STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Monday, April 25, 2011

Rapa wa Levent atua TOT-Plus

BENDI ya TOT-Plus ambayo sasa inaendelea na kambi yake ya mazoezi, Mwananyamala, jijini Dar es Salaam, imempata rapa mpya Dokta Steve 'Sauti ya Ng'ombe' kutoka bendi ya Levent Musica ya mjini Morogoro.
Kiongozi wa TOT-Plus, Badi Bakule, alisema rapa huyo alijiunga na tangu wiki iliyopita na anaendelea
na mazoezi kama kawaida akisubiri kutambulishwa rasmi.
"Tumemchukua rapa huyu ili kuziba nafasi ilioachwa na Jua Kali ambaye ameachana na TOT-Plus na kwenda kufanya kazi kwingine, Dokta Steve ameonyesha uwezo mkubwa hivyo anatufaa," alisema Bakule.
Bakule alisema bendi hiyo ambayo imekuwa na mazoezi kwa zaidi ya mwezi mmoja, inatarajia kutoka kambini Ijumaa Aprili 29 na kisha itajitambulisha rasmi Mei Mosi.
Alisema, rapa huyo kwa sasa amekuwa akijifua katika mazoezi makali kwenye kambi ya bendi hiyo iliopo eneo la Ujiji Mwananymala, jijini Dar es Salaam ili kuhakikisha kwamba anaibuka na vitu vipya.
"Pia tunataka azijue nyimbo zote mpya ambazo tayari tumezikalimisha na hata zile za zamani ambazo wanamuziki karibu wote wamezifanyia mazoezi kabla rapa huyu mpya hajajiunga na bendi yetu," alisema.
Kiongozi huyo alizitaja nyimbo hizo mpya kuwa ni 'Kilio cha Linda', 'Zai' 'Maisha Duni', Liwalo na Liwe','Dakika Tisa' na 'Riziki na Zengwe' ambazo baadhi yake tayari zimesharekodiwa.
Aliongeza kuwa 'Sauti ya Ng'ombe' atatoka kambini akiwa pia amemaliza kuzifanyia mazoezi baadhi ya nyimbo za zamani zilizochangia kuiweka TOT-Plus kwenye matawi ya juu.
"Kuna nyimbo kama Masimango, Mtaji wa Masikini, Elimu ya Mjinga, Mtoto Yatima, Mnyonge Mnyongeni na nyingine nyingi ambazo anatakiwa azifahamu vizuri kabla hatujatoka kambini," alisema.
Tangu imalize kampeni za Uchaguzi Mkuu mwishoni mwa mwaka jana, bendi hiyo bado haijafanya maonyesho na badala yake imeingia kambini ili kujipanga vizuri kwa ajili ya kuibuka kwa kishindo.

No comments:

Post a Comment