STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, September 30, 2011

Stewart ruksa kuinoa Zanzibar Heroes


UONGOZI wa klabu ya soka ya Azam, umekubali kwa moyo mmoja uteuzi wa kocha wao mkuu, Stewart Hall, kuinoa timu ya taifa ya Zanzibar, Zanzibar Heroes kwa ajili ya michuano ya Kombe la Chalanji itakayofanyika Novemba, jijini Dar es Salaam.
Chama cha Soka Visiwani Zanzibar, ZFA, kilimtangaza Stewart kuwa ndiye atakayeinoa timu hiyo katika michuano hiyo, ikiwa ni mara ya pili kwa kocha huyo kupewa kibarua hicho cha kuinoa Zanzibar Heroes.
Katibu Mkuu wa Azam, Nassor Idrissa 'Father', alisema uongozi wao, hauna tatizo la kocha wao kwenda kuinoa Zanzibar Heroes, kutokana na ukweli kwa namna moja ni faida kwa Azam ambayo hutoa wachezaji wengi katika kikosi cha timu hiyo.
Idrissa, alisema pia kocha huyo ataenda kuinoa timu hiyo wakati klabu yao itakuwa imeshawapa likizo wachezaji wao kwa ajili ya mapumziko marefu kabla ya kuanza kwa duru la pili la ligi hiyo mapema mwakani.
Katibu huyo alisema pia ni vigumu kwa Azam kumzuia kocha huyo kwenda kutekeleza jukumu lake kwa timu ya taifa, ambayo ni sehemu ya Muungano wa Tanzania, labda kama angeteuliwa kwenda kuinoa Kenya au Uganda ndio wangweka pingamizi.
"Angekuwa ameteuliwa kuinoa Kenya au Uganda, hapo ingekuwa vigumu kumruhusu lakini kama ni Zanzibar au hata kama ingekuwa Tanzania Bara, tungemruhusu kwa vile ni faida kwa maendeleo ya soka letu, kwani Stewart ni kocha mzuri," alisema.
ZFA, ilisema kocha huyo angeungana na timu hiyo ya taifa, Novemba 10, siku tano baada ya duru la kwanza la ligi kuu kumalizika.
Kabla ya kutua Azam, Stewart anayetokea Uingereza aliletwa nchini kuinoa timu hiyo ya Zanzibar kupitia kampuni ya Future Century.

No comments:

Post a Comment