STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Sunday, June 26, 2011

Dede alia na uvivu wa mawazo katika dansi



MWANAMUZIKI mkongwe nchini, Shaaban Dede 'Mzee wa Loliondo' amewaasa wanamuziki wenzake wa dansi kutobweteka na mafanikio machache waliyonayo katika sanaa zao na badala yake waumize vichwa kubuni mambo mapya kama wanavyofanya wale wa muziki wa taarab.
Dede, alisema anawafagilia wanamuziki wa taarab kwa kubuni kitu kilichouinua muziki huo nchini toka taarab asilia hadi kuwa ya kisasa ikichezeka na kupendwa na mashabiki wengi.
Alisema kuwekwa kwa rhumba na rapu katika muziki wa taarab kumeupandisha chati na kuonyesha jinsi gani wanamuziki wa dansi walivyo na changamoto ya kuumiza vichwa kuhimili ushindani wanaoupata toka kwa miondoko hiyo ya mwambao na muziki wa kizazi kipya.
"Lazima wanamuziki waumize vichwa, wasibweteke kwa kuona muziki wetu unakubalika na watu wengi, hilo linaweza kutufanya tubaki tulipo wakati wenzetu wakisonga mbele kama ambavyo taarab walivyofanya," alisema Dede.
Dede anayeifanyia kazi Msondo Ngoma, alisema kwa kuwa wanamuziki wanaojiandaa kuwarithi wakongwe katika muziki wa dansi wanapaswa kuacha kulemaa na kasumba ya kuiga kazi za nje na badala yake wakajikita katika kutafuta vyao kama ambavyo miaka ya nyuma bendi zilivyotofautiana kimipigo na kuzoa mashabiki lukuki.
Alisema tabia ya bendi kuwa na ladha yake ya kimuziki na kujitofautisha na wengine ndio iliyozifanya Sikinde na Msondo hadi leo kuwa na mashabiki wao binafsi, kitu ambacho bendi zingine za kisasa zinapaswa kufuata mkumbo huo.

No comments:

Post a Comment