STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, September 30, 2011

Yanga sasa roho kwatu!


USHINDI mnono wa mabao 5-0 iliyopata kwa Coastal Union, umewafanya wadau wa klabu ya Yanga kuchekelea wakisisitiza kuwa hawana hofu ya kutetea taji lao msimu huu.
Yanga iliyokuwa ikichechemea katika ligi hiyo, iliishindilia Coastal mabao hayo katika pambano lilkilochezwa uwanja wa Taifa, na kuipandisha mabingwa watetezi hao hadi kwenye nafasi ya nne nyuma ya timu za Simba, Azam na JKT Oljoro zilizoitangulia.
Afisa Habari wa Yanga, Louis Sendeu, alisema wanaamini ushindi waliopata kwa Wagosi wa Kaya ni salamu kwa watani zao na timu nyingine zilizokuwa zikiikejeli timu yao ilipoanza kwa kusuasua katika ligi hiyo.
Sendeu, alisema tangu awali walikuwa wakisisitiza kuwa, ligi bado mbichi na vigumu watu kuitabiria Yanga kwamba haiwezi kufurukuta msimu huu, bahati nzuri imethibitika kwa ushindi mfululizo ambao umewafanya wapinzani wao kuanza 'kuhema'.
Alisema anaamini mapumziko ya ligi kupisha pambano la Stars na Morocco itatumiwa vema na benchi lao la ufundi pamoja na wachezaji wao kuhakikisha wakirejea dimbani wanakuwa moto zaidi, ili kumaliza duru la kwanza katika nafasi stahiki.
"Nadhani waliokuwa wakitukejeli kwamba tumefulia, salama wamezipata na ninajua huko walipo presha zimeshaanza kuwapata, tunaombea tuendelee na mwendo huu huu ili tumalize duru la kwanza katika nafasi mbili za juu na kujiweka vema kulitetea taji letu," alisema.
Nao baadhi ya wadau wa klabu hiyo, wamedai pamoja na kuanza kuonyesha mwanga kwa timu yao, bado wachezaji hawapaswi kubweteka na badala yake waongeze juhudi ili kumaliza meechi tano zilizosalia kwa mafanikio.
"Tumefurahi mafanikio ya timu yetu, lakini naomba wachezaji na viuongozi wasibweteke, tuendelee kushinda mechi zijazo ikiwemo ile ya Simba Oktoba 29, ili turejeshe heshima yetu iliyopotea kwa matokeo mabaya ya mechi za awali," alisema Ramadhani Kampira.
Yanga kabla ya kuvaana na Simba katika pambano linalosubiriwa kwa hamu, itacheza na timu za Kagera Sugar, Toto Afrika na JKT Oljoro kabla ya kufunga dimba la duru la pili kwa kuumana na Polisi Dodoma mjini Dodoma Novemba 5.

No comments:

Post a Comment