STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Saturday, April 7, 2012

SIMBA YATAKATA AFRIKA, LICHA YA KIPIGO YAFUZU 16 BORA KOMBE LA SHIRIKISHO




ANGURUMAPO SIMBA MCHEZA NANI? HAKUNAGA! Ndivyo tunavyoweza kusema baada ya klabu ya soka ya Simba kupenya kwenye hatua ya 16 Bora ya KOmbe la Shirikisho Afrika, licha ya kipigo cha mabao 3-1 ilichopewa usiku wa kuamkia leo na Entente Sportive de Setif ya Algeria.
Ikicheza wachezaji 10, Simba iliweza kupigana hadi dakika za nyongeza kupata bao pekee la kufutia machozi lililokuwa na faida kubwa kwao, kuwavusha hatua hiyo wakiwaduwaza waarabu wasiamini kilichowakuta baada ya kuamini wamemng'oa mnyama.
Shujaa wa Simba katika pambano hilo lililochezeshwa na waamuzi kutoka Tunisia alikuwa ni Mganda, Emmanuel Okwi aliyefunga katrika dakika ya 92 na kuifanya timu yake isonge mbele kwa faida ya bao la ugenini kutokana na matokeo ya jumla kuwa mabao 3-3.
Simba katika pambano lao la awali lililochezwa kwenye uwanja wa Taifa, Machi 25, ilishinda mabao 2-0 na hivyo kwa sare hiyo wamevuka kwa matokeo ya kuwa mabao 4-3.
Beki wa kutumainiwa wa Simba Juma Said Nyosso alitolewa uwanjani mapema baada ya kulimwa kadi nyekundu kwa kuonyesha ubabe uwanjani dhidi ya mshambuliaji wa Setif.
Wenyeji walitumia mwanya wa kutolewa kwa Nyosso kupachika bao la kuongoza lililofungwa dakika ya 34 na Mohammed Aoudia na kurejea kipindi cha pili kwa kasi kwa kufunga bao jingine kupitia mshambuliaji huyo mkali.
Bao la tatu la Setif, iliyokuwa ikiyotawala vipindi vyote viwili, ingawa juhudi zao za kuvuna mabao mengi zilizimwa na kipa Juma Kaseka, lilifungwa katika dakika ya 52 kupitia kwa Mokhtar Benmoussa.
Baada ya kupata mabao hayo Setif ilirejea nyuma na kulinda bao wakiamini wameshamaliza kazi kabla ya Okwi kuwaduwaza baada ya kuwachambua mabeki wa timu hiyo kisha kufumua shuti kali la mbali lililomshinda nguvu kipa wa Setif na kutinga wavuni.
Kwa ushindi huo, Simba sasa itakutana na mshindi kati ya FerroviƔrio Maputo ya Msumbiji au Al Ahly Shendi ya Sudan ambazo zinatarajiwa kuumana kesho Jumapili, huku timu ya Sudan ikiwa na faida ya bao moja iliyopata katika mechi yao wiki mbili zilizopita ilipowafunga wenyeji wao bao 1-0.
Katika mchezo wa jana kikosi cha Simba kilichoaanza dhidi ya ES Setif kiliwakilishwa na Juma Kaseja, Shomari Kapombe, Amir Maftah/Said Nassoro 'Chollo' , Juma Nyoso, Kelvin Yondani, Patrick Mafisango, Salum Machaku, Mwinyi Kazimoto, Felix Sunzu, Haruna Moshi 'Boban' na Emmanuel Okwi.

No comments:

Post a Comment