STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Tuesday, June 18, 2013

Kichanga chatafunwa na mbwa baada ya kutupwa kichakani

mbwa kama huyu amemtafuna kitoto kichanga
MTOTO mchanga ameliwa na mbwa na  kubakishwa mguu, baada ya mtu asiyejulikana kukitelekeza kichakani katika eneo la Magole, mtaa wa Kivule, Manispaa ya Ilala, jijini Dar es Salaam.Tukio hilo la kusikitisha limebainika baada ya mbwa huyo kukibeba kiungo hicho kutoka kilipokuwa na kukifikisha nyumbani anakofugwa majira ya sita mchana juzi.
Mwenye mbwa huyo aliyejitambulisha kwa jina la Maria John, aliiambia NIPASHE kuwa, kabla ya kupelekwa mguu huo, jana yake mbwa huyo alikwenda na utumbo ambao hata hivyo hakuna aliyekuwa  na hofu nao, kwani walidhani ni wa kuku.
 
“Niliona ni kitu cha kawaida tu, mbwa hutembelea maeneo mbalimbali labda ameokota mzoga wa kuku, lakini leo (juzi) nilipoona mguu nilistaajabu na kufahamu kuwa ni kiungo cha binadamu nilitoa taarifa kwa majirani na kupata msaada,” alisema.
 
Alisema lengo la kutoa taarifa kwa majirani zake ni ili waweze kujadiliana na  kutamfuta aliyefanya kitendo hicho cha kikatili kisha baadaye kutoa taarifa kwa mjumbe wa mtaa huo.
 
Mmoja wa majirani waliokusanyika kushuhudia tukio hilo ambaye hakupenda jina lake liandikwe gazetini, alisema hajawahi kushuhudia tukio kama hilo.
 
“Ni tukio la kushangaza na kusikitisha sana kwa mtu kukatisha maisha ya kiumbe kisicho na hatia,kwani huwezi kujua mungu alimpangia nini duniani, hivyo kwa kweli kama mama najisikia uchungu sana,” alisema.
 
Mjumbe wa Serikali ya Mtaa wa eneo hilo, Grace Martin, alisema alipigiwa simu na mdogo wake kuwa, mbwa ameokota kiungo cha mtoto na  kutakiwa kurudi mtaani hapo haraka.
 
“Nilipofika nilihakikisha kuwa kweli ni mguu wa mtoto, niliamua kumpigia simu Mwenyekiti wa Mtaa kwa ajili ya msaada,”alisema.
 
Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Kivule,Joseph Gassaya alisema yeye alipojulishwa alitoa taarifa kwa Jeshi la Polisi kituo cha Stakishari Ukonga nao baada ya muda mfupi walifika eneo la tukio.
 
Alisema askari walitoa amri ya kukizika kiungo hicho katika eneo hilo, huku Jeshi la Polisi likiendelea na upelelezi wa kumsaka mama aliyefanya ukatili huo ili afikishwe kwenye vyombo vya sheria.
 
Chanzo:Nipashe

No comments:

Post a Comment