STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Sunday, June 26, 2011

Rufita yamnasa Kibugila



BENDI ya muziki wa dansi ya Rufita Connection 'Wana Shika Hapa Acha Hapa', imepata mcharaza solo mpya ikiwa ni wiki chache baada ya Seleman Shaibu Mumba kukimbilia Twanga Pepeta.
Kwa mujibu wa rais wa bendi hiyo, Chai Jaba, mpiga solo huyo ni Abdalah Kibugila ambaye amewahi kuwa bendi mbalimbali ambapo kwa mara ya mwisho alikuwa Bwagamoyo International ya Mwinjuma Muumin.
"Seleman alikuwa mpiga solo wetu lakini ameshahama, lakini tayari tumeshapata aliyeziba nafasi yake, kazi inaendelea kama kawaida kutokana na ukweli kwamba Kibugila ni mwanamuziki siku nyingi ana uzoefu wa kutosha," alisema.
Alisema Kibugila anashiriki maonyesho ya bendi hiyo huku akizifanyia mazoezi nyimbo za bendi hiyo zikiwemo za 'Mapenzi Yanaua', 'Nilinde Nikulinde', 'Anasa', 'Shida ya Mapenzi', 'Usia', 'Acha Pupa','Mkosi Gani' na 'Mazi'.
Akielezea zaidi mipango ya bendi hiyo, Chai Jaba inajiandaa kumalizia kazi ya kurekodi nyimbo zote na kisha kuanza kushuti video na kisha zitafuatia taratibu za kuzindua albamu.
"Nina uhakika yatakwenda vizuri na inawezekana tukakamilisha kazi ya kurekodi nyimbo zetu mwezi ujao kabla ya kuendelea na kazi ya kushuti video ili tujitambulishe zaidi kwa mashabiki wa muziki wa dansi," alisema.
Aidha, alisema bendi hiyo inajiandaa kuleta wanenguaji wapya wanne kutoka Congo (DR) watakaokuja kuungana na wenzao waliopo kwa sasa ili kuongeza nguvu kwenye safu ya ushambuliaji wa jukwaa.

No comments:

Post a Comment