STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Saturday, February 26, 2011

Simba, Mtibwa ni kisasi kitupu kesho





SIMBA na Mtibwa Sugar kesho zinakutana katika mechi yenye sura na mvuto wa pekee kwa aina yake ligi kuu bara, huku wekundu hao wa Msimbazi wakipania kuiporomosha kileleni mwa msimamo Azam FC na wapinzani wao wakipania kulipa kisasi cha kupoteza mechi ya kwanza.
Hata hivyo ushindi kwa Simba utawapeleka kileleni kwa muda tu, kwani watani wao wa jadi--Yanga wanaoshika nafasi ya pili wanaweza kuwashusha juu iwapo wataifunga Ruvu Shooting keshokutwa uwanja wa Uhuru.
Azam ina pointi 35 sawa na Yanga, lakini vijana wa Jangwani wako nyuma kwa tofauti ya mabao ya kufungwa na kufunga, na Simba inaweza kufikisha pointi 37 kama itashinda mchezo wa kesho.
Kwa upande wao Mtibwa wenye kumbukumbu nzuri ya kuwalaza Yanga, wamepania kuwazima vigogo Simba, na iwapo hilo litatimia watakuwa wamekaza mwendo wa kuelekea kileleni kwa kufikisha pointi 33.
Mtibwa imetangaza vita kwa Simba kutokana na kipigo cha bao 1-0 kwenye mechi ya kwanza iliyoghubikwa na mazingira ya tuhuma za rushwa kabla ya mechi kuchezwa.
Mtibwa itamkosa mlinda mlango wake namba moja, Shaaban Kato ambaye anatumikia adhabu ya kutocheza mechi kufuatia kuonyeshwa kadi nyekundu kwenye mechi dhidi ya Toto Afrika ya Mwanza.
Kocha msaidizi wa Mtibwa, Mecky Mexime na bosi wake Tom Olaba, kila mmoja kwa nyakati tofauti wamesema wamejiandaa kushinda mechi hiyo.
"Nia yetu si kulipa kisasi tu, tumepania kushinda mechi zote zilizosalia na kutwaa ubingwa," alisema Maxime.
Olaba alilalamikia kadi nyekundu ya Kado, lakini hata hivyo alisema kukosekana kwa mlinda mlango huyo si tatizo la kuwanyima ushindi.
"Kwetu sisi hakuna mechi rahisi, hivyo maandalizi tunayofanya ni kwa ajili ya mechi ngumu," alisema Mexime, nahodha wa zamani wa Mtibwa na Taifa Stars.
Simba wenyewe waliokutana jana kujadili mambo mbalimbali, wamesema wamepania ushindi kabla ya kwenda Zanzibar kuiwekea kambi Simba.
Katibu Mkuu wa Simba, Evodius Mtawala, alisema wamejiandaa vizuri kwa mechi hiyo.
"Tukimaliza mechi, Jumatatu asubuhi tunakwenda Zanzibar kwa ajili ya kuweka kambi kabla ya mechi inayofuata," alisema Mtawala.
Mtawala alisema Simba itaenda Zenji na kikosi chake chote isipokuwa Uhuru Seleman ambaye bado anauguza goti, huku Emmanuel Okwi, Joseph Owino na Hillary Echessa wakirejea toka kwenye majeruhi.
Simba na Yanga zinatarajiwa kukutana kwenye mechi ya marudiano itakayochezwa Machi 5 kwenye dimba la Taifa, Simba ikiwa na deni la kipigo cha bao 1-0 iliyopewa na Yanga kwenye mechi ya awali iliyochezwa jijini Mwanza kwa bao tamu la Jerry Tegete.
Mwisho

No comments:

Post a Comment