STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, September 30, 2011

Kaseba, Oswald kumaliza ubishi kesho Dar


MABONDIA Japhet Kaseba na Maneno Oswald 'Mtambo wa Gongo', leo wamepima uzito tayari kumaliza ubishi katika pambano lao linalofanyika kesho jijini Dar es Salaam.
Kaseba na Oswald watapigana kwenye pambano lisilo la ubingwa la raundi 10 la uzani wa Middle, litakalofanyika kwenye ukumbi wa Travertine Hoteli, Magomeni.
Pambano hilo lililoandaliwa na mratibu Gervas Muganda chini ya usimamizi wa Shirikisho la Ngumi za Kulipwa Tanzania, PST, litasindikizwa na mapambano kadhaa ya utangulizi yakiwemo yale ya mchezo wa kick boxing.
Mabondia hao kwa nyakati tofauti wametambiana kila mmoja akitamba ni lazima aibuke mshindi katika pambano hilo kutokana na anavyomchukulia mpinzani wake, sambamba na maandalizi wanayofanya.
Oswald, alisema kwa uzoefu alionao ni wazi atammaliza Kaseba raundi za awali, huku Kaseba, licha ya kukiri mpinzani wake ni 'ngangari', ila anaamini atampiga.
"Ni kweli Oswald ni mzuri na mzoefu wa ngumi, ndio maana amesaini mapambano mawili dhidi yangu na la Rashidi Matumla, lakini kwa nilivyojiandaa nitamshinda tu," alisema Kaseba.
Oswald nae alisema anachotaka ni mashabiki wa ngumi kufurika ukumbini kuona namna Kaseba anavyorejeshwa kwenye kick boxing, kwa jinsi atakavyompiga.
Alisema anajiamini uwezo alionao katika ngumi ni vigumu kuzuiwa na Kaseba, akisisitiza kuwa atawathibitishia wadau wa ngumi kwa nini aliitwa 'Mtambo wa Gongo' na watu wa Malawi.
Michezo ya utangulizi itakayolisindikiza pambano la Kaseba na Oswald ni la bingwa wa zamani wa ngumi za kulipwa nchini, Ernest Bujiku dhidi ya Mbukile Chuwa, Sweet Kalulu atakayepigana na Chaurembo Palasa na Venance Mponji kuzipiga na Jafar Majiha.

No comments:

Post a Comment