STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Sunday, June 26, 2011

Gilla alia na Phiri kumzibia riziki Simba



MSHAMBULIAJI chipukizi wa Simba Salim Aziz Gilla aliyetangazwa kutafutiwa timu ya kucheza kwa mkopo msimu ujao amemlaumu aliyekuwa kocha mkuu wa klabu hiyo Patrick Phiri kuwa alichangia kufifisha nyota yake kisoka.
Gilla aliyenyakuliwa na Simba kwa mkataba wa miaka mitatu mwaka 2009 baada ya kung'ara kwenye michuano ya Kombe la Taifa, alisema kutoaminiwa na Phiri kulikopelekea kushindwa kuitumikia vema Simba ndiko kulikomfanya asifurukute.
Akizungumza na MICHARAZO, Gilla alisema hata kushindwa kuitwa kwake kwenye timu za taifa, zikiwemo za vijana, inatokana na kukalishwa benchi na Phiri.
Phiri aliondoka Simba mara baada ya kumalizika kwa ligi kuu ya Bara msimu uliopita.
"Kushindwa kuaminiwa na Phiri na kunipa nafasi ya kuonyesha uwezo wangu katika kufumania nyavu umenisababishia haya yote yanayonikuta ndani ya Simba na kukosa kuitwa hata katika timu za vijana ambazo huenda ningezisaidia," alisema Gilla.
Gilla, anayekaribia umri wa miaka 21, alisema misimu miwili aliyokuwa Simba hakuwahi kupata nafasi ya kucheza dakika 90 za mchezo wowote, kitu alichodai sio kimemvuruga akili, bali kimemnyima fursa ya kuonekana kama alivyong'ara kenye Kombe la Taifa akiwa na timu ya mkoa wa Tanga.
Katika michuano hiyo, Gilla aliibuka Mchezaji Bora, huku akiteuliwa mara mbili kuwa 'nyota' wa mchezo ukiwemo ule wa kusaka mshindi wa tatu ambapo Tanga waliilaza Mwanza mabao 2-0.
Alisema hajakata tamaa kutamba kisoka, hatahivyo.
Alisema anaamini alichokutana nacho Simba ni mtihani hivyo anajipanga ili kuendeleza kipaji chake kilichomfanya aichezee Polisi Dodoma chini ya Sekilojo Chambua kabla ya kutua Simba.

No comments:

Post a Comment