya 79 kwa njia ya kichwa na dakika mbili baadaye Yobio alijhifunga bao katika harakati za kuiokoa mpira wa krosi na kuwafanya Tai hao wa Kijani kurejea nyumbani kama ilivyokuwa kwaIvory Coast, Cameroon na Ghana zilizoaga mapema na kukwama kutimiza ndoto za kutinga Robo Fainali kwa mara ya kwanza.
Katika mechi iliyiofuatailiyiochezwa Uwanja wa Beira-Rio mjini Porto Alegre, dakika 90 za mchezo kati ya Ujerumani na Algeria zilishuhudia timu hizio zikiwa nguvu sawa kwa kutofunaga na kuiongezewa dakika 30 zilizokuwa mwiba kwa Waafrika baada ya Andre Schurrle kufunga bao dakika mbili tangu kuanza kwa muda huo kabla ya Mesut Ozil kuiongeza la pili dakika ya 119.
Hata hivyo Algeria walioonyesha soka la ushindani katika michuano hiyo tofauti na walivyokuwa wakichukuliwa awali walipata bao la kufutia machozi kwenye dakika za ziada kabla ya mchezo kumalizika kupitia kwa Abdelmoumene Djabou.
Kwa matokeo hayo ni kwamba Ujerumani na Ufaransa watakutana kwenye mechi ya Robo Fainali huku timu za Afrika zikirudi nyumbani kishujaa hata hivyo.

Taifa Stars uso kwa uso na Botswana kirafiki leo Gaborone

Kikosi cha Taifa Stars
KIKOSI cha timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars jioni ya leo inatarajiwa kushuka kwenye dimba la Taifa la Botwana mjini Gaborone kuumana na wenyeji wao Botswana katika pambano la kirafiki la kimataifa.
Pambano hilo ni maalum kwa Stars kwa ajili ya kujiwinda na mchezo wao wa kuwania kufuzu kwenye Fainali za Kombe la Afrika hatua ya makundi dhidi ya Msumbiji mechi itakayopigwa wiki tatu zijazo.
Stars inayonolewa na kocha Mart Nooij, ipo Botswana tangu wiki iliyopita ikijifua na itashuka dimbani leo mjini Gaborone bila winga wake nyota Mrisho Ngassa aliyekuwa ameenda Afrika Kusini kufanya majaribio ya kucheza soka la kulipwa katika klabu ya Free State Stars, p-ia itakosa huduma za nyota wake wengine kama Mbwana Samatta na Thomas Ulimwengu wanaocheza TP Mazembe.
Hata hivyo bado ina kikosi bora kabisa ambacho kitaweza kutoa upinzani kwa wenyeji ambao wanakutana nao kwa mara ya kwanza tangu walipokutana mara ya mwisho mwaka 2012 katika pambano la kirafiki la kimataiafa lililoisha kwa sare ya 3-3 nchini humo.
Taarifa kutoka Botwana zinasema kuwa wachezaji wote wapo fiti tayari kwa mechi hiyo na baada ya hapo itashuka tena dimbani Ijumaa ya Julai 11 kuumana na Lesotho katika mchezo mwingine wa kirafiki wa kimataifa kabla ya kurejea nyumbani kuwasubiri Mamba wa Msumbiji.
Stars ambayo haijashiriki Fainali hizo za Afrika tangu ilipofanya hivyo mara ya kwanza na mwisho mwaka 1980 itarudiana na Mamba Agosti 2 mjini Maputo kama itafanikiwa kuvuka hatua hiyo itaingia kwenye kundi moja na timu za Zambia, Cape Verde na Niger kuwania kufuzu fainali zitakazofanyika mwakani nchini Morocco.