STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Sunday, July 29, 2012

Mobby Mpambala: Asiyeamini kama filamu zimempa nyumba, gari na kampuni

ALIPOSHAWISHIWA na nyota wa filamu nchini, Single Mtambalike 'Rich', aingie katika fani ya uigizaji, Mobby Mpambala, hakutilia maanani wazo hilo kutokana na imani aliyokuwa nayo juu ya sanaa ya Tanzania kwamba hailipi. Hata hivyo baada ya ushawishi wa muda mrefu na kuamua kujitosa rasmi mwaka 2000, msanii huyo amejikuta 'akiisujudia' fani hiyo kwa jinsi ilivyomwezesha kiuchumi na kimaisha tofauti na alivyofikiria mwanzoni. Mkali huyo wa filamu za mapigano na zile za kutisha, alisema kipindi kifupi cha kuweko kwake kwenye sanaa hiyo imemwezesha kujenga nyumba katika kiwanja alichokuwa nacho eneo la Gongolamboto, kununua gari na kumudu kuanzisha kampuni binafsi ya kuzalisha filamu ya 'Wizaga Entertainment'. Pia, msanii huyo anamiliki kundi la sanaa la Mtazamo Family linalojihusisha na sanaa za ngoma, maigizo na sarakasi huku akiendesha kiwanda kidogo cha kutengeneza masofa na samani nyingine za majumbani eneo la Amana-Ilala. "Sio siri kabla ya kuingia kwenye sanaa niliidharau fani hii kutokana na hali ya mambo ilivyokuwa miaka ya nyuma ambapo wasanii hawakuwa na chochote cha kujivunia, lakini leo nakiri sanaa Bongo inalipa kutokana na mafanikio makubwa niliyoyapata katika kipindi kifupi," alisema. Mpambala alisema alikutana na Rich mwaka 1996 na kumtaka ajiunge kwenye sanaa baada ya kugundua kipaji chake na umahiri wake wa michezo ya Kungfu na utunisha misuli, ila alimpuuza kwa vile aliringia ujuzi wake wa ufundi seremala. Alisema hata hivyo shinikizo la Rich pamoja na ndugu na jamaa zake waliotambua kipaji alichonacho, ndipo mwaka 2000 alipojitosa kwa kushiriki filamu ya 'Kidole Tumbo' iliyozuiwa na serikali kutoka. Mpambala alisema Rich 'alimbeba' kwa kumshirikisha katika kazi zake kadhaa kama 'Swahiba', iliyomtambulisha kwa mara ya kwanza yeye na Rose Ndauka, 'Mahabuba' na 'Heshima ya Penzi'. Alisema kazi hizo zilimfungulia neema kwa kushirikishwa kazi nyingine kadhaa zinazofikia 30 kwa sasa, akizitaja baadhi kuwa ni; 'Kamanda', 'Jozani', 'Signature', 'Secretary', '007', 'Time to Fight, 'Zuadiswa', 'Before Death', 'Hii ni Tatu', 'Criminal', 'Jamal' na 'The Chase' aliyoitaja kama filamu bomba kwake. AMRI PURI Mpambala, alisema licha ya kwamba hakuwahi kuota kuwa msanii, lakini alimzimia mno nyota wa zamani wa filamu za Kihindi, Amri Puri 'Mzee Ashanti', ambaye kwa sasa ni marehemu. Alisema alivutiwa na Amri Puri, kwa aina yake ya uigizaji kama mbabe na jitu katili, kitu alichodai amekuwa akimuiga katika baadhi ya picha alizocheza kama njia ya kumuenzi mkali huyo wa Bollywood. Mpambala anayezishabikia Simba na Manchester United, akipenda kula ugali kwa dagaa na kunywa soda ya Pepsi, alisema hakuna kitu cha furaha kwake kama siku alipomuoa mkewe wa kwanza aitwae, Jasmine mwaka 2004 na ndoa nyake ya pili dhidi ya Zola mwaka 2011. "Kwa kweli siku nilipofunga ndoa na wake zangu hawa ndio tukio la furaha kwangu, na ninahuzunishwa na kifo cha baba yangu mlezi, Abdul Ally Kibena aliyefariki mwaka 1999," alisema. Mpambala, anayechizishwa na rangi ya bluu, alisema kingine kinachompa furaha ni kufanikiwa kufyatua kazi zake binafsi tano za filamu kupitia kampuni yake ya Wizaga. Alizitaja kazi hizo kuwa ni 'I Wonder', My Brother', 'Criminal' aliyoshirikiana na 'Carlos', 'Fuvu' na 'Anti Virus' anazotarajia kuziingiza sokoni hivi karibuni. SKENDO Mpambala anayemzimia 'swahiba' wake Haji Adam 'Baba Haji', alisema kati ya vitu vinavyomkera ni tabia ya baadhi ya wasanii chipukizi kupenda kujihusisha na skendo kwa nia ya kutafuta umaarufu. Alisema vitendo vinavyofanywa na wasanii hao wasiojitambua vinaidhalilisha fani yao pamoja na kuzichafua familia za wasanii hao, licha ya wenyewe kuonekana kutojali. Mkali huyo mwenye watoto sita, alisema ifike wakati wasanii watambue umaarufu hupatikana kupitia umahiri wa kazi zao na sio kujidhalilisha ovyo magazetini. Mpambala anayependa kutumia muda wake wa ziada kufanya mazoezi na kuendesha kazi za useremala katika kiwanda chake na kundi lake la sanaa lililotoa ajira kwa vijana 30, alisema kama angekutana na Rais au Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo, angeomba sanaa isaidiwe. "Ningewaomba wasaidie iundwe kwa sheria kali ya kuthibiti wizi wa kazi za wasanii sambamba na kuwepo kwa mipango mizuri ya kutambuliwa kwetu kama ilivyo kwa watu wa kada nyingine wanaothaminiwa na kuenziwa nchini." ALIPOTOKA Mobbi Nassor Saleh Mpambala 'Mobby Mpambala', alizaliwa Novemba 28, 1965 katika wilaya ya Igunga,Tabora akiwa mtoto wa tatu kati ya nane wa familia yao. Alisoma elimu yake ya Msingi katika Shule ya Makurumla, jijini Dar kabla ya kurejea Tabora kumfuata mama yake aliyekuwa ametangana na baba yake na kujishughulisha na biashara ndogo ndogo huku akijiendeleza kwenye michezo ya sarakasi na kungfu aliyoicheza tangu utotoni. Mpambala anayewashukuru wazazi wake, Rich na mkewe wa kwanza Jasmine kwa namna walivyomsaidia kufika mahali alipo, amejaliwa kuwa na watoto sita watatu akiwapata katika ndoa yake ya kwanza nao ni Edo, 27, Mariam22 na Saleh,20. Watoto wake wengine ni Goodluck, 18, anayesoma Sekondari jijini Arusha, Zuwena, 13 aliyepo darasa la sita katika Shule ya Msingi Mapinduzi-Kigogo jijini Dar na Munira, 5 anayesoma chekechea.

No comments:

Post a Comment