STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Sunday, June 21, 2015

The Cranes yamfukuzisha kazi kocha Nooij Taifa Stars

Bechi la ufundi
Kocha Stars na wenzake wakati wa wimbo wa Taifa kabla ya kuvaana na Uganda The Cranes
Kocha Nooij akisindikizwa na Polisi mara baada ya filimbi ya mwisho ya mchezo wa timu yake dhidi ya Uganda The Cranes am,bapo Stars ilichapwa mabao 3-0 kwenye Uwanja wa Amaan Zanzibar.
Na Mwandishi Wetu Zanzibar

SAFARI ya Kocha Mkuu wa timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars imeifikia tamati baada ya Kamati ya Utendaji ya TFF, kutangaza kulipiga chini benchi nzima baada ya timu hiyo kucharazwa mabao 3-0 na Uganda The Cranes.
Stars ilitandikwa mabao hayo katika mchezo wa kwanza wa kuwania fainali za Mataifa ya Afrika kwa Wachezaji wa Ndani (CHAN) zitakazofanyika mwakani Rwanda, uliochezwa kwenye Uwanja wa Amaan, visiwani hapa.
Mara baada ya pambano hilo ambalo lilikuwa la 18 kwa Stars chini ya Kocha Nooij ikiwa imeshinda mechi tatu tu, moja likiwa la mashindano Kamati ya Utendaji ya TFF ilikutana na kutoa taarifa ya kumtimua kocha huyo na wasaidizi wake na taarifa za chini chini zinapasha kuwa Charles Boniface Mkwasa na Abdallah Kibadeni huenda wakapewa timu.

TFF ilimpa kocha Mart Nooij mtihani wa mwisho na endapo atashindwa kuipeleka Taifa Stars, basi atafute njia ya kuondoka baada ya wapenzi wa soka nchini kuchoshwa na ipigo ya timu hiyo.


Wiki iliyopita, Taifa Stars ilipokea kichapo cha idadi kama hiyo cha mabao kutoka kwa Misri katika mchezo wa kufuzu kwa fainali za Mataifa ya Afrika (Afcon) zitakazofanyika mwaka 2017 nchini Gabon.


Katika mchezo huo ambao Stars ilicheza kama isiyo na mwalimu ilijikuta ikienda mapumziko ikiwa nyuma kwa bao 1-0. bao hilo liliwekwa kimiani na Sekisambo Erisa ambaye alikuja kufunga bao jingine na kufanya aitungie Stars mara mbili na lingine lilifungwa na Miya Farouk.

Kabla ya kuanza mchezo huo, Taifa Stars ilipata pigo baada ya mchezaji wake Oscar Joshua kuugua ghafla na kuukosa mchezo huo.


Kwa mara ya mwisho Stars ilifuzu kwa fainali hizo za Chan mwaka 2009 zilipofanyika kwa mara ya kwanza nchini Iory Coast na ilitolewa katika hatua ya makundi ikiwa chini ya Mbrazil Marcio Maximo.


Mara baada ya pambano hilo mashabiki wenye hasira walitaka kumtandika kocha Nooij kabla ya askari Polisi waliokuwa uwanjani kumuokoa.
Tangu mapema mara baada ya kufungwa bao la kwanza, mashabiki waliibadilika Stars na kuanza kuizomea na kuwafanya wachezaji kupoteza kujiamini na kusababisha kufungwa mabao mengine yaliyoiweka timu hiyo katika wakati mgumu kusonga mbele kwenye michezzo hiyo ya Chan.
Stars na Uganda zitarudiana wiki mbili zijazo na mshindi atakayesonga mbele ataumana na Sudan katika raundi inayofuata.
Chini ni taarifa ya TFF juu ya kusitisha kibarua cha Kocha Nooij.

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
 20 JUNI, 2015
KAMATI YA UTENDAJI YASITISHA AJIRA YA NOOIJ
Kamati ya utendaji ya Shirikishi la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) Katika kikao chake cha leo pamoja na mambo mengine ilipitia mwenendo wa Timu ya Taifa (Taifa Stars) ikiwa ni pamoja na kuhudhuria mchezo kati ya Tanzania na Uganda, kama sehemu ya tathmin ya mwenendo wa timu.

Kamati ya utendaji kwa kauli moja imeamua yafuatayo:

1.Ajira ya Kocha Mkuu Maart Nooij inasitishwa mara moja kuanzia  tarehe 21/June/2015.

2.Benchi lote la ufundi la Taifa stars limevunjwa kuanzia tarehe 21/06/2015.

3.Uongozi wa TFF utatangaza punde benchi jipya la ufundi la timu ya Taifa.

IMETOLEWA NA SHIRIKISHO LA MPIRA WA MIGUU TANZANIA (TFF)

No comments:

Post a Comment