STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Monday, April 28, 2014

Bayern Munich kutema taji la Ulaya kesho kwa Real Madrid?

* Chelsea kujiuliza upya kwa Atletico Jumatanohttp://static.goal.com/389000/389072_heroa.jpgMABINGWA watetezi wa Ligi ya Mabingwa Ulaya, Bayern Munich ya Ujerumani kesho itakuwa na kibarua cha kuamua kusuka au kunyoa, watakapoikaribisha Real Madrid katika mechi ya mkondo wa pili wa Nusu Fainali ya michuano hiyo kabla ya Chelsea na Atletico Madrid  wakijiuliza siku ya Jumatano.

Watetezi hao walicharazwa bao 1-0 katika mechi ya mkondo wa kwanza iliyochezwa wiki iliyopita nchini Hispania ambao mabingwa wa kihistoria, Real Madrid walikosa mabao mengi ya wazi na kuwapa presha kubwa Bavarians.
Bayern italazimika kubadilisha matokeo hayo mbele ya vijana wa Carlo Ancelotti ambao wana kiu ya kutaka kunyakua taji la michuano hiyo baada ya kulikosa kwa miaka 12 na pia wakitaka kufikia idadi ya kulibeba mara 10.
Hofu ya Bavarians watakaokuwa kwenye uwanja wao wa nyumbani wa Allianz Arena ni kurejea tena kwa Cristiano Ronaldo ambaye katika mechi ya kwanza aliicheza akiwa na maumivu kabla ya kutolewa kipindi cha pili kumpisha Gareth Bale aliyekuwa akisumbuliwa na mafua.
Hata hivyo Bayern chini ya Pep Guardiola haitabali kufanywa daraja na wapinzani wao kuelekea kwenye fainali zitakazofanyika nchini Ureno katikati ya mwezi ujao.
Ikiwategemea nyota wake kama Franck Ribery, Arjen Robben, Mario Gotze, Mario Mandzukic, Dante, Thomas Muller na kiungo matata Bastian Schweinsteiger ina uhakika na kuivusha tena timu hiyo katika mchezo wa fainali kama ilivyokuwa mwaka uliopita ilipoenda kukumbana na Borussia Dortmund na kubeba taji hilo baada ya kulikosa mikononi mwa Chelsea mwaka 2012.
Kivumbi kingine cha nusu fainali kitakuwa siku ya Jumatano mjini London wakati Chelsea itakapokuwa uwanja wa Stanford Bridge kuikaribisha vinara wa La Liga, Atletico Madrid ambao wiki iliyopita wakiwasimamisha na kwenda nao suluhu ya kutofungana mjini Madrid.
Chelsea iliyofufua tumaini la kunyakua ubingwa wa Ligi Kuu ya England baada ya jana kuizabua Liverpool wanaoongoza msimamo watashuka Stanford Bridge ikiwakosa baadhi ya wachezaji wake nyota akiwamo kipa Petr Cech na nahodha John Terry walioumia katika pambano la awali.
Hata hivyo mbinu za kocha Jose Mourinho katika kukabiliana na wapinzani wake inawapa matumaini mashabiki wa Chelsea kuamini kuwa wanaweza kuwasimamisha vijana wa Diego Simeone ambayo msimu huu imekuwa moto wa kuotea mbali.
The Blues watakuwa na kazi ya kuwachunga nyota wa Atletico, Diego Costa, Diego, Koke, Thiago, David Villa, Gabi na Raul Garcia ambao wameifanya timu yao msimu huu kuzima ubabe wa Real Madrid na Barcelona nchini Hispania.
Mashabiki wana hamu kubwa ya kutaka kujua ni timu zipi mbili zitakazofuzu hatua fainali na kushuhudia moja wapo ikitawazwa kuwa bingwa mpya mjini Lisbon Ureno mnamo Mei 24.
Je Bayern itakubali kuvuliwa taji na Real Madrid au Chelsea itatepeta nyumbani dhidi ya Atletcio Madrid? Tusubiri tuone.

Newz Alert! Polisi Mbeya yatimua askari 6 kisa...!

Kamanda wa Polisi  Mkoani Mbeya  Ahmed Msangi
JESHI la Polisi Mkoani Mbeya limewafukuza kazi Askari 6 wa kikosi cha Usalama barabarani  Wilaya za Rungwe na Mbeya kwa tuhuma za kuomba,kushawishi na kupokea rushwa.

Kamanda wa Polisi  Mkoani Mbeya  Ahmed Msangi amewatataja Askari hao kuwa ni pamoja na waliokuwa wakifanya kazi wilaya ya Mbeya barabara ya Mbeya/Tunduma eneo la Songwe ni Copro Jonson,PC Rymond na PC Simon.

Msangi amewataja wengine kuwa ni pamoja Sajini Hezron,PC Shaban na PC Kajolo ambao walikuwa wanafanya kazi barabara ya Mbeya/Rungwe wilaya ya Rungwe.

Askari hao walikuwa wanakabiliwa na makosa hayo na walifikishwa katika Mahakama ya Kijeshi na Hukumu kutolewa Aprili 24 mwaka huu na kupewa adhabu ya kufukuzwa kazi.

Aidha Kamanda Msangi amesema Jeshi lake halitasita kuwafukuza kazi Askari watakaokwenda kinyume na maadili ya Jeshi la Polisi na Askari yeyote atakayekwenda kinyume atakumbwa na adhabu kali ikiwa ni pamoja na kufukuzwa kazi au kufikishwa mahakamani.

Askari wengine waliofukuzwa kazi hivi karibuni ni pamoja na PC James Kagomba ambaye amehukumiwa kifungo cha miaka 30 jela baada ya kupatikana na hatia ya wizi wa kutumia silaha,WP Prisca Kilwai anayekabiliwa na kesi ya wizi wa mtoto.

Wengine wliohukumiwa kifungo cha mwaka mmoja baada ya kukutwa na hatia ya kuua bila kukusudia ni DC Marcelino Venance mwenye namba 8084,PC Juma Idd mwenye namba 3117 na Askari wa Mgambo MG Jackson Mwakalobo ambao walidaiwa kusababisha kifo cha mwanafunzi Dentho Kajigili aliyekuwa mwanafunzi wa shule ya Sekondari Ivumwe ya Jijini Mbeya. 

Na Mbeya yetu

Subira ya Shaa apewa Adam Juma

MTAYARISHAJI mahiri wa video za muziki wa kizazi kipya nchini, Adam Juma wa Visual Lab, amepewa shavu la kurekodi video ya wimbo mpya wa mwanadada Sarah Kais 'Shaa' uitwao 'Subira'.
Wimbo huo ambao awali ulikuwa ukifahamika kama 'Sifa Ujinga' kabla ya kubadilishwa jina, unatarajiwa kurekodiwa video yake wiki ijayo.
Mmoja wa mabosi wa Shaa ambaye anafanya kazi na Mkubwa na Wanae kwa mkataba maalum, Said Fella aliiambia MICHARAZO kuwa, wameamua kumpa 'shavu' Adam Juma kuiandaa video ya wimbo huo ambao umekamilika tangu mwishoni mwa mwaka jana.
"Baada ya kutafakari kwa kina tumeamua kumpa nafsi nyingine mkali Adam Juma kufyatua video ya wimbo mpya wa Shaa uitwao 'Subira' na kazi ya kurekodi inatarajiwa kuanza wiki ijayo hapa jijini Dar es Salaam," alisema.
Fella alisema wanatarajia video hiyo iwe kali kufunika hata ile ya wimbo wa 'Sugua Gaga' ambao umekuwa ukifanya vyema kwenye vituo vya runinga nchini ikiwa ni kati ya kazi za kwanza za Shaa chini ya Mkubwa na Wanae.

Simba yaomboleza kifo cha Muchacho, yafafanua suala la katiba

http://sundayshomari.files.wordpress.com/2014/04/simba-300x286.jpg 
MWENYEKITI wa Simba SC, Mhe; Ismail Aden Rage, ametuma salamu za rambirambi kwa ndugu, jamaa, marafiki na familia ya Marehemu Abdulrahman Muchacho (66), aliyefariki dunia jijini Dar es Salaam na kuzikwa juzi katika makaburi ya Kisutu jijini.
Muchacho ni miongoni mwa wanachama wenye historia ya kipekee ndani ya klabu kwani akiwa Timu Meneja wa Timu ya Simba mwaka 1976, Simba iliifunga Yanga mabao 6-0, ambao ndiyo mshindi mnono zaidi kuwahi kutokea katika historia ya mechi za Watani wa Jadi na akiwa Mweka Hazina wa Timu katika miaka ya 1990, Simba ilicheza katika Fainali ya Kombe la CAF.
Mwanachama huyu ndiye pia chachu ya kuanzishwa kwa kundi la ushangiliaji la Muchacho ambalo ndilo chimbuko la makundi yote ya ushingilijiaji katika viwanja vya soka hapa nchini.
"Kwa kweli msiba huu umenigusa sana hasa ukizingatia kwamba niliona utendaji wake wakati mimi nikiwa mchezaji wa Simba na baadaye katika uongozi. Msiba wa Muchacho ni mkubwa kwa klabu kwa sababu jina lake litabaki kuwa sehemu ya historia iliyotukuka ya Simba SC.
"Muchacho anatoka katika familia ya wana Simba. Baba yake alikuwa shabiki mkubwa wa Sunderland na mrehemu alikuwa mrithi mzuri wa mapenzi haya ya baba yake. Kwa sababu ya mambo ambayo wameifanyia klabu, jina la Muchacho na Simba vitaendelea kudumu, daima na milele," alisema Rage.

MSAJILI.
KLABU ya Simba inapenda kukanusha upotoshaji unaofanywa na baadhi ya watu kupitia vyombo vya habari kwamba Katiba ya Simba bado haijapelekwa katika Ofisi za Msajili.
Katiba ya tayari iko kwa Msajili kwa Zaidi ya wiki moja sasa na kilichobaki ni taratibu za kawaida za serikali kuhakikisha kwamba mchakato huu unamalizika kwa faida ya pande zote.
Simba SC inatumia nafasi hii kuwaomba wanachama na wapenzi wake kuwa watulivu wakati wakisubiri Ofisi ya Msajili wa Vyama na Vilabu kufanya kazi yake. 

Tangu mwanzo tulikubali kwamba Katiba yetu itatumika mara tu baada ya kupitishwa na TFF na Ofisi ya Msajili ambao wanafanya kila kitu kwa taratibu zao.
Ni vema pia watu wakaacha kueneza maneno ya uongo kuhusu Katiba kutopelekwa kwa Msajili kwa vile taarifa kama hizo zina lengo tu la kupotosha na kutaka kusababisha rabsha hata pasipo na sababu.
Mchezo wa mpira ni wa kistaarabu na ni vema wastaarabu wote wakatulia na kusubiri majibu kutoka katika Ofisi ya Msajili.

Imetolewa na
Ezekiel Kamwaga
Katibu Mkuu
Simba SC

Barca chupuchupu, Messi aibeba yaiengua Real Madrid

http://e2.365dm.com/14/04/660x350/Lionel-Messi-Barcelona-2014_3132310.jpg?20140427222759
http://peruzonatv.com/wp-content/uploads/2014/03/Barcelona-vs-Osasuna-en-vivo.jpg?0e806a
Messi akishangilia bao lake na wachezaji wenzake wa Barcelona
KLABU ya Barcelona usiku wa kuamkia leo imeponea tundu la sindano baada ya kupata ushindi wa mabao 3-2 ugenini dhidi ya Villarreal na kuzidi kuendelea kuwepo kwenye mbio za ubingwa.
Bao la dakika ya 83 kupitia kwa Lionel Messi akimalizia kazi nzuri ya Cesc Fabregas na mawili ya kujifunga ya wachezaji ya Villarreal ndiyo yaliyoibeba Barca waliotanguliwa kufungwa na wenyeji wao.
Cani aliifungia Villarreal bao la kuongoza dakika ya 45 akimalizia kazi nzuri ya Jonathan Pereira kabla ya Trigueros kuongeza la pili dakika ya 55 baada ya kumegewa pande na Aquino.
Hata hivyo mabao mawili ya kujifunga kupitia kwa Gabriel Paulista dakika ya 65 na jingine la dakika ya 78 kupitia kwa Musacchio yalifanya matokeo kuwa mabao 2-2 kabla ya Messi kufunga bao la ushindi dakika ya 83 na kuwapa Barca ushindi huo muhimu.
Matokeo hayo yameifanya Barca kufikisha jumla ya pointi 84 na kuchupa toka nafasi ya tatu hadi ya pili wakiishusha Real Madrid yenye pointi 82, na pointi nne nyuma ya vinara Atletico Madrid.

Suarez ndiye Mwanasoka Bora England


MSHAMBULIAJI nyota wa Liverpool, Luis Suarez ambaye jana alishindwa kuinusuru timu yake kuepuka kipigo toka kwa Chelsea ameteuliwa kuwa Mwanasoka Bora wa Mwaka.
Eden Hazard wa Chelsea alishika nafasi ya pili katika tuzo hiyo ya wachezaji wa kulipwa PFA Player of the Year na kiungo wa Manchester City, Yaya Toure alinyakua nafasi ya tatu.
Suarez ambaye anakumbukwa kwa vituko alivyofanya kwa msimu uliopita anakuwa mchezaji wa pili wa Liverpool kunyakua tuzo hiyo katika miaka 25 iliyopita baada ya nahodha wa Liverpool, Steven Gerrard kufanya hivyo mwaka 2006. Klabu hiyo ilishawahi kunyakua tuzo hizo nne kati ya mwaka 1980-88 kupitia wachezaji wake wa zamani Terry McDermott, Kenny Dalglish, Ian Rush na John Barnes.
Suarez kufikia mafanaikio hayo baada ya kuifungia timu yake mabao 30 na ndiye anayeongoza matumaini ya timu yake kukatisha ukame wa miaka 24 ya kunyakua taji la Ligi Kuu ya England.Kabla ya kutwaa tuzo hiyo, Suarez alipamba vyombo vya habari za England na matukio aliyowahi kuyafanya siku za nyuma ikiwamo kumng'ata beki wa Chelsea  Chelsea Branislav Ivanovic na lile tukio la kudaiwa kumfanyia ubaguzi nahodha wa Manchester United, Patrick Evra na kutozwa faini na kusimamishwa mechi kadhaa.
Mchezaji huyo toka Uruguay pia alijumuishwa kwenye kikosi cha msimu sambamba na Eden Hazard wa Chelsea aliyetajwa kama mchezaji mchanga wa mwaka huu, Daniel Sturridge na nahodha wa Liverpool Steven Gerrard.
Wengine katika kikosi hicho ni; Kipa wa Chelsea aliye majeruhi kwa sasa Petr Cech, Gary Cahil, Yaya Toure, Vincent Kompany, Luke Shaw, Adam Lallana, Seamus Coleman wa Everton.