STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Sunday, July 29, 2012

YANGA KAMA KAWA KAMA DAWA YABEBA TENA KOMBE LA KAGAME

KLABU ya soka ya Yanga jana ilitwaa kwa staili ya aina yake ubingwa wake wa pili mfululizo na wa tano jumla wa Kombe la Kagame, la klabu bingwa ya soka ya Afrika Mashariki na Kati, kwa kuifunga Azam mabao 2-0 kwenye Uwanja wa Taifa. Ushindi huo si tu uliiwezesha kwa namna nyingi kulipa kisasi cha kudhalilishwa kwa mabao 3-1 na Azam kulikoandamana na kupigana uwanjani na kufungiwa wachezaji wake katika mchezo wa ligi kuu ya Bara Mei, bali pia ulikuwa wa kikatili. Bao la kwanza la Yanga lilifungwa na Hamisi Kiiza katika dakika ya 44 likiwa la tano kwa mchezaji huyo katika michuano ya mwaka huu, baada ya kunasa pasi ya nyuma ya beki wa pembeni wa Azam Ibrahim Shikanda. Lakini goli ambalo lilinogesha ushindi huo, na ambalo litakuwa liliikata maini vibaya Azam ni la mshambuliaji mpya hatari Said Bahanuzi la dakika ya mwisho ya majeruhi. Zikiwa zimeongezwa dakika tatu za majeruhi, mpira mrefu uliopigwa toka nyuma na beki Kelvin Yondani katika dakika ya 93 ulimkuta Bahanuzi akikabiliana na Said Morad. Akitumia ubavu aliojaaliwa na Mola, pande la mtu Bahanuzi alimzungusha Morad kabla ya kumtoka na kuachia shuti kali lililotinga kwenye nyavu za juu za goli na kumfanya mfungaji-mwenza aliyeongoza kwenye Kombe la Kagame kwa pamoja na Kiiza. Tedy Etekiama wa Vita ya JK Kongo pia alifunga mabao sita lakini CECAFA, shirikisho la soka la ukanda huo, liliwatunuku wauaji hao wa Yanga kutokana na kuipa timu yao ubingwa. Tofauti na mechi zilizotangulia, Azam ambayo ilifika fainali ya Kombe la Kagame kwa mara ya kwanza ikishiriki mara ya kwanza jana ilijenga mashambulizi yake taratibu kutokana na mpira wake wa pasi fupi fupi za kasi kuikauka. Kocha wa Yanga Tom Sentfiet aliwashukuru wachezaji wake kwa kumudu kucheza kwa "mbinu tulizopanga" na kwamba kufungwa kwao katika mechi ya kwanza kuliisadia kurekebisha makosa yaliyoipa ushindi wa mechi zote tano zilizofuata. Yanga ilikuwa pia bingwa wa Kombe la Kagame katika miaka ya 1975, 1993 na 1999 na mbali na kukata tiketi ya michuano hiyo tena mwakani imebakiza kikombe kimoja kufikia rekodi ya Simba ambayo ndiye bingwa pekee mara sita. Pia iwapo kama mwakani itafanikiwa kutetea taji hilo itakuwa timu ya pili baada ya AFC Leopard ya Kenya iliyowahi kufanya hivyo mfululizo wakati ikitamba katika soka la Afrika.
Katika vurugu za ushindi wa Azam Mei, wachezaji sita wa Yanga walitozwa faini zinazofikia jumla ya sh. milioni nane ambazo sasa zinaweza kulipwa kutoka katika zawadi ya sh. milioni 45 ya bingwa wa Kombe la Kagame. Azam inapata sh. milioni 30 wakati Vita imezawadiwa sh. milioni 15 kwa kushika nafasi ya tatu baada ya kuifunga APR ya Rwanda 2-0 mapema jana. Timu zilikuwa: YANGA: 'Barthez', Oscar Joshua, Stephano Mwasika, 'Cannavaro', Kelvin Yondani, Haruna Niyonzima, 'Chuji', Rashid Gumbo (Juma Seif dk.74), Hamisi Kiiza, Said Bahanuzi', David Luhende. AZAM: 'Dida', Ibrahim Shikanda (Samir Haji dk.68), Erasto Nyoni, Said Morad, Aggrey Moris, Jabir Aziz, Kipre Tchetche (Mrisho Ngasa dk.68), Salum Abubakar, John Bocco, Ibrahim Mwaipopo, 'Redondo'.

No comments:

Post a Comment