STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Monday, August 13, 2012

Simba, Azam, Mtibwa zafuzu semi fainali Super8

TIMU za soka za Simba na Azam zinatarajiwa kukumbushia mechi yao ya robo fainali za Kombe la Kagame 2012 zitakapokutana katika nusu fainali ya Super 8 baada ya zote kufuzu hatua hiyo ya michuano hiyo maalum inayodhaminiwa na BancABC. Simba imetinga hatua hiyo baada ya kuifunga Zimamoto ya Zanzibar mabao 2-0 kwenye Uwanja wa CCM Kirumba mjini Mwanza. Simba walioingiza kikosi chao cha pili kwenye michuano hiyo, kinachonolewa na Kocha Suleiman Abdallah Matola, ilipata mabao yote yote kupitia kwa kiungo chipukizi anayeinukia vema katika soka ya Tanzania, Christopher Edward kipindi cha pili. Christopher ambaye hukomazwa pia kwenye kikosi cha timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars na kikosi cha kwanza cha Simba, alifunga bao la kwanza penalti dakika ya 50, baada ya beki Miraj Adam kuangushwa kwenye eneo la hatari. Edward ambaye ni kipenzi cha kocha Mserbia wa Simba, Profesa Milovan Cirkovick, alifunga bao la pili dakika ya 55 baada ya kuwapiga chenga mabeki watatu wa Zimamoto kabla ya kumchambua kipa wa timu hiyo ya Zanzibar. Pamoja na Simba SC kuwania ubingwa wa michuano hiyo, lakini sasa Christopher ameingia kwenye mbio za kiatu cha dhahabu cha michuano hiyo, kwa kufikisha mabao manne, akiwa anaongoza. Katika michezo mingine ya kuhitimisha hatua ya makundi ya michuano hiyo, Uwanja wa Chamazi, Jamhuri FC iliichapa 4-0 Mtende, zote za Zanzibar mabao ya washindi yakifungwa na Sadik Rajab dakika ya 20, 44, Issa Achimwene aliyejifunga dakika ya 82 na Suleiman Khatib dakika ya 88. Kwenye Uwanja wa Ushirika mjini Moshi, Azam FC ilitoka nyuma kwa bao 1-0 na kuifunga Polisi Moro FC mabao 2-1, mabao yake yakitiwa kimiani na beki Said Mourad dakika ya 20 na Abdi Kassim ‘Babbi’ dakika ya 70, wakati la Maafande wa Morogoro lilitiwa kimiani na Mokili Rambo dakika ya kwanza. Polisi ilimpoteza mchezaji wake, Abdallah Rajab dakika ya 88 aliyetolewa nje kwa kadi nyekundu. Uwanja wa Amaan, Zanzibar, Kocha Mecky Mexime ataiongoza Mtibwa Sugar katika mchezo wa mwisho wa makundi dhidi ya wenyeji Super Falcon FC. Katika Kundi A, Simba SC inaongoza kwa pointi zake nne, baada ya kutoa sare moja na kushinda moja, ikifuatiwa na Zimamoto na Mtende zinazofungana kwa pointi tatu kila moja, wakati Jamhuri inashika mkia kwa pointi yake moja. Kundi B, Mtibwa inaongoza kwa pointi zake sita ikifuatiwa na Azam FC na Polisi Moro, zenye pointi tatu kila moja, wakati Falcon inashika mkia, ikiwa haina pointi hata moja. Kwa kufuzu hatua hiyo, Simba inatarajiwa kuvaana na Azam, ambao katika mechi yao ya Kagame waliishindilia 'Mnyama' mabao 3-1 yote yakiwekwa kimiani na John Bocco aliyepo Afrika kwa sasa kifanya majaribio katika klabu ya Super Sports. Mechi nyingine itakayochezwa mapema saa 8 siku hiyo ya Jumamosi itazikutanisha Mtibwa Sugar dhidi ya jamhuri ya Pemba. Mechi zote za Nusu fainali na fainali zote zitachezwa Dar es Salaam. Mdhamini wa michuano hiyo, Banc ABC anagharamia usafiri wa ndege kwa timu zote kutoka kituo kimoja hadi kingine, malazi na jezi. Kanuni za mashindano haya ni kushirikisha timu zilizoshika nafasi tatu za juu katika Ligi Kuu za Bara na visiwani na mbili zilioongoza katika kupanda Ligi Kuu zote mbili, lakini kwa Bara, Yanga waliokuwa washindi wa tatu msimu uliopita, walijitokea na nafasi yao ikachukuliwa na Mtibwa Sugar ambayo ilishika nafasi ya nne kwenye Ligi Kuu. Bingwa wa michuano hiyo mipya itakayokuwa ikifanyika kila mwaka, ataondoka na Sh. Milioni 40, mshindi wa pili Sh. Milioni 20, wa tatu Sh. Milioni 15 sawa na wa nne, wakati washiriki wengine wataondoka na Sh. Milioni 5 kila moja. NUSU FAINALI Agosti 15, 2012 Mtibwa Sugar Vs Jamhuri (Saa 8:00 mchana) Simba SC Vs Azam FC (Saa 10:00 jioni) (Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam)

Sunday, August 12, 2012

Chelsea, Man City kufungua pazia la msimu mpya EPL leo

PAZIA la msimu mpya wa Ligi Kuu ya England (EPL)kwa mwaka 2012/13 linatarajiwa kufunguliwa rasmi leo Jumapili kwa mechi ya kuwania Ngao ya Jamii kati ya Mabingwa wa Ligi Kuu England, Manchester City, na Mabingwa wa FA Cup, Chelsea, ambao pia ni Mabingwa wa Ulaya. Pambano la timu hizo mbili zitakazoshuka dimbani leo zikiwa na mabadiliko yanayotofautiana katika vikosi vyao unatarajiwa kuchezwa kwenye uwanja wa Villa Park, kuanzia saa 9 Alasiri kwa saa za Afrika Mashariki na Kati. Wakati Chelsea ikiwa na nyota wapya walionunuliwa hivi karibuni kwa ajili ya msimu mpya, Man City wao hawana mabadiliko yoyote. Chelsea itashuka dimbani leo ikiwa haina kinara aliyewapa mataji hayo mawili inayoyashikilia kwa sasa Didier Drogba, kutoka Ivory Coast aliyehamia katika klabu ya Shanghai Shenhua ya China akiungana na Nicolas Anelka. Vifaa vipya vilivyosajiliwa na ambavyo vimeanza kuonyesha makeke katika mechi za kujipima nguvu kujiandaa na msimu mpya utakaoanza mwishoni mwa wiki ijayo ni Eden Hazard, Marko Marin na Oscar lakini ni Hazard na Marin ambao wanaweza kucheza Mechi hii na Man City kwa vile Oscar atakuwa bado yuko na nchi yake Brazil kwenye Olimpiki. Msimu uliopita, Timu hizi ziligawana ushindi kwa Chelsea kuifunga Man City 2-1 Mwezi Desemba na Man City kuifunga Chelsea 2-1 Mwezi Machi. Katika Mechi zao za hivi karibuni, Mechi za kujipasha kwa ajili ya Msimu mpya, Chelsea imekuwa na matokeo yasiyoridhisha kwa kushinda Mechi moja tu kati ya 4 walizocheza na kufungwa zilizobaki wakati Man City wamecheza Mechi 5 na kushinda 3 na kufungwa mbili. Chelsea hawana majeruhi yeyote lakini Man City watamkosa Nahodha wao Vincent Kompany na Micah Richards ambao wameumia. Vikosi vinatarajiwa kupangwa kwa siku ya leo ni kama ifuatavyo: Chelsea [Mfumo 4-3-3]: Cech, Ivanovic, Terry, Cahill, Cole, Mikel, Meireles, Lampard, Ramires, Torres, Hazard Man City [Mfumo 4-4-2]: Hart, Zabaleta, Savic, Lescott, Clichy, Yaya Toure, De Jong, Nasri, Johnson, Tevez, Aguero

Rage adanganya Simba, alia akijitoa TFF Na Waandishi Wetu, Dodoma na Dar es Salaam

SIKU sita tangu awadanganye wanachama wa Simba kuwa mchezaji Emmanuel Okwi amefanya majaribio na kufuzu Ulaya, mwenyekiti wa klabu hiyo Isamil Aden Rage amelia hadharani akitangaza kujitoa uongozi wa moja ya kamati za TFF -- shirikisho la soka. Rage jana alitangaza kujivua nafasi ya ujumbe wa Kamati ya Katiba, Sheria, Maadili na Hadhi za Wachezaji ya TFF, akituhumu baadhi ya viongozi wa shirikisho hilo kutoitendea haki timu yake. Mwenyekiti huyo wa Simba ambaye pia ni Mbunge wa Tabora Mjini (CCM) aliwaambia wanachama wa Simba katika mkutano Jumapili iliyopita kuwa Okwi alifanya majaribio na kufuzu katika klabu ya Red Bull Salzburg ya Austria. Lakini akizungumza na Nipashe mapema wiki hii, Okwi alisema hakufanya majaribio yoyote Ulaya kutokana na kusumbuliwa na Malaria tangu awasili barani humo mpaka kurejea Uganda na kisha Simba. Alipoulizwa kama haoni kuwa aliwadanganya wanachama wa Simba alipowaeleza jambo ambalo linakanushwa na mchezaji husika jana, Rage ambaye alidai pia kuwa mchezaji huyo atakuwa akilipwa euro 300,000 kwa mwezi na Redbull alisema: "Okwi hakwenda kutalii kule... mimi ninasema kitu kilicho sahihi. "Alifanya majaribio na kufuzu. Haya maneno mengine ni ya magazeti tu... sasa kama hajafanya majaribio alienda kufanya nini kule kwa kipindi cha wiki nzima." Kwa mujibu wa taarifa za mtandao rasmi wa kompyuta wa Red Bull Salzburg, imesajili wachezaji wawili tu kati ya tarehe za Okwi kwenda Ulaya mpaka kurudi -- Valon Berisha kutoka Viking Stavanger na Havard Nielsen kutoka Valerenga Oslo. Zote za Norway. Akizungumza na waandishi wa habari Bungeni mjini Dodoma jana, Rage alisema amejitoa katika kamati hiyo baada ya kuchukizwa na kitendo cha Yanga kumsajili beki wa APR ya Rwanda, Mbuyi Twite ambaye Simba ilishaingia naye mkataba, na kwa baraka za TFF. Alisema TFF ina wajumbe wengi ambao ni wanazi wa Yanga na hivyo kushindwa kuitendea Simba haki. “Kama serikali na mamlaka za kusimamia soka zitaonekana zinapendelea timu moja, basi wapenzi na wanachama wa Simba wanaweza kuamua kuangalia kwingineko ambako wanadhani watapata haki zao za msingi,” alisema Rage na kulazimika kukatisha kwa muda mkutano wake baada ya kumwaga machozi. Rage hakufafanua Serikali inaingiaje katika suala la kuonewa kwa Simba huko anakodai, wala kama amepewa ridhaa na wanachama wa Msimbazi kuishutumu serikali yao kwa niaba yao. Wakati huo huo, Katibu Mkuu wa Yanga, Celestine Mwesigwe, amesema kuwa wanasubiri muda ufike wamtangaze rasmi Mbuyi Twite atakayechezea timu hiyo msimu ujao wa ligi kuu ya Bara. "Hiko kitu kipo (usajili wa Mbuyi), lakini siwezi kuzungumzia suala hilo kwa sasa," alisema. "Ngoja tusubiri wakati wake ufike na mchezaji ataonekana hapa kwa sababu hili sasa hivi limekuwa na mvutano kidogo." Chanzo:NIPASHE JUMAPILI

Pambano la watani wa jadi Msondo wajichimbia Dodoma, Sikinde wajificha

HOMA ya pambano la wapinzani wa jadi kwenye muziki wa dansi nchini kati ya Msondo Ngoma 'Baba ya Muziki' na Mlimani Park 'Sikinde' linalotarajiwa kufanyika Idd Mosi kwenye viwanja vya Leaders Club limechukua sura mpya baada ya bendi mmoja kukimbia mji na nyingine kwenda kusikojulikana. Bendi ya Msondo imelikimbia jiji la Dar es Salaam na kwenda kujichimbia mkoani Dodoma kujiandaa kikamilifu na pambano hilo la aina yake dhidi ya mahasimu wao. Meneja wa bendi hiyo Said Kibiriti amesema kuwa bendi iko Dodoma ikifanya mazoezi ya 'kufa mtu' ili kuwatoa nishai Sikinde na wasiwe na hamu tena ya kuomba pambano siku nyingine. "Tunataka tutoe dozi siku hiyo, tutawasambaratisha na waogope tena kupambana na sisi, mashabiki wetu wasiwe na wasiwasi bendi yetu iko sawa na sasa inajifua na siku ya Idd El Fitri wajitokeze kwa wingi kuja kuishangilia Msondo," alisema Kibiriti. Kwa upande wa Sikinde, kiongozi wa bendi hiyo Habib Jeff amesema kuwa bendi yao ipo jijini Dar es Salaam, lakini akagoma kabisa kutaja sehemu ilipojichimbia. "Ndugu yangu sisi tupo hapa hapa Dar, ila siwezi kukwambia tupo wapi, tunaogopa hujuma, si unajua tena linapokuja suala la Msondo na Sikinde ni kama Simba na Yanga kwa hiyo mashabiki watatuona tu siku siku hiyo, wala hatusemi kwa sasa yuko wapi ila hapa hapa Dar," alisema. Kiongozi huyo amewataka mashabiki wake kujazana kwa wingi siku ya Idd Mosi kwenye viwanja vya Leaders Club kuipa sapoti bendi yao ili iibwage Msondo. Pambano hilo limeandaliwa na kampuni ya Keen Arts na kudhaminiwa na Konyagi. Bendi hizo zilipambana kwenye sikukuu ya Krisimasi mwaka jana kwenye ukumbi wa TCC. Mwisho

Ruvu Shooting yatangaza kikosi chake kipya, yasajili 26

KLABU ya soka ya Ruvu Shooting Stars inayojiandaa na Ligi Kuu Tanzania Bara imetangaza usajili wa wachezaji wao 26 kwa ajili ya msimu mpya wa ligi hiyo utakaoanza mwezi ujao. Miongoni mwa waliosajiliwa na kikosi hicho kinachonolewa na kocha Charles Boniface Mkwasa ni pamoja na waliokuwa washambuliaji nyota wa Kagera Sugar, Hussein Swedi na Said Dilunga. Msemaji wa klabu hiyo, Masau Bwire aliiambia MICHARAZO leo asubuhi kuwa, usajili huo ambao unatarajiwa kuwasilishwa kesho kwenye ofisi za Shirikisho la Soka Tanzania, TFF, umezingatia umri, kipaji na uwezo wa mchezaji kutokana na mapendekezo ya kocha wao. Bwire, alisema kati ya wachezaji hao 26 waliosajiliwa na klabu yao, sita ni wachezaji wapya na waliosalia ni wale walioichezea timu hiyo msimu uliopita. Aliwataja wachezaji wapya walionyakuliwa na timu yao kuwa ni Said Dilunga, Husseni Swedi, Mau Bofu aliyekuwa akiichezea Azam, Gideon Sepo, Kulwa Mobi aliyeichezea Polisi Dodoma msimu uliopita na Philemon Mwandesile aliyekuwa timu ya Toto Afrika. Wachezaji wa zamani waliobakishwa kikosi ni pamoja na kipa Benjamin Haule, Michael Norbert, Gido Chawala, Godhard Msweku, Liberatus Manyasi, George Assey, Mangasin Mbonosi, Paul Ndauka, Jumanne Juma, Shaaban Suzan, Said Madega na Nyambiso Athuman. Wengine ni Raphael Keyala, Frank Msese, Michael Aidan, Gharib Mussa, Ayuob Kitala, Ernest Jackson na Baraka Nyakamande. Bwire alisema wachezaji waliotemwa na kikosi hicho kutokana na sababu mbalimbali ni pamoja na Mohammed Kijuso, Emmanuel Mwagamwaga, Yusuph Mgwao na Kassim Kilungo.

Timu za Maafande wa JKT waandaliwa michuano maalum wazialika Coastal, Lyon

TIMU za soka za Coastal Union ya Tanga na African Lyon ya Dar es Salaam zinatarajiwa kushiriki michuano maalum ya 6 Bora zinazozihusisha timu za maafande wa JKT, kwa ajili ya kuziandaa vema na ushiriki wao wa Ligi Kuu. Michuano hiyo itakayokuwa ikifanyika kila mwaka kulingana na uwepo wa timu hizo za maafande inatarajiwa kuanza siku ya Jumatano na itakuwa ikichezwa kwenye uwanja wa Mabatini, Mlandizi mkoani Pwani. Msemaji wa michuano hiyo itakayochezwa kama ligi hadi kupata mshindi wake, Masau Bwire aliiambia MICHARAZO mapema leo kuwa timu nne za maafande wa JKT ndizo walengwa wakuu wa michuano hiyo ila katika kuipa msisimko zaidi wamezialika Coastal Union na African Lyon. Bwire alisema wamezialika timu hizo kwa imani itazipa changamoto timu zao ili kuanza kuhimili mikikimikiki kabla ya kuanza kwa ligi kuu. "Katika kuziandaa timu zetu za JKT na kuhakikisha zinafanya vema kwenye Ligi Kuu msimu huu, tumeziandalia michuano maalum ya Sita Bora ambayo itaanza Agosti 15 na tumezialika Coastal Union na African Lyon, kutokana na kuonekana zina viwango bora," alisema Bwire. Alizitaja timu za JKT zilizolengwa kwa michuano hiyo ni wenyeji JKT Ruvu, Ruvu Shooting Stars, JKT Oljoro ya Arusha na JKT Mgambo Shooting ya Tanga iliyopanda daraja msimu huu. Bwire alisema ratiba michuano hiyo itaanza kwa kuzikutanisha timu za JKT Ruvu na Ruvu Shooting siku ya Jumatano, siku inayofuata itakuwa zamu za JKT Oljoro dhidi ya Mgambo Shooting na Agosti 17 Coastal Union itavaana na Lyon. "Hizo ni mechi za awali na ratiba kamili inatarajiwa kutolewa kuanzia Jumanne ili kuwapa fursa mashabiki wa soka kuifuatilia na hatimaye kujua nani atakayeibuka mshindi wa michuano hiyo maalum," alisema. Mwisho

Saturday, August 11, 2012

Kivumbi cha awali cha BancABC Super8 kesho

KIVUMBI cha hatua ya makundi ya michuano ya BancABC Super8 inatarajiwa kuhitimishwa kesho kwa viwanja vinne kuwaka moto katika miji tofauti ya Tanzania Bara na Zanzibar. Kwa mujibu wa ratiba ya makundi ya michuano hiyo inayoshirikisha timu nane, nne toka kila upande wa Tanzania Bara na Zanzibar ni kwamba Simba ambao walizinduka toka kwenye kipigo cha mabao 3-1 toka kwa Wakenya City Stars kwenye Simba Day kwa kuinyuka Mtende, itakuwa kwenye dimba la CCm Kirumba, Mwanza kuumana na Zimamoto ya Zanzibar. Mechi nyingine ya kundi hilo itazikutanisha timu za Jamhuri na Mtende zote za visiwani Zanzibae kwenye uwanja wa Chamazi, Dar es Salaam. Kwa mechi za kundi B ratiba inaoonyesha Mtibwa Sugar iliyoigaragaza Azam nyumbani kwao 'Chamazi' kwa mabao 2-0 itashuka dimba la Amaan Zanzibar kuumana na mabingwa wa Ze nji, Falcon iliyolala kwa Polisi Moro katika mechi yao iliyopita. Nao Polisi Moro iliyorejea Ligi Kuu msimu huu, itakuwa kwenye uwanja wa Ushirika Moshi kuumana na Azam Fc. Timu nne, mbili toka kila kundi zitakazoshika nafasi mbili za juu zitacheza hatua ya nusu fainali ambazo zitachezwa kwenye uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Wanamasumbwi chipukizi Bongo kuvuna nini Idd Pili?

MASHABIKI wa ngumi za kulipwa nchini wanatarajia kupata burudani ya aina yake siku ya Idd Pili, wakati mabondia wawili chipukizi Ramadhani Shauri na Nassib Ramadhani watakapoanda ulingoni kuzipiga. Mabondia hao walio chini ya kocha Christopher Mzazi watazipiga na mabondia kutoka Kenya na Uganda katika michez itakayofanyika kwenye ukumbi wa Diamond Jubilee, jijini Dar es Salaam kuwania mataji ya IBF. Shauri yeye atapanda ulingoni kuzichapa katika pambano la kuwania ubingwa wa IBF-Afrika uzani wa vinyoya (Featherweight) la raundi 10 dhidi ya Mganda, Sunday Kizito. Bondia Nassib anayeshikilia taji la chama cha World Boxing Forum (WBF), atatangulia kuzipiga na Twalib Mubiru kutoka Kenya katika pambano la uzani wa Bantam kuwania ubingwa wa IBF-Afrika Mashariki na Kati. Michezo hiyo yote inaratibiwa na promota Lucas Rutainurwa ambaye ni Mkurugenzi wa kampuni ya Kitwe General Traders na kusimamiwa na Kamisheni ya Ngumi za Kulipwa nchini, TPBC. Kwa mujibu wa Rais wa TPBC ambaye pia ni Rais wa IBF Afrika/USBA, Onesmo Ngowi, pambano la Shauri na Kizito ndilo pigano kuu (main bout) na limepewa jina la 'The Rumble in the City of Heaven's Peace'. Ngowi, amemtaja Shauri kama 'mfalme' mpya aliyeanza kutishia hadhi za mabondia wengine nchini kutokana na kipaji kikubwa alichonacho katika mchezo huo wa ngumi za kulipwa. Rais huyo alisema rekodi aliyonayo na namna ya uchezaji wake akiwa ulingoni imemfanya awe anamfananisa na nyota wa zamani wa ngumi za kulipwa kutoka Marekani Sugar Ray Leonard. Katika umri alionao usiozidi miaka 25, Shauri tayari amekuwa na kivutio cha aina yake kutokana na haiba yake ya uchezaji na rekodi aliyonao tangu aanze kucheza mchezo huo chini ya kocha Mzazi wa gym iliyopo Mabibo jijini Dar es Salaam. Bondia huyo amecheza mapambano 15, akishinda michezo 12, kupoteza miwili na kuambulia sare moja, huku akishikilia nafasi ya pili kati ya 40 katika orodha wa mabondia wa uzito wake akitangliwa na Roger Mtagwa. Kwa upande wa mpinzani wake yeye ana rekodi ya kucheza mapambano 22 akishinda 12, kupoteza tisa na kupata sare moja. Ngowi anaamini pambano hilo litasisimua mashabiki wengi wa ngumi ambao kwa mua mrefu hawajapata kushuhudia mabondia vijana wakiwania mataji ya kimataifa. 'Ni zamu ya kuwapa nafasi mabondia chipukizi kuonyesha vipaji vyao na kuwania mataji ya kimataifa kuitangaza Tanzania," alisema Ngowi. Kuhusu pambano la Nassib Ramadhani, Ngowi alisema nalo linatarajiwa kuwa gumzo kutoka na rekodi alizonazo bondia huyo aliyecheza mapambano 11 na kushinda tisa akipoteza mawili. Nassib pia ndiye anayeongoza orodha wa mabondia 21 wa Tanzania wa uzani wake huku katika orodha ya dunia akishika nafasi ya 88 kati ya mabondia 636. Mpinzani anayecheza nae rekodi yake inaonyesha amecheza michezo 20 akishinda 11 na kupoteza saba huku akitoka sare miwili, hali inayofanya pambano lao litakuwa na msisimko na mvuto wa aina yake. Mbali na michezo hiyo siku hiyo kwa mujibu wa Ngowi kutakuwa na michezo mingine kadhaa ya utangulizi ambayo itatoa burudani kwa mashabiki wa ngumi wa mkoa wa Dar es Salaam na mikoa ya jirani. Ngowi alisema lengo la Kamisheni la Ngumi za Kulipwa Tanzania, TPBC ni kuhakikisha kila miezi miwili kunakuwa na mapambano ya kimataifa kwa mabondia wa Tanzania baada ya kushuhudiwa 'ukame' wa mataji kwa muda mrefu. "Pia lengo letu ni kutoa nafasi kwa mabondia chipukizi kuonyesha vipaji vyao sambamba na kuendeleza mpango maalum ulianzishwa na IBF-Afrika/USBA kutangaza utalii kupitia mchezo huo wa ngumi," alisema. Tayari mabondia hao watakaoonyeshana kazi siku hiyo ya Idd Pili, wamejichimbia kambini wakijiandaa na mapambano hayo, huku mratibu Lucas Rutainurwa, akisisitiza kila kitu kinaendelea vema akiwataka mashabiki wa ngumi kujitokeza siku ya siku. Kama alivyonukuliwa Rais wa TPBO ambaye pia ni msemaji wa TPBC, Yassin 'Ustaadh' Abdallah, huenda hiyo ikawa ni nafasi nzuri kwa mabondia hao chipukizi wa Tanzania kuanza safari ndefu ya kufikia mafanikio yaliyowahi kufikiwa na wakongwe kama Rashid Matumla aliyewahi kunyakua ubingwa wa dunia wa WBU. Tusubiri tuone kipi kitakachovunwa na mabondia hao katika michezo
yao hiyo, ambayo itafanyika wiki chache kabla ya kumshuhudia Mtanzania mwingine, Thomas Mashale hajapanda ulingoni nchini Ujerumani kuwania taji la UBO Vijana uzani wa Kati kwa kupigana na mwenyeji wake Arthur Hermann. Awali pambano hilo linaloratibiwa na Becker BoxPromotion lilipangwa kufanyika wiki iliyopita nchini humo, lakini limeahirishwa hadi Septemba 5 mjini Berlin, Ujerumani.

African Lyon yamnasa kocha mpya toka Argentina

KLABU ya soka ya African Lyon jana imemtambulisha kocha wao mpya kutoka Argentina, Pablo Ignacio Velez, waliyeingia naye mkataba wa mwaka mmoja, huku mwenyewe akiahidi kufanya mabadiliko zaidi ya soka kwenye timu hiyo. Pablo raia wa Argentina aliyasema hayo jana baada ya kusaini mkataba wa mwaka mmoja kuitumikia timu hiyo na kusisitiza lengo lake kubwa ni kuhakikisha vijana wanapewa nafasi ya kuonyesha vipaji vyao na ndivyo itakavyokuwa Afrika Lyon. “Sikuja Tanzania kutafuta pesa, ndoto yangu kubwa ilikuwa kufundisha soka barani Afrika hivyo wakati ni sasa,” alisisitiza kocha anayezungumza lugha ya ‘kiispanyola’. Pablo alisema “kazi ya aina yoyote lazima ipewe muda na mchezaji lazima atengenezwe hivyo watanzania wawe na subira kwa ajili ya kupata matunda mazuri ya vijana hapo baadae kutoka African Lyon. Kocha huyo aliyewahi kuzichezea timu za taifa za vijana chini ya miaka 17 na 20 za Argentina hakusita kusisitiza suala la nidhamu kwa wachezaji wa timu hiyo ya ndani na nje ya uwanja. “Nidhamu ni muhimu kwa wachezaji wangu cha msingi tushirikiane katika kufanikisha hili kwa vijana kwani mchezaji anatakiwa kati ya miaka 18 na 19 awe ametengeneza jina kupitia soka ,” alisema Pablo. Naye Mmiliki wa African Lyon, Rahmu Kangezi alisema lengo la kumleta kocha huyo ni kuhakikisha timu hiyo inajongea mbele zaidi. Kangezi alisema licha ya kusaini mkataba wa mwaka mmoja lakini wanaweza kumtumia Pablo kwa kipindi kirefu kulingana na mfumo wa kuhakikisha wanaendeleza vijana katika timu yao. “Pablo ni zaidi ya kocha, ana uwezo pia amecheza mpira pia ni kocha wa kwanza kutoka Argentina kuja Tanzania hivyo tunaimani timu yetu ya African Lyon itafika mbali zaidi kisoka,” alisitiza Kangezi. Pablo mwenye miaka 38 aliyechukua mikoba iliyoachwa na Jumanne Chale amewai kuifundisha klabu ya Atletico Colo Colo De Chile (1998). Klabu nyingine alizowai kufundisha ni Atletico Calchin (2000), Atletico Belgrano De Cordoba (1997), Atletico River Plate (1993-1995). Klabu nyingine ni Banco De Cordoba (1991 na 1997), Deportivo Lasallano (1992) Atletico Argentino Penarol kwa miaka minne na klabu nyingine nyingi za Hispania na Argentina.

Yanga kutafuta kocha mwingine iwapo...!

UONGOZI wa mabingwa wa soka Afrika mashariki na Kati, Yanga, umesema utatafuta kocha mwingine kama mwalimu wao Tom Saintfiet atapata kazi ya kufundisha timu ya taifa ya Kenya. Hata hivyo, Yanga imesema mpaka sasa haina taarifa rasmi juu ya kocha wake huyo kutakiwa na Shirikisho la soka Kenya kwa ajili ya kuifundisha timu yake ya taifa hivyo inasubiri barua kutoka KFF. Akizungumza na Nipashe jana, Afisa habari wa Yanga, Luis Sendeu, alisema endapo KFF itaonyesha dhamira ya kumtaka Saintfiet hawatomzuia. "Hatutaweza kumzuia," alisema Sendeu. "Tutakaa naye na kujua nini cha kufanya, lakini napenda kuwaambia kuwa sisi kama Yanga hatuna taarifa za kocha wetu kutakiwa Kenya. "Ila kama tutapata taarifa rasmi uongozi utajua nini cha kufanya," alisema Sendeu. Itabidi klabu itafute kocha mwingine endapo itaridhia kusitisha mkataba wa miaka miwili wa mwalimu huyo Mbelgiji aliyeanza kuifundisha mwezi uliopita. Sendeu alisema kuwa kwa sasa kocha huyo anaendelea na programu zake za kuiandaa timu kwa ajili ya msimu ujao wa ligi kuu ya Bara ambao utaanza mwezi ujao. "Kocha Tom yupo na kikosi akikiandaa kwa ajili ya ligi kuu ya Bara... na yeye ana programu zake ambazo anazifanyia kazi kuhakikisha timu inakuwa katika kiwango cha juu zaidi ya sasa pindi ligi kuu itakapoanza," alisema. Alisema viongozi wa Yanga wanaamini uwezo ambao timu hiyo ilionyesha kwenye mashindano ya Kagame ndiyo ambao utahamishiwa kwenye ligi na kufuta makosa waliyoyafanya msimu uliopita ambapo ilivuliwa ubingwa na mahasimu wao Simba. Yanga ilionyesha soka la hali juu kwenye michuano hiyo licha ya kuanza kwa kipigo, ikishinda michezo yake sita iliyofuatia hadi kutetea Kombe la Kagame. CHANZO:NIPASHE JUMAMOSI

Mkali wa mikono aimwagia sifa Azam Fc

NYOTA wa klabu ya mpira wa mikono ya Ngome, Ally Khamis 'Muba' ameimwagia sifa klabu ya Azam Fc kwa mafanikio makubwa iliyopata kwa kipindi kifupi tangu iingie kwenye Ligi Kuu Tanzania na kudai imeleta mapinduzi yanayopaswa kuwa changamoto kwa Simba na Yanga. Muba, aliyewahi kuwa mlinda mlango enzi akisoma kabla ya kujitosa kwenye mpira wa mikono, alisema kinachofanywa na Azam, kinapaswa kuigwa na klabu nyingine katika kuendeleza mchezo huo sambamba na kurejesha heshima ya timu za Tanzania katika anga la kimataifa. Alisema, anaamini kungekuwa na klabu zenye malengo na mipango inayotekelezeka kama Azam ni wazi soka la Tanzania lingepiga hatua kubwa. "Lazima niseme ukweli mie nakunwa na mafanikio ya Azam, yanatia moyo na kuonyesha wenye timu hiyo walivyo na malengo na nadhani klabu nyingine zinapaswa kujifunza kutoka kwao iwapo zinataka kufika mbali," alisema. Muba, alisema pamoja na kuipongeza klabu hiyo, bado haipaswi kubweteka kwani safari iliyopo mbele yao ni kubwa na inayohitaji moyo wa ustahamilivu hususani katika ushiriki wao wa michuano ya kimataifa ambapo mwakani itaiwakilisha Tanzania katika Kombe la Shirikisho Afrika.

Kocha wa Juventus atupwa 'jela', kisa...Rushwa!

ROME, Italia MAHAKAMA ya Michezo ya Italia imemtupa 'jela' kocha wa mabingwa wa nchini humo, Juventus, Antonio Conte kwa muda wa miezi 10 jana kwa kosa la kushindwa kuripoti tukio la upangaji matokeo ya mechi katika kashfa ya kamari ya upangaji matokeo ambayo imetikisa soka ya Italia, shirikisho la soka limesema. Kocha huyo aliyeiongoza Juventus kutwaa ubingwa wa Serie A msimu uliopita, ameadhibiwa kwa mechi mbili za Siena za Mei 2011, wakati akiwa kocha wa timu hiyo ya daraja la kwanza, Serie B. Mahakama hiyo ilimuachia beki wa klabu hiyo Leonardo Bonucci na winga wa kulia Simone Pepe kwa kuwaona hawakuhusika na kashfa hiyo. Waendesha mashitaka walisema kundi la wacheza kamari maharamia wa kimataifa lilikuwa likilipa wachezaji ili wafungishe timu zao katika kashfa ya upangaji matokeo michezoni ambayo inafanana na ile iliyochafua sifa ya soka ya Italia katika miaka ya 1980. Shirikisho la Soka Tanzania, TFF, mpo!
Chanzo: Reuters

Mabeki wa pembeni waipa presha Simba

BAADHI ya wanachama na mashabiki wa klabu ya soka ya Simba, wameanza kuwa na wasiwasi na uwezo wa timu yao, wakiushauri uongozi kushirikiana na benchi la ufundi kuhakikisha wanaimarisha safu ya ulinzi hususani mabeki wa pembeni. Wanachama na mashabiki hao wamedai kuingiwa na wasiwasi kutokana na matokeo ya hivi karibuni iliyopata timu yao ikionekana kupwaya karibu kila idara jambo linalowatia shaka kama wataweza kutetea taji lao la Ligi Kuu Tanzania Bara. Mmoja wa wanachama hao, aliyeomba kuhifadhiwa jina lake, alisema beki za pembeni wa Simba zimepwaya na kukosekana watu wa kuifanya timu yao itishe kama ilivyozoeleka na kudai ukuta huo umeathiriwa kutokana na kuumia mara kwa mara kwa ajina Nassor Cholo na Amir Maftah. "Kwa miaka mingi Simba imekuwa ikisifika kuwa na 'ma-fullback' visiki na viungo imara, lakini kwa mechi kadhaa zilizopita tumebaini safu hizo zimepwaya na ajabu uongozi umeimarisha kiungo na kusahau beki hizo za pembeni," alisema mwanachama huyo. Naye mnazi mkubwa wa klabu hiyo Leila Mwambungu, alisema kuna haja viongozi na benchi la ufundi kuhakikisha wanasaka wachezaji wa pembeni mapema ili kuimarisha kikosi kabla ya kuanza kwa msimu mpya wa ligi kuu Septemba Mosi na michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika mwakani. "Safu ya ulinzi ya Simba ina tatizo hasa mabeki wa pembeni, hivyo viongozi na benchi la ufundi lifanyie kazi dosari hiyo mapema kabla ya kuanza kwa ligi ili tusije tukaumbuka," alisema Leila. Simba iliyong'olewa kwenye hatua ya Robo Fainali ya michuano ya Kombe la Kagame kwa kipigo cha mabao 3-1 toka kwa Azam, ilirejea kupokea kipigo kama hicho Jumatano iliyopita dhidi ya City Stars ya Kenya wakati wa sherehe za Simba Day zilizofanyika jijini Dar. Kabla ya kipigo hicho cha Wakenya, Simba ililazimishwa sare ya baoa 1-1 na Jamhuri ya Kenya katika michuano ya Super 8 baada ya kuongoza bao 1-0 katika pambano lililochezwa kwenye uwanja wa Chamazi, nje kidogo ya jijini Dar.

Sikia hii, eti :Kazimoto ni kama Xavi, Iniesta

MCHEZAJI nyota wa timu ya mpira wa kikapu ya ABC, Gilbert Batunga 'B10' amesema kwa sasa nchini hakuna kiungo mwenye kiwango cha kipekee kama alichonacho Mwinyi Kazimoto wa klabu ya Simba. Batunga, alisema kwa kiwango alichonacho Kazimoto kiuchezaji anaweza kumlinganisha na viungo nyota wa klabu ya Barcelona na timu ya taifa ya Hispania, Xavi na Andre Iniesta. Mkali huyo, alisema Kazimoto ana sifa zote za mchezaji wa nafasi yake na kudai iwapo kama atapewa nafasi zaidi huenda akafika mbali kwa sababu kokote anaweza kucheza. "Kwa kweli licha ya Tanzania kuwa na vijana wenye vipaji katika soka, binafsi sijaona kama Mwinyi Kazimoto. Huyu jamaa ana ujua na kuuchezea mpira, nadhani akipewa nafasi huenda akafika mbali na kuitangaza nchi kimataifa," alisema. Alisema, anaamini umahiri wake ndio ulioifanya Simba kuamua kumvua 'gwanda' toka JKT Ruvu ili wapate huduma zake, ingawa alisema hali ya majeruhi imekuwa ikimuangusha mkali huyo. Mwinyi Kazimoto, anayeichezea pia timu ya taifa, Taifa Stars alitua Simba msimu uliopita akitokea JKT Ruvu, amekuwa akitajwa kama mmoja wa viungo mahiri nchini kwa sasa akiwekwa kundi moja na wakali kama Salum Abubakar 'Sure Boy', Shaaban Nditi na wengineo.

Baada ya Chaguo, Richie ana Tamaa kwa Rado

BAADA ya kukamua vilivyo katika filamu ya 'Chaguo Langu', muigizaji mahiri nchini Single Mtambalike 'Richie', ameibuka katika kazi nyingine ambayo imekuwa ikifanya vema sokoni iitwayo 'Tamaa Yangu' ya msanii, Simon Mwapagata 'Rado'. Akizungumza na MICHARAZO, Rado alisema filamu hiyo miongoni mwa kazi zake tatu ambazo zimeingizwa sokoni hivi karibuni, ambapo mbali na 'Tamaa Yangu', nyingine ni 'Hatia' na 'XXL'. Rado alisema katika filamu ya 'Tamaa Yangu', mbali na Richie, pia ameigiza na wakali kama Deo Shija na mwanadada Regina Mroni, aliyewahi kutamba na filamu ya 'Aisha'. "Nimeachia kazi tatu kwa mpigo, XXL, 'Hatia' na 'Tamaa Yangu' ambayo nimeigiza na mkongwe Single Mtambalike, Deo Shija na Regina Mroni," alisema Rado. Kutoka kwa kazi hiyo ya 'Tamaa Yangu' kunamfanya Richie, aendelea kukimbiza sokoni miongoni mwa wakongwe wa fani hiyo kwani ni wiki kadhaa ameachia kazi yake mpya ya 'Chaguo Langu aliyoigiza na wakali kama Jacklyn Wolper na Adam Kuambiana. Kabla ya 'Chaguo Langu', Richie alitamba kwa muda mrefu na filamu ya 'Diana', aliyoigiza na Halima Yahya 'Davina' na Sabrina Rupia 'Cath'. Mkongwe huyo aliyewahi kutamba akiwa na makundi ya Mambo Hayo na Kamanda Assemble yaliyokuwa wakionyesha michezo yake kwenye vituo vya ITV na CTN, kwa sasa inaelezwa yupo 'location' kwa ajili ya kufyatua kazi nyingine mpya.

TAFF, Bongo Movie, wasambazaji waungana kudhibiti wezi

MAKAMPUNI ya usambazaji wa kazi za wasanii kwa kushirikiana na Shirikisho la Filamu Tanzania, TAFF na Mamlaka ya Mapato Tanzania, TRA, wameungana pamoja na kutangaza 'vita' dhidi ya maharamia na wezi wa kazi za wasanii kwa lengo la kukomesha vitendo hivyo. Wasambazaji hao, Steps Entertainment, PAPAZI, Msama Promotions na wengine wameamua kushirikiana na TRA, Bongo Movie na TAFF kwa nia ya kukomesha vitendo hivyo sawia na kulinda masilahi ya wasanii ambao wamenyonywa kwa muda mrefu. Wakizungumza katika mkutano uliofanyika jana jijini Dar es Salaam
viongozi wa 'umoja' huo walisema umefika wakati wa kukomesha tatizo hilo la muda mrefu ambalo limekuwa likiwakatisha tamaa wadau wa sanaa nchini. Rais wa TAFF, Simon Mwakifwamba, alisema wameona hakuna njia ya kukomesha hilo kama sio kufanya kazi kwa pamoja katika kulishughulikia akidai anashangazwa na kukithiri kwa hali hiyo ilihali kuna sheria juu ya udhibiti wa jambo hilo. Alisema, mbali na muunganiko wao, pia wanaiomba serikali kutekeleza ahadi yake ya kuwasaidia wasanii kupambana na maharamia, aliodai wapo kila pembe ya nchi hii wakifanya uhalifu wao kwa kujiamini kana kwamba wapo juu ya sheria. Mwakifwamba aliongeza kwa kusema lau kazi za wasanii zitasimamiwa vizuri, zitaliongezea taifa pato kubwa kw avile soko la sanaa kwa sasa limekuwa na mafanikio makubwa ingawa bado inawanufaisha wachache. Naye Mwenyekiti wa Bongo Movie, Jacob Steven 'JB' alisema sanaa inaweza kuwa na nafasi ya tatu kwa kuchangia pato la taifa ukiacha pato linalotokana na sekta za madini, maliasili na utalii. Kwa upande wa TRA, Meneja Usimamizi, Msafiri Ndimbo alisema Mamlaka hiyo imejipanga kudhibiti wizi wa kazi hizo kuanzia Januari mwakani baada ya serikali kupitia Bunge lake kukubalina kuweka mikakati ya kupamba na suala hilo.

Wednesday, August 8, 2012

Azam yazidi kung'ang'ania Redondo yaionya Simba

WAKATI kiungo Ramadhani Chombo 'Redondo' akisisitiza kuwa, hana mkataba na klabu ya Azam na ndio maana ameamua kusaini kuichezea Simba, uongozi wa klabu ya Azam umeendelea kushikilia msimamo kwamba kiungo huyo ni mali yao na Simba 'imeliwa'. Katibu Mkuu wa Azam, Idrissa Nassor alisema wao sio wehu wakurupuke kung'ang'ania kwamba Redondo ni mali yao iwapo hawana mkataba nae na kudai Simba wanajisumbua na kuweza kuwakuta kama lililowakuta kwa mchezaji Ibrahim Juma 'Jebba' waliokuwa wakimng'ang'ania kutaka kumsajili. Nassor ambaye ni maarufu kwa jina la 'Father' alisema, Redondo ni mali yao kwa vile wana mkataba utakaomalizika mwakani mwezi Juni, na hivyo Simba kama wanamhitaji kiungo huyo ni wajibu wa kuzungumza nao ili wawape kwa utaratibu unaotakiwa. "Sio sio wajinga kumng'ang'ania Redondo, pia hatuwezi kumzuia iwapo anataka kwenda Simba, ila taratibu zinatakiwa kufuatwa kwa vile tunaye mkataba nae unaomalizika Juni mwaka 2013," alisema Nassor. Alisema kinachoendelea kwa Simba na Redondo hakutofautiani na sakata la Jebba ambaye Simba ilidai kumsajili na kwenda nae kwenye michuano ya Ujirani Mwema kabla ya kubaini kwamba walikuwa wakijisumbua kutokana na ukweli mchezaji huyo alikuwa na mkataba na Azam. Hata hivyo Redondo akizungumza na vyombo vya habari jana, alisema yeye hana mkataba na Azam kwa vile mkataka wake wa awali ulishaisha tangu Juni mwaka huu, pia akisema kilichomfanya aondoke ni kutoitwa na viongozi kupewa mkataba mpya. Pia alisema 'kifungo' cha miezi minne alichopewa na uongozi wa Azam kwa tuhuma za utovu wa nidhamu ni sababu nyingine iliyomfanya 'aipe' kisogo timu hiyo na kutua Simba ambayo aliichezea kabla ya kutua Azam misimu miwili iliyopita.

Safari ya Sikinde Marekani 'yaiva'

BENDI ya muziki wa dansi ya Mlimani Park 'Sikinde', imesema itaondoka nchini kwenda Marekani, kushiriki matamasha ya kimataifa mara baada ya sikukuu ya Idd inayotarajiwa kusherehekewa mwishoni mwa mwezi huu. Katibu wa bendi hiyo, Hamis Milambo alisema mipango ya safari imekamilika ikiwemo kurejea kwa viongozi na wanamuziki wao waliokuwa nchini humo kuweka mambo sawa. Alisema viongozi hao, Hassani Bitchuka 'Stereo' na Ally Jamwaka waliowawakilisha katika mazungumzo juu ya safari hiyo walisharejea na kusema kuwa kila kitu kimeenda sawa na kilichobaki ni kukamilisha mipango ya safari yao. "Kila kitu kimeenda sawa huko Marekani na viongozi na wanamuziki wetu wamesharejea na kwa sasa tunajipanga kwa ajili ya safari hiyo ambayo itafanyika baada ya kumalizika kwa sikukuu ya Idd," alisema. Aliongeza kuwa wakati wakijiweka tayari kwa ziara hiyo, pia bendi hiyo inaendelea na mipango ya kuzimalizia nyimbo mbili zilizosalia katika albamu ijayo sawia na kujiandaa na mpambano wao na watani zao, Msondo Ngoma. Msondo na Sikinde zinatarajiwa kuchuana katika maonyesho mawili yatakayofanyika katika miji ya Dar na Zanzibar wakati wa sikukuu ya Idd.

Rado awabeba 'Watoto wa Kanumba'

NYOTA wa filamu ambaye pia ni msanii wa muziki wa kizazi kipya, Simon Mwapagata 'Rado' ameachia filamu mbili mpya za 'Hatia' na 'Tamaa Yangu', huku akijiandaa kufyatua nyingine iitwayo 'Madduhu'. Alisema filamu hiyo imesharekodiwa ikiwa imewashirikisha wasanii chipukizi
walioibuliwa na marehemu Steven Kanumba katika filamu zake za 'This is It', 'Uncle JJ' na 'Big Daddy'. Alisema anaendeleza vipaji vya wasanii chipukizi ili kuenzi mchango na juhudi za Kanumba, aliyemtaja kama msanii aliyekuwa akimzimia na kuchangia kwake kutumbukia kwenye sanaa japo alisaidiwa na Jumanne Kihangale 'Mr Tues'. "Nimeingiza sokoni filamu zangu za 'Hatia', 'Tamaa Yangu' na 'XXL', wakati nikiwa nimesharekodi filamu yangu mpya iitwayo 'Madduhu' niliocheza na 'watoto wa Kanumba', kama njia ya kuendeleza vipaji vyao na kumuenzi," alisema. Rado aliwataja wasanii hao chipukizi alioigiza nao katika filamu hiyo aliyopanga kuitoa mwezi ujao kuwa ni pamoja na Hanifa Daudi 'Jennifer', Jamila Jailawi na Jalillah Jailawi. Alisema licha ya kuendekeza 'libeneke' kwenye fani ya uigizaji akifyatua kazi zake binafsi baada ya kipindi kirefu kuzifanya kazi za wenzake, pia anaendelea kukamua kwenye muziki kama kawaida. "Siwezi kuacha muziki, mie nagonga vyote kwani hivi ni vipaji ambavyo Mungu kanijali na siwezi kuzembea kuvitumia," alisema msanii huyo aliyepata umaarufu kupitia tamthilia ya 'Jumba la Dhahabu' enzi hizo akiwa na kundi la Fukuto Arts Proffesional.

Mtanzania kuwania taji jipya la IBF/USBA

MTANZANIA Rajabu Maoja anatarajiwa kuwa bondia wa kwanza wa Tanzania kuwania taji jipya la IBF Afrika, Mashariki ya Kati na Ghuba ya Uajemi, lililoanzishwa na Shirikisho la Kimataifa la Ngumi za Kulipwa, IBF/USBA. Kwa mujibu wa Rais wa IBF/USBA kwa nchi za Afrika na Ghuba ya Uajemi, Onesmo Ngowi, Mtanzania huyo atapamba ulingoni Septemba 1, mjini Windhoek, Namibia kupigana na bingwa wa nchi hiyo, Gottlieb Ndokosho. Ngowi alisema IBF/USBA limeanzisha taji hilo kwa nia ya kupanua wigo kwa mabondia wa Afrika, Mashariki ya Kati na Ghuna ya Uajemi kujitangaza zaidi katika mchezo huo kupitia IBF/USBA. "Katika mpango kabambe wa kupanua wigo wa mabondia wa Bara la Afrika na wale wa Mashariki ya Kati na Ghuba ya Uajemi, IBF.USBA imezindua taji jipya litakalojulikana kama 'IBF Africa, Middle East and Persian Gulf Title'," alisema Ngowi. Ngowi alisema pambano la kwanza la taji hilo linalojulikana kwa kifupi kama IBF/AMEPG, litafanyikia nchini Namibia likimhusisha Maoja na Ndokosho. Alisema pambano jingine linatarajiwa kufanyika katika jiji la Accra, Ghana kati ya bondia Richard Commey wa Ghana anayejifua kwa sasa nchini Uingereza atakayepigana na bondia kutoka Qatar ambayo iko katika Ghuba ya Uajemi. Ngowi ambaye ni Rais wa Kamisheni ya Ngumi za Kulipwa Tanzania, TPBC, alisema juhudi hizo za IBF/USBA zinakuja wakati shirikisho hilo limeanzisha programu ya 'Utalii wa Michezo' na kuziteua Tanzania na Ghana kama nchi za mfano kwa kipindi cha miaka mitatu. Aliongeza fura iliyojitokeza ni fursa nzuri kwa mabondia wa Tanzania kuzichangamkia nafasi hiyo kuweza kuwania mataji makubwa na kujitambulisha kimataifa. Ngowi alibainisha kuwa kwa sasa ni mabondia wachache sana wa Tanzania wenye viwango vya juu ukilingamisha na mabondia wa nchi za Ghana, Namibia, Afrika ya Kusini, Uganda, Nigeria na Misri. Aliahidi kuwapatia mabondia wa kitanzania nafasi za kugombea mataji haya kila panapotokea nafasi hizi ili kuweza kufika walipo wenzao. Mwisho

Kiiza 'awafunika' Okwi, Ssentongo Uganda

MSHAMBULIAJI nyota wa kimataifa wa timu ya Yanga, Hamis 'Diego' Kiiza ameshinda tuzo ya Mchezaji Bora wa Uganda kwa mwezi Julai akiwafunika nyota wengine wa nchi hiyo mshambuliaji anayeichezea Simba, Emmanuel Okwi. Kwa mujibu wa mtandao wa habari za michezo wa Kawowo, Kiiza anayeichezea pia timu ya taifa ya Uganda 'The Cranes' alitangazwa kuwa mshindi wa tuzo hiyo ya Julai na Chama cha Waandishi wa Habari za Michezo nchini Uganda, USPA. Mtandao huo ulisema kuwa, Kiiza alifanikiwa kupata jumla ya kura 520, pointi 100 zaidi na aliyeshika nafasi ya pili katika uwaniaji wa tuzo hiyo, kinda la timu ya taifa ya vijana U20, Julius Ogwang aliyevuna pointi 420. Imeelezwa Kiiza amefanikiwa kupata tuzo hiyo kutokana na kuiwezesha Yanga kutwaa ubingwa wa Kombe la Kagame, kwa mara ya pili mfululizo, huku ikimfagilia kwamba licha ya kuibebesha klabu yake ubingwa, pia alinyakua kiatu cha dhahabu cha ufungaji bora kwa mabao sita aliyoyafunga. Hata hivyo ukweli aliyenyakua tuzo hiyo ni Said Bahanunzi pia wa Yanga aliyeifunga idadi kama hiyo ya mabao sita akilingana na Taddy Etekiama wa AS Vita, wakati Kiiza alionekana idadi hiyo ya mabao sita kwa kuongezewa kimakosa bao la beki Stephano Mwasika. Mbali na Kiiza na Ogwang, mwingine aliyekuwa katika Tatu Bora ya waliong'ara mwezi Julai ni mchezaji wa mpira wa wavu, Lawrence Yakan wa mabingwa wa michuano ya kimataifa ya Wavu ya Kampala (KAVC), Sport-S, aliyepata kura 415. Mwisho

Saturday, August 4, 2012

Mfano yaingiza sokoni Jasho la Mnyonge

FILAMU mpya iliyoandaliwa na kampuni ya uandaaji na usambazaji wa filamu ya Mfano Entertainment na kupewa jina la 'Jasho la Mnyonge' imeingizwa sokoni. Mkurugenzi wa kampuni hiyo na mtunzi wa filamu hiyo, Said Muinga 'Dk. Mfano', alisema filamu hiyo yenye ujumbe mahususi kwa jamii kuhusiana na vitendo viovu tayari ipi sokoni katika mikoa mbalimbali. Alisema kuwa filamu hiyo inaonyesha jinsi gani imani haba za kutaka utajiri wa haraka haraka inavyoweza kupelekea mauaji ya kutisha hasa kwa watu wenye ulemavu wa ngozi (albino). Muinga alisema kuwa kupitia katika filamu hiyo Watanzania watajionea jinsi wanavyoweza kujiingiza kwenye vitendo vya mauaji kwa ajili ya kujipatia utajiri wa haraka kutokana na kudanganywa na waganga 'feki' wa kienyeji. "Tumeingiza sokoni filamu yetu mpya ya 'Jasho la Mnyonge' , hivyo wapenzi wa filamu nchini ambao walikuwa wakiisubiri kwa hamu kubwa wanaweza kuipata kupitia kwenye maduka mbalimbai yanayojihusisha na uuzaji wa filamu, "alisema Muinga ambaye miezi kadhaa iliyopita aliingiza sokoni filamu nyingine ya 'Yai Viza' ambayo inaendelea kufanya vizuri kwa mauzo. Alisema kuwa zoezi la upigaji picha za filamu hiyo lilifanyikia katika maeneo mbalimbali kulingana na ujumbe husika ikiwemo kwenye misitu mikubwa, maeneo ya vijijini na mjini. Muinga alisema kuwa katika filamu hiyo amewashirikisha wasanii 'mastaa' pamoja na chipukizi lakini ambao wamefanya vizuri katika nafasi zao walizocheza.

Mwanahawa Ally 'Chipolopolo'; Binamu wa Mchizi Mox anayemzimia Barthez, Yanga

HAKUNA kinachomliza muimbaji anayekimbiza nchini kwa sasa katika miondoko ya taarab, Mwanahawa Ally 'Chipolopolo' kama kumshuhudia baba yake mzazi, Ally Rashid 'Mwana Zanzibar' akitelekezwea na baadhi ya wadau na wanamuziki wenzake. Mwanahawa alisema baba yake aliyewahi kutamba na bendi za Urafiki Jazz, Bima Lee, Shikamoo Jazz na Msondo Ngoma, kama mpuliza 'saksafone', alipatwa na kiharusi karibu miaka mitatu iliyopita alipoanguka ghafla akienda mazoezi ya bendi ya Msondo. Alisema tangu apate maradhi hayo baba yake hawezi kutembea wala kuzungumza akijiuguza nyumbani kwake, Keko Machungwa huku hakuna yeyote anayeenda kumjulia hali. Mwanahawa alisema kitendo hicho mbali na kumtia simanzi, pia kinampa somo kubwa katika shughuli zake za muziki akiamini thamani ya msanii huwa ni pale tu anapokuwa mzima kiafya na si vinginevyo. Alisema, cha kustaajabisha ni kwamba baadhi ya wanamuziki aliofanya kazi na babaye wanaishi karibu eneo la Keko Machungwa, lakini hawana muda wa kwenda kumjulia hali kujua anaendeleaje. "Kwa kweli hali inayomkuta baba inaniumiza na kuonyesha jinsi gani wanamuziki tusivyopendana wala kuthaminiana, tunapendana kinafiki hasa tukiwa wazima, wakati wa matatizo kila mtu hujifanya yupo 'bize', hii sio sawa inaondoa upendo baina yetu." Mwanahawa aliyepitia makundi ya Dar Modern, Zanzibar Stars, Super Shine kabla ya kupaishwa na kundi King's Modern 'Wana Kijoka Chazima Taa', alisema lazima wadau na wasanii nchini wabadilike. "Tubadilike na kusaidia kwa hali na mali muda wakati wote, kila nimuonapo baba jinsi anavyoshindwa kutembea na kuzungumza roho inaniuma kwa uchungu," alisema. URITHI Mwanahawa Ally aliyebatizwa jina la Chipolopolo alipokuwa Dar Modern ili kutofautishwa na mkongwe Mwanahawa Ally, alizaliwa mwaka 1986, Jang'ombe Zanzibar akiwa ni mtoto wa pili kati ya wanne kwa mamaye na wa saba kati ya tisa kwa baba yake aliyeoa zaidi ya mke mmoja. Alisoma Shule ya Msingi Mgulani, kabla ya kutumbukia kwenye muziki akifuata nyayo za babaye na binamu yake Taikun Ally 'Mchizi Mox'. Licha ya kurithi kipaji cha muziki toka familia yake, alikiri kuvutiwa kisanii na Zuhura Shaaban na kupenda kuimba nyimbo za wajina wake, Mwanahawa Ally kulichangia kujitosa kwake kwenye uimbaji. "Tangu utotoni nilipenda kusikiliza na kuimba nyimbo za Mwanahawa Ally na nilivutiwa na Zuhura Shaaban ninayemzimia mpaka leo kuliniingiza kwenye uimbaji, ingawa wazazi wangu hasa baba walichangia mimi kuingia katika fani," alisema. Safari yake kisanii ilianza mwaka 2005 wakati mama yake alipompeleka East African Melody kufanyiwa usaili na aliposhindwa kuchukuliwa alikimbilia Zanzibar Stars na kupokewa akipewa nafasi ya kuimba nyimbo za 'kopi'. Mwaka 2009 aliondoka ZNZ Stars na kutua Super Shine ambako pia hakupewa nafasi na lilipoanzishwa kundi la Victoria Modern mwaka 2010, alitua huko na kufyatua nao nyimbo mbili za 'Mtoto Kibamba Best' na 'Habib Chocolate'. Victoria liliposambaratika mwaka jana kulimfanya Mwanahawa anayependa kula wali 'ndondo' kwa samaki na kunywa juisi ya embe, kujiunga na King's Modern na jina lake kung'ara kupitia nyimbo za 'Dunia Duara' na 'Mchumia Juani'. Baada ya King's kumng'arisha jambo ambalo linamfanya kutolisahau kundi hilo na hasa mkurugenzi wake, Hamis Mshewa 'Majaliwa' wiki iliyopita alinyakuliwa na T-Moto kwa alichodai kusaka masilahi zaidi akitarajiwa kutambulishwa rasmi Sikukuu ya Idd. "Ukiwaondoa wazazi wangu, anayefuatia kwa shukrani ni Mkurugenzi wangu wa zamani Majaliwa na mchumba'ngu Juma Majala kwa walivyonisaidia kisanii," alisema. BARTHEZ Mwanahawa, anayekerwa na baadhi ya wasanii wa taarab kutojiheshimu na kupenda kuimba 'vijembe', alisema yeye ni 'kichaa' wa soka akiishabikia klabu ya Yanga. Alisema anayemzimia katika kikosi hicho ni kipa Ally Mustafa 'Barthez' hasa kwa alivyoisaidia Yanga kutwaa taji la michuano ya Kagame 2012. "Naipenda Yanga na ninamzimia Barthez, sio siri kipa huyu na wachezaji wengine walitubeba katika Kagame kwa kutimiza wajibu wao uwanjani," alisema. Mwanahawa anafurahia sanaa kumwezesha kununua kiwanja kilichopo Gongolamboto na kumiliki 'Video Library', alizungumzia muziki wa Bongofleva akidai ni mzuri akimtaja Ally Kiba kama anayemzimia kisanii. Hata hivyo alisema muziki huo na wasanii wake wanapaswa kubadilika kwa kuachana na tabia ya kufanya maonyesho yao kwa 'play back' badala yake wapige 'live'. "Wakiachana na mtindo huo watatamba sana, ila kwa sasa itawachukua muda mrefu kutufikia sisi wengine mahali tulipo kimuziki," alisema. KIDUKU Mwanahawa ambaye hajaolewa ingawa ana watoto wawili, Salma, 8 anayesoma darasa la nne na Mahmoud,4 aliyepo chekechea, alisema ubunifu uliofanywa na makundi ya taarab ya kuwa na vijana wa kucheza 'kiduku' umesaidia kuinua soko la muziki huo. Alidai wanaoponda mtindo huo wanashindwa kuelewa kuwa dunia imebadilika, licha ya kukiri suala la kutojiheshimu kwa baadhi ya wanamuziki na mashabiki wa taarab hasa katika mavazi na uchezaji unapunguza ustaarabu uliozoeleka. Mwanadada huyo anayechizishwa na rangi nyekundu, alisema hakuna tukio la furaha kwake kama aliposhindanishwa na wakali wa taarab nchini Khadija Kopa, Mariam Khamis 'Paka Mapepe na Isha Mashauzi katika shindano la Nani Mkali. Matarajio ya kimwana huyo anayependa kutumia muda wake za mapumziko kujitenga na watu ili kutuliza kichwa chake, ni kuja kutamba kimataifa na kupanua biashara zake pamoja na kuanzisha asasi ya kusaidia watu wenye matatizo. Mwanahawa aliyekitaja kibao cha 'Dunia Duara' kama bomba kwake, alizungumzia ugonjwa wa Ukimwi, akisema ni tishio na jamii iache kuuchezea akiwataka watu wawe makini kwa kujiheshimu na kujikinga nao akisisitiza watu kuwa waaminifu. Mwisho

Friday, August 3, 2012

Ngassa hatimaye akubali kutua Simba, wanachama wasubiri maelezo mkutano wa Jumapili

NYOTA wa kimataifa wa klabu ya Azam na Taifa Stars, Mrisho Ngassa ambaye juzi alinukuliwa kuigomea klabu yake kumpeleka Simba, hatimaye mchezaji huyo ameridhia kwenda mwenyewe Msimbazi baada ya kuahidiwa mambo mazuri katika klabu hiyo mpya. Hata hivyo kuna taarifa kwamba licha ya uongozi wa Simba kufanikiwa kumweka sawa mchezaji huyo, baadhi ya wanachama wamekuwa na mashaka na mchezaji huyo wakiamini ni mnazi mkubwa wa Yanga na hivyo watatoa hatma yake kwenye mkutano wa wanachama utakaofanyika siku ya Jumapili. Baadhi ya wanachama wa klabu hiyo waliiambia MICHARAZO kwamba hawaamini kama Ngassa atacheza kwa mapenzi katika timu yao na pia kuhoji uongozi kitu gani kilichoufanya umchukue mchezaji huyo. Ngassa alinukuliwa jana kuwa yu tayari kuichezea Simba kwa vile yeye hana mapenzi na klabu yoyote zaidi ya kulitumikia soka na mchana huu alitarajiwa kutambulishwa rasmi na uongozi huo kwa waandishi wa habari. Winga huyo aliyewahi kung'ara na timu za Toto Afrika, Kagera Sugar na Yanga kabla ya kwenda Azam, ametua Simba kwa mkopo ikidaiwa kalipwa kiasi cha Sh. Milioni 30 na gari aaina ya Verosa na atakuwa kilipwa mshahara wa Sh Milioni2 kwa mwezi. Pamoja na sakata la mchezaji huo kuonekana limeisha baada ya Azam na Simba kumalizana kufuatia Yanga kushindwa katika mbio za kumwania kumrejesha Jangwani, wanachama wa Simba wamesisitiza kuwa uongozi wao unapaswa kuwapa majibu ya kuridhisha katika mkutano wao siku ya Jumapili. Mmoja wa wanachama hao ambao yupo kwenye baraza la wazee wa klabu hiyo (jina tunalo) alisema wameshangazwa na uongozi wao kumnyakua Ngassa kabla hata hawajalimaliza sakata la beki wao Kelvin Yondani aliyetimkia Yanga, huku ikidaiwa ana makataba nae. "TUnajua soka ndivyo lilivyo, lakini naamini Ngassa anaweza asicheze kwa kiwango chake kama alivyo kwa sababu ya watu kumhisini ana uyanga, ila viongozi wajiandae Jumapili kutueleza kilichotokea na namna Yondani alivyotukimbia," alisema mwanachama huyo. Kelvin Yondani, aliyekuwa akituhumiwa kuwa mnazi wa Yanga, aliitema Simba mara baada ya kumalizika kwa ligi kuu msimu uliopita na kutua Yanga ambapo aling'ara kwenye michuano ya Kombe la Kagame. Pengo la Yondani lilionekana wazi kwenye kikosi cha Simba kilichotolewa hatua ya robo fainali kwa kunyukwa mabao 3-1 na Azam.

Okwi afuzu majaribio yake Austria

MSHAMBULIAJI tegemeo wa mabingwa wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara, Simba, Emmanuel Okwi amefuzu majaribio ya kucheza soka la kulipwa katika klabu ya Redbull Salzburg ya nchini Austria alikoenda kwa majaribio ya wiki mbili, Makamu Mwenyekiti wa Simba, Geofrey Nyange 'Kaburu' alisema jana. Hata hivyo, Okwi ambaye hakuwepo wakati Simba ikiishia robo fainali ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati (Kombe la Kagame), atarejea nchini wakati wowote ili kutibiwa malaria ambayo inamsumbua tangu alipotua Austria, alisema Kaburu. Aliongeza kuwa Simba inatarajia kulipwa Euro 600,000 kwa ajili ya kukamilisha uhamisho wa mshambuliaji huyo anayeichezea pia timu ya taifa ya Uganda (Cranes). Kaburu alisema kuwa wako katika hatua za mwisho za kukamilisha uhamisho huo na wamefurahi kuona Okwi anapata timu Ulaya na kutimiza ndoto zake. Alisema pia Simba tayari imemsajili beki wa APR, Mbuyi Twite na atatua nchini wakati wowote kabla ya tamasha la Simba Day ambalo litafanyika Agosti 8 mwaka huu kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam. Alieleza kuwa Simba imeingia mkataba wa miaka miwili na beki huyo ambaye anachukua nafasi ya Lino Masombo aliyeachwa baada ya kiwango chake kutoridhisha. Wakati huo huo, taarifa kutoka Simba zinaeleza kwamba wachezaji wake wengine chipukizi watano wa Simba B ambao walikwenda Ujerumani na timu yao ya kituo cha soka cha jijini Mwanza wamepata timu mbalimbali za kuchezea za Ujerumani na Austria. Habari zinaeleza kwamba wachezaji hao watarejea nchini na klabu hizo zitaanza taratibu za kuingia nao mikataba. Wachezaji hao yosso waliong'aa ni pamoja na kipa Aboubakar Hashim, Said Ndebla, Miraji Athumani, Frank Sekule (washambuliaji) na Hassan Hassan. Mwaka jana Simba ilimuuza mshambuliaji Mbwana Samatta kwa TP Mazembe kwa dola za Marekani 150,000 na baadaye Patrick Ochan. CHANZO:NIPASHE

Mobby Mpambala ala shavu Pilipili

MKALI wa filamu za mapigano nchini, Mobby Mpambala amelamba dume katika kampuni ya Pilipili Entertainment baada ya kupewa shavu la kutengeneza filamu mpya iitwayo 'The Same Plan'. Akizungumza na MICHARAZO, Mpambala aliyedai sehemu kubwa ya mafanikio yake kimaisha na kisanii yamechangiwa na mkewe, Jasmine, alisema kampuni ya Pilipili imempa nafasi hiyo baada ya kukutana nao katikati ya wiki iliyopita ili kufanya nao kazi. Mpambala, alisema katika mzungumzo yao na kampuni hiyo waliafikiana kufyatua kazi ya utambulisho na kudai tayari yu mbioni kuandaa filamu iitwayo 'The Same Plan', aliyodai itawashirikisha wakali kadhaa wa fani hiyo nchini ambao hata hivyo hakuweza kuwataja majina. "Namshukuru Mungu, neema zinazidi kunifungukia baada ya Pilipili Entertaiment kunipa shavu la kufanya nao kazi na natarajia kutoa filamu ya kwanza iitwayo 'The Same Plan'," alisema. Aliongeza tenda hiyo mpya imekuja wakati akijiandaa kutoa kazi mbili kwa mpigo zilizokamilika kupitia kampuni yake ya Wazagi za 'Fuvu' na Anti Virus'. Mpambala, alisema hawezi kujivunia mafanikio yote aliyonayo bila kumshukuru mkewe Jasmine, ambaye alitoka nae mbali kabla hata hajapata umaarufu kama alionao, licha ya kukiri alishakuwa na mwanamke mwingine aliyezaa nae watoto watatu na kuachana nae na pia kuoa mke mpya, Zolla. "Hakuna siri siri ya mafanikio yangu ukiondoa baraka za Mungu na za wazazi, pia mke wangu ni sehemu ya haya yote, ndio maana nimefika hapa hata kupata tenda kama ya Pilipili," alisema. Mwisho

Klabu ya Azam yafafanua sakata la Ngassa

TAARIFA hii imetolewa na Meneja wa klabu ya Azam, Patrick Kahemela Klabu ya Azam FC inapenda kutoa taarifa ya ufafanuzi juu ya sakata la mchezaji Mrisho Ngasa ambalo linaonekana kupotoshwa 1. Azam FC ilitangaza kuwa biashara ya mchezaji Mrisho Ngasa ingefungwa siku ya Jumatano 1/08/2012 saa saba mchana na ilivitaka vilabu vyenye interest na mchezaji huyo kufika makao makuu ya Azam FC ofisi ndogo zilizopo kwenye kiwanda cha unga cha Azam-Mzizima zikiwa na pesa taslimu. Bei ya mauzo iliyopangwa ilikuwa ni Dola 50,000. Lakini katika mawasiliano ya email kwa makatibu wakuu wa Simba na Yanga, Azam FC iliweka bayana kuwa ilikuwa tayari kushusha bei ya mauzo na ingemuuza Ngasa kwa timu ambayo dau lake lingekuwa kubwa zaidi ya mwenzake. Kwa maana hiyo biashara ya mchezaji mrisho ngasa ilifanyika kwa uwazi. Lengo la Azam FC lilikuwa ni kutoa haki kwa kila klabu yenye uwezo wa kifedha kuweza kupata huduma ya Ngasa. Pia tunaomba ifahamike bayana kuwa mchezaji Mrisho Ngasa alipewa taarifa kuwa anauzwa na aliombwa asaidie kushawishi klabu anayoitaka ifike kwetu na ofa yake. Ngasa alitamka bayana kuwa yupo tayari kwenda klabu yoyote ambayo Azam FC itaona imekidhi mahitaji yake kwa masharti kuwa maslahi yake ya kimkataba kati yake na Azam FC yazingatiwe. 2. Hadi kufikia siku ya Jumatano 01/08/2012 saa saba mchana. Ni klabu ya Simba pekee iliyojibu kwa maandishi na kuonesha nia ya kumchukua Ngasa. Yanga wao hawakuwahi kujibu email, ingawa kwa majibu ya simu Mjumbe wao wa Kamati ya usajili Bw Sefu Magari alitangaza kuwa Ngasa hana thamani ya zaidi ya milioni 20. Na Yanga haikuwa tayari kuboresha ofa yake. 3. Muda wa kufungwa kwa biashara ya kumuuza Ngasa ulipofika, ni simba pekee kupitia kwa makamu Mwenyekiti wake Bw Geofrey Ngange na Mhasibu wake ndiyo waliofika wakiwa na pesa taslimu shilingi milioni 25. Yanga hawakuonekana na hawakutaka kupokea hata simu walizokuwa wakipigiwa kuulizwa kama wana interest. 4. Kikao cha dharura cha Azam FC kilikaa na kuamua kuwa biashara ya kumuuza Ngasa ilishindikana kutokana na kutokupatikana kwa mnunuzi mwenye dola 50,000. Kwa maana hiyo Azam FC iliamua kumpeleka Ngasa kwa mkopo kwenye klabu iliyofika na kuonesha nia ya kumhitaji (Simba) 5. Simba walipewa sharti la kuhakikisha wanamlipa Ngasa mshahara wake kamili (TZsh 2,000,000) pamoja na stahiki zake nyingine zote za kimkataba 6. Sababu za kumpeleka Ngasa kwa mkopo ni kumuepusha na adhabu ambayo klabu ya Azam FC ingetoa kwa Ngasa kama angebaki. 7. Azam FC inapenda kuweka wazi kuwa haijamlazimisha Ngasa kwenda Simba kama inavyopotoshwa. Kama Ngasa anataka kuvunja mkataba wake au kama Yanga bado wanamhitaji basi waje na dola 50,000 na Azam FC itawauzia kwani licha ya kwamba amepelekwa kwa mkopo simba lakini Ngasa bado ni mali ya Azam FC 8. Tunaomba kuweka msimamo wetu kuwa hatupo tayari kumlipa Ngasa na kuvunja mkataba wake na hatuna sababu ya kufanya hivyo. Kama Ngasa hataki kwenda tunakompeleka Azam FC inamruhusu kubakia klabuni na kutumikia adhabu. 9. Lakini Ngasa na washauri wake waelewe kuwa akiamua kubaki Azam FC atakaa nje ya uwanja kwa muda wote uliosalia kwenye mkataba wake, kwani Azam FC haipotayari kumvisha jezi mchezaji anayefanya vitendo vya utovu wa nidhamu. 10. Kwa kuwa Sakata hili limeanza kuhusishwa na sakata la Mchezaji ramadhani Chombo. Naomba nitoe ufafanuzi kama ifuatavyo. Redondo alipewa option tatu za kuchagua baada ya kufanya vitendo vya utovu wa nidhamu timu ilipokuwa safarini Mwanza. a. Kupelekwa kwa mkopo Moro United? b. Kupatikana kwa mnunuzi mwenye shilingi milioni 40 c. Kukubali adhabu ya kufungiwa kwa miezi mitatu na kulipwa nusu mshahara wahati akitumikia adhabu. Redondo alithibitisha kuipenda Azam FC kwa kukataa kuuzwa au kupelekwa kwa mkopo. Alikubali kutumikia adhabu yake na ilipoisha alirudi na kuomba msamaha na sasa ni mmoja kati ya wachezaji wenye nidhamu ya hali ya juu sana. Azam FC inajivunia kuwa na mchezaji kama Redondo na bila kupepesa macho wala kung’ata maneno. Azam FC inamchukulia Redondo kama mtu spesho na mwenye mapenzi ya dhati na klabu yake na inamtaka aendelee kuwa na moyo huo.

Thursday, August 2, 2012

Baada ya kuiapa Yanga taji la Kagame, Saintfiet 'aibukia' Harambee Stars

MAKOCHA wa timu mbalimbali barani Afrika na waliowahi kufundisha soka barani humu, wametuma maombi ya kupata kazi ya kuifundisha timu ya taifa ya Kenya - Harambee Stars. Kwa mujibu wa kituo cha Supersport, ukiachana na makocha Otto Pfister, Adel Amrouche, Giuseppe Dossena, Ratomir Dujovic, Goran Stevanovic na Milovan Rojavic, kocha mkuu wa klabu ya Yanga kutoka Ubelgiji Tom Saintfeit nae ametuma maombi ya kutaka kuinoa Harambee Stars.
Tom Saintfiet ambaye bado hajatimiza hata mwezi mmoja tangu aje kujiunga na Yanga anapambana kocha wa zamani Ghana ambaye aliongoza Black Stars katika michuano ya African Cup of Nations 2012 na akatimuliwa baada ya timu kuondolewa kwenye michuano hatua ya nusu fainali. Japokuwa makocha ni wengi waliotuma maombi lakini Otto Pfitster anaonekana kuwa na nafasi kubwa kutokana na CV yake, akiwa tayari ameshazifundisha timu za Burkina Faso, DR Congo, Cameroon na Ghana. Pia tayari ameshachukua kombe la dunia la vijana chini ya miaka 17 na kikosi cha Ghana. Siku ya leo ndio shirikisho la soka la Kenya (FKF) kupitia kamati kuu watawatangaza makocha waliongia kwenye kinyang'anyiro cha mwisho katika kueleka kumteua kocha mkuu wa Harambee Stars. CHANZO:SHAFII DAUDA BLOGSPOT

Kocha wa Atletico ya Burundi kumrithi Stewart Azam?

KUSITISHWA mkataba kwa kocha wa Azam FC Stewart Hall kunamuweka kocha wa Atletico ya Burundi
katika nafasi nzuri ya kuifundisha timu hiyo. Baadhi ya vyombo vya habari nchini vimemkariri Stewart akikiri kusitishiwa mkataba wake huku akiweka bayana anafurahia kutimiza malengo makuu matatu katika klabu hiyo ikiwemo ujenzi wa Complex ya Chamazi, kuinua soka la vijana na kuiweka Azam katika chati ya juu katika soka la Tanzania. Uongozi wa Azam nao umekiri kuachana na kocha huyo ukidai kuwa walipofikishwa na kocha huyo kunahitaji mtu mwingine wa kuwaendeleza na kuzipuuza taarifa kwamba walimtimua Stewart kwa sababu ya kumpanga Ngassa katika mechi yao na Yanga kinyume na agizo lao. Hata hivyo uomgozi huo umesema kuwa wakati wakiendelea kumsaka kocha mpya timu itakuwa chini ya kocha wa vijana , Vivek Nagul na Kally Ongalla, ingawa taarifa ambazo bado hazijadhibitishwa ni kwamba Azam inamneyemelea kocha wa Atletico, Kaze Cedri aliyeufutia uongozi huo. Habari zilidai kuwa viongozi wa Azam walionyeshwa kuvutiwa na kocha huyo baada ya timu yake kuonyesha kandanda la kuvutia kwenye michuano hiyo. Ni siku ambayo ilicheza kandanda la kuvutia kwenye michuano ya Kagame Cup na kuichapa Yanga mabao 2-0, kabla ya kuoka sare na APR huku pia ikisakata kabumbu la uhakika. Aidha inaelezwa kuwa kutua kwa Cedri Azam itaisaidia klabu hiyo kupunguza gharama kubwa walizokuwa wakimlipa kocha huyo Muingereza ambaye aliwahi kuinoa timu ya taifa ya Zanzibar, Zanzibar Heroes kabla ya kunyakuliwa na Azam. Habari za ndani katika klabu hiyo zinasema kuwa Stewart alikuwa akipokea 'mkwanja' mnene kuliko hata unaodaiwa kulipwa kocha wa timu ya taifa, Taifa Stars na kutokea sakata la Ngassa limekuwa nafuu kwa uongozi huo kumpa mkono wa kwaheri. Juhudi zinafanywa na MICHARAZO kupata uthibitisho wa Cedri kutakiwa Azam na tukifanikiwa mtazipata kupitia hapa hapa.

Mwanahawa Chipolopolo atua T Moto

ALIYEKUWA muimbaji nyota wa kundi la King's Modern Taarab 'Wana Kijoka Kazima Taa', Mwanahawa Ally 'Chipolopolo' amelihama kundi hilo na kutua T-Moto Modern Taarab. Akizungumza na MICHARAZO
, Chipolopolo alisema ametua T-Moto wiki iliyopita baada ya kuvutiwa na masilahi aliyoahidiwa na kundi hilo na kwa sasa anajifua nao kwa ajili ya maonyesho ya sikukuu ya Eid el Fitri ambapo ndipo atakapotambulishwa rasmi. Chipolopolo, alisema ameondoka King's kundi lililomtangaza vema kwa baraka zote bila ya ugomvi wala chuki kwa lengo la kusaka ujuzi na kusaka masilahi. "Yaani ni wiki tu iliyopita ndio nimetua hapa T-Moto nikitokea King's kwa nia ya kuongeza ujuzi na kutafuta masilahi zaidi, ila sijaondoka katika kundi langu la awali kwa chuki au ugonvi," alisema. Muimbaji huyo ambaye ni mtoto wa mpuliza saksafone wa zamani wa bendi za Urafiki Jazz, Bima Lee, Shikamoo Jazz na Msondo Ngoma, Ally Rashid 'Mwana Zanzibar' alisema anaamini kuwepo kwake T-Moto kutamsaidia kumpaisha zaidi kutokana na aina ya wasanii atakaokuwa nao. Alisema pamoja na kuondoka, King's, lakini hatalisahau kundi hilo kwa kusaidia kumnyanyua baada ya kusota katika makundi ya awali aliyoyapitia katika safari yake kimuziki. "Nimeondoka King's lakini silisahau asilan kwa namna lilivyonisaidia kufika hapa nilipo hata T-Moto wakakiona kipaji changu," alisema. Mwisho

Kim Poulsen awaita Bahanunzi, Chuji kikosi cha Stars

MFUMANIA nyavu aliyefunika kwenye michauno ya Kombe la Kagame, Said Bahanunzi wa Yanga na viungo 'watukutu' Athuman Idd Chuji na Ramadhani Chombo 'Redondo' ni kati ya wachezaji 21 waliotangazwa kuitwa katika kikosi cha timu ya taifa Taifa Stars. Kocha mkuu wa timu hiyo Kim Poulsen amekitangaza kikosi hicho jana kwa ajili ya kujiandaa na pambano la kirafiki la kimataifa linalotarajiwa kuchezwa katikati ya mwezi huu nje ya nchi. Poulsen alisema kikosi hicho kinatarajiwa kuingia kambini wiki ijayo tayari kujiwinda na mechi hiyo ya kirafiki ambayo hata hivyo mpaka sasa haifahamiki itakuwa dhidi ya nchi gani. Kocha huyo alisema amewaita wachezaji hao watatu na wengine kutokana na kuonyesha uwezo mzuri wakati wa michuano ya Kagame, ambapo bahanunzi aliibuka mfungaji bora huku Chuji na Redondo waking'ara katika nafasi ya kiungo mwanzo mwisho. Kim alisema ameomba mechi hiyo ya kirafiki ambayo iko kwenye kalenda ya FIFA ichezwe ugenini kwa lengo la kuwapa uzoefu wachezaji wake. Wachezaji waliotajwa na kocha huyo ni pamoja na makipa watatu, Nahodha Juma Kaseja (Simba), Deogratias Munishi 'Dida'na Mwadini Ally (wote Azam). Mabeki ni nahodha msaidizi, Aggrey Morris na Erasto Nyoni (Azam), Kelvin Yondani (Yanga) na Shomari Kapombe (Simba). Viungo walioteuliwa katika timu hiyo ni Chuji na Frank Domayo (Yanga), Haruna Moshi 'Boban', Ramadhani Singano 'Messi' na Mwinyi Kazimito (Simba), Mrisho Ngassa,Redondo na Salum Abubakar 'Sure Boy' (Azam) na Shabani Nditi kutoka Mtibwa Sugar. Wengine ni washambuliaji John Bocco (Azam), Mbwana Samata na Thomas Ulimwengu(TP Mazembe, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo), Bahanunzi na Simon Msuva. Kocha huyo alisema ameshindwa kuwaita Amri Maftah wa Simba na Nurdin Bakari wa Yanga kwa sasa kutokana na kwamba wachezaji hao bado ni majeruhi.

Simba wamalizana na Azam kuhusu Ngassa, mwenyewe adai haendi kokote kwa vile hajashirikishwa

MABINGWA wa soka wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara, Simba wametangaza kumsajili mshambuliaji nyota wa Azam na timu ya Taifa (Taifa Stars), Mrisho Ngassa kwa mkataba wa mkopo wa mwaka mmoja. Hata hivyo Ngassa mwenyewe amesisitiza kuwa hajashirikishwa katika 'dili' hilo na kudai kama uongozi wa Azam haumtaki katika klabu yao imvunjie mkataba na kumlipa chake kuliko kumpeleka kwenye klabu ambayo hajawahi kuitoa kuichezea. Uongozi wa Simba na Azam jana ulinukuliwa kwamba umefanikisha mpango wa Ngassa kutua Msimbazi baada ya kuwazidi kete Yanga waliokuwa tayari kulipa Sh Milioni 20, milioni tano pungufu na zile walizotoa Simba. Awali, uongozi wa Azam ulishatangaza kuwa uko tayari kumuuza winga huyo kwa klabu yoyote itakayotoa dau la dola 50,000 (sawa na zaidi ya Sh. milioni 80), jambo ambalo limeonekana kuwa gumu kabla ya Simba kumpata mchezaji huyo kwa ofa ya mkopo ya Sh. milioni 25. Ngassa ambaye alitakiwa sana na kocha wa Simba, Milovan Circkovic, anatarajiwa kuichangamsha safu ya ushambuliaji ya timu yake mpya katika ligi kuu ya Bara na pia katika michuano itakayoanza mapema mwakani ya Ligi ya Klabu Bingwa Afrika. Akizungumza jana jijini Dar, Makamu Mwenyekiti wa Simba, Geofrey Nyange 'Kaburu' alisema kuwa wamemsajili Ngassa kwa mkopo na tayari wamefikia makubaliano na Azam, hivyo mchezaji huyo ataichezea timu yao katika msimu ujao wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara ambayo inatarajiwa kuanza Septemba Mosi. Kaburu alisema kuwa wamemsajili mshambuliaji huyo kutokana na maelezo ambayo walipewa na Cirkovic ili kuziba nafasi ya Emmanuel Okwi ambaye sasa anaelekeza nguvu zake katika kusaka timu atakayoichezea soka la kulipwa barani Ulaya. "Usajili wa Ngassa umeshakamilika, ni mali yetu kwa muda wa mwaka mmoja baada ya kukamilisha usajili wake wa kuichezea Simba kwa mkopo," alisema Kaburu. Naye Meneja wa Azam, Patrick Kahemele, alinukuliwa akisema wameamua kumpeleka Ngassa Simba kutokana na maelezo ya Cirkovic kumuhitaji ambapo wanaamini ataendeleza kipaji chake na kuendelea kuisaidia Taifa Stars. Kahemele alisema kuwa Azam ilifikia maamuzi ya kumuuza mshambuliaji huyo baada ya kuonyesha hadharani mapenzi aliyonayo na mabingwa wa Kombe la Kagame, Yanga, lakini alidai Yanga imekwama kumpata kwa vile iligoma kuongeza dau katika fedha ilizotaka kutoa. Azam ilitangaza kwamba iko tayari kumuuza Ngassa kwa gharama ya Dola za Marekani 50,000 baada ya nyoya huyo kuonyesha mapenzi yake kwa Yanga kwa kuvaa na kuibusu nembo ya klabu hiyo wakati akishangilia goli aliloifungia Azam katika mechi yao ya nusu fainali ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati dhidi ya AS Vita ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. Ngassa aliyeihama Yanga mwaka juzi aliisaidia Azam kumaliza kwenye nafasi ya pili katika msimu wa ligi uliopita ambapo mwakani itashiriki kwa mara ya kwanza mashindano ya Kombe la Shirikisho yanayoandaliwa na Shirikisho la Soka la Afrika (CAF). Akizungumza na MICHARAZO, Ngassa alisema hana taarifa za kupelekwa Simba na kudai kwa tararibu anazopfahamu alipaswa kushirikishwa katika mazungumzo ya klabu hizo mbili kabla ya kufikiwa maamuzi. "Kama ni kweli wamefanya hivyo hawajanitendea haki, nilipaswa kushirikishwa na kama klabu ya Azma hainitaki basi inilipe changu nijue wapi pa kwenda na sio kunipeleka sehemu kama mzigo usio na maamuzi," alisema Ngassa mtoto wa kiungo wa zamani wa Pamba na Simba, Khalfan Ngassa. Ngassa alisema yeye anauheshimu mkataba wake na Azam ambao umesaliwa muda wa mwaka mmoja, lakini ni vigumu kwake kukubali kirahisi kupelekwa Simba, ingawa hakuweka bayana atachukua hatua gani katika sakata hilo ambalo kwa kiasi fulani linataka kufanana na lile la wachezaji Mohammed Banka aliyekuwa Simba na Ramadhani Chombo wa 'Redondo' wa Azam ambao walitolewa kwa mkopo na klabu zao kwa klabu za Villa Squad na Moro United lakini wakagoma kwa vile hawakushirikishwa katika uhamisho huo.

Wednesday, August 1, 2012

Bondia Mbongo kuwania taji la IBF Afrika

BONDIA Ramadhani Shauri wa Tanzania anatarajiwa kupanda ulingoni siku ya Idd Pili kuzipiga na Mganda Sunday Kizito katika pambano la kimnataifa la kuwania ubingwa wa IBF-Afrika. Pambano hilo limepangwa klufanyika kwenye ukumbi wa Diamond Jubilee na litaratibiwa na Promota Lucas Rutainurwa. Rais wa Shirikisho la Ngumi za Kulipwa nchini, TPBC ambaye pia ni Rais wa IBF Afrika/USBA, Onesmo Ngowi, aliiambia NIPASHE jana kuwa maandalizi ya pambano hilo yameanza na litasindikizwa na michezo kadhaa ya utangulizi. Ngowi, alisema pambano hilo la Shauri na Kizito litakuwa ni la uzito wa Feather (kilo 58) kuwataja mabondia hao wana rekodi zinasisimua hivyo kutabiri pambano la aina yake siku husika. Rais huyo alisema Shauri anayetoka kambi ya kocha Christopher Mzazi ana rekodi ya mapambano 12 akishinda 11 na kupoteza moja, huku mpinzani wake akiwa na rkodi ya kucheza pia michezo12 akishinda saba ba kupoteza 9. Ngowi alisema siku ya pambano hilo Mtanzania mwingine Nassib Ramadhan atavaana na Mkenya, Twalibu Mubiru kuwania ubingwa wa IBF Afrika Mashariki na Kati. Naye promota wa pambano hilo lililopewa jina la 'The Rumble of the City' alisema ameamua kuwekeza katika Utalii wa Michezo ili kusaidia ajira kwa vijana sambamba na kukuza uchumi wa Tanzania. Rutainurwa alisema kuwa ana ratiba ya mapambano ya ubingwa wa Afrika kila baada ya miezi miwili mwaka huu na mwaka kesho ambayo itaipa Tanzania nafasi ya kunyanyua mataji na kuwawezesha vijana kujiajiri. Promota huyo aliyaomba makampuni na wadhamini mbalimbali kujitokeza kufanikisha michezo hiyo inayosimamiwa na kampuni yake ya Kitwe General Traders. Mwisho

Ngassa adaiwa kumfukisha kazi Azam kocha Stewart Hall

WINGA nyota wa timu ya Azam, Mrisho Ngassa anatajwa kuwa ndiye chanzo cha 'kutimuliwa' kwa aliyekuwa kocha mkuu wa timu hiyo, Stewart John Hall. Azam imedaiwa kumsitishia mkataba kocha huyo kutoka Uingereza ikiwa ni siku chache tu tangu aiwezeshe timu hiyo kucheza fainali za Kombe la Kagame, michuano iliyoishiriki kwa mara ya kwanza katika historia yao. Hata hivyo uongozi wa Azam umekuwa wagumu kuweka bayana ukweli juu ya taarifa hizo za kumtimua Stewart na sababu zilizowafanya waachane nae kutokana na baadhi ya viongozi wake kutupiana mpira kila walipokuwa wakitafutwa kuthibitisha ukweli. Afisa Habari wa klabu hiyo, Jafer Idd alisema asingeweza kusema lolote na kulitaka MICHARAZO iliwasiliane na Katibu Mkuu, Idrisa Nassor 'Father' ambaye naye alikwepa kijanja kuthibitisha suala hilo akidai angelitumia namba la mtu wa kulizungumzia hilo. "Aisee juu ya ukweli au la, ngoja nikutumie namba ya mtu ambaye atakuambia kila kitu," Nassor aliiahidi MICHARAZOP licha ya kutotekeleza ahadi hiyo. Hata hivyo habari zilizopatikana jana jijini zinasema kuwa, Stewart ni kweli ametemwa na Azam na sababu kuu ikiwa ni kitendo chake cha kukaidi agizo la uongozi huo juu ya kumtomchezesha winga Mrisho Ngassa. Kwa mujibu wa chanzo chetu cha habari ni kwamba uongozi wa Azam ulimtaka kocha huyo asijaribu kumuingiza uwanjani Ngassa katika mechi yao ya fainali dhidi ya Yanga kwa kukerwa na kitendo cha winga huyo kuibusu jezi ya Yanga mara baada ya pambano la nusu fainali dhidi ya As Vita ya Kongo. Inadaiwa, uongozi ulihisi winga huyo asingeitendea haki Azam kwa mapenzi makubwa aliyonayo kwa klabu yake ya zamani ya Yanga ambayo imetajwa kuchuana na Simba ili kumrejesha kikosini kwa msimu ujao.

UNAMKUMBUKA MWANA ZANZIBAR?

MPULIZA Saksafone wa zamani wa bendi ya Msondo Ngoma, Ally Rashid 'Mwana Zanzibar' yu hoi nyumbani kwake Keko Machungwa jijini Dar
kutokana na kupatwa na maradhi ya Kiharusi. Mmoja wa watoto wake, Mwanahawa Ally 'Chipolopolo' alisema baba yake alipatwa na maradhi hayo wakati akienda katika mazoezi ya bendi hiyo na kwa sasa hawezi kuzungumza wala kutembea. Kinachomliza Mwanahawa ni kitendo cha baba yake kutelekezwa na uongozi wa bendi hiyo. MICHARAZO ilijaribu uusaka uongozi wa bendi hiyo, lakini baadhi ya viongozi simu zao zilikuwa hazipatikani na nyingine zikilia bila kupokelewa bila kufahamika sababu yake.