http://www.thisday.co.tz/media/picture/large/Peter%20Kuga%20Mziray-%20%20APPT%20Maendeleo.jpg
Rais wa APPT Maendeleo, Peter Kuga Mziray
WAKATI Watanzania wa kada mbalimbali wakiendelea kuchambua na kutafakari juu ya Rasimu ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iliyozinduliwa hivi karibuni Chama cha African Progressive Party of Tanzania (APPT Maendeleo) kimeibuaka na kuwataka waipokee kwa mikono miwili kwani rasimu hiyo imekuja kutatua kero zao.
Kauli hiyo imetolewa na Rais Mtendaji wa APPT Maendeleo Peter Kuga Mziray wakati akizungumza na mwandishi wa habari hii leo jijini Dar es Salaam.
Mziray alisema tangu rasimu hiyo izinduliwe rasmi 3/6/2013 kumekuwepo na mitazamo mbalimbali ya kuipongeza na kuipinga kwa baadhi ya watu ambao kimantiki wanaipinga  ni watu wenye  malengo yao ya kuwa Marais wa Tanzania jambo ambalo linaelekea kufa.
Alisema Watanzania hasa wale wa Bara wamekuwa na kilio cha miaka mingi cha kuhitaji uwepo wa Tanganyika kama ilivyo Zanzibar lakini hawakusika jambo ambalo kwa sasa limepatiwa muafaka na Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
Rais Mtendaji alisema mapendekezo ya Tume ni mazuri kwa asilimia kubwa kwani yamezingatia maoni ya watu wengi ambao walikuwa wakihitaji rasimu ya katiba iwe hivyo bila kuogopa vivuli vya baadhi ya watu ambao wamejionyesha dhahiri kutokubaliana nayo.
“Kimsingi naunga mkono mapendekezo ya Tume kwani yamezingatia mahitaji ya Watanzania wote wa Bara na Visiwani na pia yana nia ya kuhakikisha kuwa Tanzania inaendelea kudumu bila mitafaruku,” alisema.
Alisema wapo watu wameibuka na kusema Serikali tatu zitakuwa ni kuongeza gharama kubwa kuziendesha jambo ambalo sio kweli kutokana na ukweli kuwa kila nchi itakuwa ikitumia rasilimali zilizopo katika upande wake na kuchangia Serikali ya Muungano ambayo haitakuwa kubwa.
Mziray alisema mapendekezo ya Tume yameaanisha mambo muhimu katika muungano ambayo yapo saba jambo ambalo ni ishara tosha kuwa hakukuwa na serikali kubwa kama inavyofikiriwa.
Mambo ayalitajwa kuhusika na muungano ni pamoja na katiba na mamlaka ya jamhuri ya muungano wa Tanzania, ulinzi na usalama wa jamhuri ya muungano wa Tanzania, uraia na uahamiaji, sarafu na benki kuu, mambo ya nje, usajili wa vyama vya siasa na ushuru wa bidhaa na mapato yasiyo na kodi yatokanayo na mambo ya muungano.
Aidha alisema rasimu hiyo imeenda mbali pale ilipoweka wazi kuwa ili mgombea wa Urais atangazwe anapaswa kushinda kura ambazo zitampatia 50 ya kura zote, pamoja na wagombea wa Urais kupata haki ya kuenda mahakamani kupinga matokeo.
Rais Mtendaji huyo pia alisema kupunguzwa kwa madaraka na kuwajibishwa kwa wabunge ambao hawafanyi kazi katika majimbo yao ni jambo muhimu ambalo Tume inapaswa kupongezwa kutokana na umuhimu wake hasa ukizingatia kuwa baadhi ya wawakilishi wa wananchi wamekuwa wakiishi mijini zaidi.
Maziray alisema pamoja na mapendekezo hayo ya tume ni vema mabaraza ya katiba yakapendekeza adhabu ambazo zinaweza kutolewa kwa utoro unaofanywa na wabunge jambo ambalo linaweza kurejesha hadhi ya Bunge ambalo kila siku linaonekana lipo wazi.
Kwa upande mwingine Mziray ameiomba Serikali kuanza mchakato wa uwepo wa Katiba ya Tanganyika ili iweze kuendana na mchakato wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania jambo ambalo litarahisisha uwepo kwa serikali hiyo.
Alisema bila kuwepo kwa Katiba ya Tanganyika itakuwa ngumu kutekeleza mapendekezo ya Tume ambayo yanahitaji kuwepo kwa Serikali tatu ambazo ni Tanganyika, Zanzibar na Tanzania.
Rais Mtendaji alisema mchakato huo hautakuwa na kazi ngumu kwani ukweli unaonyesha kuwa maoni mengi ambayo yapo katika rasimu na yalioachwa yalikuwa yanahusu serikali ya Tanganyika.