STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Sunday, November 10, 2013

Arsenal yafa Old Trafford, Stoke wachomoa kipigo


Waya! Wachezaji wa Arsenal hawaamini kama Robin van Persie kawatungua

BAO pekee la nyota wa zamani wa Arsenal Robin van Persie limeisaidia Manchester United kuzima ubabe wa vinara wa Ligi Kuu ya England, Arsenal kwa kuwalaza bao 1-0, huku Swansea City ikitoka nyuma na kuwalazimisha wageni wao Stoke City sare ya mabao 3-3 katika mechi nyingine ya ligi hiyo.
Van Persie alifunga bao hilo katika dakika ya 27 akimalizia kazi nzuri iliyofanywa na mshambuliaji nyota wa England, Wayne Rooney na kuifanya Mashetani Wekundu kuendeleza ubabe kwa vijana hao wa London ya Kaskazini kila timu hizo zinapokutana Old Trafford.
Kwa ushindi huo Manchester United imefikisha pointi 20 na kushika nafasi ya tano ikizishusha Everton na Tottenham Hotspur kwa uwiano wa mabao ya kufunga na kufungwa.
Katika mechi nyingine ambayo ilikuwa ya kusisimua, Stoke City ilichomoa kipigo dakika za nyongeza kwa mkwaju wa penati mbele ya Swansea ambayo ilikuwa ikionekana kuibuka na ushindi wa 3-2 baada ya kutoka nyuma.
Bao la mkwaju huo wa penati ulifungwa na Charlie Adam na kuzima ndoto za vijana wa  Michael Laudrup waliochomoa mabao waliyotanguliwa kufungwa katika kipindi cha kwanza.
Stoke walitangulia kupata bao la kwanza katika dakika ya nane kupitia kwa Jonathan  Walters na Stephen Ireland dakika ya 26 aliongeza la pili, mabao yote yakitokana na pasi ya Peter Crouch.
Wenyeji walirejesha mabao hayo kupitia kwa Wilfried Bony katika dakika ya 56 na Nathan Dyer dakika ya 74 kabla ya Bony kuelekea kuipa Swansea ushindi kwa kufunga bao la tgatu dk 86 klabla ya Stoke kuchomoa dakika ya 90+6 kwa penati na kuzifanya timu hizo zigawane pointi moja moja.

Al Ahly Mabingwa wa Afrika kwa mara ya Nane

Al Ahly celebrate their record seventh African Champions League victory
Al Ahly walipokuwa wakishangilia taji lao la mwaka jana
KLABU ya Al Ahly ya Misri imeweka rekodi ya kutwaa taji la nane la Ligi ya Mabingwa Afrika baada ya hivi punde kupata ushindi wa mabao 2-0 na kushinda kwa jumla ya mabao 3-1 dhidi ya Orlando Pirates ya Afrika Kusini.
Mabao mawili kupitia kwa nyota wake, Mohammed Aboutrika katika dakika ya 54 na jingine la Ahmed Abdul Zaher la dakika ya 78 limetosha kuwapa Wamisri hao taji hilo na kuwaacha mbali wapinzani wao katika michuano hiyo Zamalek iliyotwaa taji hilo mara tano.
Pirates waliolazimishwa sare ya 1-1 nyumbani kwao katika pambano la kwanza la Fainali hizo za Afrika, hawakuonyesha kama walikuwa na nia ya kutwaa taji kwa mara ya pili kutokana na kufunikwa na wenyeji.
Kwsa ushindi huo Al Ahly licha ya kunyakua donge nono la ushindi wa kwanza, lakini imezidi kuboresha rekodi yao ya kunyakua taji hilo baada ya kufanya hivyo katika miaka ya 1982, 1987, 2001, 2005, 2006, 2008 na 2012 kabla ya leo tena kunyakua kwa mara ya nane.

Meshack Abel kurejea Simba?

Meshack Abel wakati akiiichezea Simba
BEKI wa kimataifa wa Tanzania anayecheza soka la kulipwa nchini Kenya, Abel Meshack ameanza mazungumzo na timu yake ya zamani ya Simba ili kurejea kuja kuichezea katika duru la pili la Ligi Kuu Tanzania Bara.
Akizungumza na MICHARAZO, beki huyo wa kati mwenye mwili mkubwa, alisema viongozi wa Simba wamekuwa wakizungumza naye ili kurejea tena kuichezea timu hiyo ambayo imemaliza duru la kwanza ikiwa nafasi ya nne.
Meshack, alisema kwa jinsi mazungumzo hayo yanavyoendelea kuna uhakika wa kuichezea timu hiyo duru lijalo, licha ya kukiri mkataba wake na timu anayoichezea ya Bandari-Mombasa umebakisha miezi sita.
"Natarajia kurejea nchini Ijumaa ijayo kwa ajili ya mapumziko kwa vile Ligi Kuu Kenya imeisha na tumemaliza tukiwa nafasi ya sita, lakini tayari nimeanza mazungumzo na Simba ili kujiunga nayo," alisema Meshack.
Beki huyo aliyewahi kuzichezea pia timu za Ashanti United na African Lyon, alisema yeye binafsi angependa kuja kucheza nyumbani baada ya misimu miwili ya kucheza Kenya katika Bandari.
"Napenda kuja kucheza nyumbani baada ya kuwa nje ya nchi kwa muda, japo suala la masilahi ni kitu kitakachonishawishi zaidi," alisema.
Uongozi wa Simba haukupatikana kueleza juu ya taarifa hiyo, lakini gazeti la NIPASHE la leo lilinukuu taarifa kwamba benchi la ufundi likiwa linasaka beki wa kati ili kuimatisha safu yake ya ulinzi.
Kabla ya kwenda Kenya, Meshack alitibuana na Simba kwa kugoma kitendo cha kumpeleka kwa mkopo katika timu ya Ruvu Shooting wakati huo akiwa amepata timu ya kuceza soka la kulipwa nchini Botswana.

Al Ahly wazidi kulisogeza taji la Afrika


NI miujiza tu ndiyo itakayoweza kuizuia Al Ahly kutetea taji lao la ubingwa wa Afrika baada ya Ahmed Abdul Zaher kuiongezea bao la pili hivi punde na kuifanya Orlando Pirates kutakiwa kurudisha mabao hayo na kupata jingine la ziada iwapo wanataka kuivua taji Wamisri hao waliotawala sehemu kubwa ya pambano hilo linalochezwa mjini Cairo.
Zaher alifunga bao hilo dakika ya 78 na kuifanya Al Ahly kujiweka tayari kunyakua taji la nane la ubingwa huo na kuzidi kuweka rekodi kwa ngazi za klabu barani Afrika.

Mohammed Aboutrika aisogezea taji Al Ahly

Mohammed Aboutrika

MSHAMBULIAJI nyota wa Al Ahly, Mohammed Aboutrika ameifungia bao timu yake bao dakika chache zilizopita na kuiweka katika nafasi nzuri timu yake kutetea taji la Ligi ya mabingwa Afrika na kuzidi kuimarisha rekodi yao ya kutwaa taji hilo mara nyingi kuliko timu yoyote.
Mshambuliaji huyo mkongwe aliyenyakua tuzo mbalimbali ikiwemo ya Mchezaji Bora wa Afrika wa BBC-2008 na zile za Mchezaji anayecheza nyumbani Afrika, alifunga bao hilo dakika ya 54 akimalizia pasi murua ya Abdallah Al Said na kuiweka mbele timu yake kwa mabao ya jumla 2-1, ingawa pambano bado linaendelea. Ngoja tuone inakuwaje.

Soma Tamko Maalum toka kwa Mhe. Zitto Kabwe

Mhe. Zitto Kabwe

NILIPOKUWA katika ziara ya bara la Ulaya kati ya Oktoba 21 mpaka Novemba 2 mwaka huu (2013), nilipokea kwa njia ya barua pepe ripoti inayoitwa “Taarifa ya Siri ya Chadema” ambayo pia ilikuwa imesambazwa katika mitandao mbalimbali ya kijamii.
“Taarifa ya Chadema inasema kwamba chama hicho (chama changu) kilikuwa kimechunguza mwenendo wangu tangu mwaka 2008 hadi 2010 na kubaini kuwa mimi napokea fedha kutoka Chama Cha Mapinduzi (CCM) ili kuivuruga Chadema.
Ripoti hiyo ilinihusisha pia na mwananchi raia wa Ujerumani, Andrea Cordes ambaye, kwa mujibu wa ripoti hiyo, alinisaidia kupokea na kuhifadhi kiasi cha dola 250,000 za Marekani kupitia kwenye akaunti yake binafsi.
Taarifa hii ya kutunga na iliyojaa uongo wa kiwango cha kutisha, imenifadhaisha, kunisikitisha na kunikasirisha.
Taarifa hii iliibuliwa katika kipindi ambacho nilikuwa safarini kutetea haki za Watanzania na Waafrika ambao utajiri wao wa rasilimali unafaidiwa na watu wachache waliohifadhi mali katika nje za nje na pia kupigania makampuni ya mataifa tajiri yalipe kodi stahiki katika nchi zetu.
Pengine lengo la ripoti hiyo lilikuwa ni kutaka kunipoteza kutoka katika nia na dhamira yangu ya dhati ya kutaka Watanzania wafaidike na utajiri wao. Muda ambao watunzi wa ripoti hiyo waliamua kutoa taarifa yao unazua maswali mengi kuliko majibu.
Nafahamu kwamba mimi ni mwanasiasa ambaye nimekuwa mlengwa (target) wa mashambulizi kutoka kwa makundi mbalimbali ya wanasiasa na vikundi vyao. Kama mwanasiasa, niko tayari kupokea changamoto zozote zinazokuja na uanasiasa wangu.
Hata hivyo, ambacho sitakubali ni kwa watu kutumia jina langu na uanasiasa wangu kunichafua mimi binafsi na watu wengine wasiohusika kwa sababu ya kutaka kutimiza malengo yao ya kidhalimu.
Raia huyo wa Kijerumani tayari amekana kuhifadhi fedha zangu. Kwa maelezo yake kwa baadhi ya viongozi wa Chadema amekana kuwa na akaunti inayotajwa na amekana pia kuwepo nchini Ujerumani katika siku na wakati uliotajwa kwenye ripoti hiyo.
Ripoti hiyo imemtaja pia mtu kama Dk. Charles Kimei, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB ikidai kwamba nilikutana naye na alishiriki kwenye igizo hilo la kunipa fedha.
Niseme mapema kwamba tangu kuzaliwa kwangu sijawahi hata mara moja kukutana na Dk. Kimei popote pale ndani au nje ya nchi. Kumuingiza mtu ambaye amejenga jina lake kwenye taaluma ya kibenki kwa sababu tu ya lengo ovu la kumchafua Zitto Zuberi Kabwe si uungwana bali ni unyama.
Kutokana na uchafuzi huu wa wazi dhidi ya taswira yangu binafsi na watu wengine walioingizwa kwenye mkumbo huu, nimeandika rasmi kwa Katibu Mkuu wa Chadema, Dk.Wilbrod Slaa kumwomba athibitishe kwamba kinachoitwa Taarifa ya Siri ya Chadema ni kweli ni taarifa ya chama au kiikanushe ili niweze kuchukua hatua za kisheria dhidi ya waandishi wa hekaya hiyo.
Cha ajabu, nimepokea ujumbe wa kutishiwa maisha kutoka kwa mtu anayejiita Theo Mutahaba na kuahidiwa KUPOTEZWA endapo nitaendelea na jitihada zangu za kupambana na ufisadi na kutafuta haki kwa Watanzania wote pasipo kujali tofauti zao za kiitikadi, kikanda, kikabila na kidini.
Natarajia kuchukua hatua kali za kisheria dhidi ya wote ambao wamehusika na utungaji na uenezi wa taarifa hii. Nitahakikisha kwamba wahusika wanatafutwa na kufunguliwa mashitaka stahiki ya upotoshaji na kuchafuana.
Ni matarajio yangu kwamba wale wenye mapenzi mema na Tanzania, mimi binafsi na utawala wa sheria, wataelewa nia yangu ya kutafuta haki katika suala hili.
Nimeamua kujitolea maisha yangu kwa ajili ya Watanzania na kama alivyopata kusema Rais Mstaafu wa Afrika Kusini, Nelson Mandela; “Struggle Is My Life.”
Forward Ever, Backward Never- Kwame Nkrumah

Zitto Kabwe (Mb)
10/11/2013

Newz Alert: Majambazi yaua mfanyabiashara Moshi

WATU wanaodaiwa kuwa majambazi wamemvamia na kisha kumuua mfanyaboashara wa mbao mjini Moshi, Nickson Mushi.

Kwa mujibu wa taarifa zilizothibitishwa na Polisi mkoani Kilimanjaro zinasema kuwa tukio hilo lililotokea jana usiku na watu hao kupora kiasi cha Sh. Mil 1.7.

JF

Orlando Pirates mambo magumu Afrika

ORLANDO Pirates ipo ugenini mjini Cairo kuumana na Al Ahly ya Misri katika pambano la pili la Fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika na mpaka sasa ambapo ni mapumziko matokeo ni 0-0, huku wenyeji wakitawala sehemu kubwa ya mchezao huo.
Wenyeji wamefanya kosa kosa nyingi, lakini Orlando wameonyesha kukomaa wakisaka angalau bao moja ili kuweza kutangazwa mabingwa wapya Afrika ikiwa ni kwa mara ya pili.
Je watafanikiwa kuwavua ubingwa Al Ahly? Tusubiri baada ya kipindi cha pili kitakapomalizika.

Mashujaa wetu warejea nyumbani kuisubiri Afrika Kusini


WACHEZAJI wa timu ya Taifa ya Wanawake chini ya miaka 20, Tanzanite,
wakiwasili Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, Dar es
Salaam, leo wakitokea nchini  Msumbiji ambako jana waliichabanga timu hiyo kwa mabao 5-1  katika mchezo wa marudiano wa raundi ya pili ya michuano ya
Kombe la kuwani tiketi ya kufuzu kucheza  kombe la Dunia.
   
Katika mechi ya awali iliyochezwa jijini Dar es Salaam, Tanzanite waliisasambua Msumbiji kwa mabao 10-0 na hivyo kusonga mbele katika michuano hiyo na sasa itakutana na Afrika Kusini iliyowang'oa Botswana. Mechi ya kwanza itachezwa uwanja wa ugenini kabla ya kurudiana nao jijini Dar es Salaam.

Sunderland yaiduwaza Manchester City

Phil Bardsley scored
Kipa wa Manchester City Mannone akiwa haamini kama mpira unatinga wavuni kuipa ushindi Sunderland

KLABU ya Sunderland imeendelea kujitutumua katika Ligi Kuu ya England baada ya jioni hii kupata ushindi wake wa pili katika ligi hiyo kwa kuikwanyua Manchester City kwa bao 1-0.
Bao la dakika ya 21 kupitia kwa Phil Bardsley aliyemalizia kazi nzuri ya Wes Brown, lilitosha kuwafanya vijana wa Gustavo Poyet kuibuka na ushindi huo nyumbani japo haujawatoa kwenye nafasi ya pili toka mkiani licha ya kufikisha pointi 7.
Manchester City waliokuwa wapo kamili licha ya kufanya mabadiliko katika kipindi cha pili ili kutaka kurejesha bao hilo ilijikuta ikishindwa kufurukuta kwa vijana wa Poyet ambao walicheza 'ng'adu ng'adu' ili kulinda bao lao na mpaka filimbi ya mwisho ya mwamuzi Michael Dean, wenyeji waliibuka kidedea.
Kipindi hicho ambacho kimetokea muda mchache baada ya Tottenham Hotspur nao kulala kwa bao 1-0 toka kwa Newcastle United imeendelea kusalia na pointi zake 19 ikishika nafasi ya saba na kuna hatari ya kuporomoka iwapo pambano linaloendelea sasa kati ya Manchester United dhidi ya Arsenal litaisha kwa Mashetani Wekundu kushinda.

Inasikitisha! Walimu wafa ajalini


AJALI za barabarani zimeendelea kuchukua roho na watanzania wenzetu baada ya walimu wakuu watatu wa Shule tofauti za Tarafa za Magole, wilayani Kilosa kufariki katika ajali mbaya.
Taarifa kutoka Morogoro zinasema kuwa walimu hao watatu ambao majina yao yametajwa kuwa ni Mwl Margareth Kimbo, Mwl Agrey Kikwesha na Mwl Lanford Mhando waliaga dunia baada ya gari walilokuwa wakisafiria nalo lililobeba walimu wengine kupasuka tairi na kupinduka.
kutoka shule mbalimbali za Tarafa ya Magole wilayani Kilosa, wamefariki dunia baada ya gari walilokuwa wakisafiria kupata ajali.
Walimu wengine 17 waliokuwa katika gari hilo wamejeruhiwa baadhi hali zao zikielezwa kuwa mbaya na wamelazwa hospitalini.

Walioshuhudia wandai ajali hiyo ilitokea katika kijiji cha Mvumi, Rudewa eneo la Kisangata mkoani Morogoro wakati walimu hao walipokuwa wakiitikia wito wa ghafla toka kwa Mkuu wa Wilaya hiyo.
Inaelezwa kuwa walimu na waratibu zaidi ya 17 walikuwa katika gari hilo aina ya Toyota Hiace kabla ya tairi ya nyuma kupasuka na gari kuringika mara nne na kupelekea maafa hayo na majeruhi hao.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Morogoro Faustine Shilogile alithibitisha kuhusiana na ajali hiyo aliyodai gari hilo lilipasuka tairi kabla ya kuanguka likibiringika mara kadhaa na kusababisha vifo vya walimu hao wakuu na wengine kujeruhiwa vibaya.

Tottenham yafa tena nyumbani EPL

Newcastle United's Tim Krul (third left) punches the ball clear from Tottenham Hotspur's Younes Kaboul
Hekaheka katika lango la Newcastle United
BAO pekee lililofungwa na Loic Remy wa Newcastle United katika dakika 13 lilitosha kuipa ushindi wa ugenini timu yake walipoifuata Tottenham Hotspur kwenye uwanja wake wa White Hart Lane katika mechi ya Ligi Kuu ya England iliyoisha hivi punde.
Mfungaji wa bao hilo alimalizia kazi nzuri ya Youn Gouffran na kuifanya wageni kuondoka na ushindi wa bao 1-0 na kiufikisha jumla ya pointi 17 ikilingana na Manchester United ambayo baadaye itashuka dimba la nyumbani kuikaribisha Arsenal katika pambani jingine la ligi hiyo.
Kipigo hicho cha pili nyumbani kwa Spurs imeifanya ishindwe kurejea katika Tatu Bora ya ligi hiyo baada ya awali kunyukwa mabao 3-0 na West Ham mwezi uliopita na kuwa mchezo wa tatu kupoteza msimu huu katika ligi hiyo inayozidi kushika kasi.

Sevilla yaifumua Espanol kwao 3-1

http://www.soccersouls.com/wp-content/uploads/2013/01/1301799637-thumb02.jpg
Federico Fazio
ESPANYOL jioni hii imejikuta ikikumbana na kipigo cha paka mwizi kwa kunyukwa mabao 3-1 ikimaliza mechi yao ya nyumbani wakiwa pungufu baada ya mchezaji wake mmoja kuonyeshwa ya pili ya njano na kutolewa uwanjani na nyekundu katika mchezo uliomaliza hivi punde.
Kipigo hicho cha nyumbani Espanyol wamepewa na Sevilla ambao mpaka wakati wa mapumziko walikuwa mbele kwa mabao 2-1.
Bao la kwanza likitupiwa kambani na Federico Fazio dakika ya nne tu ya mchezo kabla ya Vitolo kuongeza la pili dakiia sita baadaye na wenyeji kupitia bao pekee kwenye dakika ya 24 kutia kwa Sergio Garcia.
Msumati wa mwisho katika jeneza la Espanyol ulipigiliwa katika dakika ya 59 na Carlos Bacca na dakika tano kabla ya mchezo kumalizika wenyeji walijikuta wakipata pengo baada ya kiungo wao Victor Sanchez kulimwa kadi nyekundu baada ya kuonyesha kadi mbili za njano ndani ya dakika tatu  ya kwanza kipewa dakika ya 82 na nyingine 85 na mwamuzi Miguel Ayza kumtoa nje.
Kwa ushindi huo Sevilla imefikisha pointi 16 ikichupa kutoka nafasi ya 14 hadi nafasi ya 10, huku wapinzani wao wakisaliwa na pointi zao 15 na kuporomoka hadi nafasi ya 12.
Ligi hiyo inatarajiwa kuendelea jioni hii kwa mechi kadhaa ikiwemo ile ya mabingwa watetezi, Barcolona itakuwa ugenini kukabiliana na wenyeji wao Real Betis.

Ni Al Ahly au Orlando Pirates Ligi ya Mabingwa Afrikawa bingwa mpya Afrika

http://news.bbcimg.co.uk/media/images/70056000/jpg/_70056514_ahly_pirates.jpg

WAKATI macho na masikio ya mashabiki wa soka yakielekezwa katika pambano la kukata na shoka baina ya Arsenal itakayokuwa ugenini Old Trafford kuwakabili wenyeji wao Manchester United, Afrika leo kuna kipute cha Ligi ya Mabingwa Afrika kati ya Al Ahly ya Misri na Orlando Pirates ya Afrika Kusini.
Pambano hilo la marudiano baina ya timu hizo linatarajiwa kufanyika saa 1 jioni mjini Cairo, huku mabingwa watetezi, Al Ahly ikipewa nafasi kubwa ya kutetea tena taji hilo baada ya kupata sare ya 1-1 katika mechi ya kwanza iliyochezwa mjini Johannesburg, Afrika Kusini.
Mechi hiyo ambayo itachezwa kwenye uwanja wa Osman Ahmed Osman (Arab Contractors) inatarajiwa kuwa na ushindani mkubwa kutokana na presha kubwa walionao mabingwa wa zamani wa ligi hiyo, Orlando ambapo kocha wake Roger De Sa, ametamba anataka kuwapa raha mashabiki wake kwa kutwaa taji hilo.
Hata hivyo kikosi hicho kinapaswa kuwa makini katika pambano hilo iwapo inataka kutwaa taji mikononi mwa Al Ahly ambayoi itashuka dimba ikiwategemea nyota wake kama Mohammed Aboutrika, Wael Gomaa, Ahmed Abdul Zaher na Waleed Soliman ambao watakuwa uwanja wa nyumbani.
Sare ya aina yoyote katika pambano hilo la leo litaiwezesha wenyeji kunyakua taji kwa mara nane na kuzidi kuweka rekodi katika michuano hiyo.
Orlando Pirates iliyoanzishwa 1937 inataka kunyakua taji hilo kwa mara ya pili baada ya kufanya hivyo kwa mara ya kwanza mwaka 1995 walipoikandika ASEC Memosas kwa jumla ya mabao 3-2.

Uchaguzi Mkuu wa TBF kufanyika Desemba 10


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Ndugu Wanahabari
Napenda kwa leo kuchukua fursa hii kutoa tangazo rasmi la tukio la uchaguzi mkuu wa viongozi wa Shirikisho la Mpira wa Kikapu Tanzania (TBF). Mwaka huu wa 2013 ndio ambao uongozi wa shirikisho unafikia ukomo wake, na kikatiba inabidi ufanyike uchaguzi kuwapata viongozi wapya watakaoendesha shughuli za shirikisho kwa miaka minne ijayo.
Hivyo basi, kwa niaba ya TBF natangaza rasmi kuwa uchaguzi mkuu wa viongozi wa shirikisho unatarajiwa kufanyika tarehe 10 Disemba 2013 huko mkoani Mbeya, ikiwa ni siku 30 kabla ya uchaguzi huo, ambapo kikanuni inapasa kutoa tangazo rasmi la uchaguzi. Uchaguzi huo utafanyika mara baada ya kumalizika kwa mashindano ya taifa cup ambayo mwaka huu yanafanyika mkoani Mbeya kuanzia tarehe 30 Novemba mpaka tarehe 8 Disemba 2013 huko jijini Mbeya.
Safu ya uongozi kikatiba wanaopaswa kuchaguliwa ni pamoja na:
  1. Rais
  2. Makamu wa Rais
  3. Katibu Mkuu
  4. Katibu Mkuu Msaidizi
  5. Mhazini
  6. Kamishna wa Mipango
  7. Kamishna wa Ufundi na Mashindano
  8. Kamishna wa Waalimu
  9. Kamishna wa Watoto na Mashule
  10. Kamishna wa Wanawake
  11. Kamishna wa Waamuzi
  12. Kamishna wa Tiba ya Wanamichezo
  13. Kamishna wa Walemavu
Taratibu zote za uchaguzi huu zitasimamiwa na Baraza la Michezo la Taifa (BMT) ambao ndio watakaokuwa wakitoa fomu za maombi ya wagombea.
Kwa niaba ya uongozi wa Shirikisho napenda kuchukua nafasi hii tena kuwaomba wadau, wapenzi wa michezo na wananchi wote kwa ujumla wenye sifa na wanaopenda kuongoza Shirikisho letu wajitokeze kwa wingi kuchukua fomu za maombi ya uongozi wa Shirikisho mara baada ya tangazo la Baraza la Michezo (BMT) la kuanza kuchukua fomu hizo kwa nafasi zote zilizo takazotangazwa. Shime wanamichezo katika kuleta mabadilko chanya katika mchezo wa mpira wa kikapu Tanzania.
Mussa Mziya
Rais
Shirikisho la Mpira wa Kikapu Tanzania(TBF

Kumekucha pazia la usajili dirisha dogo

Kipa Juma Kaseja aliyemwaga wino Yanga
USAJILI wa wachezaji kwa dirisha dogo kwa msimu wa 2013/2014 Tanzania Bara unafunguliwa Novemba 15 mwaka huu na utafungwa rasmi Desemba 15 mwaka huu.
Kwa mujibu wa kanuni, klabu zenye fursa ya kusajili wachezaji katika dirisha dogo ni zile ambazo hazijatumia nafasi zote 30 za wachezaji.
Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) na Ligi Daraja la Kwanza (FDL) zimemaliza duru la kwanza msimu huu. Duru za pili litaanza kutimua vumbi Januari mwakani.
Kwa mujibu wa Kalenda ya Matukio ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) matukio ya Novemba na Desemba ni dirisha dogo la usajili na mechi za kirafiki za Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA)- FIFA Date.
Matukio mengine ni michuano ya Kombe la Uhai inayoshirikisha wachezaji wenye umri chini ya miaka 20 wa klabu za VPL na michuano ya Kombe la Chalenji itakayofanyika Nairobi, Kenya.
Tayari baadhi ya klabu zimeshaanza kuwekana sawa na wachezaji kwa kuwasainisha mikataba kama ilivyofanya Yanga kwa kipa wa zamani wa Simba, Juma Kaseja aliyemwaga wino kwa kuichezea timu hiyo kwa miaka miwili kwa donge la Sh Mil 40.

Wanawake wa3 wacharangwa mapanga, wachomwa moto kwa tuhuma za uchawi

Picha hii haihusiani na habari
WANAWAKE watatu wa Kijiji cha Nyamikoma, wilayani Busega mkoa wa Simiyu wameuwawa kikatili wakishambuliwa kwa silaha za jadi kisha kuchomwa moto kwa kutuhumiwa wanajihusisha na vitendo vya kishirikina.
Kwa mujibu wa taarifa kutoka mkoani humo na kuthibitishwa na Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Simiyu, Salum Msangi ni kwamba wanawake hao ambao majina yao hayakupatikana mara moja wana umri kati ya miaka 30-70.
Inaelezwa kuwa kwa muda mrefu wanawake hao na mwenzao mmoja aliyenusurika na kifo walikuwa wakituhumiwa kuwafanyia wenzao ulozi na kuufanya uongozi wa kijiji hicho kuitisha mkutano ili kuwajadili.
Inaelezwa katika mkutano huo ulioitishwa na Mwenyekiti wa Kijiji uliwaamuru wanawake hao wanne kuhama kijiji hicho na wakati wakiwa katika harakati za kuhama ndipo wakavamiwa na baadhi ya wanakijiji na kuanza kuwashambulia.
Wanawake hao walishambuliwa kwa silaha kama mapanga, mawe, magogo, nondo kabla ya kuchomwa moto kama nyama ya kubanika na kupoteza uhai wao, huku pia nyumba zao zikibomolewa na watu hao waliofanya unyama huo.
Taarifa kutoka kijijini hapo zinasema kuwa kabla ya wanakijiji hao kufanya unyama huo wanadai waliwahi kumnasa mmoja wa wanawake hao aliyekuwa na umri wa miaka ya 30 akifanya ulozi katika nyumba ya wanakijiji mwenzake na kumbana kuwataja wenzake wanaoshirikiana katika vitendo hivyo.
Miongoni mwa majina 15 yaliyotajwa watatu pamoja na yeye mwenyewe ni wa kijiji hicho na ndipo ukalazimishwa kuitishwa mkutano ili kuwatimua kijijini hapo kabla ya watu wenye hasira kuwafanyia ukatili huo wa kutisha.
Kamanda wa Polisi wa Simiyu, Salum Msangi, alikiri kutokea kwa tukio hilo na kusema wanawashikilia watu 19 kuhusiana na mauaji hayo na wengine wakiendelea kusakwa huku wakiwaonya wananchi kuacha kutumia sheria mikononi na kuendesha ukatili kama huo.
Kamanda huyo alisema wananchi wanapaswa kuepuka imani potofu juu ya ushirikiana na kudai voitendo hivyo vimezidi kukithiri katika eneo lake na kudai Polisi inarudia kuwataka kuacha imani hizo.

Mwanamke anaswa kwa wizi wa kichanga, ajitetea alitaka kulinda ndoa yake isiyo na mtoto kwa muda mrefu

MWANAMKE mmoja wa Kijiji cha Kashishi, Halima Mbuja anashikiliwa na Polisi kwa tuhuma za kuiba mtoto mchanga.
Kwa mujibu wa taarifa kutoka Nzega, Tabora zilizothibitishwa na Kamanda wa Polisi wa mkoa huo, Peter Ouma zinasema kuwa mwanamke huyo alimuiba mtoto huyo Novemba 3 na kunaswa naye Novemba 9.
Taarifa hizo zinasema kuwa mtoto huyo aliibwa kutoka kwa mama yake aitwaye Tatu Mmbasha mara waliporuhusiwa kutoka hospitali ya wilaya ya Nzega baada ya kuzaliwa baada ya Halima kujifanya msamaria mwema na kumsaidia.
Inadaiwa baada ya kumpokea mtoto huyo, mwanamke huyo alitoweka naye na kumuacha katika hali ngumu mama mzazi wa kichanga hicho ambapo baada ya Polisi kupata taarifa ilishirikiana na wasamaria wema kumtafuta mtoto huyo na kumkuta katika kijiji cha Kashishi akiwa hai mwenye afya tele.
Kamanda wa Polisi alisema mtuhumiwa huyo alikiri kuiba mtoto huyo kwa nia ya kutaka kulinda ndoa yake ambayo ina miaka mingi, bila ya kuwa na mtoto na kwamba taratibu za kumfikisha mahakamani kwa kosa alililofanya zinafanyika.