STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Tuesday, December 11, 2012

Azam hatimaye yaiangukia Simba kuhusu Ngassa wakubali kugawa mgao wa usajili kwa wana Msimbazi


KLABU ya soka ya Azam imeuangukia uongozi wa klabu ya Simba wakiwaomba walimalize suala la nyota wao Mrisho Ngassa kwa njia ya amani mradi winga huyo awahi kwenda kufanyia vipimo kwa lengo la kutua rasmi katika klabu ya El Merreikh ya Sudan.
Kwa mujibu wa taarifa zilizopatikana jana jioni na kuthibitishwa na Katibu Msaidizi wa Azam, Twalim Suleiman 'Chuma' ni kwamba Azam imeuandikia barua uongozi wa Simba ukisema wapo tayari kuwapa sehemu ya fedha za usajili za Ngassa, mradi waondoe pingamizi lao lililopo TFF kabla ya saa 5 asubuhi ya leo.
Barua hiyo iliyosainiwa na Makamu Mwenyekiti wa Azam, Shani Cristom, imesema kuwa kwa vile muda wa usajili wa wachezaji kwa El Merreikh ni mfupi wangeomba Simba kutumia uungwana ili kumruhusu Ngassa aende Sudan kufanyiwa vipimo vya afya baada ya awali kusaini mkataba wa miaka miwili kuichezea timu hiyo.
Pia barua hiyo inasema Azam wapo tayari kuwapa Simba Dola za Kimarekani 25,000 na wapo (Azam) kusaliwa na Dola 50,000 katika Dola 75,000 za kumuuzia Ngassa, na kuutaka uongozi huo wa Simba kuhakikisha suala la mchezaji huyo ikiwemo kuondoa pingamizi lao TFF linafanyika kabla ya saa 5 asubuhi.
Katibu Msaidizi wa Azam, Twalib Chuma alikiri kuandikwa kwa barua hiyo na kutumwa kwa uongozi wa Simba na nakala kupelekwa TFF akisema lengo ni kuhakikisha Ngassa anapata fursa ya kujiunga na timu ya El Merreikh inayoshiriki Ligi ya Mabingwa wa Afrika mwakani.
"NI keli tumewaandikia barua Simba na kutuma nakala TFF kwa sababu ya kutaka kulimaliza suala la Ngassa kiungwana ili kumpa nafasi mchezaji huyo kwenda kucheza soka la kulipwa Sudan kwa manufaa ya taifa," alisema.
Twalib alisema anadhani jambo hilo la Ngassa litaisha kwa amani na kila upande kuridhia, japo walisema hawakuona sababu ya kulumbana na Simba ilihali klabu zote zipo kwa maendeleo ya soka la Tanzania.
Habari nyingine zilizotufikia asubuhi hii zinasema kuwa, pande mbili za klabu hizo wanatarajia kukutana kwa ajili ya kusaini makubaliano mapya juu ya uhamisho wa nyota huyo alioyeng'ara katika michuano ya Kombe la Chalenji iliyomalizika nchini Uganda hivi karibuni.




No comments:

Post a Comment