STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Wednesday, June 6, 2012

Muziki wa Dansi walilia nafasi redioni, runingani

BAADHI ya wamiliki wa bendi za muziki wa dansi wameomba nyimbo za muziki huo zipewe nafasi ya kutosha katika vipindi vya televisheni na redio ili zisikike kama ilivyo sasa kwa taarab na bongofleva. Walitoa ombi hilo jana jijini Dar es Salaam katika mkutano wao na waandishi kutoka vyombo mbalimbali vya habari huku wakibainisha kuwa nyimbo za muziki huo kwa sasa hazina nafasi kubwa kama zamani. Mratibu kamati ya muda wa wamiliki wa bendi, Khaleed Chuma 'Chokoraa' alisema kuwa wamefikia kutoa ombi hilo baada ya kuona hali inavyokwenda sivyo ndivyo na hivyo kuwa na hofu muziki huo ukapotea kama hautapewa nafasi ya kutosha kwenye vyombo hivyo vya habari. "Tunachofanya sasa ni kujaribu kuwaunganisha wamiliki wote wa bendi za muziki wa dansi wa ndani na nje ya Dar es Salaam kwa lengo ya kufanya mkutano wa pamoja ili kuzungumzia hali hii," alisema Chokoraa. Alisema kuwa tayari baadhi ya wamiliki hao wameshakubaliana katika hilo na kwamba huenda mkutano huo ukafanyika wiki chache zijazo kama watakuwa wamewasiliana kikamilifu na wamiliki wote. "Lengo letu ni kuwaomba wahusika angalau kuangalia uwezekano wa kuufanya muziki wa dansi uwe na nafasi ya kutosha kwenye redio na televisheni ili kuwaibua wanamuziki wachanga nao wajulikane, p[ia muziki wa dansi uwe na vipindi maalum kama ilivyo kwa Bongofleva na Taarab ambao karibu kila redio na televisheni una vipindi," alisema. Naye Msemaji wa kamati hiyo ya muda, Ally Choki, alisema muziki wa dansi ni muziki wa zama na zama, na umekuwa ukisaidia vijana wengine kupata ajira, kwa wamiliki kama wao kuwaajiri, lakini kama hawapewi nafasi ya kutangazika ni vigumu wamiliki kuendelea kutoa ajira hizo. Choki, alisema kama walivyoweza kupewa nafasi na kutangazika wao wakati wakiibuka ndivyo vijana walioingia katika muziki huo nao wanapaswa kutangazwa kama ilivyo kwa wenzao wa miondoko mingine. "Siombi hili labda kwa kutaka nitangazwe, ila kuna vijana ambao wapo kwenye muziki huo hawapati nafasi na hivyo kuwatia unyonge na kusababisha dansi kufa tukiondoka kizazi chetu," alisema. Aliongeza kuwa, kama bendi wamekuwa wakilipa matangazo katika redio na televisheni kwa gharama, lakini fadhila ya matangazo hayo hawayaoni kwa muziki wao kutopewa nafssi katika vituo hivyo. Pia alidai kwamba muziki wa dansi ni mrefu kwa wimbo mmoja sio ukweli kwani wimbo mmoja wa dansi hauzidi dakika 8, lakini taarab wimbo mmoja huchukua hadi robo saa, lakini wanapewa nafasi, kadhaalika nyimbo za kikongo huwa na muda zaidi lakini nazo pia zinapigwa na vituo hivyo, jambo analohisi kinachofanyika ni kama hujuma kwa dansi. Aidha, alisema kwa uchunguzi wao wamebaini watangazaji wengi wa redio na televisheni wamekuwa na mzuka na miondoko mingine zaidi ya dansi kwa vile baadhi yao ni mameneja wa wasanii wa bongofleva na wengine hutumia vikundi vya taarab kuandaa maonyesho kama waratibu hivyo hutoa upendeleo kwa ajili ya masilahi yao binafsi. Choki alisisitiza kilio chaao sio kama kuvilaumu vituo hivyo, ila wanaombwa nao wapewe nafasi kama miondoko mingine kwa sababu muziki wa dani una historia kubwa ya nchi hii pi ni ajira za watu hivyo kama bendi zinazopiga muziki huo zitasahaulika, basi hata ajira za wanamuziki zitakuwa shakani pia. Mratibu huyo alikiri kwamba muziki wa dansi unachezwa na vituo hivyo vya runinga na redio lakini akadai kuwa si kama ilivyo kwa taarab na bongofleva ambao umekuwa ukipewa nafasi kubwa.

No comments:

Post a Comment