STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Monday, November 25, 2013

Wahitimu kidato cha nne waaswa kuepuka dawa za kulevya

Meza Kuu ikifuatilia maonyesho ya wahitimu wa kidato cha nne Mwandege Boys (hawapo pichani)
DC Mercy Sillah akihutubia
DC Mkuranga akiendelea kutoa nasaha zake kwa wahitimu na wazazi na walezi waliohudhuria mahafali ya tano ya Kidato cha nne Shule ya Mwandege Boys.

MKUU wa Wilaya ya Mkuranga, Mercy Sillah, amewaasa wahitimu ya Kidato cha Nne wa mwaka 2013 wasishawishike kujihusisha na biashara ya dawa za kulevya kwa lengo la kupata utajiri wa haraka.
Aidha Mkuu huyo wa wilaya, aliwataka wazazi na walezi kusaidia kuwalea watoto wao kwa maadili ya kidini ili kulisaidia taifa kuwa na vijana waadilifu ambao watalisaidia taifa.
Akizungumza kwenye Mahafali ya Tano ya Kidato cha Nne ya Shule ya Sekondari ya Mwandege Wavulana, DC Mercy, alisema kumekuwa na wimbi kubwa la vijana wengi kuingia tamaa ya kutajirika na kujihusisha na dawa za kulevya kitu alichodai ni hatari kwa taifa.
Alisema kutokana na hilo wahitimu wa shule hiyo na wengine nchini wanapaswa kuepuka vishawishi na tamaa za njia ya mkato ya maisha na badala yake wajikite katika kujiendeleza kielimu na kudumisha nidhamu walizokuwa nazo shuleni ili wafanikiwe maishani.
"Dawa za Kulevya zimekuwa ni kishawishi kibaya kwa sasa kwa vijana wetu, msijiingize huko mkaharibu maisha yenu, jiendelezeni na tumieni nidhamu mliyojengewa kujitengenezea maisha mazuri, mkikaa bure ni rahisi shetani kuwaingiza majaribuni," alisema.
DC Mercy aliwakumbusha kuwa pia kuzingatia sheria za nchi sambamba na kutambua kuwa kuhitimu kidato cha nne siyo kumaliza kila kitu, kwani wana fursa ya kujiendeleza kwa masomo ya juu ya sekondari au ufundi ili kujitengenezea mazingira mazuri ya kujiajiri.
Mkuu huyo wa wilaya aliwakumbusha wazazi na walezi kuvitambua na kuviendelezxa vipaji vya watoto wao, sambamba na kuwalea kwa malezi bora na mazuri yanayozingatia maadili na mafunzo ya kidini ili kuwajenga kimaadili na uchaji Mungu kwa vijana hao.
Naye Mkuu wa Shule ya Mwandege Wavulana, Mwl Enock Walter, kupitia risala aliyosoma aliomba serikali kuacha kufanya majaribio katika elimu kwa kila anayeingia madarakani kujaribu mambo yake na kuacha mengine aliyoyakuta kwani yanayumbisha elimu nchini.
"Kufanya majaribio katika elimu ni kuliua taifa, utashi na maamuzi ya wanaoingia madarakani kama ilivyotokea siku za nyuma kwa kufutwa kwa baadhi ya masomo na kisha kurejeshwa kunatuyumbisha watu wa chini hasa walimu kuzalisha wasomi wazuri wa kulisaidia taifa," alisema.
Katika mahafali hayo wahitimu 105 walitunukukiwa vyeti na kuzawadiwa kwa waliofanya vyema katika masomo yake shuleni hapo na mwanafunzi Marijani Karanda, aliibuka kidedea kwa kuongoza katika masomo sita kiasi cha kumfanya DC Mercy kumzawadia fedha taslimu.

No comments:

Post a Comment