STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, September 30, 2011

Azam yagomea nyota wake kwenda likizo, kisa...!

WAKATI nyota wa Simba na Yanga wakipewa likizo fupi ya kupisha mchezo wa timu ya taifa, Taifa Stars dhidi ya Morocco utakaochezwa ugenini mwezi ujao, uongozi wa Azam umewagomea mastaa wake, ukisisitiza kuwa timu yao itaendelea kujifua kama kawaida.
Simba kupitia Afisa Habari wake, Ezekiel Kamwaga, imetangaza kuwapa likizo ya wiki moja wachezaji wao, ili kupumzika kabla ya kurejea tena kujiandaa na pambano dhidi ya African Lyon litakalochezwa Oktoba 16, jijini Dar es Salaam.
Klabu hiyo imewapa likizo wachezaji hao baada ya kazi nzuri waliyofanya kwa kuiweka kileleni mwa msimamo timu yao ikiwa na pointi 18 kutokana na kucheza mechi nane bila kupoteza hata moja, ikishinda mechi tano na kutoka sare mechi tatu, .
"Wachezaji wetu tumewapa likizo ya muda mfupi, kabla ya kurejea tena kuanza maandalizi dhidi ya mechi yetu ijayo na zile zilizosalia katika ligi hiyo," alisema Kamwaga.
Hata hivyo timu inayoifukuzia Simba katika msimamo wa ligi hiyo, Azam imesema hawaendi mapumziko kama timu nyingine, bali wataendelea kujifua kujiandaa zaidi kwa mechi zao zijazo kabla ya kumaliza duru la kwanza mnamo Novemba 5.
Katibu wa Azam, Nassor Idrissa, alisema nyota wa timu yao wataendelea kufanya mazoezi kama kawaida, licha ya kwamba hawatakuwa na mchezo wowote hadi Oktoba 15 dhidi ya 'maafande' wa JKT Ruvu.
"Nyota wetu hawataenda likizo, wataendelea kujifua mazoezi kulingana na programu za kocha kwa nia ya kuwaweka sawa wachezaji kwa mechi zilizosalia za kumalizia duru la kwanza," alisema.
Idrissa maarufu kama 'Father' alisema yapo makosa ambayo yalikuwa yakifanyika katika kikosi chao, hivyo muda uliopo utatumiwa na benchi lao la ufundi kuweka mambo sawa kabla ya kurejea tena dimbani wakiwa moto kuliko hivi sasa.
Azam iliyopanda Ligi Kuu msimu wa 2008-2009, ndiyo inayoshikilia nafasi ya pili katika msimamo wa ligi ikiwa na pointi 15, tatu zaidi ya vinara Simba.

No comments:

Post a Comment