STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, September 30, 2011

Timu za 'Maafande' zaitisha Azam Ligi Kuu T'Bara


TIMU ya soka ya Azam, imedai inakoseshwa usingizi ndani ya Ligi Kuu Tanzania Bara msimu huu na kasi ya timu za jeshi, kuliko na vigogo vya Simba na Yanga.
Aidha klabu hiyo imeisifia safu yao ya ulinzi ambayo hadi sasa imeruhusu mabao mawili, ikiwa ndio timu pekee iliyofungwa mabao machache katika ligi hiyo.
Uongozi wa klabu hiyo, umesema mwenendo wa timu hizo za majeshi zilizopo katika ligi hiyo, umeifanya ligi ya msimu huu, kiasi cha kuwanyima raha wakizifikiria.
Katibu Mkuu wa klabu hiyo, Nassor Idrissa 'Father', aliiambia MICHARAZO juzi kuwa, licha ya Simba na Yanga kuonekana tishio kwa klabu nyingine, wao Azam wanazihofu timu za JKT Oljoro, JKT Ruvu na Ruvu Shooting kwa jinsi zilivyo na upinzani mkali.
Idrissa, alisema timu hizo zimekuwa na upinzani mkali na kucheza soka la kusisimua na kutofungika kirahisi kitu kinachoifanya Azam zikiangalie kwa umakini timu hizo kuliko Simba na Yanga.
"Kwa kweli ligi ya msimu huu ni ngumu na yenye kusisimua na kati ya timu zinazotunyima raha ni timu za maafande ambazo zimekuwa na upinzania mkali na zenye kucheza soka la kusisimua," alisema Idrissa.
Alisema, timu hizo zimekuwa na matokeo bora zikiwa dimba la nyumbani au ugenini, na kudai uthibitisho wa ukali wao hata ukiziangalia kwenye msimamo zinafuata zikitofautiana kwa pointi chache na timu zilizopo juu.
Aidha Idrissa, aliipongeza safu ya ulinzi ya timu yake kwa kuruhusu kufungwa idadi ndogo ya mabao,ikiifanya iongoze kwa kuwa na ukuta mgumu hadi sasa nchini.
Azam katika mechi nane ilizokwishacheza hadi sasa imeruhusu mabao mawili, huku ikifuatiwa na Simba iliyoruhusu kufungwa mabao manne hadi hivi sasa.
"Kwa kweli tunaipongeza timu yetu na hasa safu ya ulinzi kwa kasi nzuri iliyofanya kwa kuruhusu mabao machache, naamini kwa mwenendo huu tunaweza kutimiza ndoto za kutwaa ubingwa au kuwa wawakilishi wa nchi kimataifa mwakani," alisema Idrissa.

No comments:

Post a Comment