STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Sunday, June 26, 2011

MCHANYATO WA MICHARAZO

Tisa wamwagwa Mtibwa Sugar

KLABU ya soka ya Mtibwa Sugar, imetangaza kuwatema wachezaji wake 9 akiwemo mkongwe Faustine Lukoo na kipa Soud Slim waliomaliza mkataba wa kuichezea klabu hiyo.
Kwa mujibu wa Msemaji wa klabu hiyo, Thobias Kifaru, baadhi ya wachezaji wengine waliopewa mkono wa kwaheri katika mashamba ya Manungu, Morogoro ni winga Julius Mrope aliyeenda Yanga na Obadia Mungusa aliyesajiliwa na Simba.
Kifaru, aliwataja wachezaji wengine ni Yusuph Mgwao, Yona Ndabila anayeenda kucheza soka la kulipwa nje ya nchi, Mganda Boban Zilintusa waliyeshindwa kumtumia kwa kukosa ITC, ambaye walimsajili na kushindwa kumtumia kwa kukosa ITC, na Lameck Dayton.
"Tumeacha jumla ya wachezaji tisa, akiwemo mkongwe Faustine Lukoo baada ya kumaliza mikataba ya kuitumikia klabu yetu na wengine kuhamia klabu zingine za Ligi Kuu, ila Ndabila aliyekuwa na mkataba aliomba kusitisha kwa vile anataka kwenda kucheza soka nje," alisema.
Hata hivyo Kifaru hakuweka bayana juu ya wachezaji Salum Machaku na kipa Shaaban Kado ambao wametajwa kutua kwa watani wa jadi wa soka la Tanzania, Simba na Yanga kwa msimu ujao wa ligi kuu.
Machaku anayeichezea pia timu ya taifa, Taifa Stars imedaiwa amesajiliwa Simba na Kado anayechezea timu za vijana U20 na ile ya wakubwa tayari imethibitishwa amenyakuliwa na Yanga kwa ajili ya msimu ujao utakaoanza Agosti 20 mwaka huu.
***

Fainali Pool Taifa zaiva


FAINALI za taifa za mchezo wa pool za 'Safari Lager National Pool Champioship 2011' zinatarajia kuanza mwezi ujao.
Kwa mujibu wa Meneja wa bia ya Safari Lager, Oscar Shelukindo, fainali hizo zitafanyika kati ya Julai 27-30 kwenye ukumbi wa Kilimani mkoani Dodoma.
Shelukindo alisema, fainali hizo zitatanguliwa na mashindano ya ngazi za mikoa yatakayoanza Juni 30 hadi Julai 17, ikishirikisha mikoa 14 ya Tanzania Bara.
Alisema mara baada ya mashindano hayo kukamilika katika ngazi za mikoa kila mkoa utaunda kombaini ya wachezaji kwa ajili ya kuwakilisha kila mkoa katika ngazi ya fainali hizo za taifa.
Shelukindo alisema bingwa wa fainali hizo atanyakulia Sh.mil. 5, mshindi wa pili ataondoka na mil. 3, mshindi wa tatu Mil. 2 na mshindi wa nne Mil 1.
Aliongeza fainali hizo ambazo zitahusisha na wachezaji mmoja mmoja wanaume na wanawake, bingwa kwa upande wa wanaume atazawadiwa Sh.Sh.500,000, mshindi wa pili Sh.250,000, mshindi wa tatu Sh.200,000 na mshindi wa nne Sh.100,000
Kwa upande wa wanawake bingwa atapewa Sh.350,000, mshindi wa pili Sh.200,000, mshindi wa tatu Sh.150,000 na mshindi wa nne Sh.50,000.
Aliongeza kwa kuzitaja zawadi kwa upande wa ngazi ya mikoa kuwa bingwa atajinyakulia Sh. 700,000, mshindi wa pili ataondoka na Sh.350,000, mshindi wa tatu atazawadiwa Sh.200,000 na mshindi wa nne Sh150,000.
Kwa upande wa mchezaji mmoja mmoja ngazi ya mikoa (wanaume) bingwa atajinyakulia Sh.350,000, mshindi wa pili Sh.200,000, mshindi wa tatu Sh.150,000 na mshindi wa nne Sh.100,000,
Kwa upande wa wanawake bingwa atapewa Sh.250,000, mshindi wa pili Sh.150,000, mshindi wa tatu Sh.100,000 na mshindi wa nne Sh.50,000.
Mikoa itakayoshiriki ni mabingwa watetezi Kinondoni, Ilala na Temeke, Shinyanga, Mwanza, Kagera Mbeya, Tanga, Arusha, Kilimanjaro, Dodoma, Iringa, Manyara na Morogoro.
***

Toto Afrika yazionya Kagera, Mtibwa Sugar


KLABU ya soka ya Toto Afrika ya Mwanza imezitaka klabu zinazotaka kuwasajili nyota wao kutotumia mlango wa nyuma na badala yake zionane nao na kufanya mazungumzo.
Uongozi wa Toto, umesema umelazimika kutoa tahadhari hiyo kutokana na kuwepo kwa taarifa zinazoripotiwa na vyombo vya habari juu ya timu za Kagera Sugar na Mtibwa Sugar kuwanyakua wachezaji wao wawili nyota bila ya wenyewe kujua lolote.
Wachezaji walioufanya uongozi huo kucharuka mapema ni mshambuliaji, Husseni Sued anayedaiwa kutua Kagera Sugar na kiungo Mohammed Soud aliyevumishwa kunyakuliwa na klabu ya Mtibwa ya Morogoro.
Katibu wa klabu hiyo, Salum Kaguna, alinukuliwa hivi karibuni akisema kuwa, hawana taarifa zozote za wachezaji hao kunyakuliwa na timu hizo kwa vile hakuna mazungumzo yoyote yaliyofanywa hadi ssa baina yao na klabu hizo.
Kaguna, alisema ni vema klabu zinazowataka wachezaji ziende mezani kuzungumza kwa sababu nyota hao wana mikataba na hivyo hawatakuwa radhi waondoke kienyeji.
"Hatuzuii wachezaji wetu kuondoka kama wamepata timu, muhimu ni taratibu zifuatwe, mfano Soud anayetajwa kutua Mtibwa, yeye ana mkataba wa miaka mitatu ya Toto akiwa ametumikia miaka miwili na kubakisha mmoja utakaoisha mwakani," alisema Kaguna.
Viongozi wa Mtibwa na Kagera hawakupatikana kuweka bayana kinachoendelea juu ya harakari zao za kuwanyakua wachezaji hao na onyo hilo la uongozi wa Toto Afrika ambayo imekuwa ikijinadi imepania kufanya kweli msimu ujao katika Ligi Kuu Tanzania Bara.
***

TAVA yapongezwa, yashauriwa


CHAMA cha Mpira wa Wavu nchini, TAVA, umepewa 'kifyagio' kwa kujitahidi kurejesha hadhi ya mchezo huo, lakini kikashauriwa kuwekeza nguvu zao ngazi za chini hususani katika mashule ili kuzalisha nyota wa baadaye watakaoisaidia Tanzania kimataifa.
Kifyagio na ushauri huo umetolewa na mchezaji nyota wa zamani wa klabu ya Jeshi Stars, Ibrahim Christopher 'Michael Power' alipozungumza na MICHARAZO na kusema uongozi wa TAVA umekuwa ukijitahidi katika hali ya mazingira magumu kuinua tena mchezo huo nchini.
Christopher, alisema kukosekana kwa wadhamini ni tatizo lililochangia kuufanya mchezo wa wavu kudodora, lakini jitihada za viongozi wa chama chao umesaidia kuendesha michuano ya kitaifa na kimataifa jambo la kupongezwa.
Alisema hata hivyo bado TAVA inapaswa kuelekeza nguvu zao katika ngazi za chini kusaka nyota wa baadae ikiwezekana kuendesha michuano katika shule za msingi na sekondari ili kuwapa morali vijana kujitosa kwenye mchezo huo.
"Kwa kweli TAVA inafanya kazi katika mazingira magumu kwa kutokuwa na wafadhili wala wadhamini, lakini bado naiomba waelekeza nguvu zao kwa vijana toka ngazi za chini ili waje kuchukua nafasi zetu kuendelea mchezo huu," alisema.
Nyota huyo aliyeisadia Mzinga ya Morogoro kutwaa taji la Ligi ya Muungano lililofanyika mjinio Tanga, alisema kadhalika wachezaji na viongozi wa zamani wa mchezo huo wanapaswa kujitokeza kuusaidia uongozi wa sasa katika kuhakikisha wavu inarejesha makali yake.
"Viongozi na wachezaji wa zamani wamejiweka kando, wanapaswa kutoka mafichoni kusaidiana na TAVA kurejesha makali ya mchezo huo," alisema.
***


'Wazee wa Kizigo' wapata meneja


BENDI ya Extra Bongo 'Wazee wa Kizigo', imepata meneja ambaye atabeba jukumu la kusimamia shughuli zote za bendi hiyo ili isonge mbele kufikia malengo ya kuwa matawi ya juu.
Kiongozi wa bendi hiyo Rogert Hegga, alimtaja meneja huyo mpya kuwa ni Mujibu Hamis aliyewahi kuifanya kazi katika bendi za FM Acdeamia na Mashujaa Musica.
Hegga alisema, kwa vile Mujibu ni mzoefu wa kazi hiyo kwa muda mrefu, ana uhakika mchango wake utakuwa mkubwa ndani ya Extra Bongo ambayo inazidi kupanda chati kila kukicha.
"Fitina za muziki anazijua sana na sisi tunaamini kwamba tukiwa naye kwenye bendi yetu ya Extra Bongo tutaendelea kupiga hatua zaidi ili kufikia malengo ambayo tumejiwekea," alisema Hegga.
Alisema, Extra Bongo haikuwa na meneja hali ambayo ilikuwa inachangia baadhi ya shughuli za bendi kukwama na kwamba sasa amempata Mujibu ambaye atatumia uzoefu wake kusimamisha maendeleo ya Extra Bongo.
Katika hatua nyingine kiongozi huyo alisema, Extra Bongo imeanzisha ushirikiano wa maonyesho ya pamoja na vikundi mbalimbali vya burudani ili kujenga urafiki kati ya wanamuziki wake na wasanii wa vikundi hivyo.
Alisema ushirikiano huo ulianza wiki iliyopita kwa kufanya onyesho la pamoja na vikundi vya Baikoko, Kiti Tigo, Werawera na Khanga Moja ambavyo vina umaarufu miongoni mwa mashabiki wa burudani.

No comments:

Post a Comment