STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Wednesday, March 27, 2013

Simba chali Kaitaba, Azam ikitakata Dar


WAKATI wawakilishi pekee wa Tanzania katika michuano ya Kimataifa, Azam wakitaka jijini Dar kwa kuigaragaza Prisona ya Mbeya kwa mabao 3-0, mabingwa watetezi Simba wamejikuta wakiangukia pua mjini Kagera baada ya kudunguliwa bao 1-0 na wenyeji wao Kagera Sugar.
Azam walipata ushindi huo kwenye uwanja wake wa nyumbani wa Chamazi, na kuweza kupunguza pengo la pointi kati yao na vinara wa Ligi Kuu Tanzania Bara, Yanga wanaoongoza wakiwa na pointi 48.
Mabao mawili na kinara wa ufungaji bora kwa sasa Kipre Tchetche na moja ya John Bocco 'Adebayor' yalifanya Azam ikifikishe pointi 40 na kuweka matumaini ya kuikamata Yanga ambayo haikushuka dimbani leo.
Bao la kwanza la Azam lilifungwa na Kipre katika kipindi cha kwanza kabla ya Bocco kuongeza la pili kipindi cha pili na Kipre kuongeza bao la tatu dakika za jioni na kuifanya Azam kutakata kabla ya kuvaana na Barrack YCII watakaorudiana nao katika mechi ya Kombe la Shirikisho Afrika siku ya Jumamosi.
Wakati Azam wakimeremeta Dar, mabingwa watetezi wa Ligi Kuu, Simba yenyewe walikiona cha mtema kuni baada ya kulambwa bao 1-0 na Kagrea Sugar katika pambano jingine lililochezwa uwanja wa Kaitaba, mjini Bukoba.
Bao la sekunde chache baada ya kuanza kwa kipindi cha pili lililofungwa kwa kichwa na beki Amandus Nesta akiiunganisha kona ya Salum Kanoni iliifanya Kagera kufika pointi 34 sawa na Simba.
Hata hivyo Kagera imekamata nafasi ya nne kutokana na kuzidiwa uwiano wa mabao ya kufunga na kufungwa na Simba ambao wamezidi kuwasononesha mashabiki wao ambao wamekuwa hawana raha kwa timu yao kuwa na matokeo mabaya msimu huu tofauti na matarajio yao.
Ushindi huo wa Kagera imekuwa muendelezo wa kuvinjuka 'vigogo' kwenye uwanja wake wa nyumbani kwani hata Yanga walipoenda mjini humo walipigwa bao 1-0 na kuibua tafrani kwa waandishi wa habari waliotuhumiwa kuhujumu pambano hilo.
Kagera mbali na kuikamata Simba kiponti pia imeziengua timu za Mtibwa Sugar na Coastal Union ambazo sasa zimeporomoka katika nafasi walizokuwa wakizishikilia hadi nafasi ya tano na sita badala ya zile za nne na tano walizokuwa wakishikilia awali.
Baada ya kipigo hicho Simba inatarajiwa kusafiri mpaka jijini Mwanza kuvaana na timu ya Toto Africans ambayo huwa inawasumbua kwenye dimba la CCM Kirumba.


KIDO AMTAKA TENA MCHUMIATUMBO

 

Bondia mbavu nene Ramadhan Kido anamta tena mbavunene mwenzake Alphonce mchumiatumbo warudiane baada ya pambano lao la mwanzo lilofanyika uwanja taifa kuchapwa amepania kulipa kisasi ,”mchumiatumbo amenifanya nimeshindwa kulala kwa muda mrefu nikimfikiria yeye kanipigajepigaje jibu sipati,nimeamua kurudi tena ulingoni kwa kujipima na musa mbabe jumapili ya tarehe saba mwezi wa nne pale CCM Mwinjuma,mwananyamala hapahapa jijini dar es salaam ,najua musa ni bondia mzuri lakini siwezi kupoteza mara mbili mfululizo huu mwiko wangu nitahakikisha nafia ulingoni na ntajituma  kwa nguvu zangu zote na kuhakikisha nampiga ko mbaya,kwani siku hiyo ya tarehe saba april sitakuwa na huruma hata kidogo,lolote na litokee hata nikiua sawa tu nina uchungu sana na ngumi na nataka nimuoneshe mchumia tumbo nakuja kivingine,na nikipigwa katika pambano la mwananyamala ni bora niache ngumi

Ibra Class atamba kumgaragaza Mwamakula




BONDIA Ibrahimu  Class 'King Class Mawe' anaendelea kujiandaa 
kumkabili Amosi Mwamakula katika pambano la utangulizi wakati wa
mchezo wa kati ya Francis Cheka na Thomas Mashali.
Pambono la raundi nane linatarajiwa kufanyika katika Ukumbi wa PTA
Sabasaba, Dar es Salaam Mei Mosi mwaka huu, linatarajiwa kuwa la vuta
nikuvute kutokana na kila mmoja kujigamba kujiandaa vema.
Kocha wa King Class Mawe, Rajabu Mhamila 'Super D' alisema kuwa
bondia wake anajianaa vema kwa ajili ya  kumchakaza Mwamakula bila ya huruma ili
kuendelea kujiwekea rekodi nzuri.
"Bondia wangu yuko katika maandalizi ya kutosha kuhakikisha anafanya
vizuri katika pambano hilo la utangulizi kati ya Cheka na  Mashali" alisema
Super D.Mbali na kuwepo mapambano ya ngumi kutakuwa na uuzwaji wa DVD  za mafunzo ya mchezo
huo zenye mapambano makubwa ya mabondia wa ndani na nje ya nchi.
Aliongeza kuwa baadhi ya mapambano yaliyomo ni katika CD na DVD
hizo ni ya Kalama Nyilawila dhidi ya Francis Cheka, Mbwana Matumla na
Fransic Miyeyusho, Said Mundi na King Class Mawe. nyingine zitakuwa
zenye mapambano ya mabingwa wa Dunia akiwemo Manny Paquaio, Floyd Maywherth, Roy Jones,Miguel Cotto,Linox Lewis na wengine wengi DVD hizo zilizoandaliwa kwa ubora wa hali ya juu zitakuwa zikiuzwa kwenye mpambano huo na Kocha wa Kimataifa wa mchezo huo. Rajabu Mhamila ‘Super D’, alisema kuwa kutakuwa na DVD ili kuweza kuwauzia mashabiki kwa ajili ya kujifunza Kanuni na Sheria za mchezo huo.
“Ninatarajia kuwepo kwa ajili ya kuwauzia DVD mashabiki wa ngumi watakaokuwepo katika Mpambano  ili kuweza kujifunza mambo mbalimbali ikiwa ni pamoja na sheria za mchezo wa ngumi”, alisema Super D .

FIFA KUJA KUWASIKILIZA WAGOMBEA UCHAGUZI TFF



Na Boniface Wambura
SHIRIKISHO la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) ambalo lilisimamisha mchakato wa uchaguzi wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kutokana na baadhi ya wagombea kulalamika kuenguliwa sasa litatuma ujumbe wake nchini katikati ya mwezi ujao.

Ujumbe huo ambao moja ya shughuli zake kuwasikiliza wote walioenguliwa na Kamati ya Rufani ya Uchaguzi ya TFF na hawakuridhika na uamuzi huo, utakuwepo nchini Aprili 16 na 17 mwaka huu.

Kwa mujibu wa barua ya Katibu Mkuu wa FIFA, Jerome Valcke kwenda kwa Rais wa TFF, Leodegar Tenga, kazi ya ujumbe huo ni kubaini tatizo lililopo na kutoa ripoti kwa mamlaka zinazohusika ndani ya FIFA kwa ajili ya kutoa mwongozo.

Ujumbe huo utakutana na pande mbalimbali zinazohusika wakiwemo wagombea, kamati za uchaguzi za TFF. Lakini pia ujumbe huo unatarajia kumtembelea Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk. Fenella Mukangara pamoja na watendaji wake wizarani.

Uchaguzi wa viongozi wa TFF ulikuwa ufanyike Februari 24 mwaka huu, lakini ukasimamishwa na FIFA baada ya baadhi ya wagombea walioenguliwa kulalamika kuwa hawakutendewa haki na wangependa shirikisho hilo liingilie kati.