STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, September 30, 2011

'Vijana wa Kova' wamsajili Mnigeria Ligi Daraja la Kwanza

MABINGWA wa Ligi ya TFF-Taifa, Central Stars (Polisi-Dar es Salaam), imetangaza kuwaongeza wachezaji sita wapya akiwemo Mnigeria kwa ajili ya Ligi Daraja la Kwanza Tanzania Bara inayotarajiwa kuanza Oktoba 15 katika vituo vitatu tofauti.
Uongozi wa timu hiyo umedai, umewaongeza wachezaji hao kwa lengo la kuipa nguvu timu yao inayoendelea kujifua kwenye uwanja wa Chuo cha Polisi, Kurasini kuhakikisha inakuwa miongoni mwa klabu zitakazopanda Ligi Kuu msimu ujao.
Katibu wa timu hiyo, Ngello Nyanjaba, aliiambia MICHARAZO kuwa, wachezaji hao wapya waliongezwa ni Mnigeria, Felix Ameche, Msiba Joto, Paul Skazwe, Juma Sedege na Awadh ambao tayari wameorodheshwa kwenye usajili wa timu yao.
Nyanjaba, ambaye pia ni kocha wa timu hiyo ya Polisi, alisema wachezaji hao wapya wataungana na nyota 22 wa kikosi hicho waliopandisha daraja timu hiyo kwa ajili ya ligi hiyo, akisema walitarajia kuwasilisha usajili wao wakati wowote kuanzia leo.
"Tunaendelea vema na maandalizi ya ligi daraja la kwanza, ambapo tangu turejee toka Tanga tunaendelea kujifua kwa mazoezi, lakini kubwa ni kuongeza wachezaji wapya sita akiwemo Mnigeria kwa lengo la kufanya vema kwenye michuano hiyo," alisema.
Michuano hiyo itakayochezwa kwa mtindo wa nyumbani na ugenini itashirikisha timu timu 18 zilizopangwa katika makundi matatu, ambapo Polisi-Dar, imepangwa kundi A na timu za Mgambo-Tanga, Morani-Manyara, TMK United na Transit Camp za Dar na Burkina Faso ya Morogoro.
Kundi B lina timu za Majimaji-Songea, Mbeya City Council, Mlale JKT-Ruvuma, Polisi- Iringa, Small Kids-Rukwa na Tanzania Prisons ya Mbeya.
Timu nyingine zitakazoshiriki ligi hiyo ni pamoja na 94 KJ ya Dar, AFC-Arusha, Polisi-Morogoro, Polisi-Tabora, Rhino Rangers-Tabora na Samaria-Singida, zilizopangwa katika kundi C.

Mwisho

No comments:

Post a Comment