STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, September 30, 2011

Skyner: Kisura anayetishia mastaa wa kike Bongo Movie





NI muda mfupi tangu Skyner Ally Seif, ajiingize kwenye fani ya uigizaji, ila tayari amekuwa na jina kubwa kutokana na umahiri aliouonyesha kupitia kazi alizoshiriki.
Mbali nba umahiri wa kisanii, pia mvuto wa sura na umbile vimemfanya msanii huyo, awe miongoni mwa wasanii wa kike wanaotamba nchini kwa sasa.
Sykner alikiri, licha ya kuwa na kipaji cha sanaa tangu utotoni, hakupata fursa ya kukionyesha hadi mwaka jana alipoibuliwa na Vincent Kigosi 'Ray' kupitia filamu ya 'The Second Wife'.
Alisema kabla ya 'shavu' la Ray, alishacheza kazi nyingine kama 'Mtumwa wa Mapenzi' na 'Johnson' ambazo hazikumtangaza sana.
Kazi nyingine alizoshiriki mara alipoibuliwa na Ray, ni 'What is It', 'Why I Did Love', 'I Hate My Birthday', 'Kizungumkuti', 'Unpredictable' na nyingine.
Skyner anayejiandaa kuolewa Ijumaa ijayo, alizaliwa mwaka 1992 jijini Dar, akiwa mtoto wa pili wa familia ya watoto watatu, alihitimu masomo ya sekondari Shule ya Cambridge, ya jijini Dar.
Nyota huyo, anayependa biriani na kunywa fanta, alisema licha ya kuwepo kwenye sanaa kwa muda mfupi, fani hiyo imemnufaisha mengi, akiota kuja kutamba kimataifa na mtayarishaji na muongozaji bora, akimiliki kampuni yake binafsi.
Kisura huyo, hutumia muda wake wa ziada kumuomba Mungu na kulala, pia ni shabiki wa
muziki akihusudu miondoko ya Arabian.
Juu ya madai ya rushwa na ngono katika sanaa, Skyner alikiri ni kweli amewahi kusikia, ila yeye hajawahi kukumbana nayo.
Ila, alisema wasanii wanaoombwa rushwa hiyo wana uhuru wa kukataa kwa kuringia vipaji vyao badala ya kujirahisisha na kudhalilika.
Skyner aliyewafiwa na wazazi wote mwaka 2006 wakipishana miezi mitano, akitangulia mama yake aliyefariki mwezi Aprili, kisha Septemba kufuata baba'ake, alisema licha ya kuwepo kwenye sanaa kusaka fedha, hayupo tayari kuchojoa nguo, ili acheze filamu za X.
Kimwana huyo, anayewazimia Irene Uwoya na Ray, alidai hawezi kucheza X hata akiahidiwa kiasi gani cha donge la fedha, kwa vile anajiheshimu na kujithamini kama mwanamke.
Aliwaasa wenzake, kujiheshimu na kuepukana na matendo machafu, aliyodai huwavunjia hadhi mbele ya jamii, na kusababisha sanaa yao kuonekana kama kazi ya wahuni wakati sio kweli.
Alisema, umaarufu wa msanii hupatikana kupitia ubora wa kazi zake na sio skendo chafu.
Skyner aliiomba serikali iwasaidie wasanii nchini kuweza kupambana na maharamia wanaowaibia kazi zao na kuwafanya wasanii wafe maskini tofauti na wenzao wa mataifa mengine.
Kadhalika, aliiasa jamii kuwa bega kwa bega na wasanii kwa kununua kazi zao halisi mara zitokapo, badala ya kukubali kuuziwa kazi feki, kitu kinachochangia wasanii kunyonywa na kuwafanya washindwe kusimama kimaisha na kiuchumi.

Mwisho

No comments:

Post a Comment