STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Wednesday, May 1, 2013

AZAM INA KILA SABABU ZA KUSHINDA MOROCCO

Khamis Mcha 'Vialli' nyota wa Azam katika pambano lao dhidi ya As Far Rabat jijini Dar na kuisha kwa 0-0

Kikosi Tegemeo cha Azam

Azam wakijifua mjini Rabat

Wachezaji wa Azam, walipokuwa wakijiandaa na pambano lao dhidi ya BYCII

Na Patrick Kahemela, Rabat
KIKOSI cha timu ya Azam Fc ipo mjini Rabat ikijiandaa kukabiliana na AS FAR kwenye mechi ya raundi ya mwisho ya 16 bora za kombe la shirikisho. Azam FC imetua hapa na wachezaji 23, benchi lote la ufundi isipokuwa Ibrahim shikanda pekee aliye masomoni Nairobi na uongozi karibu wote na kwa pamoja kama timu Azam FC ina dhamira ya kuifunga na kuisukuma nje ya mashindano timu ya AS FAR.
Kuna sababu sita zinazoifanya Azam FC iamini na ijiamini kuwa inaweza kushinda kwenye mtanange wa jumamosi hii. Sababu hizo ni maandalizi bora, wachezaji wazuri, Uongozi Mzuri, benchi bora la ufundi chini ya Stewart Hall, Mipango mizuri na dhamira ya kupata mafanikio. Makala hii itakayowajia katika sehemu tatu itachambua vipengele vilivyoaninishwa hapa chini.
MAANDALIZI MAZURI
Timu za Tanzania kwa miaka mingi zimekuwa zikishiriki mashindano ya kimataifa yanayoandaliwa na CAF, kwa Azam FC hii ni mara yake ya kwanza kupata nafasi hii. Lakini unaweza kuona utofauti mkubwa wa maandalizi kati ya Azam FC na timu nyingi za Tanzania na utofauti huo ndiyo unaoifanya Azam FC hadi sasa kuweza kucheza mechi tano pasi na kupoteza mchezo hata mmoja.
Azam FC baada ya kujua kuwa itawakilisha nchi kwenye mashindano ya kimataifa iliamua kufanya juhudi za makusudi za kujiandaa kwa kiwango cha mashindano hayo yanayoandaliwa na CAF.
Azam FC ilifanya ziara na kucheza mechi nane za kimataifa za kirafiki nje ya ardhi ya Tanzania, ilikwenda Kinshasa Congo DRC na kushiriki Congo Charity Cup ambako ilitwaa kikombe kabla ya kusafiri tena hadi Nairobi ambako ilipata nafasi ya kucheza mechi nyingine tatu.
Lengo la ziara hizi ilikuwa ni kuwapa ukomavu na uzoefu vijana wake ili wanapokuwa kwenye mashindano ya CAF hasa wanapocheza mechi za ugenini wasiwe na hofu. Hakika matunda ya ziara hizi tunayaona kwani Azam FC imeshinda ugenini mechi zake zote mbili za awali hadi sasa.
Maadalizi ya Azam FC kwenye mashindano haya pia yalihusisha utafutwaji na usajili wa wachezaji wenye viwango vya kuweza kucheza na kuisaidia timu, uboreshwaji wa kambi ya mazoezi ya Chamazi mapema kwa ajili ya kambi ya nyumbani, ununuzi wa vifaa bora vya mazoezi na kadhalika.
UWEZO WA WACHEZAJI
Timu ni wachezaji, bila ya wachezaji bora wenye nidhamu, viwango bora na malengo ni sawa na bure. Azam FC ililitambua hilo mapema… Azam FC haikukurupuka kusaka wachezaji kwa mkupuo, usajili wa wachezaji kwa ajili ya mashindano ya CAF ulifanyika kwa umakini kwa muda mrefu huku klabu ikijiwekea malengo ya kuwa na kikosi bora kitakochoweza kupambana na kuvifunga vigogo vya soka la Afrika.
Leo ukiwaangalia wachezaji 25 wa Azam FC waliosajiliwa kwenye mashindano ya CAF utaungana nami kuwa ni wachezaji sahihi kwa mashindano haya.
Wachezaji wa Azam FC wana nidhamu na vipaji vya hali ya juu. Wote wana viwango vya kuweza kuwemo kwenye kikosi cha timu ya Taifa ya Tanzania na kuanza kwenye kikosi cha kwanza. Hapa nitazungumzia sifa za wachezaji wa eneo la ulinzi tuu kwa ufupi… halafu muendelezo wa makala hii utawaletea wachezaji wa kiungo na baadaye washambuliaji.
MWADINI ALLY; Golikipa chaguo la kwanza la kikosi cha timu ya Taifa ya Zanzibar na sehemu ya kudumu ya kikosi cha timu ya Taifa ya Tanzania. Ana uzoefu mkubwa wa michezo ya kimataifa akiiongoza Zanzibar kushika nafasi ya tatu mara mbili kwenye mashindano ya CECAFA. Ni golikipa hodari ambaye Azam FC tunajivunia kuwa naye
AISHI MANULA, utasemaje juu ya kipaji cha kijana huyu toka Morogoro? Wengi wanamfananisha na golikipa wa zamani wa Tanzania na Simba Mohammed Mwameja. Aishi anajiamini, ana umbo zuri na kipaji kikubwa sana. Ndiyo maana haishangazi kwa nini yeye ni golikipa namba moja wa timu za vijana za taifa na chaguo namba tatu la Taifa Stars ya kocha Kim Poulsen
HIMID MAO; Ana miaka 20 tuu lakini ni mkongwe ndani ya kikosi cha Azam FC, Himid ni kiungo mwenye sifa za kukaba ambaye sasa anacheza kama beki wa kulia wa Azam FC. Hakuna aliyeshangaa jina lake lilipoitwa na Kim Poulsen kuwa sehemu ya wachezaji 30 bora nchini wanaonyemelea nafasi za walio timu ya Taifa. Himid Mao aliibukia kwenye mashindano ya Copa Cocacola na baadaye kuwa nahonda wa timu za taifa za Tanzania chini ya miaka 20. Kabla ya mwalimu wa wakati huo wa Azam FC Itamar Amorim kumpa nafasi kwenye kikosi cha kwanza akitokea Azam Academy. Himid anafanya vizuri sana kwenye kikosi cha Azam FC hadi sasa.
WAZIRI SALUM; huenda ndiye mchezaji mwenye kipaji kikubwa cha kumiliki mpira kuliko wachezaji wote nchini Tanzania kwa sasa. Waziri Salum, naye yumo kwenye daftari la kocha Kim Poulsen na ni mwanachama wa kudumu wa kikosi cha Zanzibar heroes. Mguu wake wa kushoto ni kama mkono wa paka kwani anaweza kufanya lolote na mpita kwa kutumia mguu huu. Ana mbinu za kukaba, ana krosi za hatari na chenga za maudhi. Ni hadhina kubwa kwa Azam FC na taifa la Tanzania
JOCKINS ATUDO; beki bora wa ligi kuu ya Kenya KPL msimu uliopita Jockins Atudo alitua Azam FC wakati wa dirisha dogo la Disemba mwaka jana ili kuimarisha ukuta wa Azam FC kwa ajili ya mashindano haya. Tangia atue Azam FC Atudo amethibitisha kuwa waliomchagua kuwa beki bora hawakukosea. Kocha wa zamani wa Harambee Stars James Nandwa alisema wakati tunataka maoni yake juu ya atudo kabla ya kumsajili kuwa ukiwa na beki kama Atudo unapata vitu viwili, kwanza uongozi ndani ya uwanja pili beki mwenye kipaji, nguvu, kimo na kujitolea… hakika kila kocha angependa kuwa na Atudo kwenye kikosi chake
LUCKSON KAKOLAKI; labda ndiye mchezaji mwenye busara zaidi kwenye kikosi cha Azam FC kiasi kwamba wachezaji wenzake wanamuheshimu na kumkubali kama kaka. Busara hizi za nje ya uwanja pia unaweza kuziona ndani ya uwanja mbapo Luckson amekuwa mhimili mkuu kwa Azam FC hasa pale eneo la ulinzi linapokabiliwa na majeruhi. Kiwango chake cha uchezaji kimekuwa cha uhakika wakati wote na hili alilithibitisha kwenye mechi ya awali dhidi ya AS FAR ambapo aliingia katika dakika ya sita baada ya Atudo kuumia na kucheza kwa ustadi mkubwa sana Luckson ni mchezaji mmoja wapo ambaye tunaweza kusema ana damu ya bluu (yaani ana damu yenye rangi ya Azam FC)
DAVID MWANTIKA; Tanzania tumejaaliwa kuwa na mabeki wazuri lakini hatujawahi kuwana beki wa kiwango cha David Mwantika tangia kuondoka kwenye ramani ya soka kwa Boniface Pawasa. Mwantika hapitiki kwa namna yoyote ile… Mwantika ana nguvu za asili na mwili uliojengeka. Wenyewe wanyakyusa wanamuita Bedui… Mwantika ana spidi ya upepo na amekuwa maarufu ndani ya wachezaji wa Tanzania lakini alikuwa na umaarufu mdogo nje kutokana na timu yake ya Prisons kutopewa nafasi sana na vyombo vya habari. Lakini ukikutana na washambuliaji wa ligi kuu watakuambia kuwa beki wanayemuogopa zaidi nchini ni David. Juzi kim Poulsen amemjumuisha kwenye kikosi chake na bila shaka wala wasiwasi Mwantika atavuka kwenye kikosi cha Young taifa Stars na kuingia kwenye kikosi cha kwanza cha Taifa Stars muda si mrefu
Katika makala zijazo, tutawaletea maelezo ya wachezaji waliosalia wa kiungo na ushambuliaji pamoja na sababu nyingine nne zilizosalia za kwa nini Azam FC itaifunga AS FAR ambazo ni UONGOZI BORA, BENCHI BORA LA UFUNDI, MIPANGO MIZURI, na DHAMIRA

No comments:

Post a Comment