STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Monday, May 21, 2012

Mil. 150 kudhamini tuzo za TASWA

KAMPUNI ya Bia ya Serengeti (SBL) jana imetangaza kudhamini tuzo za Mwanamichezo Bora wa Tanzania wa mwaka 2011 kwa Sh. milioni 150. Tuzo hizo zinaandaliwa na Chama cha Waandishi wa Habari za Michezo Tanzania (TASWA) na mwaka huu zitatolewa Juni 14 kwenye ukumbi wa Diamond Jubilee (VIP). Akizungumza jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi wa Mawasiliano na Uhusiano wa SBL, Teddy Mapunda, alisema kuwa lengo la kudhamini tuzo hizo ni kutaka kuona michezo na wanamichezo hapa nchini inakua na kujitangaza ndani na nje ya nchi. Alisema kampuni yake inaona fahari kuendelea kudhamini tuzo za TASWA ikiwa ni mwaka wa tatu mfululizo, hivyo mwaka huu wameongeza udhamini zaidi ili kuziboresha. Alisema tuzo hizo zitafanyika Juni 14 mwaka huu ukumbi wa Diamond Jubilee (VIP) Dar es Salaam na kwamba wana matumaini makubwa zitakuwa bora kuliko zilizopita. Mwenyekiti wa TASWA, Juma Pinto aliwashukuru Serengeti na kusema udhamini huo ni ishara ya namna kampuni hiyo inavyothamini wanamichezo nchini na kwamba umeongezeka kwa kiasi kikubwa kutoka Sh. milioni 80 ambazo walitoa mwaka jana. Pinto alisema kuwa milango bado iko wazi kwa kampuni nyingine kwa sababu bajeti nzima ya shughuli hiyo iliyopangwa ni Sh. milioni 370. Alisema kuwa mchakato wa kupata washindi wa tuzo hizo unasimamiwa na kamati maalumu iliyoteuliwa na TASWA na wanaamini inafanya kazi zake kwa uadilifu. Kwa miaka mitano iliyopita walioshinda Tuzo ya Mwanamichezo Bora wa TASWA walikuwa ni Samson Ramadhani (2006), Martin Sulle (2007), Mary Naali (2008), ambao wote ni wanariadha, wakati 2009 na 2010 alikuwa ni mcheza netiboli Mwanaidi Hassan. Mshindi wa mwaka jana, Mwanaid, ambaye alizawadiwa gari aina ya Toyota Cresta (GX 100), ndiye mfungaji aliyeisaidia timu ya taifa ya netiboli, Taifa Queens, kumaliza ikiwa ya pili kwenye mashindano ya mchezo huo ya Afrika yaliyofanyika nchini hivi karibuni.
Katibu Mkuu wa TASWA, Amir Mhando 'Mgosi'

No comments:

Post a Comment