STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, March 7, 2014

Jack Wilshere awatuliza mashabiki wa Arsenal

JACK Wilshere amewapoza mashabiki wake baada ya vipimo kwenye mguu wake kuonyesha kwamba hana tatizo kufuatia mechi ya kirafiki ya England waliyoshinda 1-0 dhidi ya Denmark juzi.
Kiungo huyo wa Arsenal, aliachwa amelala chini kwenye uwanja wa Wembley kufuatia kuchezewa vibaya na Daniel Agger tukio lililolazimisgha mchezo kusimama wakati akihitaji matibabu.
Wilshere aliendelea kucheza baadaye kabla ya kutoka na nafasi yake kuchukuliwa na Adam Lallana muda mfupi kabla ya dakika ya 60. Kiungo huyo (22) haraka aliwapoza mashabiki wake waliohofu kwamba huenda ameumizwa vibaya kufuatia kuvaana na beki huyo wa Liverpool.
"Niko poa," alisisitiza kwa Sky Sports. "Panauma kidogo lakini ni mchubuko tu. Nimefanyiwa vipimo na tayari imeonyesha ni mchubuko tu hivyo itakuwa poa."

Dihile: Bado niponipo sana langoni

Dihile (chini)
KIPA mkongwe na nyota wa zamani wa Taifa Stars, Shaaban Dihile anayeidakia JKT Ruvu ameweka bayana kwamba hana mpango wa kustaafu soka kwa sasa kama alivyotangaza nahodha wake, Husseni Bunu waliojiunga wote katika timu hiyo mwaka 2005.
Akizungumza na MICHARAZO, Dihile alisema bado yupo sana dimbani katika kuendelea kucheza soka akiamini uwezo na umri unamruhusu kufanya hivyo kwa muda mrefu.
Dihile, alisema kwa nafasi ya kipa kadiri umri unavyosonga mbele ndivyo uimara wa makipa unavyoimarika na kwamba hadhani kama atatundika 'glovu' zake mapema katika misimu ya karibuni.
"Sijafikiria kustaafu kwa sasa, bado najiona nina uwezo na umri wa kuendelea kucheza kwa muda mrefu, japo kustaafu kunategemea mambo mengi ukiacha suala la umri," alisema.
Alisema kupata majeraha makubwa ni sababu inayowaondoa wachezaji uwanjani na kwa bahati nzuri yeye hajawahi kupatwa na kitu hicho hivyo haoni sababu ya kutundika glovu zake kwa sasa, labda kama ataamua mwenyewe kwa masuala mengine ikiwamo kutaka kuzisimamia miradi yake ya biashara anayoiendesha kwa sasa.
"Ya Mungu mengi, naweza kufanya maamuzi hayo labda kutaka kusimamia biashara zangu, lakini kwa sasa zinaendelea vyema ndiyo maana sina mpango wa kustaafu kwani najiona bado sana kisoka," alisema Dihile aliyewahi kuichezea Pan Africans ya jijini Dar.
Nahodha wa JKT Ruvu, Hussein Bunu alinukuliwa na MICHARAZO katika mahojiano yake maalumu wiki iliyopita akidai huu ni msimu wake wa mwisho kucheza kwa vile atatundika 'daluga' zake na kujikita kwenye ukocha aliouanza kwa sasa.