STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Thursday, January 3, 2013

Thomas Mashali kuuanza mwaka dhidi ya Mkenya

 
Bondia Thomas Mashali
BONDIA machachari wa ngumi za kulipwa nchini Thomas Mashali anatarajiwa kupanda ulingoni Januari 12 katika ukumbi wa Friends Corner Manzese Jijini Dar es Salaam kutetea Ubingwa wa Afika  Mashariki.
 
Akiongea na waandishi wa habari Mratibu wa pambano hilo Aisha mbegu alisema mashali atapambana kuzipiga na Mkenya Bernard Mackoliech mpambano utakaokuwa wa raundi 10.
 
Alisema maandalizi yamekamilika ikiwa pia na kutumiwa tiketi kwa bondia huyo mkenya ambaye anatarajiwa kuwasili januari nane kwa ajili ya kupima uzito na kupanda ulingoni.
 
“tunataraji mpambano utakuwa mkali wa kukata na shoka ukizingatia mashali ameweka kambi kwa muda mrefu nje ya mkoa lakini pia Mackoliech ni bondia mahiri ambaye anasaka rekodi ya kwenda kucheza nje ya nchi”,alisema Aisha.
 
Alisema nafasi iko wazi kwa watu wanaotaka kudhamini ili kuhakikisha mpambano huo unafanikiwa ukizingatia ndio mpambano wa kwanza kwa mwaka 2013 na pia mashali anavutia mashabiki wengi.
 
Kwa upande wake rais wa TPBO amesema mapambano ya utangulizi yanatarajiwa kuwa manne na mabondi tayari wamesaini mikataba na watatangazwa hivi karibuni.
 
Bondia Thomas Mashali anatetea ubingwa huo wa Afrika mashariki na kati ambao aliupata baada ya kumpiga Mganda Medi Sebyala Jijini Dar es salaam mpambano uliohudhuriwa na mashabiki lukuki.
 
Mwisho.

Tangulia Sajuki, kweli wewe ulikuwa mpiganaji

Sajuki enzi za uhai wake nilipomtwanga picha nyumbani kwake Magomeni kwa Macheni


KWA kipindi cha miaka miwili mfululizo, Juma Juma Kilowoko maarufu kama Sajuki, aliweza kupigana na kupambana na maradhi yaliyokuwa yakimsumbua tangu mwaka 2010.
Pamoja na kwamba alianza kuugua tangu mwaka 2010, hakuna aliyekuwa anafahamu kutokana na kufanya usiri mkubwa akijiuguza mwenyewe na familia yake, lakini mambo yalipomzidi ndipo mapema mwaka jana alijitokeza hadharani na kuweka bayana kabla ya Mei kupelekwa India kufanyiwa upasuaji.
Tangu alipotoka India, kila aliyemuona kwa siku za karibuni aliamini amefanikiwa kuyashinda mauti, kwa vile alijichanganya na kuendelea na shughuli zake, lakini kumbe Mungu alikuwa na siri kubwa nyuma ya matukio yake kwani alimpa fursa ya kuuaga salama mwaka 2012 na kuuona mwaka mpya wa 2013 kabla ya saa chache akamchukua na kutuachia majonzi watanzania walio wengi.
Sajuki, mmoja wa waigizaji, watunzi, waongozaji na wazalishaji wa filamu nchini aliyekuwa mtu wa watu amesaliwa saa chache kabla ya kupelekwa kwenye makazi yake ya milele katika makaburi ya Kisutu, jijini Dar er Salaam baada ya kuaga dunia jana asubuhi hospitalini Muhimbili.
Binafsi nilipata taarifa hizo nikiwa nyumbani kwangu, KImara King'ongo nikijiuguza Malaria na mafua makali yaliyonishika tangu Desemba 31 mwaka jana.
Nilishtuka kwa vile zilikuja ghafla mno, japo nilikuwa nafahamu Sajuki, alikuwa kalazwa Muhimbili baada ya kuzidiwa alipokuwa kwenye ziara ya kuwashukuru Watanzania na kuchangisha fedha za kupelekwa tena India jijini Arusha.
Sikuwa na kitu kingine cha kusema zaidi ya Alhamdulillah kulingana na mafundisho ya dini yetu na kumalizia kwa Innalillah Wainaillah Rajiun, kama Mtume Muhammad SAW aliyotuelekeza kila tunapokumbwa na Msiba tuseme hivyo kwa maana kwamba 'Sisi ni waja wa Mwenyezi Mungu na kwake hakika tutarejea'.
Pamoja na kwamba Sajuki ametutoka tungali tukimuhitaji katika fani yake na namna alivyokuwa akionyesha anavyothamini kazi kuliko hata afya yake, lakini Mungu ana mapenzi zaidi na tunapaswa kumshukuru.
Namkumbuka Sajuki, aliyenidokeza jina hilo lilitokana na muunganiko wa majina ya kaka yake aitwae Salum na lake la Juma na lile la ukoo yaani Kilowoko na kuzaa SAJUKI, kwa ucheshi, utani na kujiamini kupita kiasi alikojaliwa na maanani.
Mara ya kwanza kukutana naye nakumbuka ilikuwa mwaka 2009 nyumbani kwake Magomeni Mapipa nilipoenda kufanya mahojiano naye ambapo aliweza kuweka bayana ndoto aliyokuwa nayo tangu utotoni ya kuja kuwa muigizaji mchekeshaji kama Amri Athuman maarufu kama King Majuto.
"Nilitamani sana kuwa mchekeshaji kama King Majuto, lakini filamu za Sylvester Stallone 'Rambo' na ubabe wake zilibadilisha upepo na kujikuta kwenye filamu za kawaida na hasa zile za mapugano na ubabe," aliniambia nilipozungumza naye huku jirani yake akiwepo Soud Ally maarufu kama Chomba au Akuhi.
Sajuki, ambaye majina yake kamili ni Juma Juma Issa Kilowoko, alisema hamu yake ya kufika mbali katika sanaa ya uigizaji ndiyo iliyomfanya apite kundi moja hadi jingine hadi kuangukia Kaole Sanaa, lililomtangaza vema kupitia michezo iliyokuwa ikirushwa na kituo cha runinga cha ITV.
Alisema mchezo wake wa kwanza ndani ya kundi hilo lililotoa nyota kibao wa filamu nchini ni Baragumu wa mwaka 2005 na kufuatia na michezo mingine hadi mwaka 2008 alipojitoa kundini na kujikita zaidi katika filamu, kazi yake ya kwanza ikiwa ni Revenge.
"Baada ya kupita makundi kadhaa tangu nikiwa mjini Songea nilipozaliwa, hatimaye nilitua Kaole Sanaa, lililoniivisha kabla ya kuachana nao kusaka masilahi zaidi na kujikita katika filamu," alisema.
Mbali na Revenge filamu zingine alizocheza Sajuki ni pamoja na Dhambi, Mboni Yangu, Two Brothers, Behind the Scene, Round, Shetani wa Pesa, Hero of the Church na nyinginezo.
Wakati nilipokuwa nazungumza naye alikuwa akijiandaa kutoa filamu mbili binafsi za Vita na Briefcase zilizowashirikisha nyota kadhaa nchini akiwemo mshindi wa pili wa BBA, Mwisho Mwampamba.
Sajuki alisema fani ya filamu imemnufaisha kwa mambo mengi ikiwemo kimaisha, lakini kubwa ni kufanikiwa kumuoa mke mrembo na muigizaji mwenzake, Wastara Issa Juma 'Stara'.
"Kufanikiwa kumpata Wastara na kumuoa kwangu ni jambo kubwa na la kuvutia mno kati ya mafanikio kibao niliyoyapata katika fani hii ya filamu nchini," alisema.
Mkali huyo, aliyekuwa akipenda kucheza na watoto na shabiki wa muziki wa 'Quito', alisema kama kuna kitu kinachomkera katika sanaa hiyo ni tabia za 'Wauza Sura' wanaojiingiza kwenye skendo chafu zinazowachafua wasanii wote wa tasnia hiyo mbele ya jamii.
Alisema wasanii wenye kusaka umaarufu kwa lazima wanamnyima raha kwa vile jamii inadhani wasanii wote wana silka na tabia kama za wauza sura hao wanaojirahisi na kujidhalilisha.
Kuhusu rushwa ya ngono, Sajuki mtoto wa nne kati ya watano wa Mzee Juma Issa Kilowoko, alisema wanaojihusisha nao wanafanya hivyo kwa kujitakia kwa sababu hakuna anayelazimishwa kutoa mwili wake iwapo ana uwezo na kipaji kikubwa katika sanaa hiyo.
"Rushwa ya ngono kwa watoto wakike ni kujitakia kwa vile wana akili na ufahamu wa kujua athari za kufanya hivyo na watayarishaji wanaolazimisha hawafai na wanapaswa kuchukuliwa hatua kali za kisheria," alisema Sajuki.
Sajuki, alinidokeza kuwa hakuna kitu kilichomtia simanzi na kumsikitisha kama tukio la ajali ya pikipiki iliyompata akiwa na mkewe, Wastara Juma enzi wakiwa wachumba.
Nyota huyo ambaye ameacha mjane na mtoto mmoja wa kike, aliishukuru familia yake na Vincent Kigosi 'Ray' kwa kumfikisha alipokuwapo alisema ajali hiyo sio inayomuuma, ila kitendo cha kulazimika kuidhinisha fomu hospitalini ili Wastara akatwe mguu wake uliokuwa umeharibika kwa ajali hiyo.
"Kwa kweli kile kitendo cha kuidhinisha kukatwa kwa mguu kwa Wastara kinaniuma hadi leo, lakini sikuwa na jinsi ila kufanya hivyo ili kumuokoa," Sajuki aliniambia kwa masikitiko katika mahojiano hayo.
Hata hivyo alidai alikuwa akijisikia fahari mno kuoana na kisura huyo ambaye kwa sasa anao mguu wa bandia, kwa vile wamesaidiana kuanzisha kampuni yao binafsi ya Wajey Films Production.
Sajuki alizaliwa miaka 27 iliyopita huko Songea na kusoma hadi elimu ya sekondari katika shule za Songea na Luwiko, alikoanza kuonyesha kipaji chake cha sanaa katika matamasha mbalimbali ya shule kabla ya kujitosa kwenye makundi.
Mungu ailaze mahali pema roho ya marehemu Sajuki anayezikwa kesho katia makaburi ya Kisutu.


Mwisho

Kado azivuruga Yanga, Mtibwa

Kado akitambulishwa na viongozi wa Coastal Union hivi karibuni

KLABU za Yanga na Mtibwa Sugar zimeendelea kuzozana kuhusiana na mchezaji Shaaban Kado baada ya kipa huyo kusaini mkataba wa kuichezea Coastal  Union ya Tanga kwa mwaka mmoja.
Kipa huyo ambaye aliichezea Mtibwa kwa mkopo katika mzunguko wa kwanza wa msimu akitokea Yanga, amekuwa chanzo cha malumbano baina ya klabu hizo; ambapo ‘Wanajangwani’ wanadai kuwa wana haki ya kumuuza kokote kwavile ni mchezaji wao halali huku ‘wakata miwa’ wa Mtibwa wakisisitiza kuwa anapaswa kuendelea kubaki kwao kwavile walimtwaa kwa mkataba wa kuichezea hadi mwisho wa msimu.
Hata hivyo, akizungumza jana, Kado alisema kuwa tayari ameshasaini mkataba wa mwaka mmoja kuichezea Coastal iliyowahi kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara mwaka 1988.
“Ni kweli nimesaini mkataba wa mwaka mmoja katika klabu ya Coastal… na nimeshaanza kufanya nao mazoezi,” alisema Kado.
Akieleza zaidi, kipa huyo alisema: “Kulikuwa na mvutano kati ya Yanga na Mtibwa juu yangu, lakini kila kitu kuhusiana na hilo nimewaachia wao. Naamini watamalizana,” alisema Kado.
Mratibu wa Mtibwa, Jamal Bayser, alisema jana kuwa wameshangazwa na kitendo cha Yanga kumuuza mchezaji huyo il-hali walikubaliana kuichezea timu yao (Mtibwa) hadi mwishoni mwa msimu huu wa ligi kuu ya Tanzania Bara.
Bayser alisema kuwa tayari klabu yake imewasilisha malalamiko katika Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kuhusiana na suala la kipa huyo ambaye aliwahi kuichezea Mtibwa kabla ya kuuzwa Yanga na baadaye kurejea tena klabuni hapo kwa mkopo.
“Inashangaza sana kuona klabu zinasajili wachezaji kinyume na utaratibu. Kulingana na makubaliano yetu na Yanga, Kado anatakiwa kuitumikia Mtibwa hadi mwishoni mwa msimu huu,” alisema Bayser.
“Tumeshaandika barua TFF, maana tulikubaliana na na Yanga, tena tukaweka mkataba kimaandishi. Sasa tunasubiri TFF watoe maamuzi,” aliongeza mratibu huyo.
Alipotafutwa na gazeti hili jana kuzungumzia suala hilo, Katibu Mkuu wa Yanga, Lawrence Mwalusako alisema kuwa kwa sasa hawana muda wa kuzungumzia suala hilo kwavile Kado si mali yao tena kwa sasa.
“Kado ni mali ya Coastal Union kwa sasa, siwezi kuzungumzia suala la mchezaji huyo maana siyo mali yetu tena (Yanga),” alisema Mwalusako.
Afisa Habari wa TFF, Boniface Wambura alisema kuwa sakata la mchezaji huyo limepelekwa kwenye Kamati ya Sheria, Maadili na Hadhi za Wachezaji ya TFF ili lipatiwe ufumbuzi.


Chanzo:NIPASHE

Golden Bush Veterani, Wahenga Fc kurudiana Januari 12

Kikosi cha Golden Bush Veterani ambacho kinatarajiwa kurudiana na Wahenga Fc Januari 12

BAADA ya kukaribisha mwaka kwa kipigo cha aibu cha mabao 4-3 kutoka kwa wapinzani wao, timu ya soka ya Golden Bush Veterani, imekata rufaa na sasa watarudiana na wapinzani wao Wahenga Fc Januari 12.
Tayari pande zote zimekuwa zikitoleana tambo mbalimbali Wahenga wakisisitiza kuwa waliamua kutoa zawadi ya mwaka mpya kwa watani zao kwa kuwapa kipigo hicho, huku Golden Bush kikisisitiza kuwa waliotewa na kwamba mechi hiyo ya kisasi wataifumua Wahenga mabao 7-0.
Golden Bush tayari kimeweka hadhaarani kikosi kitakachoshuka dimbani siku ya mechi hiyo ambapo golini atakuwepo Hamza, kipa wa timu yao ya vijana huku kulia atasimama Chidi Rasta, kushoto Abuu Ntiro, Mmalawi Wisdom Ndhlovu atacheza kama beki namba nne na mkoba atakuwa Majaliwa.
Kiungo nama sita atacheza Yahya Issa, wingi ya kulia atasimama mlezi wao, Onesmo Wazir 'Ticotico' na Katina Shija atazungusha dimba la juu, Herry Morris atacheza kama mshambuliaji wa kati na Kapeta atacheza namba 10 na Said Swedi Panucci atacheza wingi ya kushoto.
Pamoja na Golden Bush kujinasibu kushinda mchezo huo wa marudiano, Wahenga wamekejeli wakieleza kuwa wao hawana hofu yoyote kwa sababu soka wanalijua japo wachezaji wao hawana majina makubwa kama ya wapinzani wao ambao katika mechi zao mbili za awali walitoka sare ya 1-1 na kisha kuwanyuka mabao 4-2 kabla ya kuwazima wiki mwishoni mwa wiki kwa mabao hayop 4-3 mechi zote zikichezwa kwenye uwanja wa TP Afrika, Sinza Dar es Salaam.

Je, nani atakayeiobuka na ushindi? Tusubiri kuona hiyo Januari 12.

HALI HALISI ILIVYO NYUMBANI KWA MAREHEMU SAJUKI


Mke wa marehemu, Juma Kilowoko 'Sajuki', Wastara Juma (aliyejifunika nguo) akiwa na simanzi nzito kwa kumpoteza mumewe.
Mzee Kilowoko ambaye ni baba mzazi  wa marehemu 'Sajuki' akiwasiliana na ndugu na jamaa msibani hapo.
Mama  mzazi  wa marehemu Sajuki (wa kwanza kushoto) akiwa na majonzi.
Dada wa Wastara aitwaye Marian (aliyesujudu) akilia kwa uchungu.
 
Bibi wa marehemu Sajuki akiwasili msibani.
Pichani juu ni baadhi ya taswira za waombolezaji wakiwa nyumbani kwa marehemu Juma Kilowoko 'Sajuki', Tabata- Bima jijini Dar es Salaam. Sajuki amefariki dunia jana asubuhi akiwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili ambapo alikuwa akitibiwa.
(PICHA NA HAMIDA HASSAN / GPL)

Chelsea hoi wa QPR, Liverpool yazidi kupeta

Wachezaji wa QPR wakimpongeza Shaun Wright Phillips aliyefunga bao pekee lililoiangusha Chelsea jana usiku.

WAKATI Liverpool ikiendeleza wimbi la ushindi kwa kuisambatarisha timu ya Sunderland kwa mabao 3-0, Chelsea walijikuta wakiteleza nyumbani kwao uwanja wa Stanford Bridge kwa kudunguliwa bao 1-0 na 'vibonde' wa Ligi Kuu ya England, QPR inayonolewa na kocha Harry Redknapp.
Chelsea ilikumbana na kipigo hicho kutokana na bao la nyota wake wa zamani Shaun Wright-Phillips aliyefunga katika dakika ya 78 kutokana na kazi nzuri ya Mmorocco Adel Taarabt.
Kipigo hicho kimeiacha Chalsea kwenye nafasi ya nne ikiwa na pointi 38 ikishindwa kuipiku Tottenham waliowazidi pointi moja wanaokamata nafasi ya tatu nyuma ya Manchester City na Manchester United.
Liverpool wakiwa kwenye uwanja wao wa nyumba waliinyoa Sunderland kwa mabao 3-0, mabao wawili yakitupiwa kambani na Luis Suarez, huku bao la awali likifungwa na Raheem Sterling akimalizia kazi ya Suarez.
Katika mechi nyingine ya mfululizo wa ligi hiyo Newcastle United imeendeleza wimbi la vipigo kwa kulala nyumbani kwao mabao 2-1 toka kwa Everton.

SAJUKI  KUZIKWA KESHO MAKABURI YA KISUTU

Sajuki akichapa mzigo enzi za uhai wake
Sajuki na mkewe Wastara enzi za uhai wake
Baba yake Sajuki... Mzee Kilowoko akiwasiliana na ndugu na jamaa kwa simu wakati akiwa kwenye msiba wa mwanawe, Tabata jijini Dar es Salaam jana. Familia imeamua Sajuki azikwe makaburi ya Kisutu jijini Dar es Salaam kesho Ijumaa.

Wasanii wa vichekesho, Mtanga (kushoto) na Kiwewe (aliyejishika goti) wakiwa na waombolezaji wengine katika msiba wa Sajuk.

Waombolezaji wakiwa nyumbani kwa marehemu Sajuki
Tutakukumbuka milele Sajuki... msanii nyota wa filamu za Kibongo, Suzan Lewis 'Natasha' akiwa kwenye msiba wa Sajuki mapema leo kushiriki maandalizi ya shughuli za mazishi, eneo la Tabata jijini Dar es Salaam 
Baadhi ya waombolezaji wa msiba wa Sajuki waliofika mapema Tabta

Piga pale...! Sajuki (kulia) akiwa katika maandalizi ya filamu yake ya Vita wakati wa enzi za uhai wake.


Waombolezaji wakiwa na majozni tele katika msiba wa Sajuki, Tabata jijini Dar es Salaam.
HATIMAYE ule utata kuhusiana na mahala pa kumzika msanii Juma Kilowoko 'Sajuki' umepatiwa jibu baada ya baba yake kukubali kuwa azikwe jijini Dar es Salaam.

Kutokana na uamuzi huo, sasa msanii huyo aliyekuwa nyota na kipenzi cha wengi enzi za uhai wake atazikwa kesho 
saa 7:00 mchana baada ya swala ya Ijumaa kwenye makaburi ya Kisutu.

Awali, baba wa msanii huyo alitaka mwanawe akazikwe kwao mkoani Songea. Hata hivyo, baada ya kuketi na kujadili kwa kina na familia yake, akaamua kutangaza kuwa mwanawe huyo kipenzi atazikwa jijini Dar es Salaam ili kutoa nafasi kwa rafiki zake wengi aliokuwa akishirikiana nao katika kazi zake za kila siku za kisanii kupata nafasi ya kushiriki mazishi yake.

Mzee Kilowoko ametoa msimamo huo mpya leo hoo hii, ikiwa ni muda mfupi tu baada ya kutangaza awali kuwa mwanawe atakwenda kuzikwa Songea.

Sajuki amefariki leo asubuhi katika Hospitali ya Taifa Muhimbili alikokuwa amelazwa katika wodi ya wagonjwa mahututi na kupumua kwa msaada wa mashine kabla ya kuaga dunia mishale ya saa 1:00 asubuhi.



Mashabiki wa filamu za Kibongo nchini watamkumbuka marehemu kwa filamu zake kama 'Round', 'Shetani wa Pesa', 'Hero of the Church', 'Vita' na 'Briefcase, 'Revenge', 'Dhambi', 'Mboni Yangu', 'Two Brothers', na'Behind the Scene'.
Sajuki alizaliwa mwaka 1986 Songea mkoani Ruvuma, ameacha mke na mtoto mmoja.