STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Tuesday, July 30, 2013

Mabondia wa Tanzania huuza mechi zao Ulaya?

http://www.thehabari.com/wp-content/uploads/2011/11/Rashid-matumla.png
Rashid Matumla 'Snake Man'

Benson Mwakyembe
 

http://www.ibn-tv.com/wp-content/uploads/2012/02/Nyilawila.jpg
Karama Nyilawila aliyetwaa ubingwa wa WBF Ulaya

MABONDIA Mada Maugo na Benson Mwakyembe Jumamosi walipokea vipigo nchini Russia katika mapambano yao ya kimataifa, huku kukiwa na tuhuma kwamba mabondia wengi wa Kitanzania wanaoenda kupigana nje ya nchi 'huuza' mechi zao.
Maugo alipokea kichapo cha TKO ya raundi ya 5 katika pambano la raundi 8 dhidi ya bondia asiye na uzoefu Movsur Yusupov aliyecheza mapambano manne tu kulinganisha na Mtanzania huyo aliyepigana michezo 25.
Mtanzania mwingine, Mwakyembe alidundwa kwa KO ya raundi ya 7 ya pambano lake la raundi 8 dhidi ya bondia mwingine asiye na uzoefu Apti Ustarkhanov, ambaye hilo lilikuwa ni pambano lake la tatu na la pili kushinda tangu aingie kwenye ngumi za kulipwa.
Kina Maugo walipambana dhidi ya wenyeji wao katika mapambano ya uzito wa Super Middle ya raundi nane yaliyofanyika katika ukumbi wa Trade & Entertainment Centre 'Moskva', Kaspiysk chini ya wakala Mkenya Thomas Mutua.
Vipigo vya mabondia hao vimekuja wakati wadau wa ngumi za kulipwa wakihoji sababu zinazofanya mabondia wa Kitanzania kushindwa kutamba kila waendapo nje huku ripoti mbalimbali zikiwatuhumu mabondia wa majuu kuwatumia mabondia kutoka Afrika kupandisha chati zao katika viwango vya ubora kwa kuwanunua wawaachie washinde.
Ripoti za kuuzwa mechi au kuwapo kwa mchezo mchafu ziliwahi kutolewa na baadhi ya mabondia akiwamo Pascal Ndomba na Francis Cheka aliyepokea kichapo cha kushangaza mapema mwaka huu nchini Ujerumani.

Ndomba anayepigana uzito wa juu wa (Cruiserweight), alisema baadhi ya mawakala wa nje hutaka mabondia dhaifu wa kwenda kupigana na mabondia wao ili kupata ushindi kirahisi na kuboresha rekodi zao.
"Hili ndilo linalofanyika, bondia mkali mara chache sana kupelekwa nje na hata akienda basi atahujumiwa ili apoteze mchezo kwa manufaa ya mabondia wanaoenda kupigana nao," Ndomba alisema hivi karibuni.
Naye Cheka alitoa maelezo ya kufanyiwa 'hila' katika pambano lake dhidi ya Uensal Arik aliloongoza kwa raundi sita za mwanzo kabla ya kurushiwa kitaulo katika raundi ya saba na kupoteza mchezo kwa TKO.

Pascal Ndomba
"Sikupoteza pambano lile, ila mwenyeji alibebwa na mwamuzi aliyemaliza pambano kana kwamba nimesalimu amri, ni vigumu mabondia wa Tanzania kushinda nje," alisema Cheka mara alipotua nchini.
Cheka alisema kambi ya mpinzani wake walimfuata hadi hotelini alipofikia kuelekea pambano lao kumshawishi awaachie pambano hilo kwa ahadi ya pesa lakini alipokataa ndipo alipokuja kuhujumiwa ulingoni kwa mtu aliyekuwa upande wa kona yake kurusha taulo ulingoni ilhali alikuwa akiongoza kwa pointi.
Bondia huyo anayeaminika kuwa bora zaidi nchini kwa sasa katika uzito wake, alisema hakuambatana na kocha wake wakati akienda katika pambano hilo hivyo hata kwenye kona yake walikuwa wenyeji wake na ndiyo waliorusha taulo ulingoni.
Hata hivyo, wapo waliomtuhumu kwamba huenda Cheka alicheza 'dili' na wakala wa pambano hilo ili kutotibua rekodi ya mpinzani wake ambaye alikuwa amepoteza pambano moja tu ya 18 aliyokuwa amecheza.
NIPASHE ilizungumza na Marais wa Mashirikisho ya Ngumi za Kulipwa Tanzania, Emmanuel Mlundwa wa PST na Yasin Abdallah 'Ustaadh' wa TPBO kutaka kujua ukweli kuhusu tuhuma hizo, ambapo walikuwa na maoni tofauti .
Mlundwa alisema kinachowaponza mabondia wa Tanzania siyo hujuma wala nini ila maandalizi duni wanayofanya kabla ya mapambano yao pia kuwa na viwango duni kulinganisha na wapinzani wao wanaoenda kucheza nao.

"Ngumi za kulipwa ni biashara, mabondia wa ngumi hizo wanapotafutiwa mechi wanapaswa kujiandaa, lakini hilo halifanyiki na hivyo kwenda kulitia aibu taifa na kujiharibia soko wao wenyewe bila kujua," alisema Mlundwa.
Nyota huyo wa zamani wa kimataifa wa ngumi, alisema siyo kweli kama kuna rushwa zinazofanyika bali Watanzania wanaopewa nafasi kulingana na rekodi zao nchini huenda kupigana kichovu kwa kukosa maandalizi mazuri.
Ustaadh yeye alisema
Francis Cheka
linalowaangusha mabondia wa Tanzania nje ya nchi ni maisha wanayoishi kuwa kinyume na nidhamu ya ngumi za kulipwa na kwamba kutokuwa na mameneja ni tatizo jingine linalowakwaza.
"Mabondia wengi hawafanyi mazoezi mpaka wakati wa pambano, hapo unatarajia afanye vizuri? Pia hawaishi kwa kuzingatia miiko ya ngumi na hivyo wanapoenda nje ni rahisi kupigwa na kuhisiwa labda wanauza," anasema.

Alisema ni vyema mabondia wakafanya kazi chini ya mameneja kama ilivyokuwa kwa Rashid Matumla kwani itafanya ajikite kwenye mazoezi tu na mambo mengine kuwaachia meneja zao.
Ustaadh alisema majukumu wanayobeba mabondia ya kufanya kila kitu wakati mwingine huwafanya washindwe kujikita kwenye mazoezi na hivyo kujikuta muda wa pambano ukifika hawajajiandaa vizuri.
Rais huyo wa TPBO-Limited, alisema pia mabondia wengi hutoa visingizio kila wanapopigwa nje ya nchi bila kuangalia kama sheria za ngumi zinasemaje wanapokuwa kwenye ulingo na kutolea mfano pigano la Cheka na Arik.
"Cheka alipolalamika nilimuuliza vipi katika pambano lake na Arik, hakutupa ngumi yoyote katika raundi ya 7 na kupigwa makonde mfululizo na kunieleza mkono wa kulia ulimzingua, sheria zinasema bondia asipojibu mapigo kwa zaidi ya ngumi 10 alizorushiwa refa anaweza kuvunja pambano au wasaidizi wa bondia kuingilia kati kwa kurusha kitaulo na ndivyo ilivyotokea," alisema.
Mada Maugo

No comments:

Post a Comment