STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Monday, April 14, 2014

Mzee Gurumo kuagwa na kuzikwa kesho

Mzee Gurumo enzi za uhai wake akiwa na mkewe kipenzi, Pili bint Said Kitwana

Waombolezaji wakiwa wamekusanyika nyumbani kwa marehemu Muhidin Gurumo maeneo ya Mabibo Makuburi, Dar es Salaam.
Mke wa marehemu Gurumo (kulia) akifarijiwa na baadhi ya jamaa zake kwenye msiba wa mumewe nyumbani kwake Makuburi.
MWILI wa gwiji wa muziki wa dansi nchini, marehemu Muhidin Gurumo 'Mjomba' unatarajiwa kuagwa rasmi kesho kuanzia saa 2 asubuhi kabla ya kusafirishwa kijijini kwao Masaki kwa ajili ya maziko yatakayofanyika mchana.
Awali ilipangwa marehemu Gurumo aliyefariki jana katika hospitali ya Muhimbili azikwe leo, ila kwa kuzingatia wosia ulioachwa na kusisitizwa na gwiji huyo enzi za uhai kuwa,  asiharakishwe kuzikwa mapema familia imeamua kutii wosia huo.
Akizungumza na MICHARAZO nyumbani kwa marehemu Gurumo, Mabibo External, Msemaji wa familia, Yahya Mikole alisema mara kadha Mzee Gurumo alikuwa akiwasisitiza kuwa atakapokufa asizikwe kwa haraka.
Mikole ambaye ni mdogo binamu wa marehemu alisema, Mzee Gurumo alikuwa akimwambia kwa kuwa yeye ni mwanamuziki mkubwa na maarufu kuharakishwa kuzikwa kwake kunaweza kuwanyima wengine kumuaga au kuhudhuria maziko yake.
"Kwa kuzingatia hilo na ombo toka serikali, tumeamua kusogeza shughuli za mazishi ya merehemu kutoka leo mpaka kesho kwa utaratibu wa kuagwa kuanzia saa 2-4 asubuhi kabla ya kuondoka kwenda kumpumzisha kijijini kwao majira ya saa 7 mchana," alisema Mikole.
Msemaji huyo alieleza marehemu alikuwa akisumbuliwa na tatizo la mapafu na uigonjwa wa moyo na juzi kabla ya kifo chake alipatwa na tatizo la ukosefu wa damu ambapo alipofikishwa Muhimbili aliwekewa chupa tatu za damu.
"Tatizo la ukosefu wa damu lilijitokeza juzi na aliwekewa chupa tatu zilizoisha asubuhi ya jana kabla ya alasiri kupoteza maisha, huku akionekana mwenye afya yake ya kawaida kabisa," alisema Mikole.
Mikole alisema taratibu za mazishi ya marehemu zinaendelea kama kawaida nyumbani kwa marehemu.
Kwenye msiba huo watu mbalimbali wakiwamo wanamuziki wa zamani na walio wahi kufanya kazi na marehemu walihudhuria kama akina Juma Ubao, Mjusi Shemboza, Karama Regesu na wengine.
Marehemu Gurumo aliyezaliwa mwaka 1940 ameacha mjane mmoja na watoto sita, watatu wa kiume ambao ni Abdallah, Omar na Mwalimu na wa kike pia wakiwa watatu ambao ni Mariam, ambaye ndiye mtoto mkubwa wa marehemu, Mwazani na Kibibi aliye wa mwisho kuzaliwa.
Hata hivyo wakati wa uhai wake alipozungumza na Mmiliki wa blogu hii alisema ana watoto wanne, lakini Msemaji huyo wa familia alifafanua mzee Gurumo 'alichepuka' ila hakupenda kuzungumzia suala la watoto wake hao wengine japo wanafamilia wanawatambua na wameshajulishwa msiba huo.

No comments:

Post a Comment