STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, September 20, 2013

Waziri Mukangara mgeni rasmi Redd's Miss Tanzania

Vimwana wanaotarajiwa kuchuana kesho kwenye shindano la Redd's Miss Tanzania 2013
WAZIRI wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk Fenella Mukangara, anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika shindano la urembo la taifa mwaka huu 'Redd's Miss Tanzania 2013' litakalofanyika kesho kwenye Ukumbi wa Mlimani City, Dar se Salaam.
Gazeti la kila siku la NIPASHE linalochapishwa na Kampuni ya The Guardian Ltd ni miongoni mwa wadhamini wa shindano hilo litakalotoa mwakilishi wa nchi katika fainali za Urembo za Dunia (Miss World).
Mkurugenzi wa Kampuni ya Lino International Agency, Hashim Lundenga, alisema jana wanatarajia  kiongozi huyo wa serikali kushuhudia shindano hilo na kwamba amesharidhia kuwa mgeni rasmi.
Lundenga alisema kila kitu kimekamilika na kuwataka wadau wa sanaa ya urembo kusubiri kushuhudia shindano lililo bora zaidi ya miaka iliyopita.
"Maandalizi yamekamilika na kama ni chakula, sasa kinachosubiriwa ni kukila tu," alisema kwa kifupi mratibu huyo ambaye kampuni yake imekuwa ikiandaa shindano hilo tangu 1994.
Alisema shindano hilo litapambwa na burudani kutoka kwa mshindi wa tuzo ya mwanamuziki bora wa kike nchini, Judith Wambura 'Lady Jay Dee' ambaye kwa sasa anatamba na vibao vyake vya Yahaya na Joto Hasira, Mike Rose wa Uganda na kikundi cha ngoma za asili cha Mama Afrika.
Shindano hilo linatarajiwa kushirikisha warembo 30 kutoka sehemu mbalimbali nchini watakaowania taji linaloshikiliwa na Brigitte Alfred, kutoka Kanda ya Kinondoni jijini ambaye kwa sasa yuko Indonea akijiandaa kupanda jukwaani kuwania taji la dunia ifikapo Septemba 28, mwaka huu.
Hata hivyo, warembo watano wameshatinga hatua ya 15 bora baada ya kutwaa mataji madogo yaliyoshindanishwa wakiwa kambini.
Warembo hao ni Severina Lwinga, kutoka Chuo cha Ustawi wa Jamii jijini Dar es Salaam ambaye ni Redd's Miss Personality, Prisca Clement (Redd's Miss Tanzania Talent), Clara Bayo (Redd's Miss Sports Woman ), Happiness Watimanywa (Redd's Miss Photogenic) na Narietha Boniface ambaye ni Redd's Miss Tanzania Top Model.
Mshindi wa taji hilo mwaka huu atabeba dhamana ya kuiwakilisha nchi katika shindano la urembo la dunia mwakani na zawadi ya Sh. milioni nane pamoja na gari lenye thamani ya Sh. milioni 15.

No comments:

Post a Comment