STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Saturday, February 26, 2011

Simba wazidi kuikamia Mazembe

BAADHI ya nyota wa klabu ya Simba, wametamba kuwa hawana hofu yoyote juu ya pambano lao dhidi ya TP Mazembe ya DR Congo kwenye michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika.
Wachezaji hao wa Simba wamesema licha ya kutambua ugumu watakaopata kwa wapinzani wao ambao ni mabingwa watetezi, bado wana imani ya kurejea rekodi ya mwaka 2003 walipoing'oa waliokuwa mabingwa watetezi wa michuano hiyo, Zamalek ya Misri.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti na gazeti hili katikati ya wiki iliyopita, wachezaji wa Simba walisema kama wawakilishi wa Tanzania wataendelea kupigana kiume kuona wanasonga mbele hata kama TP Mazembe wanatisha kwa sasa katika soka la kimataifa.
Beki wa kushoto wa Simba, Juma Jabu, alisema kama mabingwa wa Tanzania wataenda Congo kupigana kiume kuipeperusha bendera ya nchi kwa kushinda, ingawa wapo watu wanaoikatia tamaa.
Jabu, alisema hata mwaka 2003 Simba ilipuuzwa ilipopangwa na Zamalek, lakini walipigana kiume na kuing'oa mabingwa hao watetezi jambo linalowezekana kutokea msimu huu.
"Hakuna ubishi Mazembe ni wazuri na wanatisha Afrika na Dunia kwa ujumla, lakini kama wawakilishi hatutishwi nao, tutapigana kiume ili kusonga mbele, muhimu Watanzania watupe sapoti badala ya kutukatisha tamaa," alisema Jabu maarufu kama JJ.
Mchezaji mwingine aliyejinadi kutokuwa na hofu na Mazembe ni Rashid Gumbo, aliyekiri ni kweli Mazembe wanatisha, lakini bado wanaweza kufungika kama timu zingine muhimu mipango mizuri na kujituma kwao uwanjani.
"Tukijipanga na kucheza jihad uwanjani tunaweza kuweka maajabu, TP Mazembe ni timu kama timu zingine licha ya kuwa tishio, tutapigana kuhakikisha tunashinda," alisema Gumbo.
Kauli ya wachezaji hao zimekuja wakati wadau wengi wa soka wakiwemo wanaojiita wachambuzi wakiikatisha tamaa Simba kwa madai haiwezi kutoka kwa mabingwa hao watetezi katika mechi zao za raundi ya kwanza .
Simba ilipata fursa hiyo kwa kuing'oa Elan de Mitsodje ya Comoro kwa jumla ya mabao 4-2, ambapo katika mechi ya awali ilitoka suluhu ugenini kabla ya kushinda mechi ya marudiano iliyochezwa uwanja wa Uhuru Dar es Salaam.

Mwisho

No comments:

Post a Comment