STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Monday, December 6, 2010

Mapacha Watatu, Sam wa Ukweli kupimana Ubavu Dar

KUNDI la Mapacha Watatu linaloundwa na waimbaji mahiri nchini, Khalid Chokoraa, Jose Mara na Kalala Junior wanatarajia kuonyeshana kazi na msanii anayekuja juu katika miondoko ya muziki wa kizazi kipya Sam wa Ukweli.
Mapacha hao watatu na Sam wa Ukweli watakutanishwa kwenye onyesho la pamoja lifahamikalo kama 'Usiku wa Sauti za Kizazi Kipya cha Dansi' litakalofanyika Desemba 13, jijini Dar es Salaam.
Mratibu wa onyesho hilo, Sauda Mwilima, aliiambia Micharazo kuwa, onyesho hilo litakalofanyika kwenye ukumbi wa Stereo Bar, Kinondoni na wasanii hao wataonyesha umahiri wao.
Mwilima alisema onyesho hilo linawagusa Mapacha Watatu, watakaofanya vitu vyao kwa kutoa burudani na watasindikizwa na msanii Salum Mohamed 'Sam wa Ukweli' anayetamba na ngoma yake iitwayo 'Sina Raha'.
"Usiku wa Sauti ya Kizazi Kipya cha Dansi utaporomoshwa na Mapacha Watatu, wakisindikizwa na shoo ya ukweli mkali wa muziki wa kizazi kipya nchini Sam wa Ukweli, yaani ni usiku usio wa kawaida," alisema Mwilima.
Mwilima ambaye ni mtangazaji wa kituo cha runinga cha Star Tv, alisema maandalizi ya onyesho hilo yanaendelea vema na kuwataka mashabiki wa muziki kukaa mkao wa kula kupata uhondo toka kwa wakali hao.
Kundi hilo la Mapacha Watatu linaundwa na waimbaji hao toka bendi hasimu za African Stars 'Twanga Pepeta' na FM Academia 'Wazee wa Ngwasuma'.

Mwisho

Mkulo: Nimewasamehe walionichafua, ila sintowasahau

WAZIRI wa Fedha na Uchumi, ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Kilosa, Mustafa Mkulo, amesema pamoja na kuwasamehe wale wote waliompakazia mabaya wakati wa uchaguzi mkuu uliopita, bado hawezi kuwasahau hadi anaingia kaburini.
Pia, amewataka wanachama wa CCM na wananchi wa Kilosa kwa ujumla, kuzika tofauti zao zilizosababishwa mchakato wa uchaguzi mkuu, ili kuweza kushikamana kuijenga wilaya na jimbo lao la Kilosa liweze kuwa mfano wa kuigwa nchini.
Akizungumza kwenye mapokezi na hafla ya kupongezwa kuteuliwa tena kuwa waziri, Waziri Mkulo, alisema kashfa alizokuwa akipewa akidaiwa sio raia wa Tanzania na kejeli zingine ni vitu ambavyo vilimuumiza, ila amewasamehe wote waliomfanyia jambo hilo.
Waziri alisema hata hivyo pamoja na kuwasamehe wahusika, katu hatawasahau kwa vile walimpa wakati mgumu na kumnyima raha, kitu alichodai kitaendelea kubaki kichwani mwake hadi kifo.
Alisema wale walioanzisha na kueneza maneno hayo na waliomtusi, wasimuogope kwa sababu anafahamu siasa ni mchezo usio na simile na wenye kuhitaji uvumilivu mkubwa kitu alichoweza kukimudu na ndio maana amewasamehe kwa yote.
"Walionitusi na kunizushia kwamba mie sio raia na wengine kufikia hata kumhusisha mke wangu, wote nimewasamehe, ila kwa hakika sintowasahau, muhimu nataka kuwaambia wahusika wasiwe na hofu juu yangu yale yamepita kwani najua siasa ndivyo zilivyo," alisema Mkulo.
Alisema kama sio mambo ya siasa, kwa hakika angeweza kuwafungulia mashtaka na kudai fidia kubwa wahusika wote waliomchafua kipindi cha kura za maoni ndani ya CCM na hata kwenye uchaguzi mkuu uliompa ushindi wa kishindo yeye Mkulo na chama chake.
Waziri Mkulo, alisema kwa kuwa uchaguzi umeshapita kwa sasa yeye ni mbunge wa wakazi wote wa Jimbo la Kilosa na hivyo atawatumikia wananchi wote kwa ajili ya kuwaletea maendeleo, akiomba kupewa ushirikiano wa kutosha kufanikisha aliyopanga kwa miaka mitano ijayo.
Wakati wa mchakato wa kura za maoni, Waziri Mkulo alivumishiwa kuwa yeye si raia wa Tanzania na kikundi cha watu waliojiita Wazee wa Kilosa, ambao walikuja kurukwa na uongozi wa Baraza la Wazee la wilaya hiyo waliodai hawakumtuma mhusika aliyeanzisha chokochoko hizo.
Pia baada ya kushinda kiti hicho cha Ubunge kwa mara ya pili, baadhi ya watu walidaiwa kuapa kuwa asingekuwa miongoni mwa wateule wa Baraza Jipya la Mawaziri, kitu kilichoenda kinyume kutokana na Rais Jakaya Kikwete kumtangaza kuendelea kushikilia wizara hiyo ya Fedha.

CCM Kilosa waambiana kweli, wapashana kuacha majungu




UONGOZI wa Chama cha Mapinduzi, CCM, Wilaya ya Kilosa, umewataka wanachama wake waache majungu na mifarakano na badala yake washikamane kukijenga chama chao pamoja na kuwapa ushirikiano wa kutosha viongozi walioshinda kwenye uchaguzi mkuu uliopita.
Viongozi wakuu wa chama hicho, Mwenyekiti Christopher Wegga na Katibu wake, Gervas Makoye walitoa wito huo kwa nyakati tofauti wakati wa mapokezi na sherehe ya kumpongeza Mbunge wa Jimbo la Kilosa, Mustafa Mkulo kuchaguliwa tena kuwa Waziri wa Fedha na Uchumi zilizofanyika wilayani humo.
Makoye, aliyehutubia katika mkutano wa mapokezi ya Mkulo, yaliyofanyika kwenye uwanja wa CCM wilayani hapo, alisema kwa kuwa uchaguzi mkuu umeshamalizika ni vema wanachama wa chama hicho wakazika tofauti zao na kushirikiana na walioshinda kukijenga chama chao.
Katibu huyo, alisema pamoja na uchaguzi huo kumalizika na chama chao kuzoa ushindi wa kishindo, bado wapo baadhi ya wanachama wanaendeleza majungu na maneno kitu alichodai haisaidii.
Alisema wanaofanya hivyo ni wanachama waliozoea kupiga mizinga (kuomba hela) na kuwataka wenye tabia hiyo kubadilika kwa sababu chama hakitawavumilia.
"Wanachama wa CCM na wana Kilosa kwa ujumla acheni kupiga maneno, acheni majungu tushikamane kukijenga chama, tuwape ushirikiano wa kutosha viongozi walioshinda kwa sababu uchaguzi umeisha na hivyo tunapaswa kuvunja kambi zetu tuwe kitu kimoja," alisema.
Naye Mwenyekiti wa chama hicho, Christopher Wegga, akihutubia kwenye hafla ya kupongeza Waziri Mkulo iliyofanyika kwenye ukumbi wa Babylon, alisema kuendeleza majungu na tofauti baada ya uchaguzi ni kukwaza maendeleo ya wilaya yao na kuwataka wananchi kushirikiana.
Alisema binafsi anampongeza Waziri Mkulo kwa kurejeshwa kwenye cheo chake cha uwaziri na kuwapongeza wazee walioandaa sherehe hiyo.
Sherehe hiyo ya kumpongeza Mkulo, iliandaliwa na Baraza la Wazee wa Kilosa, ambapo Mwenyekiti wake, Raphael Chayeka, alisema wamefurahishwa mno na kitendo cha Rais Jakaya Kikwete kumrejesha Mbunge wao kwenye nafasi hiyo kwa imani Kilosa itapata maendeleo zaidi.
"Imani yetu ni kwamba cheo ulichopewa ni fahari kwetu wana Kilosa, wewe ni kama Rais wetu na tunaamini Kilosa itasonga mbele, tunakutakia kila la heri mna mafanikio," alisema Chayeka.
Waziri Mkulo, aliwashukuru wazee hao, wanachama na wananchi wa Kilosa kwa ujumla kwa kuonyesha imani yake kwake na kuwaahidi kuwasaidia kuwaletea maendeleo ili miaka mitano ijayo Jimbo hilo libadilike na litofautiane kuliko miaka mitano iliyopita.
Ila alisema jambo la muhimu ni wananchi bila kujali itikadi za vyama, dini, jinsia, kabila kushirikiana pamoja katika kupigania wilaya yao iondokane na vitendo vinavyorudisha nyuma maendeleo yao.
****



Na Badru Kimwaga, Aliyekuwa Kilosa
WAZIRI wa Fedha na Uchumi, ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Kilosa, Mustafa Mkulo, amesema pamoja na kuwasamehe wale wote waliompakazia mabaya wakati wa uchaguzi mkuu uliopita, bado hawezi kuwasahau hadi anaingia kaburini.
Pia, amewataka wanachama wa CCM na wananchi wa Kilosa kwa ujumla, kuzika tofauti zao zilizosababishwa mchakato wa uchaguzi mkuu, ili kuweza kushikamana kuijenga wilaya na jimbo lao la Kilosa liweze kuwa mfano wa kuigwa nchini.
Akizungumza kwenye mapokezi na hafla ya kupongezwa kuteuliwa tena kuwa waziri, Waziri Mkulo, alisema kashfa alizokuwa akipewa akidaiwa sio raia wa Tanzania na kejeli zingine ni vitu ambavyo vilimuumiza, ila amewasamehe wote waliomfanyia jambo hilo.
Waziri alisema hata hivyo pamoja na kuwasamehe wahusika, katu hatawasahau kwa vile walimpa wakati mgumu na kumnyima raha, kitu alichodai kitaendelea kubaki kichwani mwake hadi kifo.
Alisema wale walioanzisha na kueneza maneno hayo na waliomtusi, wasimuogope kwa sababu anafahamu siasa ni mchezo usio na simile na wenye kuhitaji uvumilivu mkubwa kitu alichoweza kukimudu na ndio maana amewasamehe kwa yote.
"Walionitusi na kunizushia kwamba mie sio raia na wengine kufikia hata kumhusisha mke wangu, wote nimewasamehe, ila kwa hakika sintowasahau, muhimu nataka kuwaambia wahusika wasiwe na hofu juu yangu yale yamepita kwani najua siasa ndivyo zilivyo," alisema Mkulo.
Alisema kama sio mambo ya siasa, kwa hakika angeweza kuwafungulia mashtaka na kudai fidia kubwa wahusika wote waliomchafua kipindi cha kura za maoni ndani ya CCM na hata kwenye uchaguzi mkuu uliompa ushindi wa kishindo yeye Mkulo na chama chake.
Waziri Mkulo, alisema kwa kuwa uchaguzi umeshapita kwa sasa yeye ni mbunge wa wakazi wote wa Jimbo la Kilosa na hivyo atawatumikia wananchi wote kwa ajili ya kuwaletea maendeleo, akiomba kupewa ushirikiano wa kutosha kufanikisha aliyopanga kwa miaka mitano ijayo.
Wakati wa mchakato wa kura za maoni, Waziri Mkulo alivumishiwa kuwa yeye si raia wa Tanzania na kikundi cha watu waliojiita Wazee wa Kilosa, ambao walikuja kurukwa na uongozi wa Baraza la Wazee la wilaya hiyo waliodai hawakumtuma mhusika aliyeanzisha chokochoko hizo.
Pia baada ya kushinda kiti hicho cha Ubunge kwa mara ya pili, baadhi ya watu walidaiwa kuapa kuwa asingekuwa miongoni mwa wateule wa Baraza Jipya la Mawaziri, kitu kilichoenda kinyume kutokana na Rais Jakaya Kikwete kumtangaza kuendelea kushikilia wizara hiyo ya Fedha.

Mwisho
Mwisho

BFT yaandaa kozi ya ukocha, Super D apigwa tafu

SHIRIKISHO la Ngumi za Ridhaa Tanzania, BFT, limeandaa kozi ya ukocha wa mchezo huo kwa vijana na walimu wa Shule za Msingi na Sekondari, ili kukuza na kuendeleza ngumi nchini.
Afisa Habari wa BFT, Eckland Mwaffisi, aliiambia Micharazo kuwa, kozi hiyo ya siku 10 inatarajiwa kuanza Desemba 14-24 ikifanyika jijini Dar es Salaam.
Mwaffisi alisema kozi hiyo itahusisha vijana wenye kupenda kufundisha mchezo huo, pia wangependa walimu wa shule za Msingi na Sekondari wajitokeze kwa wingi kwa sababu lengo lao ni kutaka kuusambaza mchezo huo shuleni kwa manufaa ya baadae kwa taifa.
"BFT katika mikakati yake ya kukuza na kuendeleza michezo kuanzia mitaani hadi shuleni imeandaa kozi ya siku 10 itakayowahusisha wote wenye 'idea' ya mchezo wa ngumi kwa lengo la kwenda kufundisha wenzao ili kuufanya mchezo huo urejee katika hadhi yake," alisema Mwaffisi.
Alisema tayari baadhi ya wanaopenda kushiriki kozi hiyo wameshaanza kujitokeza na alizidi kutoa wito kwa wenye kuhitaji kujifunza ukocha wa ngumi kujitokeza mapema iwezekanavyo.
Katika hatua nyingine, Kocha wa Ngumi wa Klabu ya Ashanti, Rajabu Mhamila 'Super D' amepewa msaada wa Sh. Laki 1.5 zitakazomwezesha kushiriki kozi ya siku 10 ya ukocha iliyoandaliwa na Shirikisho la Ngumi za Ridhaa Tanzania (BFT).
Msaada huo ambao ni wa pili kwa kocha huyo kupewa ulitolewa na mdau wa michezo Zulfiqal Ali kumwezesha Super D kufanikisha malengo yake ya kuendeleza mchezo wa ngumi kwa vijana
Akizungumza Dar es Salaam, wakati akimkabidhi pesa hizo Zulfiqal alisema ameamua kufanya hivyo ili kuungana na wadau wengine wa michezo ikiwemo serikali katika kuendeleza michezo.
Hata hivyo Zulfiqal amewaomba wadau wengine kujitokeza kuungana na jamii kusaidia kukuza michezo ili kuwawezesha vijana wasio na ajira waweze kujiajili.
Naye Super D alisema anashukuru na kuahidi kuzingatia kozi hiyo siku zote ili aweze kupanua ujuzi ambao utawawezesha kuwasaidia mabondia wanaochipukia hapa nchini.
Awali kocha huyo alipewa msaada wa vifaa vya michezo vyenye thamani ya shilingi laki tatu na zaidi kwa ajili ya mazoezi ya mabondia wanaohudhuria mafunzo yanayotolewa na kocha huyo

Extra Bongo kupeleka Vuvuzela Kilosa



BENDI ya Extra Bongo, inayotamba na mitindo ya 'Vuvuzela' na 'Kizigo' inatarajiwa kwenda kusherehekea Sikukuu ya Krismasi na wakazi wa Kilosa watakapoenda kufanya onyesho wilayani humo.
Extra Bongo inayomilikiwa na mtunzi na muimbaji mahiri nchini, Ally Choki, itaenda Kilosa kufanya onyesho siku ya sikukuu hiyo kwenye ukumbi wa Babylon Luxury Pub.
Meneja wa ukumbi huo, Robert Chipindula, aliiambia MICHARAZO, kwa muda mrefu wamekuwa wakiombwa na mashabiki wa muziki kuwapelekea bendi hiyo ya Extra Bongo na ndio maana wameialika kwenda kutumbuiza wakati wa sikukuu hiyo.
Chipindula, alisema tayari wameshamalizana kila kitu na uongozi wa bendi hiyo na kukubali kutua wilayani humo kwa onyesho hilo litakaloenda sambamba na utambulisho wa nyimbo na miondoko mipya ya bendi hiyo.
Extra Bongo iliyokuwa ikifahamika kwa miondoko ya Kujinafasi Next Level kwa sasa inatamba na mitindo yao mipya miwili ya Kizigo na Vuvuzela, ambayo wamekuwa wakiitambulisha kila wanapoenda kufanya maonyesho katika maeneo mbalimbali.
Bendi hiyo inayotamba na albamu yao mpya ya Mjini Mipango, tayari imeshaanza kufyatua vibao vipya kwa ajili ya albamu ya pili, baadhi ya nyimbo hizo ni Nguvu na Akili na Neema ambazo zimekuwa zikiwachengua mashabiki wa muziki wa dansi kila zinapopigwa ukumbini.

Wahanga wa Kilosa waulalamika kutelekezwa







WAHANGA wa Mafuriko ya Kilosa, wanaoishi kwenye Kambi ya Mazulia wilayani humo, wameulalamikia uongozi wa wilaya hiyo kwa kuwatelekeza bila msaada wowote, huku vyakula vyao vya misaada vikiharibika na kutupwa na vingine kuchomwa moto jalalani.
Pia wahanga hao wamedai hadi sasa hawajui hatma yao ndani ya kambi hizo zilizopo Kata ya Magomeni, kutokana na mara kwa mara kupokea vitisho vya kuhamishwa vinavyotolewa na watendaji wa wilaya hiyo wanaodai wanatumwa na Mkuu wao wa wilaya, Halima Dendegu.
Wakizungumza na Micharazo kwenye kambi hizo, iliyopo Kata ya Magomeni, wahanga hao walidai uongozi wa wilaya hiyo umewatelekeza bila kuwapa misaada iliyotolewa na wasamaria wema na badala yake vyakula na misaada hiyo ikiharibika na kutupwa au kuchomwa moto.
Wakazi hao walisema mara ya mwisho kupelekewa misaada ilikuwa ni Mwezi Machi na kwa mujibu wa makubaliano ya awali ni kwamba wangekuwa wakipewa misaada hiyo kila baada ya miezi mitatu vitu ambavyo havikufanyika.
Walisema misaada ya mwezi Juni hawakupewa kwa maelezo ya kwamba walilimiwa mashamba na uongozi wa serikali ya wilaya, ambayo walidai hayakutoa mavuno ya kutosha kwa vile yalilimwa wakati mbaya na cha ajabu tangu hapo hawajapewa tena.
"Hatujapewa misaada tangu Machi na hivi karibuni baadhi ya misaada yetu kama nguo na chakula vilienda kutupwa eneo la Ilonga kutokana na kuharibika na Novemba 18 vyakula vyetu vilichomwa moto kwa maelezo vimeharibika, hii ni haki kweli?" alihoji Peter Thomas, 68.
Thomas, alisema hata pale wanapojaribu kuulizia sababu ya kufanyiwa ukatili huo kana kwamba wamependa kuishi kambini hapo, wamekuwa wakipokea vitisho ikiwemo watu walioenda kwao kama Tume maalum ya kuhakiki kambi hiyo waliowaeleza karibia watahamishwa warejee makwao.
"Yaani kwa kifupi tumekuwa tukiishi kwa mashaka bila kujua hatma yetu ndani ya kambi hii, misaada yetu inayeyuka na kibaya tunatishwa tukiambiwa tulikuwa tukibembelezwa kwa sababu ya uchaguzi tu, na sasa uchaguzi umeisha tutalijua jiji," alisema Thomas.
Naye Verena Philipo Mcharo, alisema hivi karibuni mkuu wao wa wilaya aliwapelekea msaada wa mabati sita, mbao moja, misumari kilo moja na mfuko mmoja wa saruji kwa wale waliobomokewa na nyumba zao ili kwenda kujenga katika viwanja walivyopewa bila kujua vilipo.
"Ebu fikiria vifaa hivyo vitatosha nini kama sio kutaka kuwadhihaki watu, tena sio wote waliopewa hati za viwanja walivyoelezwa wametengewa kwenda kujenga makazi yao mapya na sisi tuliokuwa wapangaji tumeambiwa tujue la kufanya kwani misaada hiyo haituhusu," alisema.
Verana, alisema yeye alipohoji kubaguliwa huko miongoni mwa wahanga wa janga hilo la Mafuriko lililotokea mwishoni mwa mwaka jana, aliambiwa anapaswa kurejea kwao Iringa, bila kujali kama alikuja Kilosa kama raia mwingine kwa ajili ya kutafuta maisha.
Mwenyekiti wa kambi hiyo, Msagati, alisema kwa kifupi ni kwamba wao hawajui hatma yao ndani ya kambi hiyo kutokana na mambo yanavyoendelea, huku akitaka waonyeshwe viwanja walivyopewa hati ya kuvimiliki wajue cha kufanya ili kuondokana na dhiki wazipatazo.
Naye Tabia Athuman Matiangu, 71, alidai Septemba 20, mwaka huu alipigwa kofi na Mkuu wa Wilaya kwa kile kilichoelezwa kuwa na kiherehere cha kuwasemea wenzake wakati wa ukaguzi wa wahanga kambini hapo.
Madai ya ajuza huyo, yalithibitishwa pia na baadhi ya wahanga hao, wakidai lilifanyika kama moja ya vitisho dhidi ya malalamiko yao kwa uongozi huo wa wilaya.
Micharazo iliwasiliana na Mkuu wa Wilaya hiyo, Halima Dendegu, aliyekuwa safarini kuelekea jijini Dar es Salaam, kwa njia ya simu ambapo alikiri kusikia malalamiko hayo, ila alisema ni 'mtandao' maalum ulioundwa kumchafua kutokana na msimamo wake wa kuwakomalia watendaji wa halmashauri hiyo.
"Madai ya wananchi hao hata mie yamenifikia, lakini mengi ni yenye nia ya kutaka kunichafua na yanafanywa na watu wa halmashauri kutokana na madudu yao yaliyofanya hadi wilaya hii ipewe hati chafu kwa upotevu wa fedha kibao za miradi ya maendeleo," alisema Dendegu.
Alikiri kuchomwa kwa vyakula, bila kufananua kiwango chake na sababu zilizofanya kufanywa kwa kitendo hicho kwa madai yupo nje ya ofisi na hivyo isingekuwa rahisi kwake kukumbuka kila kitu na kumuomba mwandishi huyu aonane nae baada ya kurejea ofisini kitu kilichoshindikana.
Hata hivyo kwa mujibu wa taarifa zisizo rasmi zilizopatikana ndani ya wilaya hiyo chakula kilichoharibika na kuchomwa moto vikijumuisha Maharage, Ngano, Mchele na Unga wa Sembe ni karibu tani mbili (kilo 1,700).
Alipoulizwa juu ya dai la kumpiga kofi mmoja wa wahanga hao, Mkuu huyo, alionyesha mshangao na kukanusha, huku akihoji mambo hayo yameibukia wapi kipindi hiki ambacho ofisi yake inajitahidi kwa hali na mali kuwasaidia wahanga hao.
Juu ya mgao wa vifaa vya ujenzi kwa wahanga hao, alisema ni kweli alitoa mgao huo kiduchu kutokana na jinsi msaada wenyewe ulivyoletwa kwenye ofisi yake.
"Ni kweli niliwapa vifaa hivyo kama walivyokuambia, ila vinaonmekana vichache kwa sababu ndivyo vilivyolewa na wasamaria wema, hatuna mahali pa kuhifadhia hivyo tumewapa wahifadhi wenyewe wakati tunasubiri vingine," alisema.
Mkuu huyo wa wilaya, alisema, anaamini wanaeneza taarifa hizo kwa kutumia vyombo vya habari wana nia ya kumchafua mbele ya umma, ila alisisitiza hatishiki kwa vile tangu aanze kuaminiwa na serikali na kuteuliwa hajawahi kuharibu mahali popote.

Mwisho