STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Wednesday, November 20, 2013

Coastal yamsubiri Chippo kusajili dirisha dogo

Yusuph Chippo
MABINGWA wa zamani wa kandanda nchini, Coastal Union ya Tanga imesema haitakurupuka kufanya usajili katika dirisha dogo mpaka ipate maelekezo kutoka kwa kocha wao mpya, Mkenya Yusuf Chippo.
Aidha klabu hiyo imesema mpaka sasa haijapata taarifa zozote toka Simba juu ya kumrejesha kiungo wao, Uhuru Suleiman aliyekuwa akiichezea Coastal kwa mkopo katika duru la kwanza la Ligi Kuu Tanzania Bara.
Afisa Habari wa Coastal Union, Hafidh Kido, aliiambia MICHARAZO kuwa, ili kuepuka kufanya majukumu yasiyo yao, wameamua kumsubiri kocha wao mpya kuamua kwenye dirisha dogo kama atataka mchezaji mpya au la badala ya uongozi kukurupuka kulifanya zoezi hilo.
Kido alisema Chippo ambaye alikuwepo kushuhudia pambano la kufungia dimba la duru la kwanza kati ya Coastal na JKT Ruvu, ndiye mwenyewe jukumu la kuuelekeza uongozi kipi kifanyike katika dirisha dogo.
Alisema kwa vile hajapata muda wa kukaa na kuwafahamu wachezaji, viongozi wameamua kuiita mapema timu hiyo kambi ya mazoezi Desemba 2 ili kumpa wasaa kocha wao kujipanga upya kuanza kuinoa timu.
"Kambi ya mazoezi ya Coastal itaanza Desemba 2, lengo ni kutaka kumpa muda mzuri kocha wetu kuwasoma wachezaji na kama atabaini mapungufu katika idara za kikosi chake ndipo atapendekeza na sisi tutamsaidia kumtafutia mchezaji anayemtaka kwa nafasi anayotaka irekebishwe," alisema Kido.
Aliongeza baada ya kocha huyo kupata muda wa kukiangalia kikosi chake watamtafutia mechi za kirafiki za kujipima nguvu zitakazochezwa ndani na nje ya nchi kabla ya kuikabili Ligi Kuu duru la pili litakaloanza Januria 25.
Aidha klabu hiyo imesema haijapata  taarifa rasmi juu ya kurejea katika klabu ya Simba kiungo Uhuru Suleiman aliyekuwa akiichezea timu hiyo kwa mkopo, ingawa imesema haiwezi kumng'ang'ania mchezaji huyo.
Uhuru alinukuliwa kuwa ameamua kurejea Simba kumaliza mkataba wake na uongozi wa Simba kuthibitisha hilo, lakini Coastal wanasema haijapatiwa taarifa rasmi.
Coastal iliyomaliza duru la kwanza katika nafasi ya saba, iliachana na aliyekuwa kocha wake, Hemed Morocco aliyemaliza mkataba na kuamua kumnyakua Chippo aliyewahi kuzinoa Bandari-Mombasa, Nzoia, aliwahi  Mkurugenzi wa Ufundi (TD) wa Ulinzi na kuwa kocha msaidizi wa timu ya taifa la Kenya, Harambee Stars.

No comments:

Post a Comment